Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Ni Nani Ameijua Akili ya Yehova?”

“Ni Nani Ameijua Akili ya Yehova?”

“Ni Nani Ameijua Akili ya Yehova?”

“‘Ni nani ameijua akili ya Yehova, ndipo amfundishe?’ Lakini sisi tunayo akili ya Kristo.”—1 KOR. 2:16.

1, 2. (a) Watu wengi wanakabili tatizo gani? (b) Tunahitaji kukumbuka nini kuhusu njia yetu ya kufikiri na njia ya Yehova ya kufikiri?

JE, UMEWAHI kuona kwamba ni vigumu kuelewa jinsi mtu mwingine anavyofikiri? Labda ulifunga ndoa hivi karibuni, na unahisi kwamba huwezi kuelewa kikamili jinsi mwenzi wako wa ndoa anavyofikiri. Kwa kweli, wanaume na wanawake wanafikiri na hata kuzungumza kwa njia tofauti. Na katika tamaduni fulani, wanaume na wanawake wanazungumza wakitumia matamshi tofauti ya lugha ileile! Zaidi ya hayo, watu wanaweza kufikiri na kutenda kwa njia tofauti kwa sababu ya tofauti za kitamaduni na lugha. Hata hivyo, kadiri unavyoendelea kuwafahamu watu wengine, ndivyo unavyopata nafasi zaidi za kuanza kuelewa njia yao ya kufikiri.

2 Kwa hiyo, hatupaswi kushangaa kwamba njia yetu ya kufikiri inatofautiana kabisa na njia ya Yehova ya kufikiri. Kupitia nabii wake Isaya, Yehova aliwaambia hivi Waisraeli: “Mawazo yenu si mawazo yangu, wala njia zangu si njia zenu.” Kisha, Yehova akatoa mfano ili kuonyesha jambo hilo, akisema: “Kwa maana kama vile mbingu zilivyo juu kuliko dunia, ndivyo njia zangu zilivyo juu kuliko njia zenu, na mawazo yangu kuliko mawazo yenu.”—Isa. 55:8, 9.

3. Ni njia gani mbili ambazo tunaweza kutumia ili tuwe na “urafiki wa karibu pamoja na Yehova”?

3 Lakini je, hilo linamaanisha kwamba hatupaswi hata kujaribu kuelewa njia ya Yehova ya kufikiri? Hapana. Ingawa hatuwezi kamwe kuelewa kikamili mawazo yote ya Yehova, bado Biblia inatutia moyo tutafute “urafiki wa karibu pamoja na Yehova.” (Soma Zaburi 25:14; Methali 3:32.) Njia moja ambayo tunaweza kumkaribia zaidi Yehova ni kuthamini na kuchunguza kwa makini utendaji wake mbalimbali ulioandikwa katika Neno lake, Biblia. (Zab. 28:5) Njia nyingine ni kujitahidi kujua “akili ya Kristo,” ambaye ni “mfano wa Mungu asiyeonekana.” (1 Kor. 2:16; Kol. 1:15) Tukitenga wakati wa kujifunza masimulizi ya Biblia na kuyatafakari, tunaweza kuanza kuelewa sifa mbalimbali za Yehova na njia yake ya kufikiri.

Epuka Mwelekeo Mbaya

4, 5. (a) Ni mwelekeo gani mbaya ambao tunapaswa kuepuka? Eleza. (b) Waisraeli walianza kufikiri kwa njia gani yenye makosa?

4 Tunapotafakari kuhusu utendaji mbalimbali wa Yehova, tunapaswa kuepuka mwelekeo wa kumhukumu Mungu tukitumia viwango vya wanadamu. Mwelekeo huo unaonyeshwa na maneno haya ya Yehova yaliyoandikwa katika Zaburi 50:21: “Ulidhani kwamba kwa hakika mimi ningekuwa kama wewe.” Ni kama vile msomi mmoja wa Biblia alivyosema miaka zaidi ya 175 iliyopita: “Watu wana mwelekeo wa kumhukumu Mungu wakitumia viwango vyao wenyewe, na kufikiri kwamba Mungu anaongozwa na sheria ambazo wanadamu wanapaswa kuzifuata.”

