Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Anasikiliza Kilio cha Mtu wa Hali ya Chini

Yehova Anasikiliza Kilio cha Mtu wa Hali ya Chini

Yehova Anasikiliza Kilio cha Mtu wa Hali ya Chini

KAMA Mfalme Sulemani mwenye hekima wa taifa la kale la Israeli alivyosema, ‘wakati na tukio lisilotazamiwa hutupata sote.’ (Mhu. 9:11) Msiba au jaribu lenye kuumiza linaweza kuvuruga kabisa maisha yetu. Kwa mfano, kifo cha ghafula cha mshiriki wa karibu wa familia kinaweza kusababisha maumivu makali sana moyoni. Kwa majuma na miezi mingi inayofuata, mtu anaweza kulemewa sana na hisia za huzuni na kuvunjika moyo. Anaweza kuchanganyikiwa sana na kuhisi kwamba hastahili kumfikia Yehova katika sala.

Mtu aliye katika hali kama hiyo anahitaji kutiwa moyo, kupendwa, na kuonyeshwa kwamba wengine wanamjali. Mtunga-zaburi Daudi aliimba maneno haya yanayotia moyo: “Yehova anawategemeza wote wanaoanguka, naye anawainua wote ambao wameinama chini.” (Zab. 145:14) Biblia inatuambia kwamba “macho [ya Yehova] yanaenda huku na huku duniani kote ili aonyeshe nguvu zake kwa ajili ya wale ambao moyo wao ni mkamilifu kumwelekea yeye.” (2 Nya. 16:9) Yehova anakaa “pamoja na mtu aliyepondwa na mwenye roho ya unyenyekevu, ili kuipa uhai roho ya watu wa hali ya chini na kuupa uhai moyo wa wale wanaopondwa.” (Isa. 57:15) Yehova anamtegemeza na kumfariji jinsi gani mtu aliyepondwa na mwenye roho ya unyenyekevu?

“Neno Linalosemwa Wakati Unaofaa”

Njia moja ambayo Yehova anatumia kutusaidia kwa wakati unaofaa ni kupitia undugu wa Kikristo. Wakristo wanahimizwa ‘waseme kwa kuzifariji nafsi zilizohuzunika.’ (1 The. 5:14) Maneno ya upendo na ya kujali yanayosemwa na waamini wenzake wenye huruma yanaweza kumtia mtu nguvu wakati wa shida na huzuni. Maneno yenye kufariji yanayosemwa hata katika mazungumzo mafupi yanaweza kumtia moyo sana mtu aliyeshuka moyo. Maneno hayo ya kujali yanaweza kusemwa na mtu fulani ambaye amevumilia maumivu kama hayo ya kiakili na kihisia. Au rafiki mwenye uzoefu sana katika maisha anaweza kusema maneno ya busara yenye kutia moyo. Kupitia njia hizo zinazofaa kabisa, Yehova anaweza kuitia nguvu roho ya mtu wa hali ya chini.

Fikiria kisa cha mzee Mkristo anayeitwa Alex, ambaye alikuwa ameoa karibuni lakini mke wake akafa kwa ghafula kutokana na ugonjwa usioweza kutibiwa. Mwangalizi mmoja anayesafiri mwenye huruma alichukua hatua ya kumwambia Alex maneno yanayofariji. Yeye pia alikuwa amefiwa na mke wake lakini alioa mke mwingine. Mwangalizi huyo anayesafiri alieleza jinsi alivyolemewa sana na hisia. Alijisikia vizuri alipokuwa na wengine katika huduma na katika mikutano ya kutaniko. Hata hivyo, aliporudi katika chumba chake na kufunga mlango alijisikia mpweke sana. Alex anasema hivi: “Nilipata faraja kama nini kujua kwamba hisia ambazo nilikuwa nazo zilikuwa za kawaida na wengine wamewahi kuhisi hivyo.” Bila shaka, “neno linalosemwa wakati unaofaa” linaweza kumfariji mtu na kumtegemeza wakati wa taabu.—Met. 15:23.

