Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tutatembea Katika Utimilifu Wetu!

Tutatembea Katika Utimilifu Wetu!

Tutatembea Katika Utimilifu Wetu!

“Mimi nami nitatembea katika utimilifu wangu.”—ZAB. 26:11.

1, 2. Ayubu alisema nini kuhusu utimilifu wake, na kitabu cha Ayubu sura ya 31 kinaonyesha nini kumhusu?

NYAKATI za kale, mara nyingi vitu vilipimwa uzito kwa kutumia mizani. Kwa kawaida, mizani ilitengenezwa kwa chuma kilichoshikiliwa na nguzo katikati. Sahani ilining’inia kila upande wa mizani hiyo. Kitu kilichopimwa uzito kiliwekwa kwenye sahani moja na jiwe la kupima uzito liliwekwa upande mwingine. Watu wa Mungu walipaswa kutumia mizani na mawe sahihi.—Met. 11:1.

2 Ayubu, mtu aliyemwogopa Mungu, alipokuwa akiteseka kutokana na mashambulizi ya Shetani, alisema hivi: “[Yehova] atanipima katika mizani sahihi na Mungu atajua utimilifu wangu.” (Ayu. 31:6) Kuhusu jambo hilo, Ayubu alitaja hali mbalimbali ambazo zingeweza kujaribu utimilifu wa mtu. Lakini kwa kweli Ayubu alifanikiwa kushinda majaribu hayo, kama inavyoonyeshwa na maneno yake katika kitabu cha Ayubu sura ya 31. Huenda mfano wake mzuri ukatuchochea kutenda kwa njia hiyohiyo na kusema kwa usadikisho kama alivyosema mtunga-zaburi Daudi: “Mimi nami nitatembea katika utimilifu wangu.”—Zab. 26:11.

3. Kwa nini ni jambo la maana kuwa mwaminifu kwa Mungu katika mambo makubwa na madogo pia?

3 Ingawa Ayubu alijaribiwa vikali sana, alibaki mwaminifu kwa Mungu. Huenda wengine hata wakasema kwamba Ayubu alikuwa mfano mzuri sana wa utimilifu ingawa alijaribiwa vikali sana. Mateso yetu hayalingani kabisa na mateso ya Ayubu. Hata hivyo, ikiwa tutaimarisha msimamo wetu wa kuwa watimilifu na kuunga mkono enzi kuu ya Mungu, ni lazima tuwe waaminifu kwa Mungu katika mambo makubwa na madogo pia.—Soma Luka 16:10.

Ni Jambo la Maana Kushika Utimilifu wa Maadili

4, 5. Ayubu aliepuka mwenendo gani akiwa mtu anayeshika utimilifu?

4 Ili tudumishe utimilifu wetu kwa Yehova, ni lazima tushikamane na viwango vyake vya maadili, kama alivyofanya Ayubu. Alisema hivi: “Nimefanya agano pamoja na macho yangu. Basi nawezaje kukaza fikira kwa bikira? . . . Ikiwa moyo wangu umeshawishiwa kumwelekea mwanamke, nami nikaendelea kuvizia katika mlango wa rafiki yangu, basi mke wangu na amsagie mwanamume mwingine, wanaume wengine na wainame juu yake.”—Ayu. 31:1, 9, 10.

5 Kwa kuwa aliazimia kudumisha utimilifu kwa Mungu, Ayubu aliepuka kuendelea kumtazama mwanamke kwa kumtamani. Akiwa mwanamume aliyeoa, hakumchezea kimahaba mwanamke mseja au kupendezwa kimapenzi na mke wa mwanamume mwingine. Katika Mahubiri ya Mlimani, Yesu alisema maneno yenye nguvu kuhusu maadili katika ngono, ambayo bila shaka watu wanaoshika utimilifu wanahitaji kukumbuka.—Soma Mathayo 5:27, 28.

Usitumie Kamwe Mbinu za Ujanja

6, 7. (a) Kama ilivyokuwa katika kisa cha Ayubu, Mungu anatumia nini ili kupima utimilifu wetu? (b) Kwa nini hatupaswi kuwa wajanja au wadanganyifu?

