Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vijana—Mwongozwe na Neno la Mungu

Vijana—Mwongozwe na Neno la Mungu

Vijana—Mwongozwe na Neno la Mungu

“Jipatie hekima, jipatie uelewaji.”—MET. 4:5.

1, 2. (a) Ni nini kilichomsaidia mtume Paulo kukabiliana na vita vilivyokuwa ndani yake? (b) Unaweza kupata jinsi gani hekima na uelewaji?

“NINAPOTAKA kufanya yaliyo sawa, yaliyo mabaya yapo pamoja nami.” Je, unajua ni nani aliyesema maneno hayo? Si mwingine ila ni mtume Paulo. Ingawa Paulo alimpenda Yehova, nyakati nyingine alipambana ili afanye yaliyo sawa. Alihisi namna gani kuhusu vita hivyo vilivyokuwa ndani yake? Aliandika hivi: “Maskini mimi!” (Rom. 7:21-24) Je, unaelewa jinsi Paulo alivyohisi? Je, nyakati nyingine unaona kwamba ni vigumu kufanya jambo lililo sawa? Je, hilo linakufanya uhisi umevunjika moyo kama Paulo? Ikiwa ndivyo, usikate tamaa. Paulo alifanikiwa kushinda matatizo aliyokabili, na wewe pia unaweza kuyashinda.

2 Paulo alifanikiwa kwa sababu alikubali kuongozwa na “maneno yenye afya.” (2 Tim. 1:13, 14) Matokeo ni kwamba alipata hekima na uelewaji ambao alihitaji ili kukabiliana na matatizo na kufanya maamuzi mazuri. Yehova Mungu anaweza kukusaidia kupata hekima na uelewaji. (Met. 4:5) Ametupatia mashauri bora kabisa katika Neno lake, Biblia. (Soma 2 Timotheo 3:16, 17.) Chunguza jinsi unavyoweza kufaidika na kanuni zinazopatikana katika Maandiko unaposhughulika na wazazi wako, unapopanga jinsi ya kutumia pesa, na unapokuwa peke yako.

Kuongozwa na Neno la Mungu Katika Familia

3, 4. Kwa nini huenda ikawa vigumu kwako kutii sheria za wazazi wako, na kwa nini wazazi wanaweka sheria?

3 Je, unaona kwamba ni vigumu kuishi kulingana na sheria za wazazi wako? Kwa nini unahisi hivyo? Huenda sababu moja ni kwamba unatamani kupata uhuru wa kadiri fulani. Ni jambo la kawaida kuhisi hivyo. Ni hatua ya kukomaa na kuwa mtu mzima. Hata hivyo, unapokuwa nyumbani una wajibu wa kuwatii wazazi wako.—Efe. 6:1-3.

4 Inaweza kuwa rahisi zaidi kwako kutii sheria na matakwa ya wazazi wako ikiwa utasitawisha maoni yanayofaa kuelekea sheria na matakwa hayo. Ni kweli kwamba huenda nyakati nyingine ukahisi kama Brielle * mwenye umri wa miaka 18, ambaye alisema hivi kuhusu wazazi wake: “Wamesahau kabisa jinsi walivyohisi walipokuwa na umri kama wangu. Hawataki nitoe maoni yangu, nifanye maamuzi, au niwe mtu mzima.” Kama Brielle, huenda ukahisi kwamba wazazi wako wanakunyima uhuru zaidi kuliko unavyotaka. Hata hivyo, wazazi wako wanaweka sheria hasa kwa sababu wanakujali. Kwa kuongezea, wazazi Wakristo wanajua kwamba watatoa hesabu mbele za Yehova kuhusu jinsi wanavyokutunza.—1 Tim. 5:8.

