Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vijana—Msikubali Kusongwa na Marafiki

Vijana—Msikubali Kusongwa na Marafiki

Vijana—Msikubali Kusongwa na Marafiki

“Maneno yenu na yawe . . . yenye kukolezwa chumvi, ili mjue jinsi mnavyopaswa kumjibu kila mtu.”—KOL. 4:6.

1, 2. Vijana wengi wanahisi namna gani kuhusu kuwa tofauti na wengine, na kwa nini?

BILA shaka, umesikia usemi “kushinikizwa,” “kubanwa” au “kusongwa na marafiki,” lakini pia umejionea jambo hilo wewe mwenyewe. Labda wakati fulani umewahi kusukumwa ufanye jambo ambalo unajua ni kosa. Unahisi namna gani jambo kama hilo linapotokea? Christopher aliye na umri wa miaka 14 anasema hivi: “Nyakati nyingine ninatamani tu nitoweke, au labda niwe kama wanafunzi wenzangu ili nisionekane kuwa tofauti nao.”

2 Je, vijana wenzako wana uvutano wenye nguvu juu yako? Ikiwa ndivyo, ni kwa nini? Je, huenda ni kwa sababu unataka wakukubali? Tamaa hiyo si mbaya nyakati nyingine. Hata watu wazima wanataka kukubaliwa na wenzao. Hakuna mtu anayependa kuchukiwa, awe kijana au mzee. Hata hivyo, ukweli ni kwamba mara nyingi ukijitahidi kufanya mambo yaliyo sawa utachukiwa na watu fulani. Hata Yesu alikabiliana na hali hiyo. Ingawa hivyo, sikuzote Yesu alifanya jambo lililo sawa. Hata ingawa watu fulani walimfuata na kuwa wanafunzi wake, wengine walimdharau Mwana wa Mungu na ‘kumhesabu kuwa asiye na maana.’—Isa. 53:3.

Msongo wa Kuwa Kama Marafiki Wako Una Nguvu Nyingi Kadiri Gani?

3. Kwa nini ni kosa kufuata viwango vya vijana wenzako?

3 Nyakati nyingine, unaweza kushawishiwa kufuata viwango vya vijana wenzako kwa sababu tu unataka wakukubali. Hilo lingekuwa kosa. Wakristo hawapaswi ‘kuwa watoto wachanga, wanaorushwa huku na huku kama kwa mawimbi.’ (Efe. 4:14) Ni rahisi kwa watoto wadogo kushawishiwa na wengine. Hata hivyo, ukiwa kijana unaelekea kuwa mtu mzima. Hivyo, ukiamini kwamba kufuata viwango vya Yehova ni jambo zuri kwako, utafaidika kwa kuishi kulingana na usadikisho wako. (Kum. 10:12, 13) Kutenda kinyume na hilo kungeonyesha kwamba umeshindwa kuongoza maisha yako. Ukweli ni kwamba unapokubali kusongwa na wengine, unakuwa kama kitu cha kuchezewa kinachoongozwa na wengine.—Soma 2 Petro 2:19.

4, 5. (a) Haruni alishindwa jinsi gani baada ya kusongwa na Waisraeli wenzake, na ni mambo gani ambayo unaweza kujifunza kutokana na hilo? (b) Vijana wenzako wanaweza kutumia njia gani mbalimbali ili kujaribu kukusonga?

4 Pindi moja, Haruni ndugu ya Musa, alishindwa kubaki imara aliposongwa na wengine. Waisraeli walipomsukuma awatengenezee mungu, alifanya hivyo. Haruni hakuwa mwoga. Hapo mwanzoni, alikuwa pamoja na Musa walipokutana uso kwa uso na Farao, ambaye alikuwa mtu mwenye mamlaka zaidi huko Misri. Kisha Haruni akazungumza kwa ujasiri na kumtangazia ujumbe wa Mungu. Lakini Waisraeli wenzake walipomsonga na kumbana, Haruni alishindwa. Kusongwa na marafiki ni jambo lenye nguvu kama nini! Ilikuwa rahisi zaidi kwa Haruni kusimama mbele ya mfalme wa Misri kuliko kukataa kusongwa na Waisraeli wenzake.—Kut. 7:1, 2; 32:1-4.

