Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wasaidie Watoto Waelewe Tengenezo la Yehova

Wasaidie Watoto Waelewe Tengenezo la Yehova

Wasaidie Watoto Waelewe Tengenezo la Yehova

WATOTO wanataka kujifunza. Fikiria maswali au maulizo ambayo huenda watoto Waisraeli waliuliza huko Misri usiku wa sherehe ya kwanza ya Pasaka: ‘Kwa nini ilikuwa lazima mwana-kondoo achinjwe?’ ‘Kwa nini Baba anapaka damu juu ya mlango?’ ‘Tunaenda wapi?’ Amri ambayo Yehova aliwapa akina baba Waisraeli ilionyesha wazi kwamba Yehova alitazamia watoto waulize maswali kama hayo. Yehova aliwaambia hivi kuhusu maadhimisho ya wakati ujao ya Pasaka: “Wana wenu watakapowaambia, ‘Utumishi huu unamaanisha nini kwenu?’ ndipo mtakaposema, ‘Ni dhabihu ya pasaka kwa Yehova, aliyepita juu ya nyumba za wana wa Israeli huko Misri alipowaletea Wamisri pigo, lakini akazikomboa nyumba zetu.’” (Kut. 12:24-27) Baadaye, Yehova aliwakumbusha wazazi Waisraeli kwamba ni jambo la maana kujibu maswali ya watoto wao kuhusu “masharti na maamuzi ya hukumu” ambayo Yehova alikuwa amewaamuru washike.—Kum. 6:20-25.

Ni wazi kwamba Yehova alitaka watoto wapate majibu yanayoridhisha ya maswali yao kuhusu ibada ya kweli—majibu ambayo yangewachochea kumpenda Yehova akiwa Mungu wao na Mwokozi wao. Leo, Yehova anatamani kuona vijana wetu wakifanya vivyo hivyo. Njia moja ambayo wazazi wanaweza kuwafundisha watoto wao kumpenda Mungu kutoka moyoni na kuwapenda watu wake ni kuwasaidia kuelewa tengenezo la Yehova na kuelewa jinsi mipango ya tengenezo inavyowanufaisha. Kwa hiyo, acheni tuzungumzie njia fulani za kuwasaidia watoto wajifunze mambo mengi zaidi kuhusu tengenezo la Mungu.

Kutaniko Lenu

Watoto wanahitaji kujua vizuri kutaniko ambalo familia yenu inashirikiana nalo. Ili kutimiza jambo hilo, mkiwa wazazi mnahitaji kwenda na watoto wenu katika mikutano yote ya Kikristo. Kwa njia hiyo, mnafuata kielelezo ambacho Yehova aliwawekea Waisraeli, ambao waliamriwa hivi: “Wakutanishe watu, wanaume na wanawake na watoto wadogo . . . , ili wasikilize na ili wajifunze, kwa maana ni lazima wamwogope Yehova Mungu wenu na kuwa waangalifu kuyatimiza maneno yote ya sheria hii. Na wana wao ambao hawakujua wanapaswa kusikiliza, nao lazima wajifunze kumwogopa Yehova Mungu wenu.”—Kum. 31:12, 13.

Tangu wakiwa wachanga, watoto wanaweza kuanza kujifunza kuhusu Neno la Yehova. Mtume Paulo alisema hivi kumhusu Timotheo: “Tangu utoto mchanga umeyajua maandishi matakatifu.” (2 Tim. 3:15) Kwenye mikutano katika Jumba la Ufalme, hata watoto wachanga sana wanaweza kuanza kuelewa habari ambayo inazungumziwa na kuanza kufahamu nyimbo za Ufalme. Kwenye mikutano, wanajifunza kutumia na kuiheshimu Biblia na vichapo vinavyotegemea Biblia. Zaidi ya hayo, wakiwa kwenye mikutano wataona sifa ambayo inawatambulisha wafuasi wa kweli wa Kristo, yaani, upendo wa kweli. Yesu alisema hivi: “Ninawapa ninyi amri mpya, kwamba mpendane; kama vile ambavyo nimewapenda ninyi, ninyi nanyi mpendane vivyo hivyo. Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.” (Yoh. 13:34, 35) Upendo mchangamfu na usalama wa kweli ambao unaonekana wazi katika Jumba la Ufalme utawavutia watoto na kuwasaidia kuazimia kuhudhuria mikutano ya Kikristo katika muda wote wa maisha yao.

