Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Heshimu Ndoa kwa Kuwa Ni Zawadi Kutoka kwa Mungu

Heshimu Ndoa kwa Kuwa Ni Zawadi Kutoka kwa Mungu

Heshimu Ndoa kwa Kuwa Ni Zawadi Kutoka kwa Mungu

“Hiyo ndiyo sababu mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake nao watakuwa mwili mmoja.”—MWA. 2:24.

1. Kwa nini Yehova anastahili kupokea heshima kutoka kwetu?

YEHOVA MUNGU, ambaye ni Mwanzilishi wa ndoa, bila shaka anastahili kupokea heshima kutoka kwetu. Akiwa Muumba, Mwenye Enzi Kuu, na Baba yetu wa mbinguni, anaelezwa kwa kufaa kuwa Mpaji wa “kila zawadi njema na kila tuzo kamilifu.” (Yak. 1:17; Ufu. 4:11) Hilo linaonyesha upendo wake mwingi. (1 Yoh. 4:8) Kila jambo ambalo ametufundisha, kila jambo ambalo ametuomba tufanye, na kila jambo ambalo ametupatia ni kwa faida na hali yetu njema tu.—Isa. 48:17.

2. Yehova aliwapa wenzi wa kwanza wa ndoa maagizo gani?

2 Biblia inaonyesha kwamba ndoa ni kati ya zawadi hizo “njema” kutoka kwa Mungu. (Rut. 1:9; 2:12) Yehova alipowaunganisha wenzi wa ndoa wa kwanza, Adamu na Hawa, aliwapa maagizo kamili kuhusu jinsi ya kufanikiwa. (Soma Mathayo 19:4-6.) Ikiwa wangefuata mwongozo wa Mungu, wangepata furaha ya kudumu. Hata hivyo, kwa upumbavu walipuuza amri ya Mungu wakapata matokeo mabaya sana.—Mwa. 3:6-13, 16-19, 23.

3, 4. (a) Watu wengi leo wanakosa jinsi gani kuheshimu ndoa na pia Yehova Mungu? (b) Tutazungumzia mifano gani katika habari hii?

3 Kama wenzi hao wa kwanza wa ndoa, watu wengi leo hawajali sana au wanapuuza mwongozo wa Yehova wanapofanya maamuzi katika ndoa. Watu fulani wanapinga ndoa moja kwa moja, na wengine wanajaribu kufafanua ndoa kwa njia yao ili watosheleze tamaa zao wenyewe. (Rom. 1:24-32; 2 Tim. 3:1-5) Wanapuuza uhakika wa kwamba ndoa ni zawadi kutoka kwa Mungu, na wanakosa kuiheshimu zawadi hiyo na hivyo kukosa pia kumheshimu Mpaji wa zawadi hiyo, Yehova Mungu.

4 Nyakati nyingine, hata watu fulani wa Mungu wanaacha kuwa na maoni kama ya Yehova kuhusu ndoa. Wenzi fulani wa ndoa Wakristo wanaamua kutengana au kutalikiana bila msingi wa Kimaandiko. Hali hizo zinaweza kuepukwa jinsi gani? Mwongozo wa Mungu katika Mwanzo 2:24 unaweza kuwasaidia jinsi gani Wakristo waliofunga ndoa kutia nguvu ndoa yao? Na wale ambao wanafikiria kufunga ndoa wanaweza kujitayarisha jinsi gani? Acheni tuchunguze ndoa tatu zilizofanikiwa katika nyakati za Biblia ambazo zinaonyesha jinsi ambavyo kumheshimu Yehova ni ufunguo wa maana wa ndoa yenye kudumu.

Sitawisha Ushikamanifu

5, 6. Huenda Zekaria na Elisabeti walijaribiwa na hali gani, na walithawabishwa jinsi gani kwa sababu ya ushikamanifu wao?

5 Zekaria na Elisabeti walifanya mambo yote kwa njia inayofaa. Kabla ya kufunga ndoa, kila mmoja wao alikuwa mtumishi mshikamanifu wa Yehova. Zekaria alitimiza kwa uaminifu migawo yake ya kikuhani, na wote wawili walishika Sheria ya Mungu kwa uwezo wao wote. Bila shaka, walikuwa na sababu nyingi za kumshukuru Yehova. Hata hivyo, ikiwa ungewatembelea katika nyumba yao huko Yuda, ungegundua mara moja kwamba kuna kitu walichokosa. Hawakuwa na watoto. Elisabeti alikuwa tasa, na wote wawili walikuwa na umri mkubwa sana.—Luka 1:5-7.