5 Tunapaswa kuwa waangalifu ili maoni yetu kumhusu Yehova yasiongozwe na viwango na tamaa zetu. Kwa nini hilo ni jambo la maana? Tunapojifunza Maandiko, huenda matendo fulani ya Yehova yakaonekana si sawa kabisa kulingana na maoni yetu yenye mipaka na yasiyo makamilifu. Waisraeli wa kale walifikiri kwa njia hiyo na wakakata kauli yenye makosa kuhusu jinsi Yehova alivyoshughulika nao. Ona jinsi Yehova alivyowaambia: “Nanyi hakika mtasema: ‘Njia ya Yehova si sawa.’ Sikia, tafadhali, Ee nyumba ya Israeli. Je, njia yangu mwenyewe si sawa? Je, njia zenu ninyi sizo ambazo si sawa?”—Eze. 18:25.

6. Ayubu alijifunza somo gani, na tunaweza kufaidika jinsi gani na mfano wake?

6 Jambo kuu ambalo linaweza kutusaidia kuepuka mtego wa kumhukumu Yehova kulingana na viwango vyetu wenyewe ni kutambua kwamba maoni yetu yana mipaka na nyakati nyingine ni yenye makosa kabisa. Ayubu alihitaji kujifunza somo hilo. Alipokuwa akiteseka, Ayubu alipambana na hisia za kuvunjika moyo na kwa njia fulani akaanza kujifikiria mwenyewe. Alisahau kwamba kuna masuala makuu zaidi. Lakini kwa upendo Yehova alimsaidia kupanua maoni yake. Kwa kumuuliza Ayubu maswali au maulizo zaidi ya 70 tofauti-tofauti, ambayo Ayubu hangeweza kujibu hata moja, Yehova alikazia kwamba uelewaji wa Ayubu ulikuwa na mipaka. Ayubu alikubali kwa unyenyekevu, na akabadili maoni yake.—Soma Ayubu 42:1-6.

Kupata “Akili ya Kristo”

7. Kwa nini kuchunguza utendaji mbalimbali wa Yesu kunatusaidia kuelewa njia ya Yehova ya kufikiri?

7 Yesu alimwiga Baba yake kikamili katika kila jambo alilosema na kutenda. (Yoh. 14:9) Kwa hiyo, kuchunguza utendaji mbalimbali wa Yesu kunatusaidia kuelewa njia ya Yehova ya kufikiri. (Rom. 15:5; Flp. 2:5) Hivyo basi, acheni tuchunguze masimulizi mawili ya Injili.

8, 9. Kama ilivyoandikwa katika Yohana 6:1-5, ni hali gani ambayo ilimfanya Yesu amuulize Filipo swali, na kwa nini Yesu alifanya hivyo?

8 Wazia tukio hili. Muda mfupi tu kabla ya Pasaka ya mwaka wa 32 W.K. Mitume wa Yesu walikuwa wamerudi baada ya safari ndefu ya kuhubiri kotekote katika Galilaya. Kwa sababu walikuwa wamechoka kutokana na utendaji huo wote, Yesu aliwapeleka mahali pasipo na watu upande wa kaskazini-mashariki kwenye ufuo wa Bahari ya Galilaya. Hata hivyo, maelfu ya watu waliwafuata huko. Baada ya Yesu kuuponya umati huo na kuwafundisha mambo mengi, tatizo fulani lilitokea. Watu hao wote wangeweza kupata jinsi gani chakula katika eneo hilo la mbali? Akitambua tatizo hilo, Yesu alimuuliza hivi Filipo, ambaye alitoka katika eneo hilo: “Tutanunua wapi mikate ili hawa wale?”—Yoh. 6:1-5.