Mzee mwingine Mkristo, ambaye anawafahamu watu wengi ambao walifiwa na wenzi wao wa ndoa, alichochewa kuzungumza na Alex maneno machache yenye kutia moyo. Akiwa na hisia-mwenzi, alimwambia kwa upendo kwamba Yehova anajua jinsi tunavyohisi na tunachohitaji. Ndugu huyo alisema hivi: “Ikiwa katika miezi na miaka inayokuja, utahisi kwamba unahitaji mwenzi wa ndoa, kwa upendo Yehova ameweka sasa uandalizi wa kuoa au kuolewa tena.” Bila shaka, si kila mtu aliyefiwa na mwenzi wa ndoa na ambaye anatamani kuoa au kuolewa tena anayeweza kufanya hivyo. Lakini alipotafakari kuhusu maneno ya ndugu huyo, Alex alisema hivi: “Kukumbushwa kwamba huo ni uandalizi wa Yehova kunaondoa mawazo yoyote yasiyofaa ya kwamba kuoa au kuolewa tena wakati ujao ni kukosa ushikamanifu kwa mwenzi wako wa ndoa aliyekufa au kwa mpango wa ndoa wa Yehova.”—1 Kor. 7:8, 9, 39.

Mtunga-zaburi Daudi, ambaye alikabili majaribu na matatizo mengi, alikiri hivi: “Macho ya Yehova yanawaelekea waadilifu, na masikio yake yanakielekea kilio chao cha kuomba msaada.” (Zab. 34:15) Kwa hakika, Yehova anaweza kujibu kilio cha mtu wa hali ya chini kwa wakati unaofaa kupitia maneno yenye busara na ya utambuzi ya Wakristo wenzetu wakomavu na wenye huruma. Uandalizi huo ni wenye thamani na faida.

Yehova Anatusaidia Kupitia Mikutano ya Kikristo

Mtu aliyeshuka moyo anaweza kuwa na mawazo yasiyofaa ambayo yanaweza kumfanya ajitenge na wengine. Hata hivyo, andiko la Methali 18:1 linaonya hivi: “Mtu anayejitenga na wengine atatafuta mapendezi yake mwenyewe; atashindana na hekima yote inayotumika.” Alex alikubali hivi: “Mwenzi wako wa ndoa anapokufa, mawazo yasiyofaa yanajaa katika akili yako.” Anakumbuka kwamba alijiuliza hivi: “‘Je, kuna jambo lolote ambalo ningefanya kwa njia tofauti? Je, ningeweza kuwa mwenye ufikirio zaidi na mwenye kujali zaidi?’ Sikutaka kuwa peke yangu. Sikutaka kuwa mjane. Ni vigumu sana kuacha mawazo hayo kwa sababu kila siku unakumbushwa kwamba uko peke yako.”

Mtu ambaye amepondeka roho anahitaji ushirika wenye kujenga wakati huu kuliko wakati mwingine wowote. Anaweza kuupata kwa urahisi katika mikutano ya kutaniko. Katika mazingira hayo, tunafungua akili yetu ili ipokee mawazo yanayofaa na yenye kujenga kutoka kwa Mungu.

Mikutano ya Kikristo inatusaidia kuwa na maoni yanayofaa kuhusu hali yetu. Tunaposikiliza na kutafakari kuhusu maandiko ya Biblia, tunakazia fikira masuala ambayo ni ya maana kikweli, yaani, kutetewa kwa enzi kuu ya Yehova na kutakaswa kwa jina lake, badala ya kufikiria tu mateso yetu wenyewe. Zaidi ya hayo, tunapofundishwa mambo ya kiroho mikutanoni, tunatiwa nguvu tunapojua kwamba hata ikiwa wengine hawatambui mateso tunayokabili au hawaelewi jinsi tunavyohisi, bila shaka Yehova anaelewa. Anajua kwamba “kwa sababu ya maumivu ya moyo roho hupata pigo.” (Met. 15:13) Mungu wa kweli anataka kutusaidia, na hilo linatutia nguvu na kutuchochea kuendelea.—Zab. 27:14.