6 Katika taifa la kale la Israeli, kuzaa watoto kulionwa kuwa jambo lenye kuheshimika sana, na mara nyingi familia zilikuwa kubwa sana. (1 Sam. 1:2, 6, 10; Zab. 128:3, 4) Wakati huo, mwanamume Mwisraeli angeweza kumtaliki mke wake kwa hila ikiwa hakumzalia watoto. Hata hivyo, Zekaria aliendelea kukaa kwa ushikamanifu na Elisabeti. Hakutafuta njia rahisi ya kuvunja ndoa yao, wala mke wake hakufanya hivyo. Ingawa walihuzunika kwa sababu ya kutokuwa na watoto, waliendelea kumtumikia Yehova pamoja kwa uaminifu. Baada ya muda, Yehova aliwathawabisha sana walipozaa mtoto wa kiume kimuujiza wakiwa wamezeeka.—Luka 1:8-14.

7. Elisabeti alionyesha ushikamanifu kwa mume wake kwa njia gani nyingine?

7 Elisabeti alionyesha ushikamanifu wa pekee kwa njia nyingine. Mwana wake, Yohana, alipozaliwa, Zekaria hangeweza kuzungumza kwa kuwa alikuwa amefanywa bubu kwa sababu ya kumtilia shaka malaika wa Mungu. Hata hivyo, ni wazi kwamba Zekaria alimwambia mke wake kwa njia fulani kwamba malaika wa Yehova alikuwa amemwambia amwite mtoto huyo wa kiume “Yohana.” Majirani na watu wa ukoo walitaka kumwita mtoto huyo jina la baba yake. Lakini Elisabeti alitii kwa ushikamanifu maagizo ambayo mume wake alimpa. Elisabeti alisema hivi: “Sivyo hata kidogo! bali ataitwa Yohana.”—Luka 1:59-63.

8, 9. (a) Ushikamanifu unatia ndoa nguvu jinsi gani? (b) Mume na mke wanaweza kuonyesha ushikamanifu katika njia gani hasa?

8 Kama Zekaria na Elisabeti, wenzi wa ndoa leo wanapatwa na mambo yanayovunja moyo na matatizo mengine. Ndoa ambayo haina ushikamanifu haitadumu. Kuwachezea wengine kimapenzi, ponografia (picha au habari za ngono), uzinzi, na hali nyingine hatari zinaweza kuharibu ndoa nzuri na kufanya wenzi wa ndoa waache kabisa kuaminiana. Na wenzi wa ndoa wanapoacha kabisa kuaminiana, upendo unaanza kupoa. Kwa njia fulani, ushikamanifu ni kama ukuta wenye kulinda unaozunguka nyumba ya familia ili kuzuia hatari mbalimbali na watu wasiotakiwa wasiingie, na hivyo wale walio ndani ya nyumba hiyo wanahisi wakiwa na usalama wa kadiri fulani. Hivyo, mume na mke wanapokuwa washikamanifu kwa mmoja na mwenzake, wanaweza kukaa pamoja kwa usalama na kuambiana mambo na hisia zilizo moyoni mwao, wakiruhusu upendo wao ukue. Ndiyo, ushikamanifu ni sifa ya maana sana.

9 Yehova alimwambia Adamu hivi: “Mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake.” (Mwa. 2:24) Hilo linamaanisha nini? Ni lazima mahusiano ya zamani pamoja na marafiki na watu wa ukoo yabadilike. Ni lazima kila mwenzi wa ndoa atumie wakati pamoja na mume au mke wake na kumpa uangalifu. Mtu hapaswi kuendelea kutanguliza marafiki au watu wa ukoo na kupuuza familia yake mpya; na wenzi hao wa ndoa hawapaswi kuruhusu wazazi waingilie maamuzi au mizozano ya familia yao. Ni lazima sasa wenzi hao wa ndoa washikamane pamoja. Huo ndio mwongozo wa Mungu.