9 Kwa nini Yesu alimuuliza Filipo swali hilo? Je, Yesu alikuwa na wasiwasi kwa sababu hakujua jambo la kufanya? Hapana. Alikuwa akifikiria nini hasa? Mtume Yohana, ambaye pia alikuwa mahali hapo, anaeleza hivi: “[Yesu] alikuwa akisema hilo ili amjaribu, kwa maana yeye mwenyewe alijua alilokuwa karibu kufanya.” (Yoh. 6:6) Hapo, Yesu alikuwa akiwajaribu wanafunzi wake ili aone maendeleo yao ya kiroho. Kwa kuuliza swali hilo, aliwafanya wamkazie fikira naye akawapa nafasi ya kuonyesha kwamba wana imani katika jambo ambalo angefanya. Lakini hawakutumia nafasi hiyo kuonyesha imani yao na hivyo wakafunua kwamba maoni yao hayakuwa yamepanuka. (Soma Yohana 6:7-9.) Kisha, Yesu akaonyesha kwamba alikuwa na uwezo wa kufanya jambo ambalo hata hawakuwa wamewazia. Aliwalisha kimuujiza maelfu ya watu hao wenye njaa.—Yoh. 6:10-13.

10-12. (a) Huenda ni kwa nini Yesu hakutimiza papo hapo ombi la yule mwanamke Mgiriki? Eleza. (b) Tutachunguza nini sasa?

10 Simulizi hilo linaweza kutusaidia kuelewa jinsi Yesu alivyokuwa akifikiri katika pindi nyingine. Muda mfupi baada ya kulisha kikundi hicho kikubwa cha watu, Yesu na mitume wake walisafiri kuelekea kaskazini, wakavuka mpaka wa Israeli na kufika karibu na Tiro na Sidoni. Wakiwa huko, walikutana na mwanamke Mgiriki ambaye alimsihi Yesu amponye binti yake. Mwanzoni, Yesu alimpuuza mwanamke huyo. Lakini mwanamke huyo alipoendelea kusisitiza, Yesu alimwambia hivi: “Kwanza acha watoto washibe, kwa maana si sawa kuuchukua mkate wa watoto na kuwatupia mbwa wadogo.”—Marko 7:24-27.

11 Kwa nini mwanzoni Yesu alikataa kumsaidia mwanamke huyo? Je, Yesu alikuwa akimjaribu, kama alivyomjaribu Filipo, ili aone jinsi ambavyo angetenda, na kumpa nafasi ya kuonyesha imani yake? Yesu hakuongea kwa sauti ambayo ingemvunja moyo mwanamke huyo, ingawa simulizi hilo halifunui jambo hilo. Kwa kutumia maneno “mbwa wadogo” alifanya mfano huo usimuumize mwanamke huyo hisia. Kwa hiyo, huenda Yesu alikuwa akitenda kama mzazi ambaye anataka kumpa mtoto kitu ambacho ameomba lakini mzazi huyo anakosa kuonyesha dalili zozote kwamba anataka kumpa ili aone kama kweli mtoto huyo anataka kitu hicho. Kwa vyovyote vile, mara tu mwanamke huyo alipoonyesha imani yake, Yesu alitimiza ombi lake kwa kupenda.—Soma Marko 7:28-30.

12 Masimulizi hayo mawili ya Injili yanatupatia ujuzi wenye thamani kuhusu “akili ya Kristo.” Acheni sasa tuone jinsi masimulizi hayo yanavyoweza kutusaidia kuelewa vizuri zaidi akili ya Yehova.

Jinsi Yehova Alivyoshughulika na Musa

13. Kuelewa njia ya Yesu ya kufikiri kunatusaidia jinsi gani?

13 Kuelewa njia ya Yesu ya kufikiri kunaweza kutusaidia kuelewa masimulizi ya Maandiko ambayo huenda ni vigumu kuyaelewa. Kwa mfano, fikiria maneno ambayo Yehova alimwambia Musa baada ya Waisraeli kutengeneza ndama wa dhahabu wa kuabudu. Mungu alisema hivi: “Nimewatazama watu hawa na, kumbe, ni watu wenye shingo ngumu. Basi sasa, niache, ili hasira yangu iwake juu yao nami niwaangamize, nami nikufanye wewe kuwa taifa kubwa.”—Kut. 32:9, 10.

