Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tumia Vizuri Kabisa Useja Wako

Tumia Vizuri Kabisa Useja Wako

Tumia Vizuri Kabisa Useja Wako

‘Yule anayeweza kuupa nafasi na aupe nafasi.’—MT. 19:12.

1, 2. (a) Yesu, Paulo, na wengine walikuwa na maoni gani kuhusu useja? (b) Kwa nini huenda wengine wakafikiri kwamba useja si zawadi?

BILA shaka, ndoa ni moja kati ya zawadi zenye thamani zaidi ambazo Mungu amewapa wanadamu. (Met. 19:14) Hata hivyo, Wakristo wengi waseja wanafurahia pia maisha mazuri yenye kuridhisha. Harold, ndugu mwenye umri wa miaka 95 ambaye hajawahi kamwe kuoa, anasema hivi: “Ingawa ninafurahia kuwa pamoja na wengine na kuwakaribisha, ninapokuwa peke yangu sijisikii kamwe nikiwa mpweke. Ninafikiri inaweza kusemwa kwamba kwa kweli nina zawadi ya useja.”

2 Kwa kweli, Yesu Kristo na mtume Paulo walisema kwamba useja, kama ndoa, ni zawadi kutoka kwa Mungu. (Soma Mathayo 19:11, 12; 1 Wakorintho 7:7.) Hata hivyo, ni wazi kwamba si kila mtu ambaye hajafunga ndoa amechagua kuwa mseja. Nyakati nyingine hali zinafanya iwe vigumu kupata mwenzi wa ndoa anayefaa. Au wengine ambao wamekaa katika ndoa kwa miaka mingi, wanajikuta kwa ghafula wakiwa peke yao tena kwa sababu ya talaka au kifo cha mwenzi wao wa ndoa. Basi, ni katika maana gani useja unaweza kuwa zawadi? Na Wakristo waseja wanaweza kutumia vizuri zaidi useja wao jinsi gani?

Zawadi ya Pekee

3. Kwa kawaida ni faida gani ambazo Wakristo waseja wanafurahia?

3 Kwa kawaida, mseja ana wakati zaidi na uhuru zaidi kuliko mtu aliyefunga ndoa. (1 Kor. 7:32-35) Hizo ni faida za pekee ambazo zinaweza kumruhusu mseja apanue huduma yake, apanuke katika kuwaonyesha wengine upendo, na kumkaribia Yehova zaidi. Kwa hiyo, Wakristo wengi wametambua na kuthamini faida za useja na wameamua ‘kuupa nafasi,’ kwa muda fulani. Huenda mwanzoni wengine hawakupanga kuwa waseja, lakini hali zao zilipobadilika, walisali na kutafakari kuhusu hali yao, kisha wakatambua kwamba Yehova anaweza kuwasaidia ili watulie moyoni. Hivyo, walikubali hali zao zilizobadilika na kuupa useja nafasi.—1 Kor. 7:37, 38.

4. Kwa nini Wakristo waseja wanaweza kuhisi kwamba wametosheka katika utumishi wa Mungu?

4 Wakristo waseja wanajua kwamba si lazima wafunge ndoa ili watambuliwe au kuthaminiwa na Yehova au tengenezo lake. Mungu anampenda kila mmoja wetu. (Mt. 10:29-31) Hakuna mtu yeyote wala kitu chochote kinachoweza kututenga na upendo wa Mungu. (Rom. 8:38, 39) Iwe tumefunga ndoa au sisi ni waseja, tuna kila sababu ya kuhisi kwamba tumetosheka katika utumishi wa Mungu.

5. Ni nini kinachohitajiwa ili mtu afaidike kikamili na useja?

5 Hata hivyo, ili mtu afaidike kikamili na zawadi ya useja ni lazima aisitawishe kama watu wanavyokuza au kusitawisha zawadi nyingine kama vile ustadi wa kucheza muziki au michezo. Basi, Wakristo waseja leo, wawe ni ndugu au dada, wenye umri mdogo au mkubwa, wawe wamechagua kuwa waseja au ni waseja kwa sababu ya hali, wanaweza jinsi gani kutumia vizuri hali yao maishani? Acheni tuzungumzie mifano fulani yenye kutia moyo kutoka katika kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza ili tuone mambo tunayojifunza.