10. Ni nini kitakachowasaidia wenzi wa ndoa wasitawishe ushikamanifu?

10 Hata katika nyumba ambazo zimegawanyika kidini, ushikamanifu unathawabisha. Dada mmoja mwenye mume ambaye si mwamini alisema hivi: “Ninamshukuru sana Yehova kwa kunifundisha jinsi ya kujitiisha chini ya mume wangu na kumheshimu sana. Kwa sababu ya kuendelea kuwa mshikamanifu, nimefurahia kukaa kwa miaka 47 katika ndoa yenye heshima na upendo wa kudumu.” (1 Kor. 7:10, 11; 1 Pet. 3:1, 2) Kwa hiyo, jitahidi sana kumfanya mwenzi wako wa ndoa ajihisi salama. Kwa maneno na matendo yako, tafuta njia za kumhakikishia mwenzi wako kwamba unamwona kuwa mtu wa maana zaidi duniani. Kwa kadiri ambavyo inakutegemea wewe, usiache mtu yeyote wala kitu chochote kije kati yako na mwenzi wako. (Soma Methali 5:15-20.) Ron na Jeannette, ambao wamekuwa na ndoa yenye furaha kwa miaka zaidi ya 35, wanasema hivi: “Ndoa yetu ina furaha na imefanikiwa kwa sababu tunafanya kwa ushikamanifu yale ambayo Mungu anataka tufanye.”

Umoja Unafanya Ndoa Iwe na Nguvu

11, 12. Akila na Prisila walishirikiana jinsi gani (a) nyumbani, (b) katika kazi yao ya kimwili, na (c) katika huduma ya Kikristo?

11 Mtume Paulo alipozungumza kuhusu marafiki wake wa karibu Akila na Prisila, hakumtaja mmoja bila kumtaja mwenzake. Wenzi hao wa ndoa wenye umoja ni mfano mzuri unaoonyesha jambo ambalo Mungu alimaanisha aliposema kwamba mume na mke wanapaswa kuwa “mwili mmoja.” (Mwa. 2:24) Sikuzote walifanya mambo pamoja katika nyumba yao, katika kazi yao ya kimwili, na katika huduma ya Kikristo. Kwa mfano, Paulo alipofika Korintho mara ya kwanza, Akila na Prisila walimkaribisha kwa fadhili ili akae katika nyumba yao, ambamo inaelekea aliishi baadaye kwa muda huku akiendelea na utendaji wake. Baadaye, huko Efeso, Akila na Prisila walitumia nyumba yao kwa ajili ya mikutano ya kutaniko na walishirikiana katika kuwasaidia wapya, kama vile Apolo, kukua kiroho. (Mdo. 18:2, 18-26) Kisha, wenzi hao wa ndoa wenye bidii walienda Roma, ambako walitoa tena nyumba yao ili itumiwe kwa ajili ya mikutano ya kutaniko. Baadaye, walirudi Efeso na kuwatia nguvu akina ndugu.—Rom. 16:3-5.

12 Kwa muda fulani, Akila na Prisila walishirikiana na Paulo kufanya kazi ya kutengeneza mahema. Kwa mara nyingine tena, tunaona wenzi hao wa ndoa wakishirikiana pamoja bila mashindano wala ugomvi. (Mdo. 18:3) Hata hivyo, bila shaka ndoa yao ilikuwa katika hali nzuri sana ya kiroho kwa sababu ya wakati walioshiriki pamoja katika utendaji mbalimbali wa Kikristo. Walijulikana kotekote kuwa ‘wafanyakazi wenzi katika Kristo Yesu,’ iwe ni Korintho, Efeso, au Roma. (Rom. 16:3) Walishirikiana bega kwa bega ili kuendeleza kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme mahali popote ambapo walitumika.

13, 14. (a) Ni hali gani zinazoweza kuharibu umoja katika ndoa? (b) Taja mambo fulani ambayo wenzi wa ndoa wanaweza kufanya ili kutia nguvu kifungo chao wakiwa “mwili mmoja.”

13 Kwa kweli, ndoa inakuwa na nguvu wakati wenzi wa ndoa wanapokuwa na umoja katika utendaji mbalimbali na miradi yao. (Mhu. 4:9, 10) Inasikitisha kwamba wenzi wengi wa ndoa leo wanatumia muda mfupi sana pamoja. Kila mmoja wao anafanya kazi yake ya kimwili kwa saa nyingi. Wengine wanasafiri-safiri sana kwa ajili ya kazi yao ya kimwili au wanahamia nchi za kigeni bila mwenzi wao ili kufanya kazi na kutuma pesa nyumbani. Hata wakiwa nyumbani, wenzi fulani wa ndoa wanajikuta wametengana kwa sababu ya muda wanaotumia kutazama televisheni, kufanya mambo wanayopenda, kucheza michezo ya video na michezo mingine, au kutumia Intaneti. Je, ndivyo ilivyo katika nyumba yenu? Ikiwa ndivyo ilivyo, je, mnaweza kurekebisha hali zenu ili mtumie wakati zaidi pamoja? Namna gani mkishirikiana katika kazi za kila siku kama vile kutayarisha vyakula, kuosha vyombo, au kutunza bustani? Je, mnaweza kushirikiana katika kuwatunza watoto au kuwasaidia wazazi wenu wanaozeeka?

