Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Ana Maoni Gani Kuhusu Visingizio?

Yehova Ana Maoni Gani Kuhusu Visingizio?

Yehova Ana Maoni Gani Kuhusu Visingizio?

“MWANAMKE uliyenipa awe pamoja nami, alinipa tunda kutoka katika ule mti nami nikala,” akasema mwanamume. “Yule nyoka—alinidanganya nami nikala,” akajibu mwanamke. Maneno hayo ambayo Mungu aliambiwa na wazazi wetu wa kwanza wa kibinadamu, Adamu na Hawa, yalikuwa mwanzo wa historia ndefu ya wanadamu ya kutoa visingizio.—Mwa. 3:12, 13.

Hukumu ya Yehova juu ya Adamu na Hawa kwa sababu walichagua kimakusudi kutotii ilionyesha wazi kwamba Yehova hakukubali visingizio vyao. (Mwa. 3:16-19) Hivyo basi, je, tukate kauli kwamba Yehova hakubali visingizio vyote? Au je, anaona visingizio fulani kuwa vinafaa? Ikiwa ndivyo, tunaweza kutofautisha jinsi gani visingizio vinavyofaa na visivyofaa? Ili kujibu swali hilo, acheni tuchunguze kwanza maana ya neno “kisingizio.”

Kisingizio ni sababu inayotolewa ili kueleza kwa nini jambo fulani limefanywa, au halikufanywa, au halitafanywa. Kisingizio kinaweza kuwa maelezo yanayofaa kuhusu kosa fulani au huenda pia kikawa kuomba msamaha kikweli ili kuweka msingi wa kuonyeshwa rehema au kusamehewa. Hata hivyo, kama ilivyokuwa katika kisa cha Adamu na Hawa, kisingizio kinaweza pia kuwa dai, yaani, sababu isiyo ya kweli inayotolewa ili kufunika jambo halisi. Kwa kuwa mara nyingi visingizio vinatolewa kwa sababu hiyo, kwa kawaida vinaonwa kuwa visivyoaminika.

Tunapotoa visingizio, hasa ikiwa vinahusiana na utumishi wetu kwa Mungu, ni lazima tuwe waangalifu ili tuepuke ‘kujidanganya wenyewe kwa mawazo yasiyo ya kweli.’ (Yak. 1:22) Kwa hiyo, acheni tuchunguze kanuni na mifano fulani katika Biblia ambayo itatusaidia ‘kuendelea kuhakikisha lile linalokubalika kwa Bwana.’—Efe. 5:10.

Mambo Ambayo Mungu Anatutazamia Tufanye

Katika Neno la Mungu tunapata amri hususa ambazo tunahitaji kutii tukiwa watu wa Yehova. Kwa mfano, amri iliyotolewa na Kristo aliposema “nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote,” bado inafuatwa na wafuasi wa kweli wa Kristo. (Mt. 28:19, 20) Kwa kweli, kutimiza amri hiyo ni jambo la maana sana hivi kwamba mtume Paulo alisema: “Ole wangu mimi ikiwa sitangazi habari njema!”—1 Kor. 9:16.

Hata hivyo, watu fulani ambao wamekuwa wakijifunza Biblia pamoja nasi kwa muda mrefu bado wanasitasita kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu. (Mt. 24:14) Wengine ambao zamani walishiriki katika kazi ya kuhubiri wameacha kufanya hivyo. Nyakati nyingine wale ambao hawashiriki katika kazi ya kuhubiri wanatoa sababu gani? Yehova alitenda jinsi gani kuelekea wale ambao hapo zamani walisitasita kutii amri fulani hususa ambazo alitoa?

Visingizio Ambavyo Havikubaliwi na Mungu

“Ni vigumu sana.” Hasa kwa wale ambao kiasili ni waoga, huenda likaonekana kuwa jambo gumu sana kwao kushiriki katika kazi ya kuhubiri. Hata hivyo, ona yale tunayoweza kujifunza kutokana na mfano wa Yona. Alipewa mgawo ambao aliuona kuwa mgumu sana—Yehova alimwambia atangaze uharibifu wa Ninawi uliokuwa ukija. Si vigumu kuelewa kwa nini Yona aliogopa sana kutimiza mgawo huo. Ninawi ulikuwa mji mkuu wa nchi ya Ashuru, na Waashuru walijulikana kuwa wakatili sana. Huenda Yona alijiuliza: ‘Nitafaulu jinsi gani katikati ya watu hao? Watanitendea namna gani?’ Muda mfupi baadaye, alikimbia. Hata hivyo, Yehova hakukubali kisingizio cha Yona. Badala yake, Yehova alimtuma tena kwenda kuwahubiria Waninawi. Wakati huu, Yona alitimiza mgawo wake kwa uhodari, na Yehova alibariki matokeo ya kazi yake.—Yona 1:1-3; 3:3, 4, 10.