Mfalme Daudi alipoteswa sana na maadui wake, alimlilia Mungu hivi: “Roho yangu inazimia ndani yangu; moyo wangu wenyewe umekufa ganzi katikati yangu.” (Zab. 143:4) Kwa kawaida, matatizo yanamfanya mtu adhoofike kabisa kimwili na kihisia, na hata yanaufanya moyo ufe ganzi. Tunaweza kuteseka kwa sababu ya ugonjwa au udhaifu fulani wa kimwili unaodumu kwa muda mrefu. Tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atatusaidia kuvumilia. (Zab. 41:1-3) Ingawa Mungu hamponyi kimuujiza mtu yeyote leo, anampa mtu huyo anayeteseka hekima na nguvu anazohitaji ili kuvumilia hali yake. Kumbuka kwamba Daudi alipolemewa na majaribu, alimwomba Yehova msaada. Aliimba hivi: “Nimezikumbuka siku za zamani za kale; nimetafakari juu ya utendaji wako wote; kwa kupenda niliendelea kuhangaikia kazi ya mikono yako mwenyewe.”—Zab. 143:5.

Kwa kuwa maneno hayo yaliyoongozwa na roho takatifu yameandikwa katika Neno la Mungu, hilo linaonyesha kwamba Yehova anaelewa jinsi tunavyohisi. Maneno kama hayo yanatuhakikishia kwamba anasikiliza maombi yetu. Tukikubali msaada wa Yehova, ‘yeye mwenyewe atatutegemeza.’—Zab. 55:22.

‘Sali Bila Kuacha’

Andiko la Yakobo 4:8 linasema hivi: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.” Njia moja ya kumkaribia Mungu ni kupitia sala. Mtume Paulo anatuhimiza ‘tusali bila kuacha.’ (1 The. 5:17) Hata ikiwa tunalazimika kujitahidi sana ili kumweleza Mungu jinsi tunavyohisi, “roho yenyewe hutuombea pamoja na kuugua kusikotamkwa.” (Rom. 8:26, 27) Bila shaka, Yehova anaelewa jinsi tunavyohisi.

Monika, ambaye ana uhusiano huo wa karibu pamoja na Yehova, anasema hivi: “Kupitia sala, usomaji wa Biblia, na funzo la kibinafsi, nimeona kwamba Yehova amekuwa Rafiki yangu wa karibu zaidi. Amekuwa halisi sana kwangu hivi kwamba ninaona jinsi anavyonisaidia sikuzote katika maisha yangu. Inafariji kujua kwamba ananielewa hata wakati ambapo siwezi kueleza jinsi ninavyohisi. Ninajua kwamba fadhili na baraka zake hazina mwisho.”

Basi, acheni tufanye yote tunayoweza kukubali maneno ya upendo na yenye kufariji ya Wakristo wenzetu, kufuata mashauri yenye fadhili na vikumbusho vyenye kutia imani nguvu ambavyo tunasikia katika mikutano ya Kikristo, na kumimina mambo yaliyo katika mioyo yetu mbele za Yehova katika sala. Kupitia maandalizi hayo ya wakati unaofaa, Yehova anaonyesha kwamba anatujali. Alex anasema hivi kutokana na mambo aliyojionea mwenyewe: “Tukitimiza sehemu yetu kwa kutumia maandalizi yote ambayo Yehova Mungu anatupatia ili kutusaidia kuwa wenye nguvu kiroho, tutakuwa na ‘nguvu zinazopita zile za kawaida’ za kutuwezesha kuvumilia jaribu lolote ambalo huenda tukakabili.”—2 Kor. 4:7.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 18]

Faraja kwa Mtu wa Hali ya Chini

Zaburi zimejaa maneno yanayoonyesha hisia za wanadamu na pia zinatuhakikishia tena na tena kwamba Yehova anasikiliza kilio cha mtu wa hali ya chini ambaye amelemewa na mikazo ya kihisia. Fikiria vifungu vifuatavyo:

“Katika taabu yangu niliendelea kumwita Yehova, nami niliendelea kumlilia Mungu wangu kwa ajili ya msaada. Kutoka katika hekalu lake aliisikia sauti yangu, nacho kilio changu cha msaada mbele zake sasa kikafika masikioni mwake.”—Zab. 18:6.

“Yehova yuko karibu na wale waliovunjika moyo; naye huwaokoa wale waliopondwa roho.”—Zab. 34:18.

“[Yehova] anawaponya wenye mioyo iliyovunjika, naye anafunga sehemu zao zenye maumivu.”—Zab. 147:3.

[Picha katika ukurasa wa 17]

“Neno linalosemwa wakati unaofaa” linaweza kufariji kama nini katika siku ya taabu!