Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wewe Ni wa Kwanza Katika Kuwaheshimu Waamini Wenzako?

Je, Wewe Ni wa Kwanza Katika Kuwaheshimu Waamini Wenzako?

Je, Wewe Ni wa Kwanza Katika Kuwaheshimu Waamini Wenzako?

“Katika upendo wa kindugu iweni na upendo mwororo kwa mtu na mwenzake. Katika kuonyeshana heshima iweni wa kwanza.”—ROM. 12:10.

1, 2. (a) Ni shauri gani ambalo Paulo anatoa katika barua yake kwa Waroma? (b) Ni maswali au maulizo gani ambayo tutachunguza?

KATIKA barua yake kwa Waroma, mtume Paulo anakazia umuhimu wa kuonyesha upendo katika kutaniko tukiwa Wakristo. Anatukumbusha kwamba upendo wetu unapaswa kuwa “bila unafiki.” Anataja pia “upendo wa kindugu” na anasema kwamba upendo huo unapaswa kuonyeshwa kwa ‘wororo.’—Rom. 12:9, 10a.

2 Bila shaka, kuwa na upendo wa kindugu kunatia ndani mengi zaidi ya kuwa tu na hisia zenye shauku kuelekea wengine. Hisia hizo zinahitaji kuonyeshwa kwa matendo. Kwa kweli, hakuna mtu ambaye atajua kwamba tuna hisia hizo za upendo kuelekea wengine tusipozionyesha kwa njia fulani. Kwa hiyo, Paulo anaongeza shauri hili: “Katika kuonyeshana heshima iweni wa kwanza.” (Rom. 12:10b) Ni mambo gani yanayohusika katika kuonyesha heshima? Kwa nini ni jambo la maana kuwa wa kwanza katika kuwaonyesha heshima waamini wenzetu? Tunaweza kufanya hivyo jinsi gani?

Staha na Heshima

3. Neno “heshima” linamaanisha nini katika lugha za zamani za Biblia?

3 Neno la msingi la Kiebrania linalotafsiriwa kuwa “heshima” linamaanisha kihalisi “uzito.” Mtu ambaye anaheshimiwa anaonwa kuwa mzito au wa maana sana. Mara nyingi, neno hilohilo la Kiebrania linatafsiriwa pia katika Maandiko kuwa “utukufu,” neno ambalo linaonyesha zaidi heshima ya juu ambayo mtu mwenye kuheshimiwa anaonyeshwa. (Mwa. 45:13) Neno la Kigiriki linalotafsiriwa kuwa “heshima” katika Biblia linamaanisha kustahi, kuthamini, kuona kuwa -enye thamani. (Luka 14:10) Ndiyo, watu ambao tunawaheshimu ni wenye thamani sana kwetu.

4, 5. Kuonyesha heshima na kuwa mwenye staha kunahusiana jinsi gani? Toa mfano.

4 Kuwaheshimu wengine kunahusisha nini? Kunaanza na kuwastahi. Kwa kweli, maneno “heshima” na “staha” mara nyingi yanatumiwa pamoja kwa sababu yanahusiana sana. Kuonyesha heshima kunamaanisha kuonyesha staha kwa nje au waziwazi. Kwa maneno mengine, staha inahusiana hasa na jinsi tunavyomwona ndugu yetu lakini heshima inahusiana na jinsi tunavyomtendea ndugu yetu.

5 Mkristo anaweza jinsi gani kuwaonyesha waamini wenzake heshima ya kweli ikiwa hawastahi kutoka moyoni? (3 Yoh. 9, 10) Kama vile tu mmea unavyoweza kusitawi na kudumu ikiwa tu umetia mizizi ndani ya udongo mzuri, ndivyo heshima inavyoweza kuwa ya kweli na yenye kudumu ikiwa tu imetia mizizi ndani ya staha inayotoka moyoni. Kwa kuwa heshima ya unafiki haitokani na staha ya kweli, baada ya muda heshima hiyo itatoweka. Kwa hiyo, haishangazi kwamba kabla ya Paulo kutoa shauri lake kuhusu kuonyesha heshima alisema maneno haya ya waziwazi: “Upendo wenu na uwe bila unafiki.”—Rom. 12:9; soma 1 Petro 1:22.