Ikiwa unafikiri kwamba mgawo wa kuhubiri habari njema ni mgumu sana kwako, kumbuka kwamba “mambo yote yanawezekana kwa Mungu.” (Marko 10:27) Unaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atakutia nguvu ukiendelea kumwomba akusaidie na kwamba atakubariki unapojitahidi kupata uhodari ili kutimiza huduma yako.—Luka 11:9-13.

“Sitaki.” Unaweza kufanya nini ikiwa huna tamaa au nia ya kutoka moyoni ya kutimiza huduma yako ya Kikristo? Kumbuka kwamba Yehova anaweza kutenda ndani yako na kuongoza tamaa yako. Paulo alisema hivi: “Mungu ndiye ambaye, kwa ajili ya mapenzi yake mema, anatenda ndani yenu ili ninyi muwe na nia na kutenda pia.” (Flp. 2:13) Kwa hiyo, unaweza kumwomba Yehova akupe nia ya kutaka kufanya mapenzi yake. Hivyo ndivyo Mfalme Daudi alivyofanya. Alimsihi Yehova hivi: “Nitembeze katika kweli yako.” (Zab. 25:4, 5) Unaweza kufanya vivyo hivyo kwa kusali kwa bidii ili Yehova akuchochee kuwa na nia ya kufanya mambo yanayompendeza.

Ni kweli kwamba tunapochoka au kuvunjika moyo, huenda nyakati nyingine tukahitaji kujilazimisha kuhudhuria mkutano fulani kwenye Jumba la Ufalme au kushiriki katika huduma. Ikiwa ndivyo ilivyo, je, tunapaswa kukata kauli kwamba kwa kweli hatumpendi Yehova? Hapana. Watumishi waaminifu wa Mungu katika nyakati za kale walihitaji pia kujitahidi sana ili kufanya mapenzi ya Mungu. Kwa mfano, Paulo alisema kwamba ‘aliupigapiga mwili wake,’ kwa njia ya mfano, ili aweze kutii amri za Mungu. (1 Kor. 9:26, 27) Hivyo, hata ikiwa nyakati nyingine tunajilazimisha kutimiza huduma yetu, tunaweza kuwa na hakika kwamba tutabarikiwa na Yehova. Kwa nini? Kwa kuwa tunajilazimisha wenyewe kufanya mapenzi ya Mungu tukiwa na sababu nzuri, yaani, kwa sababu tunampenda Yehova. Kwa kufanya hivyo, tunajibu dai la Shetani la kwamba watumishi wa Mungu watamkana ikiwa watajaribiwa.—Ayu. 2:4.

“Nina shughuli nyingi.” Ikiwa hushiriki katika huduma kwa sababu unahisi kwamba una shughuli nyingi, ni jambo la maana sana kwamba uchunguze upya mambo unayotanguliza maishani. Yesu alisema hivi: “Basi, endeleeni kuutafuta kwanza ufalme.” (Mt. 6:33) Ili kufuata kanuni hiyo inayotuongoza, huenda ukahitaji kurahisisha mtindo wako wa maisha au kupunguza wakati ambao unatumia katika burudani na kuutumia katika huduma. Bila shaka, burudani na mambo mengine ya kibinafsi yana mahali pake, lakini mambo hayo si kisingizio kinachofaa cha kupuuza huduma yetu. Mambo ya Ufalme ndiyo yanayochukua nafasi ya kwanza katika maisha ya mtumishi wa Mungu.

