Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nimekuwa na Mengi ya Kufanya Katika Tengenezo la Yehova

Nimekuwa na Mengi ya Kufanya Katika Tengenezo la Yehova

Nimekuwa na Mengi ya Kufanya Katika Tengenezo la Yehova

Limesimuliwa na Vernon Zubko

NILILELEWA katika shamba moja huko Stenen, kijiji kilicho katika jimbo la Saskatchewan, nchini Kanada. Wazazi wangu, Fred na Adella, walijitahidi sana kutimiza mahitaji ya kiroho na ya kimwili ya dada yangu mkubwa, Aurellia, na pia mahitaji yangu na ya ndugu na dada zangu wachanga, Alvin, Allegra, na Daryl. Mpaka leo hii, bado tunashukuru kwamba wazazi wetu walitufundisha kweli.

Baba, akiwa Mkristo mtiwa-mafuta, alikuwa mweneza-injili asiyeogopa. Alifanya kazi kwa bidii ili kupata riziki, lakini alihakikisha pia kwamba kila mtu alijua yeye ni Shahidi. Sikuzote alizungumza kuhusu kweli. Nitakumbuka sikuzote mfano wake mzuri wa bidii na ujasiri. Mara nyingi aliniambia hivi: “Uwe na mengi ya kufanya katika tengenezo la Yehova, na utaepuka matatizo mengi.”

Mara nyingi, tulihubiri barabarani huko Stenen na katika maeneo jirani. Haikuwa rahisi kwangu sikuzote kufanya hivyo. Katika kila mji kulikuwa na watoto waliotuchokoza, ambao walitufuata sisi wachanga na kutudhihaki. Wakati fulani nilipokuwa na umri wa miaka minane, nilikuwa nimesimama kwenye kona ya barabara nikiwa na magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! kikundi cha watoto kiliponizunguka. Walinyakua kofia yangu mpya kutoka kichwani na wakaiweka kwenye nguzo iliyokuwa kando yangu. Nilishukuru kwamba ndugu mmoja aliyezeeka aliyekuwa akinilinda aliona kile kilichokuwa kikitukia. Alikaribia na kuniuliza, “Vern, kuna tatizo?” Vijana hao wa kiume walitoweka haraka. Ingawa jambo hilo lilinihuzunisha kidogo, lilinifundisha kwamba unapohubiri barabarani ni vizuri kutembea-tembea badala ya kusimama mahali pamoja kama nguzo. Mazoezi hayo niliyopata nilipokuwa mtoto yalinipa pia ujasiri ambao nilihitaji ili kuhubiri nyumba kwa nyumba.

Mimi na Alvin tulibatizwa Mei (Mwezi wa 5) 1951. Nilikuwa na umri wa miaka 13. Bado ninakumbuka kwamba Ndugu Jack Nathan, ambaye alitoa hotuba ya ubatizo, alituhimiza tusiruhusu kamwe mwezi upite bila kusema kumhusu Yehova. * Katika familia yetu, utumishi wa painia ulionwa sikuzote kuwa kazi bora zaidi ya maisha. Hivyo katika mwaka wa 1958, baada ya kumaliza shule, nilihamia Winnipeg, Manitoba, ili kufanya upainia. Ingawa Baba yangu alifurahia kufanya kazi pamoja nami katika biashara yetu ya familia nikiwa mpigaji-randa, yeye na Mama walinitia moyo sana kufuatia huduma ya wakati wote na walikubali nihame kwenda kufanya upainia.

Makao Mapya na Mwenzi Mpya

Katika mwaka wa 1959, ofisi ya tawi ilitoa ombi ili mtu yeyote ambaye angeweza ahamie Quebec, ambako kulikuwa na uhitaji mkubwa wa waeneza-injili. Nilienda kufanya utumishi wa painia huko Montreal. Yalikuwa mabadiliko makubwa kama nini! Kujifunza kuzungumza Kifaransa na kuzoea utamaduni tofauti, yalikuwa mambo mapya kabisa katika maisha yangu. Mwangalizi wetu wa mzunguko aliniambia hivi: “Usiseme kamwe, ‘Hivi ndivyo tulivyofanya jambo hili nyumbani kwetu.’” Hilo lilikuwa shauri zuri.—1 Kor. 9:22, 23.