6 Hatuwezi kutenda kwa ujanja ikiwa tunataka kuhesabiwa kati ya watu wanaoshika utimilifu. (Soma Methali 3:31-33.) Ayubu alisema hivi: “Ikiwa nimetembea na watu wasiosema kweli, na mguu wangu unaharakisha kuelekea udanganyifu, [Yehova] atanipima katika mizani sahihi na Mungu atajua utimilifu wangu.” (Ayu. 31:5, 6) Yehova anawapima wanadamu wote katika “mizani sahihi.” Kama katika kisa cha Ayubu, Mungu anatumia kiwango chake kikamilifu cha haki kupima utimilifu wetu tukiwa watumishi wake waliojiweka wakfu.

7 Ikiwa tutakuwa wajanja au wadanganyifu, hatutakuwa tukidumisha utimilifu wetu kwa Mungu. Watu ambao wanashika utimilifu ‘wameyakataa mambo ya kichinichini ambayo ni ya kuonea aibu’ na ‘hawatembei kwa ujanja.’ (2 Kor. 4:1, 2) Lakini namna gani ikiwa tunakuwa wajanja katika usemi au matendo, na hivyo kumfanya mwamini mwenzetu amwombe Mungu msaada? Hilo lingekuwa jambo baya sana kwetu! Mtunga-zaburi aliimba hivi: “Nilimwita Yehova katika taabu yangu, naye akanijibu. Ee Yehova, uikomboe nafsi yangu kutokana na midomo ya uwongo, kutokana na ulimi wenye ujanja.” (Zab. 120:1, 2) Ni vizuri kukumbuka kwamba Mungu anaweza kuchunguza ndani kabisa ya moyo wetu, huku ‘akipima moyo na figo’ ili kuona ikiwa sisi tunashika utimilifu kwelikweli.—Zab. 7:8, 9.

Uwe Mfano Mzuri Unaposhughulika na Wengine

8. Ayubu aliwatendea wengine jinsi gani?

8 Ili kudumisha utimilifu wetu, tunahitaji kuwa kama Ayubu, ambaye alikuwa mwenye haki, mnyenyekevu, na aliwajali wengine. Alisema hivi: “Ikiwa nilikuwa nikikataa hukumu ya haki ya mtumwa wangu au ya kijakazi wangu katika kesi yao juu yangu, basi naweza kufanya nini wakati Mungu atakaposimama? Na wakati atakapotoza hesabu, naweza kumjibu nini? Je, Yeye aliyenifanya mimi tumboni hakumfanya yeye, na je, si yeye Mmoja tu aliyetufanya sisi katika tumbo la uzazi?”—Ayu. 31:13-15.

9. Ayubu alionyesha sifa gani aliposhughulika na watumishi wake, na tunapaswa kutenda jinsi gani kuhusu jambo hilo?

9 Katika siku za Ayubu, inaonekana kwamba hakukuwa na utaratibu wenye kutatanisha wa kuendesha kesi za kisheria. Kesi ziliendeshwa kwa njia ya utaratibu, na mahakama zilishughulikia hata kesi za watumwa. Ayubu aliwatendea watumishi wake kwa haki na rehema. Ikiwa tutatembea katika utimilifu wetu, ni lazima tuonyeshe sifa kama hizo, hasa ikiwa tunatumikia tukiwa wazee katika kutaniko la Kikristo.

Uwe Mkarimu, Usiwe na Tamaa Mbaya

10, 11. (a) Tunajua jinsi gani kwamba Ayubu alikuwa mkarimu na aliwasaidia wengine? (b) Andiko la Ayubu 31:16-25 huenda likatukumbusha shauri gani la Kimaandiko ambalo liliandikwa baadaye?

10 Ayubu alikuwa mkarimu na aliwasaidia wengine, hakuwa mchoyo wala mwenye tamaa mbaya. Alisema hivi: ‘Ikiwa niliyafanya macho ya mjane yaishiwe nguvu, na kula tonge langu peke yangu, huku mvulana asiye na baba akiwa hali kutokana nalo. Ikiwa nilikuwa nikiona mtu yeyote akiangamia kwa kukosa vazi. Ikiwa nilitikisa mkono wangu huku na huku juu ya mvulana asiye na baba, wakati nilipokuwa nikiona msaada wangu unahitajiwa katika lango, acha mfupa wa bega langu uanguke kutoka katika bega lake, na acha mkono wangu uvunjwe kutoka kwenye mfupa wake wa juu.’ Na Ayubu hangeshika utimilifu wake ikiwa angeiambia dhahabu: “Wewe ni tegemeo langu!”—Ayu. 31:16-25.