14 Jambo la maana zaidi ni kutumia wakati pamoja kwa ukawaida katika utendaji unaohusiana na ibada ya Yehova. Kuzungumzia andiko la kila siku pamoja na kushiriki katika ibada ya familia ni nafasi bora zaidi za kuhakikisha kwamba familia yenu ina umoja katika fikira na miradi. Mshiriki pia pamoja katika huduma. Ikiwezekana, mjaribu kufanya upainia pamoja, hata ikiwa hali zenu zinawaruhusu kufanya hivyo kwa mwezi mmoja au mwaka mmoja tu. (Soma 1 Wakorintho 15:58.) Dada mmoja ambaye alifanya upainia pamoja na mume wake anasema hivi: “Huduma ni moja ya njia ambazo zilituwezesha kutumia wakati pamoja na kuzungumza kikweli. Kwa sababu sote wawili tulikuwa na mradi mmoja wa kuwasaidia wengine kiroho, nilihisi kwamba tulishirikiana kwa umoja kabisa. Nilimkaribia zaidi si kwa sababu tu ni mume wangu bali pia kwa sababu ni rafiki mzuri.” Unaposhiriki na mwenzi wako katika utendaji wa maana, mapendezi yako, mambo unayotanguliza, na mazoea yako yatapatana hatua kwa hatua na ya mwenzi wako, na mwishowe mtaanza kufikiri, kuhisi, na kutenda mkiwa “mwili mmoja” kama Akila na Prisila.

Mtangulizeni Mungu ili Awaongoze Katika Ndoa Yenu

15. Ni nini ufunguo wa kuwa na ndoa yenye mafanikio? Eleza.

15 Yesu alijua umuhimu wa kumtanguliza Mungu katika ndoa. Aliona Yehova akiwaunganisha wenzi wawili wa kwanza wa ndoa. Aliona jinsi Adamu na Hawa walivyofurahi walipofuata mwongozo wa Mungu, naye alijionea matatizo yaliyotokea walipopuuza mwongozo huo. Kwa hiyo, Yesu alipowafundisha wengine, alirudia kutaja maagizo ya Baba yake katika Mwanzo 2:24. Aliongeza wazo hili pia: “Kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe.” (Mt. 19:6) Basi, kumheshimu sana Yehova bado ndio ufunguo wa kuwa na ndoa yenye furaha na yenye mafanikio. Kuhusiana na hilo, wazazi wa Yesu hapa duniani, Yosefu na Maria, waliweka mfano mzuri sana.

16. Yosefu na Maria walionyesha jinsi gani kwamba walithamini mambo ya kiroho katika maisha yao ya familia?

16 Yosefu alimtendea Maria kwa fadhili na heshima. Mwanzoni, Yosefu alipopata habari kwamba Maria alikuwa na mimba, alitaka kumtendea kwa huruma, hata kabla malaika wa Mungu hajamweleza kilichompata Maria. (Mt. 1:18-20) Wenzi hao wa ndoa walitii amri ya Kaisari na pia walifuata kabisa Sheria ya Musa. (Luka 2:1-5, 21, 22) Na ingawa wanaume peke yao ndio waliotakiwa kuhudhuria sherehe kuu za kidini huko Yerusalemu, Yosefu na Maria, pamoja na washiriki wa familia yao walihudhuria sherehe hizo kila mwaka. (Kum. 16:16; Luka 2:41) Katika njia hizo na njia nyingine, wenzi hao wa ndoa waliomwogopa Mungu walijitahidi kumpendeza Yehova na waliheshimu sana mambo ya kiroho. Haishangazi kwamba Yehova alikuwa amewachagua ili wamtunze Mwana wake katika sehemu ya kwanza ya maisha ya Yesu duniani.

17, 18. (a) Ni katika njia gani mbalimbali wenzi wa ndoa wanaweza kumtanguliza Mungu katika familia yao? (b) Watafaidika jinsi gani wakifanya hivyo?