Nilipohamia Quebec sikuwa na mwenzi katika kazi ya upainia. Hata hivyo, dada mmoja kijana aliyeitwa Shirley Turcotte, ambaye nilikutana naye huko Winnipeg, alikuja kuwa mwenzi wangu wa kudumu wakati tulipooana mnamo Februari (Mwezi wa 2) 1961. Yeye pia alitoka katika familia ambayo ilimpenda Yehova. Hata hivyo, wakati huo sikutambua kikamili kwamba kwa miaka mingi angenitia nguvu na kunitia moyo sana.

Kutembelea Eneo Lote la Gaspé

Miaka miwili baada ya arusi yetu, tuliwekwa rasmi kuwa mapainia wa pekee na tukatumwa huko Rimouski, Quebec. Katika majira yaliyofuata ya kiangazi, ofisi ya tawi ilituomba tuhubiri eneo lote la Rasi ya Gaspé, kwenye pwani ya mashariki ya Kanada. Mgawo wetu ulikuwa ni kupanda mbegu nyingi za kweli kadiri iwezekanavyo. (Mhu. 11:6) Tulijaza gari letu magazeti 1,000 na vitabu 400 hivi, na pia chakula na nguo, tukaanza safari ndefu ya kuhubiri kwa muda wa mwezi mzima. Tulihubiri hatua kwa hatua katika vijiji vyote vidogo huko Gaspé. Kituo cha redio cha eneo hilo kiliwaonya watu kwamba Mashahidi wanakuja na kuwaambia wasikubali vichapo vyetu. Hata hivyo, wakaaji wengi walielewa vibaya tangazo hilo na wakaamini kwamba lilikuwa linawatia watu moyo wasome vichapo vyetu, hivyo walikubali vichapo vyetu.

Miaka hiyo, katika sehemu fulani za Quebec hatukuwa na uhuru wa kuhubiri, na lilikuwa jambo la kawaida kusimamishwa na polisi. Hilo lilitukia katika jiji moja ambako tuliwaachia watu vichapo katika karibu kila nyumba. Ofisa mmoja alituomba tumfuate kwenye kituo cha polisi, nasi tukakubali. Nikiwa huko nilipata habari kwamba mwanasheria wa jiji hilo alikuwa ametoa amri ya kutuzuia kuhubiri. Kwa kuwa mkuu wa polisi hakuwepo siku hiyo, nilimpa mwanasheria huyo barua ndefu kutoka kwenye ofisi ya tawi ya Toronto ambayo ilieleza kuhusu haki yetu ya kuhubiri. Baada ya kusoma barua hiyo, mwanasheria huyo akasema hivi haraka-haraka: “Tazama, sitaki shida yoyote. Kasisi wa parokia ndiye aliyeniambia niwazuie.” Kwa kuwa tulitaka watu wa eneo hilo watambue kwamba kazi yetu ni halali, papo hapo tulirudi katika eneo ambalo tulikuwa tumesimamishwa na polisi na kuanza tena kuhubiri.

Asubuhi iliyofuata wakati tuliporudi kumwona mkuu wa polisi, alikasirika kusikia kwamba tulizuiwa kuhubiri. Alimkasirikia sana mwanasheria huyo kwenye simu! Mkuu huyo wa polisi alituambia kwamba ikiwa tungepata shida yoyote, tungeweza kumpigia simu moja kwa moja ili atatue shida hiyo. Hata ingawa tulikuwa wageni na hatukujua Kifaransa sana, tuliona kwamba watu walikuwa wenye fadhili na wakaribishaji. Lakini tulijiuliza, ‘Je, watawahi kujua kweli?’ Tulipata jibu miaka mingi baadaye tuliporudi kujenga Majumba ya Ufalme katika eneo lote la Gaspé. Tuligundua kwamba watu wengi ambao tulihubiria sasa ni ndugu zetu. Kwa kweli, Yehova ndiye anayekuza mbegu ya kweli.—1 Kor. 3:6, 7.

Tunapata Urithi

Binti yetu Lisa alizaliwa mwaka wa 1970. Urithi huo kutoka kwa Yehova uliongeza zaidi shangwe yetu maishani. Shirley na Lisa walifanya kazi pamoja nami katika miradi mingi ya ujenzi wa Majumba ya Ufalme. Baada ya Lisa kumaliza shule, alisema hivi: “Mama na Baba, kwa kuwa niliwaondoa kwa muda katika utumishi wa wakati wote, nitajaribu kujazia nafasi hiyo kwa kuwa painia.” Zaidi ya miaka 20 baadaye, Lisa bado anatumika akiwa painia, lakini sasa anatumika pamoja na mume wake, Sylvain. Wakiwa pamoja, wamekuwa na pendeleo la kufanya kazi katika miradi mingi ya ujenzi ulimwenguni. Mradi wetu tukiwa familia ni kuendelea kuwa na maisha rahisi na kujitoa kwa ajili ya utumishi wa Yehova. Sijawahi kamwe kusahau maneno ambayo Lisa alisema alipoanza utumishi wa painia. Kwa kweli, alinichochea kurudi tena katika utumishi wa wakati wote katika mwaka wa 2001, na tangu wakati huo mimi ni painia. Kufanya upainia kunaendelea kunifundisha kumtegemea Yehova katika kila jambo na kuishi maisha rahisi lakini yenye kuridhisha na yenye furaha.