5 Kama mfano wa Haruni unavyoonyesha, kusongwa na marafiki si jambo linalowapata vijana tu, wala si tatizo linalowapata wale tu walio na mwelekeo wa kufanya mabaya. Hata watu ambao wanataka kufanya yaliyo sawa, kutia ndani wewe, wanaweza kusongwa na marafiki. Vijana wenzako wanaweza kukushawishi ufanye makosa kwa kukuchochea ufanye jambo hatari, kukushtaki kwa uwongo, au kukudhihaki. Hata ujaribiwe katika njia gani, ni vigumu kukabiliana na msongo wa marafiki. Ili ushinde hali hiyo ni lazima kwanza ujitahidi kusadiki mambo unayoamini.

“Endeleeni Kuthibitisha Ninyi Wenyewe Jinsi Mlivyo”

6, 7. (a) Kwa nini ni jambo la maana kusadiki mambo unayoamini, na unaweza kusitawisha usadikisho jinsi gani? (b) Ni maswali gani ambayo unaweza kujiuliza ili utie nguvu usadikisho wako?

6 Ili ushinde msongo wa marafiki, ni lazima kwanza usadiki kwamba mambo unayoamini na viwango unavyofuata vinafaa. (Soma 2 Wakorintho 13:5.) Usadikisho utakusaidia kuwa jasiri ikiwa wewe ni mwoga. (2 Tim. 1:7, 8) Lakini hata ikiwa kwa kawaida mtu ni jasiri, inaweza kuwa vigumu sana kwake kutetea jambo ambalo anaamini kwa moyo nusunusu. Basi, kwa nini usijithibitishie kwamba mambo ambayo umefundishwa kutoka katika Biblia ni ya kweli? Anza kwa kuchunguza mambo ya msingi. Kwa mfano, unaamini kwamba kuna Mungu na umesikia watu wengine wakieleza kwa nini wanaamini kwamba kuna Mungu. Hivyo basi, jiulize, ‘Ni nini kinachonithibitishia mimi kwamba kuna Mungu?’ Kusudi la swali hilo si kukufanya uwe na mashaka bali ni kuitia nguvu imani yako. Vivyo hivyo, jiulize, ‘Ninajua jinsi gani kwamba Maandiko yameongozwa na roho ya Mungu?’ (2 Tim. 3:16) ‘Kwa nini nina hakika kwamba hizi ndizo “siku za mwisho”?’ (2 Tim. 3:1-5) ‘Ni nini kinachofanya niamini kwamba kufuata viwango vya Yehova ni kwa faida yangu?’—Isa. 48:17, 18.

7 Huenda ukasitasita kujiuliza maswali kama hayo kwa sababu unaogopa kwamba hutapata majibu. Hata hivyo, kufanya hivyo ni kama kusitasita kuangalia kifaa kinachoonyesha kiasi cha mafuta katika tangi la gari lako, kwa sababu unaogopa kwamba tangi halina mafuta! Ikiwa tangi halina mafuta, unahitaji kujua ili uchukue hatua inayofaa. Vivyo hivyo, ni jambo bora kabisa kwako kutambua mambo ambayo unaona kwamba huyasadiki kisha ujitahidi kufanya marekebisho.—Mdo. 17:11.