Waheshimu Wale Walioumbwa “kwa Mfano wa Mungu”

6, 7. Kwa nini tunapaswa kuwaheshimu wengine?

6 Kwa kuwa staha inayotoka moyoni ndio ufunguo wa kuwaonyesha wengine heshima, hatupaswi kamwe kusahau kwa nini Maandiko yanatutia moyo tuwastahi ndugu zetu wote. Kwa hiyo, acheni tuchunguze sababu mbili.

7 Tofauti na viumbe wengine duniani, wanadamu waliumbwa “kwa mfano wa Mungu.” (Yak. 3:9) Kwa hiyo, tuna sifa za kimungu kama vile upendo, hekima, na haki. Ona jambo lingine ambalo tulipokea kutoka kwa Muumba wetu. Mtunga-zaburi anasema hivi: “Ee Yehova . . . , wewe ambaye utukufu wako unasimuliwa juu ya mbingu! . . . Pia ulimfanya [mwanadamu] mdogo kidogo kuliko wale walio kama Mungu, kisha ulimvika taji la utukufu na fahari [“heshima,” Union Version].” (Zab. 8:1, 4, 5; 104:1) * Kwa ujumla, Mungu amewavika wanadamu taji, au kuwapamba heshima na utukufu kwa kadiri fulani. Hivyo, tunapomheshimu mtu mwingine, kwa kweli, tunamtambua Yehova ambaye ndiye Chanzo cha heshima ambayo wanadamu wanayo. Sasa, ikiwa tuna sababu nzuri za kuwaheshimu wanadamu kwa ujumla, je, hatupaswi hata zaidi kuwaheshimu waamini wenzetu!—Yoh. 3:16; Gal. 6:10.

Washiriki wa Familia Moja

8, 9. Paulo anataja sababu gani inayopaswa kutufanya tuwaheshimu waamini wenzetu?

8 Paulo anataja sababu nyingine inayoonyesha kwa nini tunapaswa kuonyeshana heshima. Kabla tu ya kutoa himizo la kuwaonyesha wengine heshima, anasema hivi: “Katika upendo wa kindugu iweni na upendo mwororo kwa mtu na mwenzake.” Neno la Kigiriki linalotafsiriwa kuwa “upendo mwororo” linamaanisha kifungo chenye nguvu ambacho kinaunganisha familia yenye upendo na yenye kutegemezana. Hivyo, kwa kutumia maneno hayo, Paulo anakazia kwamba mahusiano katika kutaniko yanapaswa kuwa yenye nguvu na yenye shauku kama ilivyo katika familia yenye umoja. (Rom. 12:5) Zaidi ya hayo, kumbuka kwamba Paulo aliwaandikia maneno hayo Wakristo watiwa-mafuta, ambao wote walikuwa wamefanywa kuwa watoto na Baba yuleyule, Yehova. Hivyo, katika maana pana zaidi, walikuwa familia yenye umoja. Kwa hiyo, Wakristo watiwa-mafuta katika siku za Paulo kwa kweli walikuwa na sababu yenye nguvu ya kuonyeshana heshima. Hivyo ndivyo ilivyo pia kwa watiwa-mafuta leo.

9 Namna gani wale ambao ni “kondoo wengine”? (Yoh. 10:16) Ingawa kondoo wengine hawajafanywa kuwa watoto wa Mungu, wanaweza kwa kufaa kuitana ndugu na dada kwa sababu wao ni familia moja ya Kikristo ya ulimwenguni pote yenye umoja. (1 Pet. 2:17; 5:9) Kwa hiyo, ikiwa washiriki wa kondoo wengine wanathamini kabisa yale ambayo wanasema wanapotumia maneno “ndugu” au “dada,” basi wao pia wana sababu yenye nguvu ya kuwaheshimu kutoka moyoni waamini wenzao.—Soma 1 Petro 3:8.

Kwa Nini Ni Jambo la Maana Sana Kuheshimiana?