Useja Wakati wa Ujana

6, 7. (a) Mabinti wa Filipo ambao walikuwa mabikira walipata pendeleo gani katika utumishi wa Mungu? (b) Ni katika njia gani Timotheo alitumia vizuri miaka yake ya useja, na alibarikiwa jinsi gani kwa sababu ya kuwa tayari kutumika akiwa kijana?

6 Mweneza-injili Filipo alikuwa na mabinti wanne mabikira ambao walikuwa na bidii ya kueneza injili kama baba yao. (Mdo. 21:8, 9) Kutoa unabii kulikuwa kati ya zawadi za kimuujiza za roho takatifu, na wanawake hao vijana walitumia zawadi hiyo kulingana na utimizo wa andiko la Yoeli 2:28, 29.

7 Timotheo alikuwa kijana ambaye alitumia vizuri useja wake. Tangu alipokuwa mtoto mchanga alifundishwa “maandishi matakatifu” na mama yake, Eunike, na nyanya yake, Loisi. (2 Tim. 1:5; 3:14, 15) Lakini inaelekea kwamba walikubali Ukristo wakati tu wa ziara ya kwanza ya Paulo huko Listra, mji wao wa nyumbani, karibu mwaka wa 47 W.K. Miaka miwili baadaye, Paulo alipofanya ziara ya pili huko, labda Timotheo alikuwa katika miaka yake ya mwisho ya utineja au alikuwa na umri wa miaka 20 hivi. Hata ingawa alikuwa na umri mdogo na alikuwa mpya katika kweli, “alishuhudiwa vema” na wazee Wakristo huko Listra na mji jirani wa Ikoniamu. (Mdo. 16:1, 2) Kwa hiyo, Paulo alimwalika Timotheo ajiunge naye akiwa msafiri mwenzake. (1 Tim. 1:18; 4:14) Hatuwezi kusema kwa hakika kwamba Timotheo hakuoa kamwe. Lakini tunajua kwamba akiwa kijana, alikubali kwa uchangamfu mwaliko wa Paulo, na kwa miaka mingi baada ya hapo, alitumikia akiwa mmishonari na mwangalizi mseja.—Flp. 2:20-22.

8. Ni nini kilichomsaidia Yohana Marko kufuatia miradi ya kiroho, na alipata baraka gani kwa kufanya hivyo?

8 Yohana Marko alipokuwa kijana alitumia pia miaka yake ya useja kwa njia nzuri. Yeye na mama yake, Maria, na pia binamu yake Barnaba walikuwa washiriki wa kwanza wa kutaniko la Yerusalemu. Huenda familia ya Marko pia ilikuwa na maisha mazuri, kwa sababu walikuwa na nyumba yao wenyewe mjini na walikuwa na mtumishi. (Mdo. 12:12, 13) Hata hivyo, ingawa maisha yake yalikuwa mazuri, Marko, hata akiwa kijana, hakuishi maisha ya kichoyo au ya kufuatia raha; wala hakutosheka tu kuishi mahali pamoja na kuwa na maisha ya familia yenye starehe. Inaelekea kwamba ushirikiano wake wa mapema na mitume ulimchochea kutamani utumishi wa umishonari. Kwa hiyo, alifurahi sana kujiunga na Paulo na Barnaba katika safari yao ya kwanza ya umishonari na alitumika akiwa mtumishi wao. (Mdo. 13:5) Baadaye, alisafiri pamoja na Barnaba, na baada ya muda, tunamwona akitumika pamoja na Petro huko Babiloni. (Mdo. 15:39; 1 Pet. 5:13) Hatujui Marko aliendelea kuwa mseja kwa muda gani. Lakini alisifiwa sana kwa sababu alikuwa tayari kuwatumikia wengine na kufanya mengi katika utumishi wa Mungu.