“Sina uwezo.” Huenda ukahisi kwamba hustahili kuwa mhudumu wa habari njema. Watumishi fulani waaminifu wa Yehova katika nyakati za Biblia walihisi kwamba hawakuwa na uwezo wa kutimiza migawo ambayo Yehova aliwapa. Fikiria mfano wa Musa. Alipopewa kazi ya pekee na Yehova, Musa alisema hivi: “Nakuomba radhi, Yehova, lakini mimi si msemaji mzuri, tangu jana wala tangu kabla ya hapo wala tangu uliposema na mtumishi wako, kwa maana kinywa changu ni kizito na ulimi wangu ni mzito.” Ingawa Yehova alimpa uhakikisho, Musa alijibu: “Nakuomba radhi, Yehova, lakini tuma, tafadhali, kupitia mkono wa yule utakayemtuma.” (Kut. 4:10-13) Yehova alitenda jinsi gani?

Yehova hakukubali visingizio vya Musa vya kukataa kutimiza mgawo huo. Hata hivyo, Yehova alimweka rasmi Haruni ili amsaidie Musa kutimiza mgawo huo. (Kut. 4:14-17) Zaidi ya hayo, katika miaka iliyofuata, Yehova alimtegemeza Musa na kumpa chochote alichohitaji ili kufanikiwa katika kutimiza migawo aliyopewa na Mungu. Leo, unaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atawachochea waamini wenzako wenye uzoefu wakusaidie pia ili utimize huduma yako. Zaidi ya yote, Neno la Mungu linatuhakikishia kwamba Yehova atatuwezesha tuwe na sifa zinazostahili ili tutimize kazi ambayo ametuamuru kufanya.—2 Kor. 3:5; ona sanduku  “Miaka Yenye Furaha Zaidi Katika Maisha Yangu.”

“Mtu fulani aliniumiza hisia.” Wengine wanaacha kushiriki katika huduma au kuhudhuria mikutano ya kutaniko kwa sababu waliumizwa hisia, huku wakifikiri kwamba Yehova bila shaka atakubali kisingizio hicho cha kuacha kushiriki katika utendaji wa Kikristo. Ingawa ni jambo linaloeleweka kwamba tunakasirika kwa sababu tuliumizwa hisia na mtu fulani, je, kweli ni kisingizio kinachofaa kuacha kushiriki katika utendaji wa Kikristo? Huenda Paulo na mwamini mwenzake Barnaba waliumia hisia baada ya hali ya kutoelewana kati yao kusababisha “hasira kali.” (Mdo. 15:39) Lakini je, kutoelewana huko kulimfanya yeyote kati yao aache kushiriki katika huduma? Hapana!

Vivyo hivyo, unapoumizwa hisia na mwamini mwenzako, kumbuka kwamba adui yako si ndugu yako Mkristo asiye mkamilifu bali ni Shetani, ambaye anataka kukumeza. Hata hivyo, Ibilisi hatafaulu ikiwa ‘utachukua msimamo kumpinga yeye, ukiwa imara katika imani.’ (1 Pet. 5:8, 9; Gal. 5:15) Ikiwa una imani kama hiyo, bila shaka ‘hutakata tamaa.’—Rom. 9:33.

Tufanye Nini Ikiwa Hatuna Uwezo wa Kutimiza Mengi?

Kutokana na mifano hiyo michache kuhusu visingizio, ni wazi kwamba Maandiko hayana visingizio ambavyo vinafaa vya kutotimiza amri hususa za Yehova, kutia ndani kazi ya kuhubiri habari njema. Hata hivyo, kwa sababu ya udhaifu fulani huenda tukawa na sababu nzuri za kutotimiza huduma yetu kikamili. Huenda madaraka mengine ya Kimaandiko yakapunguza muda ambao tunaweza kutumia katika kazi ya kuhubiri. Pia, pindi kwa pindi tunaweza kuchoka kikweli au kuwa wagonjwa sana tusiweze kufanya yale ambayo tungependa kutimiza katika utumishi wa Yehova. Hata hivyo, Neno la Mungu linatuhakikishia kwamba Yehova anajua tamaa yetu ya moyoni na anafikiria udhaifu wetu.—Zab. 103:14; 2 Kor. 8:12.