10, 11. Kwa nini ni jambo la maana sana kuwastahi na kuwaonyesha wengine heshima?

10 Kwa nini ni jambo la maana sana kuwastahi na kuwaonyesha wengine heshima? Sababu ni hii: Kwa kuwaonyesha ndugu na dada zetu heshima, tunasaidia sana kutaniko lote kuwa na umoja na hali njema.

11 Bila shaka, tukiwa Wakristo wa kweli tunatambua kwamba kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova na kupata msaada wa roho yake ndivyo vyanzo vikuu zaidi vinavyotutia nguvu. (Zab. 36:7; Yoh. 14:26) Wakati huohuo, tunatiwa moyo waamini wenzetu wanapoonyesha kwamba wanatuthamini. (Met. 25:11) Tunatiwa nguvu mtu fulani anaposema au kufanya jambo linaloonyesha kwamba anatuthamini na kutuheshimu kutoka moyoni. Hilo linatupatia nguvu zaidi za kuazimia kuendelea kutembea kwa shangwe kwenye barabara ya uzima. Bila shaka, wewe pia umewahi kuhisi hivyo.

12. Kila mmoja wetu anaweza kuchangia jinsi gani hali ya shauku na upendo katika kutaniko?

12 Sasa, kwa kuwa Yehova anajua kwamba tulizaliwa tukiwa na uhitaji wa kuheshimiwa, kupitia Neno lake anatuhimiza kwa kufaa ‘tuwe wenye bidii katika kuonyeshana heshima.’ (Rom. 12:10; Today’s English Version; soma Mathayo 7:12.) Wakristo wote ambao wanachukua kwa uzito shauri hilo lisilobadilika wanachangia hali yenye shauku na upendo katika undugu wa Kikristo. Kwa hiyo, tunapaswa kutua na kujiuliza, ‘Ni wakati gani nilipomwonyesha mara ya mwisho ndugu au dada fulani katika kutaniko heshima kwa maneno na matendo kutoka moyoni?’—Rom. 13:8.

Ni Daraka la Kila Mmoja Kuonyesha Heshima

13. (a) Ni nani wanaopaswa kuwa wa kwanza katika kuwaonyesha wengine heshima? (b) Maneno ya Paulo katika Waroma 1:7 yanaonyesha nini?

13 Ni nani wanaopaswa kuwa wa kwanza katika kuonyesha heshima? Katika barua yake kwa Waebrania, Paulo anawaita wazee Wakristo “wale wanaoongoza katikati yenu.” (Ebr. 13:17) Ni kweli kwamba wazee wanaongoza katika utendaji mwingi. Hata hivyo, wakiwa wachungaji wa kundi, bila shaka wanahitaji kuongoza katika kuwaheshimu waamini wenzao, kutia ndani wazee wenzao. Kwa mfano, wazee wanapokutana ili kuzungumzia mahitaji ya kiroho ya kutaniko, wanaheshimiana kwa kusikiliza kwa makini maelezo yanayotolewa na wazee wenzao. Zaidi ya hayo, wanaonyesha heshima kwa kufikiria maoni na maelezo ya wazee wote wakati wanapofanya maamuzi. (Mdo. 15:6-15) Hata hivyo, tunapaswa kukumbuka kwamba barua ya Paulo kwa Waroma haikuelekezwa kwa wazee tu bali pia kwa kutaniko lote. (Rom. 1:7) Hivyo, kwa kuongezea, himizo la kuwa wa kwanza katika kuwaonyesha wengine heshima linatuhusu sisi sote leo.

14. (a) Eleza tofauti kati ya kuonyesha heshima na kuwa wa kwanza katika kuwaonyesha wengine heshima. (b) Tunaweza kujiuliza swali gani?