11 Maneno hayo ya kishairi huenda yakatukumbusha maneno yafuatayo ya mwanafunzi Yakobo: “Namna ya ibada iliyo safi na isiyotiwa unajisi kwa maoni ya Mungu wetu na Baba ni hii: kuwatunza mayatima na wajane katika dhiki yao, na kuendelea kujitunza bila doa kutokana na ulimwengu.” (Yak. 1:27) Huenda tukakumbuka pia onyo hili la Yesu: “Endeleeni kufungua macho yenu na mjilinde na kila namna ya tamaa, kwa sababu hata wakati mtu ana vitu vingi uzima wake hautokani na vitu alivyo navyo.” Kisha, Yesu akatoa mfano kuhusu mtu mmoja tajiri mwenye tamaa aliyekufa na ambaye ‘hakuwa tajiri kwa Mungu.’ (Luka 12:15-21) Ili tuwe watu wanaoshika utimilifu, ni lazima tuepuke tamaa yenye dhambi au pupa. Tamaa ni ibada ya sanamu kwa sababu kitu kinachotamaniwa kinawakengeusha watu kutoka kwa Yehova na hivyo kinakuwa sanamu. (Kol. 3:5) Hatuwezi kushika utimilifu na wakati huohuo kuwa wenye pupa!

Shikamana Kabisa na Ibada ya Kweli

12, 13. Ayubu aliweka mfano gani katika kuepuka ibada ya sanamu?

12 Watu wanaoshika utimilifu hawaachi ibada safi. Ayubu hakufanya hivyo, kwa kuwa alisema hivi: “Ikiwa nilikuwa nikiona nuru wakati ilipowaka, au mwezi wenye fahari ukisonga, na moyo wangu ukaanza kushawishiwa kisiri na mkono wangu ukakibusu kinywa changu, hilo pia lingekuwa kosa la kufikiriwa na waamuzi, kwa maana ningekuwa nimemkana Mungu wa kweli aliye juu.”—Ayu. 31:26-28.

13 Ayubu hakuabudu vitu visivyo hai. Ikiwa moyo wake ulianza kushawishiwa kisiri baada ya kutazama vitu vya mbinguni, kama vile mwezi, na ikiwa ‘mkono wake ulikibusu kinywa chake,’ labda kwa kuubusu mkono wake na kuuelekeza mbinguni katika tendo la kuabudu sanamu, angekuwa mwabudu-sanamu aliyemkana Mungu. (Kum. 4:15, 19) Ili kudumisha utimilifu wetu kwa Mungu, ni lazima tuepuke ibada yote ya sanamu.—Soma 1 Yohana 5:21.

Usilipize Kisasi au Kuwa Mnafiki

14. Kwa nini tunaweza kusema kwamba Ayubu hakuwa mwenye chuki?

14 Ayubu hakuwa mwenye chuki wala mkatili. Alijua kwamba tabia hizo mbaya zingeonyesha kwamba hana utimilifu, kwa kuwa alisema hivi: “Ikiwa nilikuwa nikishangilia kuangamia kwa mtu anayenichukia vikali, au kuchangamka kwa sababu uovu umempata . . . , sikuruhusu kaakaa langu kutenda dhambi kwa kuomba laana juu ya nafsi yake.”—Ayu. 31:29, 30.

15. Kwa nini ni vibaya kushangilia wakati mtu fulani anayetuchukia anapopatwa na msiba?

15 Ayubu aliyekuwa mnyoofu hakushangilia kamwe msiba ulipompata mtu fulani aliyemchukia. Methali moja iliyoandikwa baadaye inaonya hivi: “Adui yako anapoanguka, usishangilie; naye anapokwazwa, moyo wako usiwe na shangwe, ili Yehova asipate kuona jambo hilo nalo liwe baya machoni pake, naye aigeuzie hasira yake mbali naye.” (Met. 24:17, 18) Kwa kuwa Yehova anaweza kusoma moyo, anajua ikiwa tunashangilia kisiri mtu mwingine anapopatwa na msiba na bila shaka hakubali mtazamo kama huo. (Met. 17:5) Mungu anaweza kushughulika nasi ipasavyo, kwa kuwa anasema hivi: “Kisasi ni changu, na malipo.”—Kum. 32:35.

