Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Mambo Aliyotenda Yanaambatana Naye Moja kwa Moja’

‘Mambo Aliyotenda Yanaambatana Naye Moja kwa Moja’

‘Mambo Aliyotenda Yanaambatana Naye Moja kwa Moja’

THEODORE JARACZ, mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, alikufa Jumatano (Siku ya tatu) asubuhi, Juni 9, 2010 (9/6/2010) akiwa na tumaini la kwenda mbinguni. Alikuwa na umri wa miaka 84 na ameacha mke wake Melita, ambaye ameishi naye kwa miaka 53. Ameacha watu wengine kutia ndani dada yake mmoja, mpwa mmoja wa kiume, na pia wapwa wawili wa kike.

Ndugu Jaracz alizaliwa Septemba 28, 1925 (28/9/1925), huko Pike County, Kentucky, Marekani, na akajiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa Agosti 10, 1941, akiwa na umri wa miaka 15. Miaka miwili baadaye, akiwa na umri wa miaka 17, alianza kazi ya upainia wa kawaida, na huo ukawa ndio mwanzo wa kazi ya muda mrefu ya karibu miaka 67 ya utumishi wa wakati wote.

Katika mwaka wa 1946, akiwa na umri wa miaka 20, Ndugu Jaracz alihudhuria darasa la saba la Shule ya Gileadi (Watchtower Bible School of Gilead). Baada ya kuhitimu au kumaliza shule hiyo, Ndugu Jaracz alipewa mgawo wa kutumikia akiwa mwangalizi anayesafiri huko Cleveland, Ohio, Marekani. Katika mwaka wa 1951, alipewa mgawo kwenye ofisi ya tawi ya Australia, ambako alitumika akiwa mtumishi wa ofisi ya tawi. Kitabu cha Mwaka wa 1983 cha Mashahidi wa Yehova kiliripoti kwamba Ndugu Jaracz “aliwatia moyo sana akina ndugu kotekote nchini kwa bidii yake kwa ajili ya utaratibu wa kitheokrasi na kwa uongozi mzuri katika kazi ya kuhubiri.”

Baada ya kurudi Marekani, Ndugu Jaracz alifunga ndoa na Melita Lasko mnamo Desemba 10, 1956. Walianza maisha yao ya ndoa katika kazi ya kusafiri, wakatumikia kwa bidii katika mizunguko na wilaya katika sehemu kubwa ya Marekani. Mwishoni mwa mwaka wa 1974, Ndugu Jaracz alialikwa kuwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova.

Ndugu Jaracz atakumbukwa kwa muda mrefu kuwa mtumishi wa Yehova aliyejiweka wakfu na mshikamanifu, ambaye alikazia fikira kwa moyo wote utendaji wa kitheokrasi. Alikuwa mume mwenye upendo na mwenye kujali na pia mwanamume wa kiroho ambaye alitanguliza faida za wengine kabla ya faida zake mwenyewe. (1 Kor. 13:4, 5) Alionyesha kuwa alipendezwa kikweli na wengine kwa kuhangaikia sana kwamba watu wote watendewe kwa haki na rehema. Zaidi ya hayo, alionyesha kwamba aliwapenda sana watu na kuwahangaikia bila kuchoka kwa kushiriki kwa bidii katika huduma ya shambani.

Ingawa tunahuzunika sana kwa sababu ya kifo cha mfanyakazi huyo mwenye bidii na mshiriki mpendwa wa familia ya Betheli na ya undugu wa ulimwenguni pote, tunashangilia kwa sababu Ndugu Jaracz amemtumikia Yehova kwa ushikamanifu kwa miaka mingi. Tuna hakika kwamba ‘amekuwa mwaminifu hata kufikia kifo na amepokea taji la uzima.’ (Ufu. 2:10) Pia, tuna hakika kwamba ‘mambo aliyotenda yanaambatana naye moja kwa moja.’—Ufu. 14:13.