5. Unaweza kufaidika jinsi gani ukitii wazazi wako?

5 Kwa kweli, kutii sheria za wazazi wako ni kama kulipa deni ambalo unadaiwa na benki—kadiri unavyotegemeka zaidi katika kulipa deni, ndivyo wasimamizi wa benki watakavyokuwa tayari zaidi kukupa deni. Vivyo hivyo, wazazi wako wanakudai heshima na utii. (Soma Methali 1:8.) Kadiri unavyokuwa mtiifu zaidi, ndivyo inavyoelekea kwamba wazazi wako watakupa uhuru zaidi. (Luka 16:10) Bila shaka, ukiendelea kuvunja sheria, usishangae ikiwa wazazi wako watapunguza au hata kufunga “mpango wa kukupa deni” la mfano, yaani, uhuru.

6. Wazazi wanaweza kuwasaidia jinsi gani vijana kuwa watiifu?

6 Njia moja ambayo wazazi wanaweza kuwasaidia vijana wao watii sheria ambazo wanaweka ni kupitia mfano wao. Wazazi wanapaswa kuonyesha kwamba sheria za Mungu ni zenye usawaziko kwa kutii matakwa ya Yehova kwa kupenda. Hilo litafanya iwe rahisi zaidi kwa vijana kuwa na maoni kama hayo kuelekea sheria za wazazi wao. (1 Yoh. 5:3) Zaidi ya hayo, Biblia inataja pindi fulani ambapo Yehova aliwapa watumishi wake nafasi ya kutoa maoni yao kuhusu mambo fulani. (Mwa. 18:22-32; 1 Fal. 22:19-22) Je, kuna nyakati fulani ambazo wazazi wanaweza kuwapa watoto wao nafasi ya kutoa maelezo kuhusu mambo mbalimbali?

7, 8. (a) Vijana fulani wanakabiliana na tatizo gani? (b) Unapaswa kutambua jambo gani ambalo litakusaidia kufaidika na nidhamu?

7 Vijana wanaweza pia kukabiliana na tatizo lingine la kufikiri kwamba wazazi wao wanawachambua-chambua bila sababu. Huenda nyakati nyingine ukahisi kama kijana anayeitwa Craig, ambaye alisema hivi: “Mama yangu alikuwa kama polisi wa upelelezi—sikuzote akitafuta-tafuta makosa yangu.”

8 Mara nyingi tunatiwa nidhamu au kurekebishwa tunapochambuliwa. Biblia inakubali kwamba ni vigumu kukubali nidhamu, hata inapotolewa kwa haki kabisa. (Ebr. 12:11) Ni nini kinachoweza kukusaidia ili ufaidike na nidhamu unayopewa? Jambo la maana unalopaswa kukumbuka ni kwamba inaelekea wazazi wako wanakushauri kwa sababu wanachochewa na upendo wao kukuelekea. (Met. 3:12) Wanataka kukusaidia ili usiwe na tabia mbaya na kukusaidia usitawishe tabia nzuri. Inaelekea wazazi wako wanatambua kwamba ikiwa hawatakurekebisha, watakuwa wakionyesha kwamba wanakuchukia! (Soma Methali 13:24.) Pia, unapaswa kuelewa kwamba kufanya makosa ni sehemu ya kujifunza. Hivyo basi, unaporekebishwa kwa nini usitafute hekima katika maneno unayoambiwa? “Kuwa [na hekima] kama mapato ni bora kuliko kuwa na mapato ya fedha na kuwa nayo kama mazao ni bora kuliko dhahabu yenyewe.”—Met. 3:13, 14.

9. Vijana wanaweza kufanya nini badala ya kukazia fikira jambo ambalo wanahisi kwamba wameonewa?

9 Hata hivyo, nyakati nyingine wazazi wanakosea. (Yak. 3:2) Wanapokutia nidhamu, huenda pindi fulani wakazungumza bila kufikiri. (Met. 12:18) Ni nini kinachoweza kufanya wazazi wako watende kwa njia hiyo? Huenda wanakabiliana na mkazo, au wanaweza kufikiri kwamba makosa yako yanaonyesha kuwa wameshindwa. Badala ya kukazia fikira jambo ambalo unahisi kwamba umeonewa, kwa nini usionyeshe unathamini jitihada zao za kutoka moyoni za kukusaidia? Uwezo wa kukubali nidhamu utakusaidia sana utakapokuwa mtu mzima.