17 Je, mnamtanguliza Mungu ili awaongoze katika maisha yenu ya familia? Kwa mfano, mnapofanya maamuzi ya maana, je, mnafanya utafiti kwanza kuhusu kanuni za Biblia, kusali kuhusu jambo hilo, na kisha kutafuta mashauri kutoka kwa Wakristo wakomavu? Au je, mna mwelekeo wa kutatua matatizo kwa kufuata hisia zenu wenyewe au hisia za watu wenu wa familia na marafiki? Je, mnajitahidi kufuata mapendekezo mengi yenye faida kuhusu ndoa na maisha ya familia yanayochapishwa na mtumwa mwaminifu? Au je, mnajikuta mkifuata tu desturi za kwenu au mashauri ya kilimwengu yanayopendwa na wengi? Je, mnasali na kujifunza pamoja kwa ukawaida, mkijiwekea miradi ya kiroho, na kuzungumza kuhusu mambo ambayo mnatanguliza mkiwa familia?

18 Ray anasema hivi kuhusu miaka 50 ya ndoa yao yenye furaha: “Hatujawahi kamwe kushindwa kutatua tatizo lolote, kwa sababu tulihakikisha kwamba Yehova ni sehemu ya ‘kamba yetu yenye nyuzi tatu.’” (Soma Mhubiri 4:12.) Danny na Trina wanakubali jambo hilo. Wanasema hivi: “Ndoa yetu imekuwa na nguvu zaidi kadiri tunavyomtumikia Mungu pamoja.” Wameishi pamoja kwa furaha katika ndoa kwa miaka zaidi ya 34. Sikuzote mkimtanguliza Yehova katika ndoa yenu, atawasaidia kufanikiwa na atawabariki sana.—Zab. 127:1.

Endeleeni Kuheshimu Zawadi ya Mungu

19. Kwa nini Mungu aliwapa wanadamu zawadi ya ndoa?

19 Jambo la maana kwa watu wengi leo ni kujitafutia tu furaha. Lakini mtumishi wa Yehova anaona mambo kwa njia tofauti. Anajua kwamba Mungu aliwapa wanadamu zawadi ya ndoa ili kuendeleza kusudi Lake. (Mwa. 1:26-28) Ikiwa Adamu na Hawa wangeheshimu zawadi hiyo, dunia yote ingekuwa paradiso iliyojaa watumishi wa Mungu ambao ni waadilifu na wenye furaha.

20, 21. (a) Kwa nini tunapaswa kuiona ndoa kuwa takatifu? (b) Tutajifunza kuhusu zawadi gani juma lijalo?

20 Zaidi ya mambo yote, watumishi wa Mungu wanaona ndoa kuwa nafasi ya kumletea Yehova utukufu. (Soma 1 Wakorintho 10:31.) Kama tulivyoona, ushikamanifu, umoja, na kumtanguliza Mungu katika ndoa ni sifa za kimungu ambazo zinafanya ndoa iwe na nguvu. Kwa hiyo, iwe tunajitayarisha kufunga ndoa, tunaitia nguvu ndoa yetu, au kujitahidi kuokoa ndoa yetu, ni lazima kwanza tuthamini kwamba ndoa ni mpango mtakatifu ulioanzishwa na Mungu. Kuweka kweli hiyo katika akili kutatuchochea tujitahidi kadiri tunavyoweza kufanya maamuzi ya ndoa yanayotegemea Neno la Mungu. Kwa njia hiyo tunaonyesha kwamba tunaheshimu si zawadi ya ndoa tu bali pia Mpaji wa zawadi hiyo, Yehova Mungu.

21 Bila shaka, ndoa si zawadi pekee ambayo Yehova ametupatia; wala si njia pekee ya kupata furaha maishani. Katika habari yetu inayofuata, tutaona zawadi nyingine yenye thamani kutoka kwa Mungu—zawadi ya useja.

Ungesema Nini?

• Ushikamanifu unapaswa kuwa na uvutano gani kwa Wakristo waliofunga ndoa?

• Kwa nini kufanya mambo pamoja kwa umoja kutafanya ndoa iwe na nguvu?

• Ni katika njia gani watu waliofunga ndoa wanaweza kumtanguliza Mungu ili awaongoze katika ndoa yao?

• Tunaweza kuonyesha jinsi gani kwamba tunamheshimu Yehova ambaye ndiye Mwanzilishi wa ndoa?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 15]

Kufanya mambo pamoja kunawasaidia wenzi wa ndoa kukaa kwa umoja