Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Haijawa Kuchelewa Sana Kumtumikia Mungu

Haijawa Kuchelewa Sana Kumtumikia Mungu

Haijawa Kuchelewa Sana Kumtumikia Mungu

Huko Málaga, kusini mwa Hispania, mama na binti yake—ambao wote wanaitwa Ana—walibatizwa Desemba 19, 2009 (19/12/2009). Walikuwa kati ya watu 2,352 waliochukua hatua hiyo huko Hispania mwaka wa 2009. Lakini kulikuwa na jambo fulani la pekee kuhusu mama huyo na binti yake, yaani, umri wao. Mama alikuwa na umri wa miaka 107 na binti yake miaka 83!

Ni nini kilichowachochea kubatizwa ili kuonyesha wakfu wao kwa Yehova? Mwanzoni mwa miaka ya 1970, jirani yao alikuwa akimwalika yule binti Ana kuhudhuria Funzo la Kitabu la Kutaniko ambalo lilifanyiwa katika nyumba ya jirani huyo Shahidi. Ana alihudhuria mara kwa mara. Hata hivyo, Ana hakufanya maendeleo zaidi kwa sababu ya kazi yake ya kimwili.

Miaka kumi hivi baadaye, watoto fulani wa Ana walianza kujifunza Biblia na baada ya muda wakawa watumishi wa Yehova. Mmoja wao, Mari Carmen, mwishowe alimchochea mama yake kuanza tena kupenda kweli ya Biblia na akamsaidia kukubali funzo la Biblia. Kisha, nyanya (bibi) ya Mari Carmen, ambaye ni yule Ana mzee zaidi, alianza pia kupendezwa na Biblia. Mwishowe, washiriki kumi wa familia hiyo walichukua hatua ya kubatizwa.

Siku ambayo walibatizwa, Ana hao wawili, mama na binti yake, walifurahi sana. Ana mwenye umri wa miaka 107 alisema hivi: “Yehova amekuwa mwema sana kwangu, ameniruhusu nimjue.” Binti yake aliongezea hivi: “Kabla ya Paradiso kuja, ninataka kumtumikia Yehova, nikifanya mapenzi yake na kuhubiri habari njema kadiri ninavyoweza.”

Wajane hao wawili wanapata shangwe ya pekee wanapohudhuria mikutano. Mzee mmoja katika kutaniko lao anasema hivi: “Hawakosi mkutano hata mmoja. Sikuzote wako tayari kutoa maelezo katika Funzo la Mnara wa Mlinzi.”

Mfano wao wa uaminifu unatukumbusha mjane aliyeitwa Ana, “ambaye alikuwa hakosi kamwe kuwa katika hekalu, akitoa utumishi mtakatifu usiku na mchana kwa kufunga na dua.” Hilo lilifanya apate pendeleo la kumwona Yesu akiwa mtoto mchanga. (Luka 2:36-38) Akiwa na umri wa miaka 84, Ana hakuwa amezeeka sana asiweze kumtumikia Yehova, ndivyo ilivyo leo kuhusu yule mama na binti yake ambao wote wanaitwa Ana.

Je, una watu wa ukoo ambao wako tayari kusikiliza ujumbe wa Biblia? Au je, umekutana na mtu aliyezeeka anayependezwa ambaye yuko tayari kukusikiliza unapomhubiria nyumbani kwake? Watu hao wanaweza kuwa kama wale Ana wawili katika simulizi hili, kwa kuwa haijawa kuchelewa sana kuanza kumtumikia Mungu wa kweli, Yehova.

[Blabu katika ukurasa wa 25]

“Yehova amekuwa mwema sana kwangu”

[Blabu katika ukurasa wa 25]

“Kabla ya Paradiso kuja, ninataka kumtumikia Yehova”