10. Unaweza kufanya nini ili iwe rahisi zaidi kwako kutii sheria na kukubali kurekebishwa na wazazi wako?

10 Je, ungependa iwe rahisi zaidi kwako kutii sheria na kukubali kurekebishwa na wazazi wako? Ikiwa ndivyo, unahitaji kuboresha uwezo wako wa kuwasiliana. Unaweza kufanya hivyo jinsi gani? Hatua ya kwanza ni kusikiliza. Biblia inasema hivi: ‘Uwe mwepesi kuhusu kusikia, si mwepesi wa kusema, si mwepesi wa ghadhabu.’ (Yak. 1:19) Badala ya kufanya haraka kujitetea, jaribu kuzuia hisia zako na usikilize mambo ambayo wazazi wako wanasema. Kazia fikira mambo wanayosema, si jinsi wanavyoyasema. Kisha, kwa maneno yako mwenyewe waambie wazazi wako kwa heshima mambo ambayo wamekuambia. Ukifanya hivyo utawahakikishia kwamba ulisikia mambo waliyosema. Namna gani ikiwa unataka kueleza kwa nini ulisema au kutenda jambo fulani? Mara nyingi, ni jambo la hekima ‘kuzuia midomo yako’ mpaka unapomaliza kufanya jambo ambalo umeambiwa na wazazi wako. (Met. 10:19) Wazazi wako wakiona kwamba umewasikiliza, watakuwa tayari zaidi kukusikiliza. Unapotenda kwa njia hiyo ya ukomavu, unathibitisha kwamba unaongozwa na Neno la Mungu.

Kuongozwa na Neno la Mungu Unapopanga Matumizi ya Pesa

11, 12. (a) Neno la Mungu linatutia moyo tufanye nini kuhusu pesa, na kwa nini? (b) Wazazi wako wanaweza kukusaidia jinsi gani kupanga matumizi ya pesa?

11 Biblia inasema kwamba “pesa ni ulinzi.” Lakini mstari huohuo unaonyesha kwamba hekima ni yenye thamani zaidi kuliko pesa. (Mhu. 7:12) Neno la Mungu linatutia moyo tuheshimu pesa, lakini tusizipende. Kwa nini unapaswa kuepuka kusitawisha upendo wa pesa? Fikiria mfano huu: Kisu chenye makali ni kifaa cha maana sana kwa mpishi mwenye ustadi. Lakini kisu hichohicho kikiwa katika mikono ya mtu asiye mwangalifu au asiyejali kinaweza kusababisha madhara makubwa. Vivyo hivyo, pesa zinapotumiwa kwa ustadi, zinaweza kuleta faida. Hata hivyo, mara nyingi wale ambao “wameazimia kuwa matajiri” wanapoteza marafiki, wanaharibu mahusiano ya kifamilia, na hata uhusiano wao na Mungu. Matokeo ni kwamba wanajichoma wenyewe “kila mahali kwa maumivu mengi.”—Soma 1 Timotheo 6:9, 10.

12 Unaweza kujifunza jinsi gani kupanga kwa busara matumizi ya pesa? Kwa nini usiwaombe wazazi wako mashauri kuhusu kupanga bajeti au jinsi ya kutumia pesa zako? Mfalme Sulemani aliandika hivi: “Mtu mwenye hekima atasikiliza na kupata mafundisho zaidi, naye mtu mwenye uelewaji ndiye anayepata mwongozo stadi.” (Met. 1:5) Mwanamke kijana anayeitwa Anna aliomba mwongozo stadi kutoka kwa wazazi wake. Anasema hivi: “Baba yangu alinifundisha jinsi ya kupanga bajeti, na akanionyesha kwa nini ni jambo la maana kupanga vizuri matumizi ya pesa za familia.” Mama ya Anna alimfundisha pia mambo ya maana. Anna anasema hivi: “Alinionyesha kwa nini ni jambo la maana kulinganisha bei kabla ya kununua kitu.” Anna amefaidika jinsi gani? Anajibu hivi: “Sasa ninajua jinsi ya kutumia pesa zangu vizuri. Ninapanga kwa hekima jinsi nitakavyotumia pesa zangu, hivyo nina uhuru na amani ya akili inayotokana na kuepuka madeni yasiyo ya lazima.”

