Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unashiriki Katika Kufanya Mikutano ya Kikristo Iwe Yenye Kujenga?

Je, Unashiriki Katika Kufanya Mikutano ya Kikristo Iwe Yenye Kujenga?

Je, Unashiriki Katika Kufanya Mikutano ya Kikristo Iwe Yenye Kujenga?

“Mnapokuja pamoja, . . . mambo yote na yatendeke kwa ajili ya kujenga.”—1 KOR. 14:26.

1. Kulingana na andiko la 1 Wakorintho sura ya 14, mikutano ya Kikristo inatimiza kusudi gani la maana?

‘MKUTANO wa leo umekuwa wenye kujenga sana!’ Je, umewahi kusema hivyo baada ya kuhudhuria mkutano kwenye Jumba la Ufalme? Bila shaka umewahi kusema hivyo! Kwa kweli, mikutano ya kutaniko inatutia moyo sana, lakini hilo si jambo la kushangaza. Kwa kuwa, kama vile ilivyokuwa katika siku za Wakristo wa mapema, kusudi la maana la mikutano yetu leo ni kuwatia nguvu kiroho watu wote wanaohudhuria. Ona jinsi mtume Paulo alivyokazia kusudi hilo moja la mikutano ya Kikristo katika barua yake ya kwanza kwa Wakorintho. Katika sura yote ya 14, anataja tena na tena kwamba kila sehemu katika mikutano ya kutaniko inapaswa kutimiza kusudi hilohilo, yaani, “kulijenga kutaniko.”—Soma 1 Wakorintho 14:3, 12, 26. *

2. (a) Ni nini kinachofanya mikutano iwe yenye kujenga? (b) Tutazungumzia swali au ulizo gani?

2 Kwanza kabisa, tunatambua kwamba uvutano wa roho ya Mungu ndio unaofanya mikutano iwe yenye kujenga au yenye kuelimisha. Kwa hiyo, katika kutaniko tunaanza kila mkutano kwa kusali kwa Yehova kutoka moyoni na kumwomba Baba yetu wa mbinguni abariki mkutano wetu kupitia roho yake takatifu. Hata hivyo, tunajua kwamba washiriki wote wa kutaniko wanaweza kushiriki katika kufanya programu ya mikutano iwe yenye kujenga kadiri iwezekanavyo. Hivyo basi, ni hatua gani ambazo kila mmoja wetu anaweza kuchukua ili kuhakikisha kwamba sikuzote mikutano ya kila juma ambayo inaongozwa katika Jumba letu la Ufalme inaburudisha na kutia moyo kiroho?

3. Mikutano ya Kikristo ni ya maana kadiri gani?

3 Ili kujibu swali hilo, tutachunguza mambo fulani ambayo wale wanaoongoza wanapaswa kukumbuka kuhusu mikutano yetu. Pia, tutazungumzia jinsi kutaniko lote kwa ujumla linavyoweza kushiriki katika kufanya mikutano iwe pindi ambazo zinawatia moyo wote wanaohudhuria. Tunapendezwa sana na habari hiyo kwa sababu mikutano yetu ni mitakatifu. Kwa kweli, kuhudhuria na kushiriki katika mikutano ni mambo ya maana ya ibada yetu kwa Yehova.—Zab. 26:12; 111:1; Isa. 66:22, 23.

Mkutano Unaokusudiwa Kutusaidia Kujifunza Biblia

4, 5. Ni nini kusudi la Funzo la Mnara wa Mlinzi?

4 Sisi sote tunataka kufaidika kikamili kutokana na Funzo letu la kila juma la Mnara wa Mlinzi. Hivyo, ili tuelewe kusudi kuu la mkutano huo, acheni tujikumbushe marekebisho fulani ambayo yamefanywa katika gazeti la Mnara wa Mlinzi na katika habari au makala za funzo.

5 Kuanzia toleo la kwanza la funzo la gazeti la Mnara wa Mlinzi la Januari 15, 2008 (15/1/2008), jambo fulani muhimu liliongezwa kwenye jalada la mbele. Je, uliona jambo hilo? Chunguza kwa uangalifu jalada la mbele la gazeti ambalo umeshika. Chini ya picha ya mnara, utaona Biblia iliyofunguliwa. Picha hiyo ya Biblia iliongezwa ili ikazie kusudi la Funzo letu la Mnara wa Mlinzi. Gazeti hili linakusudiwa kutusaidia kujifunza Biblia. Ndiyo, katika Funzo letu la kila juma la Mnara wa Mlinzi, Neno la Mungu ‘linafafanuliwa,’ na ‘maana yake inaelezwa’ kama tu ilivyokuwa zamani katika siku za Nehemia.—Neh. 8:8; Isa. 54:13.

