Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Yesu aliwaambia wasikilizaji wake hivi: “Lazima ninyi . . . muwe wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu.” Leo, wanadamu wanaweza ‘kuwa wakamilifu’ jinsi gani?—Mt. 5:48.

Kupata jibu la swali hilo kunategemea uelewaji wa jinsi maneno “kamilifu” na “ukamilifu” yanavyotumiwa katika Biblia. Si kila kitu ambacho Maandiko yanaeleza kuwa “kikamilifu” kinachoweza kuwa kikamilifu katika maana kamili. Bila shaka, Yehova ni mkamilifu kikamili. Watu au vitu vinaweza kuwa vikamilifu kwa kadiri fulani. Maneno ya Biblia ya Kiebrania na Kigiriki yanayotafsiriwa “kamilifu” mara nyingi yanamaanisha “kamili,” “komavu,” au “bila kosa” kulingana na viwango vinavyowekwa na mtu mwenye mamlaka. Katika mazungumzo ya kila siku, kwa kawaida neno hilo linatumiwa kuonyesha ukamilifu wa kadiri tu. Mfano mmoja ni maneno “majira makamilifu.”

Adamu na Hawa waliumbwa wakiwa wakamilifu kiadili, kiroho, na kimwili. Walikuwa wakamilifu kulingana na viwango vilivyowekwa na Muumba wao. Hawakutimiza viwango hivyo kwa sababu ya kutotii na hivyo wakapoteza ukamilifu wao na wa wazao wao. Hivyo, wanadamu walirithi dhambi, kutokamilika, na kifo kutoka kwa Adamu.—Rom. 5:12.

Hata hivyo, kama Yesu alivyoeleza wazi katika Mahubiri ya Mlimani, hata watu wasio wakamilifu wanaweza kuwa wakamilifu kwa kadiri fulani. Katika hotuba hiyo, aliweka viwango vya upendo mkamilifu au ulio kamili. Huo ni upendo kama ule ambao Mungu anawaonyesha wanadamu. Yesu alisema: “Endeleeni kuwapenda adui zenu na kusali kwa ajili ya wale wanaowatesa ninyi; ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni, kwa kuwa yeye hulichomoza jua lake juu ya watu waovu na wema na hunyesha mvua juu ya watu waadilifu na wasio waadilifu.” (Mt. 5:44, 45) Kwa kuonyesha upendo kwa kadiri hiyo, wanafunzi wa Yesu watakuwa wanaiga mfano mkamilifu wa Mungu.

Leo, Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote wanajitahidi kudumisha kiwango cha juu cha upendo kuelekea wengine. Wanatamani kuwasaidia watu wa malezi, rangi, na dini mbalimbali ili wapate ujuzi sahihi wa kweli ya Biblia. Kwa sasa, Mashahidi wanaongoza mafunzo ya Biblia zaidi ya 7,000,000 pamoja na watu wanaopendezwa katika nchi 236.

Yesu aliuliza hivi: “Mkiwapenda wale wanaowapenda ninyi, mna thawabu gani? Je, wakusanya-kodi pia hawafanyi jambo hilohilo? Na mkiwasalimu ndugu zenu tu, mnafanya jambo gani linalozidi lile la kawaida? Je, watu wa mataifa pia hawafanyi jambo hilohilo?” (Mt. 5:46, 47) Wakristo wa kweli hawabagui watu kwa sababu ya elimu au kabila lao; wala hawawapendi tu wale ambao wanaweza pia kuwapenda. Badala yake, wanawasaidia maskini na wagonjwa, vijana na wazee. Katika njia hizo, Wakristo wanaweza kuiga upendo wa Yehova na hivyo kuwa wakamilifu kwa kadiri fulani.

Je, tutawahi kufurahia ukamilifu ambao Adamu alipoteza? Ndiyo, kwa kuonyesha imani katika fidia au dhabihu ya ukombozi ya Yesu, wanadamu watiifu watafikia hali ya ukamilifu wakati wa Utawala wa Miaka Elfu Moja wa Kristo, wakati ‘Mwana wa Mungu atakapozivunja kazi za Ibilisi.’—1 Yoh. 3:8.