Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unakumbuka?

Je, Unakumbuka?

Je, Unakumbuka?

Je, umefurahia kusoma matoleo ya hivi karibuni ya Mnara wa Mlinzi? Ona kama unaweza kujibu maswali yafuatayo:

• Watu wanaoamini fundisho la kwamba maisha ya mwanadamu yameamuliwa mapema ni wafuasi wa nani?

Wafuasi wa dini ya Calvin wanafuata sana fundisho la kwamba maisha ya mwanadamu yameamuliwa mapema. Mafundisho ya Jean Cauvin (John Calvin), ambaye alihusika katika kuleta Marekebisho ya Kidini, bado yana uvutano juu ya dini kama vile kanisa la Reformed, Presbiteri, Congregational, na Wapuriti.—9/1, ukurasa wa 18-21.

• Kaini alipata wapi mke wake?

Ni lazima iwe kwamba mke wa Kaini alikuwa mzao wa Hawa, ambaye alizaa “wana na mabinti.” (Mwa. 5:4)—9/1, ukurasa wa 25.

• Mungu alimtuma malaika yupi mbele ya Waisraeli walipokuwa wakitoka Misri? (Kut. 23:20, 21)

Ni jambo linalopatana na akili kuamini kwamba malaika huyo ambaye ‘jina la Yehova lilikuwa ndani yake,’ alikuwa Mwana-mzaliwa wa kwanza wa Mungu, ambaye baadaye alikuja kuwa Yesu.—9/15, ukurasa wa 21.

• Kwa nini kitabu cha Kwanza cha Wakorintho kinazungumza kuhusu nyama iliyotolewa dhabihu kwa sanamu?

Wanyama walitolewa dhabihu katika mahekalu ya Wagiriki na Waroma, lakini nyama ambayo haikuliwa wakati wa sherehe ingeuzwa sokoni. Wakristo hawakushiriki katika ibada ya kipagani; na hawakuhitaji kuona nyama iliyotolewa dhabihu ambayo iliuzwa sokoni kuwa imetiwa unajisi. Mtume Paulo aliandika hivi: “Endeleeni kula kila kitu kinachouzwa katika soko la nyama, bila kuchunguza kwa sababu ya dhamiri yenu; kwa maana ‘dunia na vyote vinavyoijaza ni vya Yehova.’” (1 Kor. 10:25, 26)—10/1, ukurasa wa 12.

• Kuhusu ibada ya kweli, ni visingizio gani ambavyo havikubaliwi na Mungu?

‘Ni vigumu sana. Sitaki. Nina shughuli nyingi. Sina uwezo. Mtu fulani aliniumiza hisia.’ Hivyo si visingizio vinavyofaa vya kutotimiza amri za Mungu.—10/15, ukurasa wa 12-15.

• Unaweza kufanya mambo gani ili mikutano ya Kikristo ikujenge na kuwajenga wengine?

Tayarisha mapema. Hudhuria kwa ukawaida. Fika kwa wakati. Beba vifaa vyote. Epuka mambo yanayokengeusha fikira. Shiriki. Toa maelezo mafupi. Timiza migawo yako. Wapongeze washiriki. Zungumza na wengine kabla na baada ya mikutano.—10/15, ukurasa wa 22.

• Ukoma, unaotia ndani ugonjwa ambao leo unaitwa Hansen, unatajwa katika simulizi gani la Biblia linalohusisha msichana mdogo?

Andiko la Wafalme wa Pili sura ya 5 linamtaja msichana Mwisraeli, ambaye alikuwa mtumishi katika nyumba ya mkuu wa jeshi la Siria aliyeitwa Naamani. Msichana huyo alipendekeza kwamba Naamani amwone nabii Elisha ili aponywe ukoma wake.—11/1, ukurasa wa 22.

• Tunaweza kujifunza nini kutokana na kisa cha Haruni kukubali kusongwa na wengine?

Musa alipokuwa ameondoka, Waisraeli walimsukuma Haruni awatengenezee mungu. Alishindwa naye akafanya hivyo. Hilo linaonyesha kwamba kusongwa na marafiki si jambo linalowapata vijana tu. Hata watu wenye umri mkubwa ambao wanataka kufanya yaliyo sawa wanaweza kusongwa na wengine. Tunahitaji kupinga msongo usiofaa wa marafiki.—11/15, ukurasa wa 8.

• Ni kweli, au si kweli?

Shetani ni kiumbe halisi: kweli. (2 Kor. 11:14) Baada ya kufa watu wote wanaenda katika makao ya roho: si kweli. (Mhu. 9:5) Malaika waaminifu wanatujali: kweli. (Zab. 34:7) Yesu ni sawa na Mungu: si kweli. (1 Kor. 11:3)—12/1, ukurasa wa 8-9.