6. (a) Ni marekebisho gani yaliyofanywa katika Funzo la Mnara wa Mlinzi? (b) Tunapaswa kukumbuka nini kuhusu maandiko yenye neno “soma”?

6 Kwa kuwa Biblia ndicho kitabu chetu kikuu cha mafundisho, marekebisho yalifanywa katika Funzo la Mnara wa Mlinzi. Maandiko fulani yanayotajwa katika makala za funzo yana neno “soma.” Sisi sote tunatiwa moyo kutumia nakala yetu ya Biblia kufuata usomaji wa maandiko hayo wakati wa mkutano. (Mdo. 17:11) Kwa nini? Kwa sababu tunapoona mashauri ya Mungu katika Biblia yetu wenyewe, yanatugusa moyo zaidi. (Ebr. 4:12) Kwa hiyo, kabla ya maandiko hayo kusomwa kwa sauti, yule anayeongoza mkutano huo anapaswa kuwapa wahudhuriaji wote wakati wa kutosha kufungua maandiko hayo na kufuata usomaji wa mistari hiyo.

Sasa Tuna Wakati Zaidi wa Kueleza Imani Yetu

7. Sasa tuna nafasi gani wakati wa Funzo la Mnara wa Mlinzi?

7 Marekebisho mengine ambao yalifanywa katika makala za funzo la Mnara wa Mlinzi yanahusu urefu wa makala hizo. Katika miaka ya hivi karibuni, makala hizo zimefupishwa. Hivyo, wakati wa Funzo la Mnara wa Mlinzi, wakati mchache zaidi unatumiwa kusoma mafungu na wakati mwingi zaidi unatumiwa kutoa maelezo. Sasa watu wengi zaidi katika kutaniko wana nafasi ya kutangaza waziwazi imani yao kwa kujibu swali ambalo limechapishwa, kueleza matumizi ya andiko, kusimulia jambo fupi lililoonwa ambalo linaonyesha hekima ya kufuata kanuni za Biblia, au katika njia nyingine mbalimbali. Muda fulani unapaswa kutumiwa kuzungumzia picha zilizo katika gazeti.—Soma Zaburi 22:22; 35:18; 40:9.

8, 9. Kiongozi wa Funzo la Mnara wa Mlinzi ana daraka gani?

8 Hata hivyo, tutakuwa na wakati zaidi wa kutoa maelezo mbalimbali ikiwa tu washiriki wanatoa maelezo mafupi na yule anayeongoza mkutano huo anaepuka kutoa-toa maelezo kila wakati katika Funzo la Mnara wa Mlinzi. Hivyo basi, ni nini kinachoweza kumsaidia kiongozi awe na usawaziko unaofaa anapotoa maelezo yake na kutaniko linapotoa maelezo ili mkutano uwajenge watu wote?

9 Ili kujibu swali hilo, fikiria mfano ufuatao. Funzo la Mnara wa Mlinzi ambalo linaongozwa vizuri ni kama shada au fungu la maua ambalo linavutia macho. Kama vile ambavyo fungu kubwa la maua linavyotengenezwa kutokana na maua mengi tofauti-tofauti, ndivyo Funzo la Mnara wa Mlinzi linavyofanyizwa na maelezo mengi tofauti-tofauti. Na kama vile tu ambavyo ua moja katika fungu hilo lilivyo na ukubwa na rangi tofauti na maua mengine, ndivyo maelezo yanayotolewa kwenye mkutano yanavyotofautiana katika urefu na jinsi yanavyotolewa. Kiongozi wa funzo hilo ana daraka gani? Maelezo yake ya mara moja moja ni kama mimea michache ya kijani-kibichi ambayo inaongezwa kwa uangalifu kwenye fungu la maua. Mimea hiyo michache haitawali; badala yake, inasaidia kuboresha na kuunganisha fungu lote la maua. Vivyo hivyo, yule anayeongoza anahitaji kukumbuka kwamba daraka lake si kutawala mazungumzo, bali ni kukamilisha maelezo ya kumsifu Mungu ambayo yanatolewa na kutaniko. Ndiyo, maelezo mengi mbalimbali yanayotolewa na kutaniko yakiunganishwa kwa ustadi na maelezo machache yanayotolewa wakati unaofaa na yule anayeongoza, yanakuwa kama fungu maridadi la maneno ambalo litawavutia wote wanaohudhuria.