Mnapokuwa na zoea la kufika mapema kwenye Jumba la Ufalme na kukaa kidogo baada ya mikutano, watoto wako watakuwa na nafasi ya kupata marafiki. Badala ya kuwaruhusu washirikiane tu na watoto wenzao, kwa nini usiwatambulishe kwa ndugu na dada wenye umri mbalimbali? Watoto wako wakiwafahamu watu wenye umri mkubwa zaidi, watagundua kwamba watu hao waliozeeka wana hazina yenye kuvutia ya uzoefu na hekima. Ndugu na dada hao ambao wamekuwa wakimtumikia Yehova kwa uaminifu kwa miaka mingi wanakuwa na uvutano mzuri juu ya watoto leo, kama vile ambavyo Zekaria aliyekuwa “akiwafundisha watu kumwogopa Mungu wa kweli” katika nyakati za kale, alivyokuwa na uvutano mzuri juu ya kijana Uzia, mfalme wa Yuda. (2 Nya. 26:1, 4, 5) Ukiwa katika Jumba la Ufalme, unaweza pia kuwaeleza watoto wako jinsi maktaba inavyotumiwa, kazi ya ubao wa matangazo, na vitu vingine.

Tengenezo la Ulimwenguni Pote

Watoto wanahitaji kuelewa kwamba kutaniko lenu ni sehemu ya tengenezo la ulimwenguni pote lenye makutaniko zaidi ya 100,000. Waeleze mambo mbalimbali kuhusu tengenezo hilo, jinsi linavyofanya kazi, na daraka ambalo watoto wanatimiza katika kuunga mkono kazi hiyo. Waeleze kwa nini unatazamia kwa hamu makusanyiko ya mzunguko, makusanyiko ya wilaya, na ziara za mwangalizi wa mzunguko.—Ona sanduku lenye kichwa  “Mambo ya Kuzungumzia Wakati wa Ibada ya Familia,” kwenye ukurasa wa 28.

Ukipata nafasi, waalike waangalizi wanaosafiri, wamishonari, na washiriki wa familia ya Betheli, na watumishi wengine wa wakati wote katika nyumba yenu kwa ajili ya chakula. Usifikiri kwamba hawana wakati wa kuwa pamoja na watoto. Watumishi hao wa wakati wote wanajitahidi kumwiga Yesu, ambaye sikuzote aliwakaribisha watoto na kuzungumza nao. (Marko 10:13-16) Watoto wako wakiwasikia watumishi hao wa Yehova wakisimulia mambo yaliyoonwa na kuona shangwe yao katika utumishi mtakatifu, wanaweza pia kujiwekea mradi wa kuingia katika utumishi wa wakati wote.

Ni nini kingine mnachoweza kufanya mkiwa familia ili kuwasaidia watoto wenu kuelewa zaidi tengenezo la Yehova? Hapa pana mapendekezo fulani: Mkiwa familia wekeni mradi wa kujifunza kitabu Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu. Kazieni ujitoaji, unyenyekevu, na ushikamanifu ambao watumishi wa Yehova wameonyesha. Onyesheni jinsi Yehova alivyowatumia kueneza habari njema katika dunia yote. Tumieni video zilizotayarishwa na tengenezo la Yehova kuwafundisha masomo muhimu ya nyakati za kale na leo. Ikiwa mnaweza, tembeleeni ofisi ya tawi na Betheli katika nchi yenu na labda hata katika nchi nyingine mbalimbali. Matembezi kama hayo yatawasaidia watoto wenu kuelewa jinsi sehemu ya kidunia ya tengenezo la Yehova chini ya mwongozo wa jamii ya mtumwa mwaminifu ilivyopangwa ili kuwaandalia akina ndugu ulimwenguni pote chakula cha kiroho na mwongozo, kama vile jamii hiyo ilivyofanya katika karne ya kwanza W.K.—Mt. 24:45-47; Mdo. 15:22-31.