14 Ona pia jambo hili katika shauri hilo la Paulo. Hakuwahimiza tu waamini wenzake huko Roma wawaonyeshe wengine heshima bali aliwahimiza wawe wa kwanza katika kuonyesha heshima. Kuna tofauti gani? Fikiria mfano huu. Je, mwalimu angehimiza kikundi cha wanafunzi wanaojua kusoma na kuandika wajifunze kusoma? Hapana. Tayari wanajua kusoma. Badala yake, mwalimu angetaka kuwasaidia wanafunzi wajue kusoma vizuri zaidi. Vivyo hivyo, kuwa na sifa ya upendo kati yetu, ambayo inawatambulisha Wakristo wa kweli, kunatuchochea kuwaonyesha wengine heshima. (Yoh. 13:35) Hata hivyo, kama vile tu wanafunzi wanaojua kusoma na kuandika wanavyoweza kufanya maendeleo zaidi kwa kuboresha uwezo wao wa kusoma, ndivyo tunavyoweza kufanya maendeleo zaidi kwa kuwa wa kwanza katika kuwaonyesha wengine heshima. (1 The. 4:9, 10) Kila mmoja wetu amepewa daraka la kuwa wa kwanza katika kuwaonyesha wengine heshima. Tunaweza kujiuliza, ‘Je, ninafanya hivyo kwa kuwa wa kwanza kuwaheshimu wengine katika kutaniko?’

Waheshimu “Watu wa Hali ya Chini”

15, 16. (a) Tunapowaonyesha wengine heshima, ni nani ambao hatupaswi kuwapuuza, na kwa nini? (b) Ni nini kinachoweza kufunua kwamba tunawaheshimu kutoka moyoni ndugu na dada zetu wote?

15 Tunapoonyesha heshima, ni nani ambao hatupaswi kuwapuuza katika kutaniko? Neno la Mungu linasema hivi: “Anayemwonyesha kibali mtu wa hali ya chini anamkopesha Yehova, na Yeye atamlipa matendo yake.” (Met. 19:17) Kanuni inayopatikana katika maneno hayo inapaswa kuwa na uvutano gani juu yetu tunapojitahidi kuwa wa kwanza katika kuwaonyesha wengine heshima?

16 Utakubali kwamba watu wengi wanawaonyesha wakubwa wao heshima, lakini watu haohao huenda wakawatendea kwa njia isiyo ya heshima sana au bila heshima watu ambao wanawaona kuwa wako chini yao. Hata hivyo, Yehova hafanyi hivyo. Anasema hivi: “Wale wanaoniheshimu nitawaheshimu.” (1 Sam. 2:30; Zab. 113:5-7) Yehova anawaonyesha heshima wote ambao wanamtumikia na kumheshimu. Hawapuuzi “watu wa hali ya chini.” (Soma Isaya 57:15; 2 Nya. 16:9) Bila shaka, tungependa kumwiga Yehova. Kwa hiyo, kama tunataka kujua ikiwa tunawaonyesha wengine heshima ya kweli, tunapaswa kujiuliza hivi: ‘Ninawatendea jinsi gani watu ambao si mashuhuri, au hawana madaraka katika kutaniko?’ (Yoh. 13:14, 15) Jibu la swali hilo linafunua ni kwa kadiri gani tunawaheshimu wengine kutoka moyoni.—Soma Wafilipi 2:3, 4.

Kuonyesha Heshima kwa Kutumia Wakati Wetu

17. Ni katika njia gani kubwa tunaweza kuwa wa kwanza katika kuwaonyesha wengine heshima, na kwa nini ndivyo ilivyo?

17 Ni katika njia gani kubwa tunaweza kuwa wa kwanza katika kuwaonyesha wote heshima kutanikoni? Kwa kutumia wakati wetu kwa ajili ya wengine. Kwa nini ndivyo ilivyo? Tukiwa Wakristo, tuna maisha yenye shughuli nyingi, na tunatumia wakati wetu mwingi kutimiza utendaji wetu mbalimbali wa maana katika kutaniko. Kwa hiyo, haishangazi kwamba tunaona wakati kuwa wenye thamani. Pia, tunatambua kwamba hatupaswi kudai ndugu na dada zetu watumie wakati wao mwingi kupita kiasi ili kutushughulikia. Vivyo hivyo, tunathamini wakati wengine katika kutaniko wanapoelewa kwamba hawapaswi kudai tutumie wakati wetu mwingi sana kuwashughulikia.