8. Eleza jinsi unavyoweza kutia nguvu uhakika wako katika hekima ya amri ya Mungu ya kujiepusha na uasherati.

8 Fikiria mfano huu. Biblia inakuhimiza ‘ukimbie uasherati.’ Jiulize, ‘Kwa nini ni jambo la hekima kufuata amri hiyo?’ Fikiria sababu zote ambazo zinawafanya vijana wenzako wajiendeshe kwa njia hiyo. Fikiria pia sababu mbalimbali ambazo zinaonyesha kwamba mtu anayefanya uasherati “anautendea dhambi mwili wake mwenyewe.” (1 Kor. 6:18) Sasa chunguza sababu, na ujiulize hivi: ‘Ni njia gani bora zaidi ya kufuata? Je, kweli inafaa kujihusisha na mwenendo mbaya kingono?’ Fikiria jambo hilo kwa undani zaidi, na ujiulize hivi: ‘Ningehisi namna gani ikiwa ningetumbukia katika upotovu wa maadili katika ngono?’ Huenda ukakubaliwa mara moja na vijana wenzako, lakini ungehisi namna gani baadaye ukiwa pamoja na wazazi wako au Wakristo wenzako katika Jumba la Ufalme? Ungehisi namna gani ikiwa ungejaribu kusali kwa Mungu? Je, ungekuwa tayari kupoteza msimamo safi mbele za Mungu ili uwapendeze tu wanafunzi wenzako?

9, 10. Kuwa na uhakika katika mambo unayoamini kutakusaidia jinsi gani kuwa na uhakika zaidi unapokuwa na vijana wenzako?

9 Ikiwa wewe ni kijana anayebalehe, uko katika kipindi cha maisha ambapo ‘nguvu zako za kufikiri’ zinakua kuliko wakati mwingine wowote. (Soma Waroma 12:1, 2.) Tumia kipindi hicho kufikiria kwa uzito kwa nini kuwa Shahidi wa Yehova ni jambo la maana kwako binafsi. Kutafakari kwa njia hiyo kutakusaidia kuwa na uhakika katika mambo unayoamini. Kisha, utakaposongwa na marafiki, utajibu papo hapo kwa uhakika. Utahisi kama dada mmoja kijana Mkristo, anayesema hivi: “Ninapokataa kusongwa na marafiki, ninawaonyesha wengine msimamo wangu. Hii si ‘dini fulani’ tu. Ni msingi wa fikira zangu, miradi, maadili na maisha yangu yote.”

10 Ndiyo, unahitaji kujitahidi ili uendelee kushikamana na mambo ambayo unajua kwamba ni sawa. (Luka 13:24) Na huenda ukajiuliza kama kuna faida yoyote ya kufanya hivyo. Lakini kumbuka jambo hili: Ikiwa una wasiwasi au unaaibika kwa sababu ya msimamo wako, wengine watatambua jambo hilo, na huenda wakakusonga hata zaidi. Hata hivyo, ukizungumza kwa usadikisho, huenda ukashangaa kuona vijana wenzako wakiacha papo hapo kukusonga.—Linganisha na Luka 4:12, 13.

‘Tafakari ili Ujibu’

11. Kuna faida gani ya kujitayarisha kukabiliana na msongo wa marafiki?

11 Hatua nyingine ya maana katika kushinda msongo wa marafiki ni kujitayarisha. (Soma Methali 15:28.) Kujitayarisha kunamaanisha kufikiria mapema hali ambazo inaelekea kwamba zitatokea. Nyakati nyingine kujitayarisha mapema kukabiliana na hali fulani kunaweza kuzuia mzozano mkubwa. Kwa mfano, tuseme unaona kikundi cha wanafunzi wenzako wakitembea mbele yako huku wakivuta sigara. Kuna uwezekano gani kwamba watakupa sigara uvute? Ukitambua kwamba tatizo litatokea, unaweza kufanya nini? Andiko la Methali 22:3 linasema hivi: “Mtu mwerevu ni yule ambaye ameona msiba na kujificha.” Ukifuata njia tofauti, huenda ukafaulu kuepuka kukutana nao kabisa. Hatua hiyo haionyeshi kwamba wewe ni mwoga; ni jambo la hekima kufanya hivyo.