Miradi ya Ujenzi Inahitaji Upendo, Ushikamanifu, na Uaminifu

Yehova amenifundisha kwamba tukijitoa na kukubali mgawo wowote ule ambao anatupatia, tunavuna baraka nyingi. Kutumikia katika Halmashauri ya Ujenzi ya Mkoa na kufanya kazi katika miradi ya ujenzi pamoja na ndugu na dada zangu katika eneo lote la Quebec na kwingineko ni pendeleo lenye thamani sana.

Ingawa wajitoleaji wengine huenda wasiwe wasemaji wazuri kwenye jukwaa, wanang’aa kama nyota katika miradi ya ujenzi wa Majumba ya Ufalme. Wapendwa hao wanajitoa kwa moyo wao wote katika kazi, na vipawa au uwezo wao unaonekana waziwazi. Matokeo ni kwamba sikuzote wanajenga jengo maridadi ambalo linatumiwa katika ibada ya Yehova.

Nimekuwa nikiulizwa, “Ni sifa gani za maana zaidi ambazo mjitoleaji kwenye mradi wa ujenzi wa Jumba la Ufalme anapaswa kuwa nazo?” Kutokana na uzoefu wangu, nimeona kwamba mtu anapaswa kwanza kabisa kumpenda Yehova, Mwana wake, na pia ndugu na dada. (1 Kor. 16:14) Pili, anahitaji sifa ya ushikamanifu na uaminifu. Mambo yasipofanyika kwa njia ambayo tunataka, na hilo litatokea, mtu mshikamanifu ataendelea kuunga mkono mpango wa kitheokrasi. Uaminifu utamchochea kujitolea kwa ajili ya miradi mingine ya wakati ujao.

Ninamshukuru Yehova

Ingawa baba yangu alikufa mwaka wa 1985, bado ninakumbuka shauri ambalo alinipa la kuendelea kuwa na mengi ya kufanya katika tengenezo la Yehova. Kama watiwa-mafuta wengine ambao tayari wamepokea migawo yao katika sehemu ya kimbingu ya tengenezo la Yehova, bila shaka yeye pia ana mengi ya kufanya huko. (Ufu. 14:13) Sasa Mama ana umri wa miaka 97. Kwa sababu ya ugonjwa wa kupooza au kiharusi, hawezi kuzungumza kama zamani; lakini bado anaijua Biblia yake. Ananukuu maandiko katika barua zake na anatutia moyo kuendelea kumtumikia Yehova kwa uaminifu. Sisi watoto wote tunashukuru kama nini kwa sababu ya kuwa na wazazi kama hao wenye upendo!

Ninamshukuru pia Yehova kwa sababu ya Shirley, mke na mwenzi wangu mwaminifu. Bado ameweka moyoni mwake shauri ambalo mama yake alimpa, “Vern atakuwa na mengi ya kufanya katika kweli, na utahitaji kujifunza kumwacha awasaidie wengine.” Tulipofunga ndoa miaka 49 iliyopita, tuliazimia kwamba tutazeeka pamoja, tukimtumikia Yehova, na ikiwa tutaokoka pamoja mwisho wa mfumo huu, tutarudi tena kuwa vijana pamoja na kuendelea kumtumikia milele. Ndiyo, tumekuwa na “mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.” (1 Kor. 15:58) Yehova kwa upande wake ametutunza kikweli na amehakikisha kwamba hatujakosa kamwe kitu chochote kilicho kizuri.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Ona gazeti la Mnara wa Mlinzi, la Septemba 1, 1990, ukurasa wa 10-14, kuhusu simulizi la maisha la Jack Halliday Nathan.

[Picha katika ukurasa wa 31]

“Mradi wetu tukiwa familia ni kuendelea kuwa na maisha rahisi na kujitoa kwa ajili ya utumishi wa Yehova”