“Sikuzote na Tumtolee Mungu Dhabihu ya Sifa”

10. Wakristo wa mapema walikuwa na maoni gani kuhusu mikutano ya kutaniko?

10 Maelezo ya Paulo katika andiko la 1 Wakorintho 14:26-33 kuhusu mikutano ya Kikristo yanatusaidia kuelewa zaidi jinsi mikutano hiyo ilivyoongozwa katika karne ya kwanza. Akieleza kuhusu mistari hiyo, msomi mmoja wa Biblia aliandika hivi: “Ni wazi kwamba jambo ambalo lilikuwa la pekee sana katika ibada ya Kanisa la mapema ni kwamba karibu kila mtu alihudhuria akihisi kwamba ana pendeleo na daraka la kuchangia jambo fulani kwenye ibada hiyo. Mtu hakuja akiwa tu na kusudi la kuwa msikilizaji; hakuja kupokea tu bali pia kutoa.” Kwa kweli, Wakristo wa mapema waliona mikutano ya kutaniko kuwa nafasi za kueleza imani yao.—Rom. 10:10.

11. (a) Ni nini kinachosaidia sana kufanya mikutano iwe yenye kujenga, na kwa nini? (b) Tunaweza kuboresha maelezo yetu kwenye mikutano tukifuata mapendekezo gani? (Ona maelezo ya chini.)

11 Kueleza imani yetu kwenye mikutano kunasaidia sana “kulijenga kutaniko.” Bila shaka, utakubali kwamba hata kama tumekuwa tukihudhuria mikutano miaka mingapi, bado tunafurahia kwelikweli kusikiliza maelezo ya ndugu na dada zetu. Tunaguswa moyo na maelezo yanayotoka moyoni ya mwamini mwenzetu mwaminifu ambaye amezeeka; tunahisi kwamba tumetiwa moyo na maelezo ya busara yanayotolewa na mzee wa kutaniko mwenye kujali; na tunajikuta tukitabasamu wakati mtoto anapotoa maelezo kutoka moyoni kuonyesha kwamba anampenda Yehova kikweli. Ni wazi kwamba tunapotoa maelezo, sote tunashiriki katika kufanya mikutano ya Kikristo iwe yenye kujenga. *

12. (a) Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Musa na Yeremia? (b) Sala inatimiza sehemu gani katika kutoa maelezo?

12 Hata hivyo, inaweza kuwa vigumu sana kwa watu ambao wanaona haya kutoa maelezo. Ikiwa unaona haya, huenda ikafaa kukumbuka kwamba wengine pia wanakabili hali hiyo. Kwa kweli, hata watumishi waaminifu wa Mungu kama vile Musa na Yeremia walikuwa na shaka kuhusu uwezo wao wa kusema mbele ya watu. (Kut. 4:10; Yer. 1:6) Lakini, Yehova atakusaidia ili umtolee dhabihu za sifa kama vile alivyowasaidia watumishi hao wa zamani kumsifu mbele ya watu wote. (Soma Waebrania 13:15.) Yehova anaweza kukusaidia jinsi gani kushinda woga wa kutoa maelezo? Kwanza, tayarisha mikutano vizuri. Kisha, kabla ya kwenda kwenye Jumba la Ufalme, sali kwa Yehova na umwombe waziwazi akupe ujasiri wa kutoa maelezo. (Flp. 4:6) Unaomba jambo ambalo ‘linalingana na mapenzi yake,’ hivyo, unaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atajibu sala yako.—1 Yoh. 5:14; Met. 15:29.

Mikutano Ambayo Inakusudiwa ‘Kujenga, Kutia Moyo, na Kufariji’

13. (a) Mikutano yetu inapaswa kuwa na matokeo gani kwa wale wanaohudhuria? (b) Ni swali gani ambalo ni muhimu sana kwa wazee?

13 Paulo anasema kwamba kusudi la maana la mikutano ya kutaniko ni ‘kuwajenga, kuwatia moyo, na kuwafariji’ wale wanaohudhuria. * (1 Kor. 14:3) Wazee Wakristo leo wanaweza kufanya nini ili kuhakikisha kwamba sehemu zao za mikutano zinawatia moyo kikweli akina ndugu na dada na kuwafariji? Ili kujibu swali hilo, acheni tuchunguze mkutano ambao Yesu aliongoza muda mfupi baada ya kufufuliwa.

14. (a) Ni mambo gani yaliyotukia kabla ya mkutano ambao ulipangwa na Yesu? (b) Kwa nini ni wazi kwamba mitume walifarijiwa ‘Yesu alipokaribia na kusema nao’?