14. Musa alitenda jinsi gani baada ya kusikia maneno ya Yehova?

14 Simulizi hilo linaendelea kusema hivi: “Musa akaanza kuutuliza uso wa Yehova Mungu wake na kusema: ‘Kwa nini, Ee Yehova, hasira yako iwake juu ya watu wako ambao uliwatoa katika nchi ya Misri kwa nguvu kuu na kwa mkono wenye nguvu? Kwa nini Wamisri waseme, “Aliwatoa kwa nia mbaya ili awaue katikati ya milima na kuwaangamiza kutoka katika uso wa nchi”? Geukia mbali uiache hasira yako inayowaka na ujute kuhusu uovu huo juu ya watu wako. Wakumbuke Abrahamu, Isaka na Israeli watumishi wako, uliowaapia kwa jina lako mwenyewe, kwa kuwa uliwaambia, “nitauzidisha uzao wenu kama nyota za mbinguni, nayo nchi hii yote ambayo nimeichagua, nitaupa uzao wenu, ili kwa kweli wapate kuimiliki mpaka wakati usio na kipimo.”’ Naye Yehova akaanza kujuta juu ya ule uovu aliokuwa amesema kwamba atawafanyia watu wake.”—Kut. 32:11-14. *

15, 16. (a) Ni nafasi gani ambayo Musa alipata kwa sababu ya maneno ambayo Yehova alisema? (b) Yehova ‘alianza kujuta’ katika maana gani?

15 Je, kwa kweli Musa alihitaji kurekebisha njia ya Yehova ya kufikiri? Bila shaka hapana! Ingawa Yehova alisema jambo ambalo inaelekea angefanya, huo haukuwa uamuzi wake wa mwisho. Kwa kweli, hapa Yehova alikuwa akimjaribu Musa, kama vile ambavyo baadaye Yesu alimjaribu Filipo na yule mwanamke Mgiriki. Musa alipewa nafasi ya kutoa maoni yake. * Yehova alikuwa amemchagua Musa awe mpatanishi kati Yake na Israeli, na Yehova aliheshimu uamuzi Wake wa kumweka rasmi Musa atimize daraka hilo. Je, Musa angejiacha alemewe na hisia za kukata tamaa? Je, angetumia nafasi hiyo kumhimiza Yehova asahau Israeli na kutokeza taifa lenye nguvu kutokana na wazao wa Musa mwenyewe?

16 Jibu la Musa lilionyesha kwamba alikuwa na imani na uhakika katika haki ya Yehova. Jibu lake lilionyesha kwamba hakuwa na ubinafsi, lakini alihangaikia jina la Yehova. Hakutaka jina hilo liharibiwe sifa. Hivyo basi, Musa alionyesha kwamba alielewa “akili ya Yehova” kuhusu jambo hilo. (1 Kor. 2:16) Matokeo yalikuwa nini? Kwa sababu Yehova hakuwa ameamua kabisa kuchukua hatua fulani, simulizi hilo lililoongozwa na roho ya Mungu linasema kwamba ‘alianza kujuta.’ Katika Kiebrania, maneno hayo yanaweza kumaanisha tu kwamba Yehova hakuleta msiba ambao inaelekea angeleta juu ya taifa lote.

Jinsi Yehova Alivyoshughulika na Abrahamu

17. Yehova alionyesha jinsi gani subira nyingi aliposhughulika na mambo yaliyokuwa yakimhangaisha Abrahamu?

17 Mfano mwingine unaoonyesha jinsi Yehova anavyowapa watumishi wake nafasi ya kuonyesha imani yao na kuonyesha kwamba wanamtegemea ni ombi la Abrahamu kuhusu Sodoma. Katika simulizi hilo, Yehova alionyesha subira nyingi kwa kumruhusu Abrahamu aulize maswali manane mfululizo. Katika mazungumzo hayo, Abrahamu alitoa ombi hili lenye kugusa moyo: “Ni jambo lisilowaziwa kwako kwamba unatenda namna hii kuua mtu mwadilifu pamoja na mwovu hivi kwamba mtu mwadilifu apatwe na jambo lilelile kama ilivyo kwa mwovu! Ni jambo lisilowaziwa kwako. Je, Mwamuzi wa dunia yote hatafanya lililo sawa?”—Mwa. 18:22-33.