Kwa hiyo, tunahitaji kuwa waangalifu ili tusijihukumu wenyewe au kuwahukumu wengine vikali katika mambo hayo. Mtume Paulo aliandika hivi: “Wewe ni nani ili umhukumu mtumishi wa nyumbani wa mwingine? Kwa bwana wake mwenyewe yeye husimama au kuanguka.” (Rom. 14:4) Badala ya kulinganisha hali yetu na ile ya wengine, tunapaswa kukumbuka kwamba “kila mmoja wetu atatoa hesabu kwa Mungu kwa ajili yake mwenyewe.” (Rom. 14:12; Gal. 6:4, 5) Tunapomfikia Yehova katika sala na kutoa visingizio vyetu kwake, ni vizuri kila mmoja wetu afanye hivyo kwa “dhamiri nyoofu.”—Ebr. 13:18.

Kwa Nini Kumtumikia Yehova Kunatuletea Shangwe?

Sisi sote tunaweza kumtumikia Yehova tukiwa na shangwe moyoni kwa sababu matakwa yake—hata tuwe na hali gani maishani—ni yenye usawaziko sikuzote na tunaweza kuyatimiza. Kwa nini tunaweza kusema hivyo?

Neno la Mungu linasema hivi: “Usiwanyime watu mema wanayostahili, mkono wako ukiwa na uwezo wa kuyafanya.” (Met. 3:27) Umeona nini katika methali hiyo kuhusu matakwa ya Mungu? Yehova hakuamuru ujitahidi kuwa na uwezo kama ule ulio katika mkono wa ndugu yako bali anakuomba umtumikie na ‘uwezo ulio katika mkono wako.’ Ndiyo, kila mmoja wetu—iwe ana nguvu nyingi au chache katika mkono wake—anaweza kumtumikia Yehova kwa moyo wote.—Luka 10:27; Kol. 3:23.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 14]

 “Miaka Yenye Furaha Zaidi Katika Maisha Yangu”

Hata ikiwa tuna udhaifu mkubwa wa kimwili au wa kihisia, hatupaswi kukata kauli haraka kwamba udhaifu huo utatuzuia kushiriki kwa ukamili katika huduma. Kwa mfano, ona kile kilichompata Ernest, ndugu Mkristo huko Kanada.

Ernest alikuwa na kigugumizi na alikuwa mwenye haya sana. Baada ya kuumia vibaya mgongoni, aliacha kazi yake ya ujenzi. Ingawa sasa alikuwa mlemavu, hali zake za sasa zilimruhusu kutumia wakati mwingi zaidi katika huduma. Himizo ambalo lilitolewa kwenye mikutano ya kutaniko la kufanya upainia msaidizi lilimchochea sana kufanya utumishi huo. Hata hivyo, alihisi kwamba hastahili kufanya huduma ya aina hiyo.

Ili kujithibitishia mwenyewe kwamba hakuwa na uwezo wa kuwa painia msaidizi, alijaza fomu ili atumikie akiwa painia msaidizi kwa mwezi mmoja. Alishangaa sana alipofanikiwa kutimiza mgawo huo. Kisha alianza kuwaza, ‘Ninajua siwezi kamwe kufanya hivyo tena.’ Ili kuthibitisha maoni yake, alijaza fomu ili awe painia kwa mwezi wa pili, na kwa mara nyingine tena, akatimiza mgawo huo.

Ernest alitumika akiwa painia msaidizi kwa mwaka mzima, lakini alisema, “Ninajua kwa hakika siwezi kamwe kuwa painia wa kawaida.” Tena, ili kuthibitisha maoni yake, alijaza fomu ya utumishi wa painia wa kawaida. Alishangaa alipoweza kukamilisha mwaka wa kwanza akiwa painia wa kawaida. Aliamua kuendelea na alibarikiwa kwa kuwa alipata shangwe ya kutumikia akiwa painia wa kawaida kwa miaka miwili, mpaka alipokufa kutokana na matatizo ya mgongo wake ulioumia. Hata hivyo, kabla ya kifo chake, mara nyingi aliwaambia hivi watu waliomtembelea huku akitokwa na machozi, “Miaka hiyo ambayo nimemtumikia Yehova nikiwa painia ndiyo miaka yenye furaha zaidi katika maisha yangu.”

[Picha katika ukurasa wa 13]

Tunaweza kushinda tatizo lolote lile ambalo linaweza kutuzuia tusitimize huduma yetu

[Picha katika ukurasa wa 15]

Yehova anafurahi tunapomtumikia kwa nafsi yote kwa kufanya yote ambayo hali zetu zinaturuhusu kufanya