18. Kama inavyoonyeshwa na picha kwenye ukurasa wa 18, tunaweza kuonyesha jinsi gani kwamba tuko tayari kutumia wakati fulani kwa ajili ya waamini wenzetu?

18 Hata hivyo, tunatambua pia (hasa wale ambao ni wachungaji katika kutaniko) kwamba kuwa tayari kuacha kazi zetu ili tutumie wakati fulani kuwashughulikia waamini wenzetu kunaonyesha kwamba tunawaheshimu. Katika njia gani? Unapoacha kazi zako ili kutumia wakati fulani kwa ajili ya ndugu zako, ni kana kwamba unawaambia, ‘Ninyi ni wenye thamani sana machoni pangu hivi kwamba ni jambo la maana zaidi kwangu kutumia wakati fulani kwa ajili yenu kuliko kuendelea na mambo ninayofanya.’ (Marko 6:30-34) Kinyume cha wazo hilo pia ni kweli. Ikiwa hatuko tayari kuacha kazi zetu ili kutumia wakati fulani kwa ajili ya ndugu yetu, tunaweza kumfanya ahisi kwamba hana thamani kubwa kwetu. Bila shaka, ni jambo linaloeleweka kwamba nyakati nyingine hatuwezi kukatiza jambo linalohitaji kufanywa haraka. Hata hivyo, kuwa tayari au kutokuwa tayari kutumia wakati fulani kwa ajili ya wengine, kunafunua mengi kuhusu kina cha heshima tuliyo nayo moyoni kuelekea ndugu na dada zetu.—1 Kor. 10:24.

Azimia Kuwa wa Kwanza Katika Kuonyesha Heshima

19. Zaidi ya kutumia wakati wetu, ni katika njia gani nyingine tunaweza kuwaonyesha heshima waamini wenzetu?

19 Kuna njia nyingine za maana ambazo tunaweza kuwaonyesha heshima waamini wenzetu. Kwa mfano, tunapotumia wakati wetu pamoja nao, tunapaswa pia kuwapa uangalifu wetu. Kwa mara nyingine tena, Yehova anatuwekea mfano. Mtunga-zaburi Daudi anasema hivi: “Macho ya Yehova yanawaelekea waadilifu, na masikio yake yanakielekea kilio chao cha kuomba msaada.” (Zab. 34:15) Tunajitahidi kumwiga Yehova kwa kuwatazama, kuwasikiliza, na kuwakazia kabisa fikira ndugu zetu, hasa wale wanaotuomba tuwasaidie. Kwa kufanya hivyo, tunawaonyesha heshima.

20. Ni vikumbusho gani kuhusu kuwaonyesha wengine heshima ambavyo tunataka kukumbuka?

20 Kama vile ambavyo tumeona, tunataka kukumbuka waziwazi kwa nini tunapaswa kuwaheshimu kutoka moyoni waamini wenzetu. Zaidi ya hayo, tunatafuta nafasi za kuwa wa kwanza katika kuwaonyesha wote heshima, kutia ndani watu wa hali ya chini. Tukichukua hatua hizo, tutatia nguvu kifungo cha upendo wa kindugu na umoja katika kutaniko. Basi, acheni sisi sote tuendelee si kuonyesha tu heshima bali hasa kuwa wa kwanza katika kuonyeshana heshima. Je, hivyo ndivyo umeazimia kufanya?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Maneno ya Daudi katika Zaburi ya 8 ni maneno ya kinabii pia, ambayo yanamhusu mwanadamu mkamilifu Yesu Kristo.—Ebr. 2:6-9.

Je, Unakumbuka?

• Kuna uhusiano gani kati ya heshima na staha?

• Tuna sababu gani za kuwaheshimu waamini wenzetu?

• Kwa nini ni jambo la maana kuonyeshana heshima?

• Tunaweza kuwaonyesha waamini wenzetu heshima katika njia gani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 18]

Tunaweza jinsi gani kuwaonyesha waamini wenzetu heshima?