12. Unaweza kufanya nini ili kukomesha msongo?

12 Namna gani ikiwa huwezi kuepuka hali fulani? Tuseme kijana mwenzako anakuuliza hivi kwa mshangao: “Bado wewe ni bikira?” Siri ni kufuata himizo la Wakolosai 4:6: “Maneno yenu na yawe yenye neema sikuzote, yenye kukolezwa chumvi, ili mjue jinsi mnavyopaswa kumjibu kila mtu.” Kama andiko hilo linavyoonyesha, utajibu swali hilo kulingana na hali zilizopo. Huenda huhitaji kuanza kutoa hotuba ndefu ya Biblia. Labda itatosha tu kutoa jibu rahisi lililo thabiti. Kwa mfano, unapojibu swali hilo kuhusu kuwa bikira, unaweza kusema tu, “Ndiyo, mimi ni bikira,” au, “Kwa kweli hilo ni jambo la kibinafsi.”

13. Utambuzi unaweza kukusaidia jinsi gani unapomjibu kijana mwenzako anayekudhihaki?

13 Mara nyingi Yesu alitoa jibu fupi alipoona kwamba hakuna faida ya kusema maneno mengi. Hata alipoulizwa maswali na Herode, Yesu hakusema lolote. (Luka 23:8, 9) Mara nyingi, kunyamaza ni njia nzuri ya kukabiliana na maswali yanayokusudiwa kukuaibisha. (Met. 26:4; Mhu. 3:1, 7) Kwa upande mwingine, huenda ukatambua kwamba mtu fulani anashangazwa kwa unyoofu na mwenendo wako—kwa mfano, kuhusu maadili katika ngono—hata ikiwa mwanzoni mtu huyo alikutukana. (1 Pet. 4:4) Katika kisa hicho, huenda ikafaa kueleza kwa undani zaidi kuhusu msimamo wako unaotegemea Biblia. Ikiwa ndivyo ilivyo, usisitesite kwa sababu ya woga. Sikuzote uwe “tayari kujitetea.”—1 Pet. 3:15.

14. Unaweza kumsonga au kumbana jinsi gani kwa busara mtu anayekubana?

14 Katika hali fulani, unaweza kuwasonga au kuwabana wale wanaokubana. Hata hivyo, ni lazima ujaribu kufanya hivyo kwa busara. Kwa mfano, ikiwa mwanafunzi mwenzako anakushawishi uvute sigara, unaweza kusema, “Hapana sitaki” kisha useme, “Nilifikiri kwamba una akili ya kutosha kutovuta sigara!” Je, umeona jinsi ya kumsonga au kumbana mtu anayekubana? Badala ya kulazimika kueleza kwa nini huvuti sigara, kijana mwenzako analazimika kufikiria kwa nini anavuta sigara. *

15. Ni wakati gani inapofaa kuondoka wakati vijana wenzako wanapojaribu kukusonga, na kwa nini?

15 Namna gani ikiwa unaendelea kusongwa hata baada ya kujitetea? Katika hali kama hiyo, jambo bora ni kuondoka. Kadiri unavyoendelea kukaa ndivyo itakavyokuwa rahisi zaidi kwako kulegeza msimamo wako kwa njia fulani. Kwa hiyo, ondoka mahali hapo. Unaweza kufanya hivyo bila kuhisi kwamba umeshindwa. Ukweli ni kwamba wewe ndiye uliyechukua hatua. Ulikataa kuongozwa vibaya na marafiki wako, na ulifanya moyo wa Yehova ushangilie.—Met. 27:11.