18. Tunajifunza nini kutokana na jinsi Yehova alivyoshughulika na Abrahamu?

18 Kutokana na simulizi hilo, tunajifunza nini kuhusu njia ya Yehova ya kufikiri? Je, Yehova alihitaji kusadikishwa na Abrahamu ili afanye uamuzi unaofaa? Hapana. Bila shaka, Yehova angesema tu mwanzoni sababu za kufanya uamuzi huo. Lakini kupitia maswali hayo, Yehova alimpa Abrahamu wakati ili akubali uamuzi huo na kuelewa fikira Zake. Vilevile, hatua hiyo ilimsaidia Abrahamu kuelewa jinsi Yehova alivyo na huruma nyingi na haki. Ndiyo, Yehova alishughulika na Abrahamu kama rafiki.—Isa. 41:8; Yak. 2:23.

Mambo Tunayojifunza

19. Tunaweza kumwiga Ayubu jinsi gani?

19 Tumejifunza nini kuhusu “akili ya Yehova”? Tunapaswa kuruhusu Neno la Mungu litufinyange ili tuelewe akili ya Yehova. Hatupaswi kamwe kumwekea Yehova mipaka yetu na kumhukumu kulingana na viwango na fikira zetu. Ayubu alisema hivi: “[Mungu] si mwanadamu kama mimi ndipo nimjibu, kwamba tuje pamoja katika hukumu.” (Ayu. 9:32) Kama Ayubu, tunapoanza kuelewa akili ya Yehova, tunachochewa kusema hivi: “Tazama! Hizo ndizo kingo za njia zake, nao ni mnong’ono ulioje wa jambo lililosikiwa juu yake! Lakini kuhusu mngurumo wake wenye nguvu ni nani anayeweza kuonyesha uelewaji?”—Ayu. 26:14.

20. Tunapaswa kufanya nini tunaposoma sehemu fulani ya Maandiko ambayo ni vigumu kwetu kuelewa?

20 Tunaposoma Maandiko, tunapaswa kufanya nini tunapopata sehemu fulani ambayo ni vigumu kuelewa, hasa inayohusu jinsi Yehova anavyofikiri? Ikiwa bado hatuelewi kabisa sehemu hiyo hata baada ya kufanya utafiti, tunaweza kuona hilo kuwa jaribu la kuonyesha kwamba tunamtegemea Yehova. Kumbuka kwamba nyakati nyingine, maneno fulani katika Biblia yanatupatia nafasi ya kuonyesha imani yetu katika sifa za Yehova. Acheni tukubali kwa unyenyekevu kwamba hatuelewi kila jambo analofanya. (Mhu. 11:5) Hivyo tutachochewa kukubaliana na maneno haya ya mtume Paulo: “Lo! Jinsi kilivyo kina cha utajiri wa Mungu na hekima na ujuzi! Jinsi hukumu zake zisivyochunguzika na njia zake zisivyotafutika! Kwa maana ‘ni nani amekuja kuijua akili ya Yehova, au ni nani amekuwa mshauri wake?’ Au, ‘Ni nani amempa yeye kwanza, hivi kwamba iwe lazima arudishiwe?’ Kwa sababu vitu vyote ni kutoka kwake na kwa yeye na kwa ajili yake. Kwake yeye na kuwe na utukufu milele. Amina.”—Rom. 11:33-36.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 14 Simulizi linalofanana na hilo linapatikana katika Hesabu 14:11-20.

^ fu. 15 Wasomi fulani wanasema kwamba usemi wa mfano wa Kiebrania uliotafsiriwa “niache” katika Kutoka 32:10 unaweza kuonwa kuwa mwaliko, pendekezo la kwamba Musa aruhusiwe kuingilia kati, au ‘kusimama katika mwanya,’ uliokuwapo kati ya Yehova na taifa hilo. (Zab. 106:23; Eze. 22:30) Iwe ilikuwa hivyo au hapana, bila shaka Musa alijihisi huru kumweleza Yehova maoni yake bila woga.

Je, Unakumbuka?

• Ni nini ambacho kitatusaidia kuepuka mwelekeo wa kumhukumu Yehova kulingana na viwango vyetu wenyewe?

• Kuelewa matendo ya Yesu kunaweza kutusaidia jinsi gani kupata “urafiki wa karibu pamoja na Yehova”?

• Umejifunza mambo gani kutokana na mazungumzo kati ya Yehova na Musa na vilevile na Abrahamu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 5]

Tunajifunza nini kuhusu njia ya Yehova ya kufikiri kutokana na jinsi alivyoshughulika na Musa na pia Abrahamu?