16. Hata ingawa sisi si matajiri, tunaweza kuonyesha jinsi gani sifa ya kuwakaribisha wageni?

16 Ayubu aliwakaribisha wageni. (Ayu. 31:31, 32) Ingawa huenda tusiwe matajiri, tunaweza ‘kufuata mwendo wa ukaribishaji-wageni.’ (Rom. 12:13) Tunaweza kula pamoja na wengine chakula chepesi, huku tukikumbuka kwamba “afadhali chakula cha mboga za majani mahali penye upendo kuliko ng’ombe-dume aliyenoneshwa pamoja na chuki.” (Met. 15:17) Kula chakula chepesi katika mazingira yenye upendo pamoja na Mkristo mwenzetu ambaye anashika utimilifu kutafanya hata chakula hicho kiwe chenye kufurahisha na bila shaka tutafaidika kiroho.

17. Kwa nini hatupaswi kujaribu kuficha dhambi nzito?

17 Ni wazi kwamba watu walijengwa kiroho walipoonyeshwa ukarimu na Ayubu, kwa sababu hakuwa mnafiki. Hakuwa kama watu wasiomwogopa Mungu ambao waliingia kisirisiri ndani ya kutaniko la karne ya kwanza na ambao ‘walistaajabia watu mashuhuri kwa ajili ya faida yao wenyewe.’ (Yuda 3, 4, 16) Ayubu hakufunika dhambi yake wala ‘kuficha kosa lake katika mfuko wa shati lake,’ huku akiogopa kudharauliwa ikiwa wengine wangejua kuhusu kosa hilo. Alikuwa tayari kuchunguzwa na Mungu, ambaye angeungama kwake dhambi yoyote. (Ayu. 31:33-37) Tukitenda dhambi nzito, tusijaribu kuficha kosa kama hilo ili kuepuka aibu. Tunaweza kuonyesha namna gani kwamba tunajitahidi kudumisha utimilifu wetu? Kwa kukubali kosa letu, kutubu, kutafuta msaada wa kiroho, na kufanya yote tunayoweza ili kurekebisha mambo.—Met. 28:13; Yak. 5:13-15.

Alikuwa Tayari Kuthibitisha Utimilifu Wake

18, 19. (a) Kwa nini inaweza kusemwa kwamba Ayubu hakumtendea kamwe isivyo haki mtu yeyote? (b) Ayubu alikuwa tayari kufanya nini ikiwa angepatikana na hatia?

18 Ayubu alikuwa mnyoofu na mwenye haki. Hivyo, alisema hivi: “Ikiwa nchi yangu ingelia kwa sababu yangu ipate msaada, na mitaro yake ingelia pamoja; ikiwa nimekula matunda yake bila pesa, na nafsi ya wamiliki wake nimeifanya ipumue, basi magugu yenye miiba na yatokee badala ya ngano, na magugu yenye kunuka badala ya shayiri.” (Ayu. 31:38-40) Ayubu hakunyakua kamwe mashamba ya wengine, naye hakuwatendea isivyo haki wafanyakazi. Tunahitaji kudumisha utimilifu kwa Yehova katika mambo makubwa na madogo kama Ayubu alivyofanya.

19 Ayubu alieleza kuhusu maisha yake akiwa mbele ya marafiki wake watatu na kijana Elihu. Ayubu alimwomba mtu yeyote ambaye alikuwa na kesi juu yake atoe mashtaka kuhusu maisha yake au rekodi yake ambayo ilikuwa na “sahihi” yake. Ayubu alikuwa tayari kuadhibiwa ikiwa ingethibitishwa kwamba ana hatia. Kwa hiyo, alipeleka kesi yake na kungoja ahukumiwe na mahakama ya Mungu. Hivyo, ‘maneno ya Ayubu yakafika mwisho.’—Ayu. 31:35, 40.