Uwe na ‘Mipango Inayoleta Faida’

16. Vijana fulani wanaodai kuwa Wakristo wanaweza jinsi gani kukusonga?

16 Nyakati nyingine, huenda vijana fulani wanaodai kuwa watumishi wa Yehova wakakusonga kufanya mambo ambayo hayafai. Kwa mfano, namna gani ukifika kwenye tafrija ambayo imepangwa na kijana kama huyo kisha utambue kwamba hakuna mtu mzima anayesimamia? Au namna gani ikiwa kijana anayedai kuwa Mkristo analeta pombe kwenye tafrija, na wewe na wengine walio hapo hamjafikisha umri ambao serikali inamkubali mtu kunywa pombe? Hali mbalimbali zinaweza kutokea ambapo utahitaji kufuata dhamiri yako iliyozoezwa na Biblia. Kijana mmoja Mkristo ambaye ni tineja anasema hivi: “Mimi na dada yangu tuliondoka katika jumba la sinema kwa sababu sinema hiyo ilikuwa imejaa maneno machafu. Wengine katika kikundi chetu waliamua kubaki. Wazazi wetu walitusifu kwa sababu ya hatua ambayo tulichukua. Hata hivyo, wengine katika kikundi chetu walikasirika kwa sababu tulifanya waonekane kuwa wabaya.”

17. Ni hatua gani ambazo unaweza kuchukua ili uendelee kushikamana na viwango vya Mungu unapohudhuria tafrija?

17 Kama mfano uliotajwa unavyoonyesha, kufuata dhamiri yako iliyozoezwa na Biblia kunaweza kufanya uonekane kuwa mbaya. Lakini endelea kushikamana na yale ambayo unaamini kwamba ni sawa. Uwe tayari. Ikiwa unaenda kwenye tafrija, uwe na mpango wa kutoka ikiwa mambo hayataenda jinsi ulivyotazamia. Vijana fulani wanakubaliana na wazazi wao kwamba waje mapema kuwachukua kwenye tafrija watakapowapigia simu. (Zab. 26:4, 5) ‘Mipango kama hiyo inaleta faida.’—Met. 21:5.

“Shangilia Katika Ujana Wako”

18, 19. (a) Kwa nini unaweza kuwa na hakika kwamba Yehova anataka uwe na furaha? (b) Mungu anahisi namna gani kuhusu wale wanaoshinda msongo wa marafiki?

18 Yehova alikuumba ukiwa na uwezo wa kufurahia maisha, na anataka uwe na furaha. (Soma Mhubiri 11:9.) Kumbuka kwamba kile ambacho vijana wenzako wengi wanafanya ni ‘kufurahia dhambi kwa muda tu.’ (Ebr. 11:25) Mungu wa kweli anataka upate kitu bora zaidi kuliko hicho. Anataka uwe na furaha milele. Hivyo, unaposhawishiwa kufanya jambo ambalo unajua ni baya machoni pa Mungu, kumbuka kwamba mwishowe, mambo ambayo Yehova anataka ufanye ni kwa faida yako sikuzote.

19 Ukiwa kijana, unahitaji kujua kwamba hata ukikubaliwa na vijana wenzako, inaelekea kwamba miaka mingi kutoka sasa wengi wao hata hawatakumbuka jina lako. Kinyume na hilo, unaposhinda msongo wa marafiki, Yehova anaona jambo hilo, na hatakusahau kamwe au kusahau uaminifu wako. ‘Atakufungulia malango ya mbinguni na kukumwagia baraka hata kusiwe na uhitaji tena.’ (Mal. 3:10) Zaidi ya hayo, anakupa kwa ukarimu roho yake takatifu ili ikupe msaada wowote ule ambao unahitaji sasa. Ndiyo, Yehova anaweza kukusaidia kushinda msongo wa vijana wenzako!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 14 Ona chati yenye kichwa “Kukabiliana na Mkazo” katika kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2, ukurasa wa 132 na 133.

Je, Unakumbuka?

• Kusongwa na marafiki kunaweza kuwa na nguvu kadiri gani?

• Usadikisho unahusika jinsi gani katika kushinda msongo wa marafiki?

• Unaweza kujitayarisha jinsi gani kukabiliana na msongo wa marafiki?

• Unajua jinsi gani kwamba Yehova anathamini uaminifu wako?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 8]

Kwa nini Haruni alikubali kutengeneza yule ndama wa dhahabu?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Uwe tayari—amua mapema mambo ambayo utasema