13. Unaweza kujitia nidhamu jinsi gani inapohusu kutumia pesa?

13 Unaweza kwa urahisi kujikuta ukiwa na madeni mengi ikiwa utanunua vitu bila kupanga au kutumia pesa ili kuwafurahisha tu marafiki wako. Ni nini kinachoweza kukusaidia kuepuka mitego hiyo? Ni lazima ujifunze kujitia nidhamu inapohusu kutumia pesa. Hivyo ndivyo anavyofanya Ellena ambaye ana umri wa miaka 20 na kitu. Anasema hivi: “Ninapoenda kutembea pamoja na marafiki ninapanga mapema na kutenga kiasi cha pesa ambacho nitatumia. . . . Pia, ninaona kwamba ni jambo la hekima kwenda kununua vitu nikiwa pamoja na marafiki wangu ambao wanatumia pesa kwa uangalifu na ambao watanitia moyo kulinganisha bei za vitu badala ya kununua kitu cha kwanza ninachopata dukani.”

14. Kwa nini unapaswa kujilinda na “nguvu za udanganyifu za utajiri”?

14 Kupata pesa na kupanga jinsi ya kuzitumia ni sehemu ya maana katika maisha. Hata hivyo, Yesu alisema kwamba watu “wanaotambua uhitaji wao wa kiroho” ndio wanaopata furaha ya kweli. (Mt. 5:3) Alionya kwamba hali ya mtu ya kupendezwa na mambo ya kiroho inaweza kusongwa na mambo kama vile “nguvu za udanganyifu za utajiri.” (Marko 4:19) Hivyo basi, ni jambo la maana kama nini kwako kukubali kuongozwa na Neno la Mungu na kudumisha maoni yanayofaa kuelekea pesa!

Kuongozwa na Neno la Mungu Unapokuwa Peke Yako

15. Inaelekea ushikamanifu wako kwa Mungu utajaribiwa zaidi wakati gani?

15 Unafikiri ushikamanifu wako kwa Mungu utajaribiwa zaidi wakati gani—je, ni wakati unapokuwa na wengine au unapokuwa peke yako? Ni kweli kwamba unapokuwa shuleni au kazini, inaelekea kwamba ulinzi wako wa kiroho unakuwa imara. Unakuwa macho kuona hatari yoyote ya kiroho. Lakini unapostarehe na kuacha kujilinda ndipo unapokuwa katika hatari kubwa zaidi ya kushambuliwa kiadili.

16. Kwa nini unapaswa kumtii Yehova hata unapokuwa peke yako?

16 Kwa nini unapaswa kumtii Yehova hata unapokuwa peke yako? Kumbuka jambo hili: Unaweza kuumiza hisia za Yehova au kuufanya moyo wake ushangilie. (Mwa. 6:5, 6; Met. 27:11) Yehova anafurahishwa au kuumizwa na matendo yako kwa sababu ‘anakujali.’ (1 Pet. 5:7) Anataka umsikilize ili ujifaidi mwenyewe. (Isa. 48:17, 18) Watumishi fulani wa Yehova katika Israeli la kale walipopuuza mashauri yake, walimfanya ahisi uchungu. (Zab. 78:40, 41) Kwa upande mwingine, Yehova alimpenda sana nabii Danieli, kwa kuwa malaika alimwita “mtu mwenye kutamanika sana.” (Dan. 10:11) Kwa nini? Kwa sababu Danieli aliendelea kuwa mshikamanifu kwa Mungu si mbele ya watu tu bali pia akiwa peke yake.—Soma Danieli 6:10.