Kufanya Habari Imfae Kila Mtoto

Mnapowafundisha watoto wenu mnapaswa kukumbuka jinsi Yesu alivyowafundisha mitume wake. Wakati fulani aliwaambia hivi: “Bado nina mambo mengi ya kuwaambia, lakini hamwezi kuyastahimili kwa sasa.” (Yoh. 16:12) Yesu hakuwalemea wanafunzi wake kwa kuwapa habari nyingi. Badala yake, aliwafundisha hatua kwa hatua kweli muhimu ili waweze kuzielewa kwa njia inayofaa. Vivyo hivyo, usiwalemee watoto wako na habari nyingi. Kwa kuwalisha kidogo-kidogo lakini kwa ukawaida ujuzi kuhusu tengenezo, utawachochea wapendezwe na habari hiyo nao watafurahia kujifunza kuhusu kutaniko la Kikristo. Kadiri mahitaji ya watoto wenu yanavyobadilika, mnaweza kurudia na kupanua mambo ambayo tayari wamejifunza.

Kutaniko la Kikristo ni ngome ya kupata nguvu za kiroho, na watoto ambao wanashiriki kwa bidii katika utendaji wa kutaniko wanakuwa wametayarishwa vizuri zaidi kushinda uvutano wa ulimwengu wa Shetani. (Rom. 12:2) Tuna hakika kwamba mtapata shangwe zaidi ya kuwasaidia watoto wenu waelewe tengenezo la Yehova. Yehova na awabariki watoto wenu ili waendelee kushikamana kabisa na tengenezo hilo na kukaa katika upendo wa Mungu ambaye tunamtumikia.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 28]

 Mambo ya Kuzungumzia Wakati wa Ibada ya Familia

Yafuatayo ni mambo machache kuhusu tengenezo ambayo mnaweza kujifunza wakati wa jioni ya Ibada ya Familia.

▪ Zungumzieni historia ya kutaniko lenu. Lilianzishwa wakati gani na jinsi gani? Kutaniko lenu lilitumia Majumba gani mbalimbali ya Ufalme? Wakati wa mazungumzo hayo, kwa nini msimwalike nyumbani kwenu mshiriki wa zamani wa kutaniko ili ajibu maswali ya watoto wenu?

▪ Elezeni kusudi la mikutano mbalimbali ya kutaniko na makusanyiko makubwa na jinsi watoto wanavyoweza kufaidika kutokana nayo.

▪ Zungumzieni kusudi la shule mbalimbali zilizoanzishwa na tengenezo la Yehova. Simulieni mambo yaliyoonwa yanayoonyesha mambo mazuri ambayo yametimizwa na wale waliohitimu au kumaliza mafunzo ya shule hizo.

▪ Wasaidieni vijana waone umuhimu wa kuwa wahubiri wa kawaida wa habari njema. Waonyeshe jinsi wanavyoweza kuchangia ripoti ya ulimwenguni pote ambayo inachapishwa katika Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova.

▪ Zungumzieni aina mbalimbali za utumishi wa wakati wote ambao vijana wanaweza kushiriki katika tengenezo la Yehova. Sura ya 10 ya kitabu Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova ina habari nyingi kuhusu jambo hilo.

▪ Wasaidieni vijana waelewe kwa nini utaratibu mbalimbali unafuatwa katika kutaniko. Elezeni kwa nini wanapaswa kulitegemea tengenezo la Yehova hata katika mambo madogo badala ya kujitegemea wenyewe. Waonyesheni jinsi wanavyoweza kuchangia hali ya utaratibu katika kutaniko kwa kufuata miongozo ya wazee.

[Picha]

Watoto wako watafaidika wakipata marafiki ambao wamemtumikia Yehova kwa muda mrefu

[Picha katika ukurasa wa 26]

Kama ilivyokuwa katika Israeli la kale, leo wazazi wanajitahidi kujibu kwa njia ya kuridhisha maswali wanayoulizwa kuhusu tengenezo la Yehova