14 Kwanza, angalia mambo ambayo yalitukia kabla ya mkutano huo. Kabla tu ya Yesu kuuawa, mitume ‘walimwacha na kukimbia,’ na kama ilivyotabiriwa, ‘walitawanyika na kwenda kila mmoja kwenye nyumba yake.’ (Marko 14:50; Yoh. 16:32) Kisha, baada ya Yesu kufufuliwa, aliwaalika mitume wake walioshuka moyo wahudhurie mkutano wa pekee. * Basi, “wale wanafunzi kumi na mmoja wakaingia Galilaya mpaka kwenye mlima ambako Yesu alikuwa amewafanyia mpango.” Walipofika, ‘Yesu alikaribia na kusema nao.’ (Mt. 28:10, 16, 18) Wazia jinsi mitume walivyofarijiwa wakati Yesu alipochukua hatua hiyo! Yesu alizungumzia mambo gani?

15. (a) Yesu alizungumzia mambo gani, lakini hakuzungumza kuhusu nini? (b) Mkutano huo ulikuwa na matokeo gani kwa mitume?

15 Yesu alianza kwa kutangaza hivi: “Nimepewa mamlaka yote.” Kisha, akawapa mgawo: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi.” Mwishowe, akawahakikishia hivi kwa upendo: “Mimi nipo pamoja nanyi siku zote.” (Mt. 28:18-20) Lakini je, uliona jambo ambalo Yesu hakufanya? Hakuwakemea mitume wake; wala hakutumia mkutano huo kutilia shaka nia yao au kuwafanya wahisi kwamba wana hatia zaidi kwa kutaja udhaifu wa imani ambao walionyesha kwa muda mfupi. Badala yake, Yesu aliwahakikishia tena upendo wake na wa Baba yake kwa kuwapa mgawo mzito. Njia ambayo Yesu alitumia ilikuwa na matokeo gani kwa mitume? Walijengwa, walitiwa moyo, na kufarijiwa sana hivi kwamba muda mfupi baada ya mkutano huo, walianza tena “kufundisha na kutangaza habari njema.”—Mdo. 5:42.

16. Wazee Wakristo leo wanaiga mfano wa Yesu jinsi gani wanapoongoza mikutano ambayo ni chanzo cha burudisho?

16 Leo, wazee wanamwiga Yesu kwa kuona mikutano kuwa nafasi za kuwahakikishia waamini wenzao kwamba Yehova ana upendo wa kudumu kuelekea watu wake. (Rom. 8:38, 39) Hivyo, wanaposhughulikia sehemu zao katika mikutano, wazee wanakazia sifa nzuri za ndugu zao, bali si udhaifu wao. Hawatilii shaka nia ya ndugu zao. Badala yake, maneno yao yanaonyesha wazi kwamba wanawaona waamini wenzao kuwa watu mmoja-mmoja ambao wanampenda Yehova na wanaotaka kufanya mambo yaliyo sawa. (1 The. 4:1, 9-12) Bila shaka, nyakati nyingine huenda wazee wakahitaji kutoa mashauri ya kulirekebisha kutaniko kwa ujumla, lakini ikiwa ni watu wachache tu wanaohitaji kurekebishwa, kwa kawaida ni vizuri kuzungumza faraghani na wale wanaohusika na kuwapa mashauri hayo. (Gal. 6:1; 2 Tim. 2:24-26) Wazee wanapotoa hotuba mbele ya kutaniko lote, kusudi lao ni kutoa pongezi wakati wowote inapofaa kufanya hivyo. (Isa. 32:2) Wanajitahidi kuzungumza kwa njia ambayo inawafanya wote waliohudhuria wahisi kwamba wameburudishwa na kutiwa nguvu baada ya mkutano.—Mt. 11:28; Mdo. 15:32.

Mahali Salama

17. (a) Kwa nini ni muhimu zaidi leo kuliko wakati mwingine wowote kwa mikutano yetu kuwa mahali salama? (b) Wewe binafsi unaweza kufanya nini ili mikutano iwe yenye kujenga? (Ona sanduku “Njia Kumi za Kufanya Mikutano Ikujenge na Kuwajenga Wengine.”)