17. Ni maswali gani ambayo unaweza kujiuliza unapochagua burudani?

17 Ili uendelee kuwa mshikamanifu kwa Mungu unapokuwa peke yako, ni lazima usitawishe ‘nguvu zako za ufahamu ili kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia’ na kisha uzoeze nguvu hizo ‘kwa kuzitumia’ unapotenda kulingana na mambo unayojua kwamba ni sawa. (Ebr. 5:14) Kwa mfano, unapochagua muziki utakaosikiliza, sinema utakazotazama, au vituo vya Intaneti, mambo yafuatayo yatakusaidia kuchagua yaliyo sawa na kuepuka yaliyo makosa. Jiulize maswali au maulizo yafuatayo: ‘Je, habari hii itanitia moyo kuwa mwenye huruma nyororo au je, itanichochea nishangilie “msiba wa mwingine”?’ (Met. 17:5) ‘Je, itanisaidia “kupenda yaliyo mema” au je, itafanya iwe vigumu kwangu “kuchukia yaliyo mabaya”?’ (Amo. 5:15) Mambo unayofanya ukiwa peke yako yanafunua yale ambayo kwa kweli unathamini.—Luka 6:45.

18. Unapaswa kufanya nini ikiwa umekuwa ukifanya dhambi kwa siri, na kwa nini ufanye hivyo?

18 Unapaswa kufanya nini ikiwa umekuwa na mwenendo ambao unajua haufai? Kumbuka, “anayefunika makosa yake hatafanikiwa, lakini yeye anayeyaungama na kuyaacha ataonyeshwa rehema.” (Met. 28:13) Lingekuwa jambo lisilo la hekima kama nini kuendelea kufanya dhambi na ‘kuihuzunisha roho takatifu ya Mungu’! (Efe. 4:30) Kwa kweli una wajibu mbele za Mungu, mbele ya wazazi wako, na kwako mwenyewe kuungama kosa lolote. Kuhusiana na jambo hilo, “wanaume wazee wa kutaniko” wanaweza kukusaidia sana. Mwanafunzi Yakobo anasema hivi: “Nao wasali juu [ya mkosaji], wakimpaka mafuta katika jina la Yehova. Na sala ya imani itamponya huyo asiyejisikia vizuri, na Yehova atamwinua. Pia, ikiwa amefanya dhambi, atasamehewa.” (Yak. 5:14, 15) Ni kweli kwamba huenda hilo likatokeza aibu na labda matokeo yasiyopendeza. Lakini ukiwa na ujasiri wa kuomba msaada, utaepuka matatizo mengine zaidi na utapata kitulizo cha kuwa tena na dhamiri safi.—Zab. 32:1-5.

Furahisha Moyo wa Yehova

19, 20. Yehova anataka upate nini, lakini ni lazima ufanye nini?

19 Yehova ni Mungu “mwenye furaha,” na anataka uwe na furaha. (1 Tim. 1:11) Anapendezwa na wewe kikweli. Hata ikiwa hakuna mtu anayeona jinsi unavyojitahidi kufanya yaliyo sawa, yeye anaona. Hakuna kitu ambacho kimefichwa mbele za macho ya Yehova. Anaangalia, si ili apate makosa, bali ili akutie nguvu unapojitahidi kufanya mambo mazuri. “Macho [ya Mungu] yanaenda huku na huku duniani kote ili aonyeshe nguvu zake kwa ajili ya wale ambao moyo wao ni mkamilifu kumwelekea yeye.”—2 Nya. 16:9.

20 Kwa hiyo, kubali kuongozwa na Neno la Mungu, na ufuate mashauri yaliyomo. Ukifanya hivyo utapata hekima na uelewaji unaohitaji ili kushinda matatizo magumu na kufanya maamuzi magumu maishani. Utawafurahisha wazazi wako na Yehova, na pia utakuwa na maisha yenye furaha kwelikweli.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Majina yamebadilishwa.

Ungesema Nini?

• Vijana wanaweza kufanya nini ili wafaidike kwa kutii sheria na kukubali kurekebishwa na wazazi wao?

• Kwa nini ni jambo la maana kusitawisha maoni yanayofaa kuhusu pesa?

• Unaweza kuendelea jinsi gani kuwa mshikamanifu kwa Yehova hata unapokuwa peke yako?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 6]

Je, utaendelea kuwa mshikamanifu kwa Mungu unapokuwa peke yako?