Unaweza Kudumisha Utimilifu

20, 21. (a) Kwa nini Ayubu aliweza kudumisha utimilifu? (b) Tunaweza kusitawisha jinsi gani upendo kumwelekea Mungu?

20 Ayubu aliweza kudumisha utimilifu wake kwa sababu alimpenda Mungu, na Yehova alimpenda na kumsaidia. Ayubu alisema hivi: “[Yehova] umenipa uzima na fadhili zenye upendo [upendo mshikamanifu]; na uangalizi wako mwenyewe umeilinda roho yangu.” (Ayu. 10:12) Zaidi ya hayo, Ayubu aliwaonyesha wengine upendo, huku akitambua kwamba mtu yeyote anayekataa kuwaonyesha wanadamu wenzake upendo mshikamanifu ataacha kumwogopa na kumheshimu Mweza-Yote. (Ayu. 6:14) Watu wanaoshika utimilifu wanampenda Mungu na jirani.—Mt. 22:37-40.

21 Tunaweza kusitawisha upendo kuelekea Mungu kwa kusoma Neno lake kila siku na kutafakari juu ya mambo ambayo linafunua kumhusu. Tunaweza kusali kutoka moyoni na kumsifu Yehova na pia kumshukuru kwa ajili ya wema ambao ametutendea. (Flp. 4:6, 7) Tunaweza kumwimbia Yehova na kufaidika kwa kushirikiana kwa ukawaida na watu wake. (Ebr. 10:23-25) Pia, upendo wetu kwa Mungu utaongezeka tunaposhiriki katika huduma na kutangaza “habari njema za wokovu wake.” (Zab. 96:1-3) Katika njia hizo, tunaweza kudumisha utimilifu, kama alivyofanya mtunga-zaburi ambaye aliimba hivi: “Kumkaribia Mungu ni kwema kwangu. Nimeweka kimbilio langu katika Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.”—Zab. 73:28.

22, 23. Tukiwa watu wanaounga mkono enzi kuu ya Yehova, utendaji wetu unafanana jinsi gani na utendaji wa wale walioshika utimilifu zamani?

22 Kwa karne nyingi, Yehova amewapa watu wanaoshika utimilifu migawo mingi mbalimbali. Noa alijenga safina na alikuwa “mhubiri wa uadilifu.” (2 Pet. 2:5) Yoshua aliwaongoza Waisraeli kuingia katika Nchi ya Ahadi, lakini alifanikiwa kwa sababu tu alisoma ‘kitabu cha sheria mchana na usiku’ na kutenda kulingana nacho. (Yos. 1:7, 8) Wakristo wa karne ya kwanza walifanya wanafunzi na walikutana kwa ukawaida ili kujifunza Maandiko.—Mt. 28:19, 20.

23 Tunaunga mkono enzi kuu ya Yehova na kudumisha utimilifu wetu kwa kuhubiri uadilifu, kufanya wanafunzi, kufuata mashauri ya Maandiko, na kukusanyika pamoja na waamini wenzetu katika mikutano na makusanyiko. Utendaji huo mbalimbali unatusaidia kuwa jasiri, wenye nguvu kiroho, na kufanikiwa katika kufanya mapenzi ya Mungu. Hatuwezi kushindwa kufanya hivyo kwa sababu tunategemezwa na Baba yetu wa mbinguni na Mwana wake. (Kum. 30:11-14; 1 Fal. 8:57) Zaidi ya hayo, tunategemezwa na “ushirika mzima wa akina ndugu,” ambao pia wanatembea katika utimilifu na kumheshimu Yehova akiwa Bwana wao Mwenye Enzi Kuu.—1 Pet. 2:17.

Ungesema Nini?

• Tunapaswa kuwa na maoni gani kuhusu viwango vya Yehova vya maadili?

• Ni sifa gani za Ayubu ambazo hasa zinakuvutia?

• Kama inavyoonyeshwa katika Ayubu 31:29-37, Ayubu alijiendesha jinsi gani?

• Kwa nini tunaweza kudumisha utimilifu wetu kwa Mungu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 29]

Ayubu alidumisha utimilifu wake kwa Yehova. Sisi pia tunaweza!

[Picha katika ukurasa wa 32]

Tunaweza kudumisha utimilifu wetu!