17 Ulimwengu wa Shetani unapoendelea kuwakandamiza watu zaidi na zaidi, tunahitaji kuhakikisha kwamba mikutano yetu ya Kikristo ni mahali salama—chanzo cha faraja kwa wote. (1 The. 5:11) Dada mmoja ambaye alivumilia jaribu kali sana pamoja na mume wake miaka mingi iliyopita anakumbuka hivi: “Nilipokuwa kwenye Jumba la Ufalme nilihisi ni kana kwamba nilikuwa nimebebwa na mikono ya upendo ya Yehova. Muda wote tulipokuwa huko, tukiwa tumezungukwa na ndugu na dada zetu Wakristo, tulihisi kwamba tuliweza kumtupia Yehova mzigo wetu, na kwa kadiri fulani tulipata utulivu wa moyoni.” (Zab. 55:22) Acheni watu wote wanaohudhuria mikutano yetu wahisi kwamba wametiwa moyo na kufarijiwa vivyo hivyo. Ili kuhakikisha kwamba itakuwa hivyo, na tuendelee kutimiza sehemu yetu katika kufanya mikutano ya Kikristo iwe yenye kujenga.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 1 Ilitabiriwa kwamba mambo fulani yaliyofanywa kwenye mikutano ya Kikristo katika karne ya kwanza yangekoma. Kwa mfano, ‘hatusemi tena kwa lugha’ au ‘kutoa unabii.’ (1 Kor. 13:8; 14:5) Hata hivyo, maagizo ya Paulo yanatusaidia kuelewa jinsi mikutano ya Kikristo inavyopaswa kuongozwa leo.

^ fu. 11 Unaweza kupata mapendekezo kuhusu kuboresha maelezo yako kwenye mikutano katika gazeti la Mnara wa Mlinzi, la Septemba 1, 2003 (1/9/2003), ukurasa wa 19-22.

^ fu. 13 Kamusi moja (Vine’s Expository Dictionary of Old and New Testament Words) ikieleza tofauti kati ya maneno “tia moyo” na neno “fariji,” inasema kwamba neno la Kigiriki ambalo limetafsiriwa “fariji” linamaanisha “wororo wa hali ya juu zaidi kuliko [kutia moyo].”—Linganisha na Yohana 11:19.

^ fu. 14 Huenda hiyo ndiyo pindi ambayo Paulo alitaja baadaye aliposema kwamba Yesu “aliwatokea ndugu zaidi ya mia tano.”—1 Kor. 15:6.

Ungesema Nini?

• Mikutano ya Kikristo ni ya maana kadiri gani?

• Kwa nini maelezo yanayotolewa kwenye mikutano yanasaidia “kulijenga kutaniko”?

• Tunajifunza nini kutokana na mkutano ambao Yesu aliongoza akiwa na wafuasi wake?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 22, 23]

NJIA KUMI ZA KUFANYA MIKUTANO IKUJENGE NA KUWAJENGA WENGINE

Tayarisha mapema. Unapojifunza mapema habari ambazo zitazungumziwa kwenye Jumba la Ufalme, utafurahia zaidi mikutano na itakugusa moyo zaidi.

Hudhuria kwa ukawaida. Unawatia wengine moyo unapohudhuria mikutano, kwa kuwa kila mtu anatiwa moyo zaidi wengi wanapohudhuria.

Fika kwa wakati. Ukiketi kabla ya programu kuanza, unaweza kushiriki katika wimbo na sala ya kufungua, mambo ambayo ni sehemu ya ibada yetu kwa Yehova.

Beba vifaa vyote. Beba Biblia yako na kichapo au vichapo vinavyotumiwa katika mikutano ili uweze kufuata na kuelewa vizuri zaidi mambo yanayozungumziwa.

Epuka mambo yanayokengeusha fikira. Kwa mfano, soma ujumbe kwenye simu ya mkononi baadaye, si wakati, wa mikutano. Ukifanya hivyo, unaweka mambo yako ya kibinafsi mahali panapofaa.

Shiriki. Watu wengi zaidi wanapotoa maelezo, wengi wanatiwa moyo na kujengwa na maelezo mbalimbali ya imani.

Toa maelezo mafupi. Kufanya hivyo kunawapa watu wengi iwezekanavyo nafasi ya kushiriki katika kutoa maelezo.

Timiza migawo yako. Ikiwa wewe ni mwanafunzi katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi au una sehemu katika Mkutano wa Utumishi, tayarisha vizuri, fanya mazoezi mapema, na ujitahidi kabisa kutokosa mgawo wako.

Wapongeze washiriki. Waambie wale ambao wana mgawo katika mkutano au wale wanaotoa maelezo kwamba jitihada zao zinathaminiwa sana.

Zungumza na wengine. Salamu zenye fadhili na mazungumzo yenye kujenga kabla na baada ya mikutano yanachangia sana furaha na baraka ambazo tunapata tunapohudhuria.