9, 10. Vijana waseja Wakristo wana nafasi gani leo za kupanua utumishi wao? Toa mfano.

9 Vijana wengi katika kutaniko leo wanafurahi pia kutumia miaka yao ya useja ili kupanua utumishi wao kwa Mungu. Kama Marko na Timotheo, wanatambua kwamba useja unawaruhusu “kumhudumia Bwana daima bila kukengeushwa fikira.” (1 Kor. 7:35) Kwa kweli, hiyo ni faida kubwa. Waseja wana njia au nafasi nyingi za kumtumikia Yehova, kama vile kufanya upainia, kutumikia katika maeneo yenye uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri wa Ufalme, kujifunza lugha ya kigeni, kusaidia katika ujenzi wa Jumba la Ufalme au ofisi ya tawi, kuhudhuria Shule ya Mazoezi ya Kihuduma, na kutumika Betheli. Ikiwa wewe bado ni kijana na hujafunga ndoa, je, unatumia vizuri nafasi ulizo nazo?

10 Ndugu mmoja anayeitwa Mark alianza kufanya upainia katika miaka yake ya mwisho ya utineja, akahudhuria Shule ya Mazoezi ya Kihuduma, na ametumika katika migawo mbalimbali ulimwenguni pote. Anapoangalia miaka 25 ambayo ameshiriki katika utumishi wa wakati wote, anasema hivi: “Nimejitahidi kuwatia moyo watu wote katika kutaniko kwa kuhubiri pamoja nao, kuwafanyia ziara za uchungaji, kuwaalika katika nyumba yangu kwa ajili ya chakula, na hata kupanga tafrija zinazojenga kiroho. Mambo hayo yote yameniletea shangwe kubwa sana.” Kama maelezo ya Mark yanavyoonyesha, shangwe kubwa zaidi maishani inatokana na kutoa, na tunapata nafasi nyingi za kuwahudumia wengine tunapotumia maisha yetu yote katika utumishi mtakatifu. (Mdo. 20:35) Hata uwe unapendezwa na mambo gani, uwe na ustadi, au uzoefu gani maishani, kuna mengi ambayo vijana wanaweza kufanya leo katika kazi ya Bwana.—1 Kor. 15:58.

11. Kuna faida gani za kutokimbilia kufunga ndoa?

11 Ingawa mwishowe vijana wengi wangependa kufunga ndoa, kuna sababu nzuri za kutokimbilia kufunga ndoa. Paulo aliwatia moyo vijana wangoje mpaka wanapopita “upeo wa ujana” wakati ambapo tamaa ya ngono ina nguvu sana. (1 Kor. 7:36) Unahitaji muda ili ujielewe na kupata uzoefu wa maisha unaohitajiwa ili kumchagua mwenzi anayefaa. Kufanya nadhiri ya ndoa ni uamuzi mzito, ambao unapaswa kudumu katika muda wote wa maisha.—Mhu. 5:2-5.

Useja Katika Miaka ya Baadaye ya Maisha

12. (a) Ana, ambaye alikuwa mjane, alitumia jinsi gani hali zake zilizobadilika? (b) Alipata pendeleo gani?

12 Inaelekea kwamba Ana, ambaye anatajwa katika Injili ya Luka, alihuzunika sana mume wake alipokufa kwa ghafula baada ya kukaa naye katika ndoa kwa miaka saba tu. Hatujui ikiwa walikuwa na watoto wowote au ikiwa Ana alifikiria kuolewa tena. Lakini Biblia inasema kwamba Ana alikuwa bado mjane alipokuwa na umri wa miaka 84. Kutokana na yale ambayo Biblia inasema, tunaweza kukata kauli kwamba Ana alitumia hali zake zilizobadilika kumkaribia Yehova zaidi. Alikuwa “hakosi kamwe kuwa katika hekalu, akitoa utumishi mtakatifu usiku na mchana kwa kufunga na dua.” (Luka 2:36, 37) Kwa hiyo, alitanguliza mambo ya kiroho katika maisha yake. Aliazimia na kujitahidi kabisa kufanya hivyo, lakini alithawabishwa sana. Alipata pendeleo la kumwona Yesu akiwa mtoto, na akawatolea wengine ushahidi kuhusu ukombozi ambao ungeletwa na Masihi huyo aliyekuwa akija.—Luka 2:38.

13. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba Dorkasi alikuwa mwenye bidii katika kutaniko? (b) Dorkasi alithawabishwa jinsi gani kwa sababu ya wema na fadhili zake?

13 Mwanamke anayeitwa Dorkasi, au Tabitha, aliishi Yopa, mji wa zamani wenye bandari upande wa kaskazini-magharibi wa Yerusalemu. Kwa kuwa Biblia haisemi kwamba alikuwa na mume, inaelekea kwamba hakuwa ameolewa wakati huo. Dorkasi “alizidi katika matendo mema na zawadi za rehema.” Inaonekana kwamba alitengeneza mavazi mengi kwa ajili ya wajane maskini na watu wengine, na hivyo walimpenda sana. Kwa hiyo, alipopata ugonjwa na kufa kwa ghafula, kutaniko lote liliwatuma watu wamsihi Petro ili amfufue dada yao mpendwa. Habari za kufufuliwa kwake zilipoenea kotekote katika Yopa, watu wengi wakawa waamini. (Mdo. 9:36-42) Huenda Dorkasi mwenyewe alishiriki katika kuwasaidia wengine wao kupitia fadhili zake za pekee.

14. Ni nini kinachowachochea Wakristo waseja kumkaribia Yehova zaidi?

14 Kama Ana na Dorkasi, wengi katika makutaniko leo wanajikuta wakiwa waseja katika miaka yao ya baadaye ya maisha. Huenda wengine hawajapata mwenzi wa ndoa anayefaa. Wengine wao wametalikiana au ni wajane. Mara nyingi Wakristo waseja wanajifunza kumtegemea zaidi Yehova kwa kuwa hawana mwenzi wa ndoa wa kuzungumza naye mambo yao ya kibinafsi. (Met. 16:3) Silvia, dada mseja ambaye ametumika Betheli kwa miaka zaidi ya 38, anaona hiyo kuwa baraka. Anakubali hivi: “Nyakati nyingine ninachoka kujitia nguvu. Ninajiuliza, ‘Ni nani atakayenitia moyo?’” Lakini anaongezea hivi: “Kuwa na hakika kwamba Yehova anajua kile ninachohitaji kuliko ninavyojua kunanisaidia kumkaribia zaidi. Na sikuzote ninapata kitia-moyo, nyakati nyingine kutoka vyanzo ambavyo sitazamii kamwe.” Kila mara tunapomkaribia Yehova zaidi, anatenda sikuzote kwa njia ya upendo kabisa na yenye kutia moyo.

15. Wakristo ambao hawajafunga ndoa wanaweza ‘kupanuka’ jinsi gani katika upendo wao?

15 Useja ni nafasi ya pekee ya ‘kupanuka’ katika upendo. (Soma 2 Wakorintho 6:11-13.) Jolene, dada mseja ambaye amekuwa katika utumishi wa wakati wote kwa miaka 34, anasema hivi: “Nimejitahidi sana kuanzisha urafiki wa karibu na watu wa kila aina, si watu tu wa umri wangu. Useja ni nafasi nzuri sana ya kumtumikia Yehova, familia yako, na ndugu na dada zako, na pia majirani wako. Kadiri ninavyozeeka, ndivyo ninavyofurahia zaidi hali yangu ya useja.” Bila shaka, watu waliozeeka, wagonjwa, wazazi wasio na wenzi, vijana, na wengine katika kutaniko wanathamini utegemezo usio wa kichoyo ambao wanapata kutoka kwa waseja. Kwa kweli, kila mara tunapowaonyesha wengine upendo, tunapata furaha sisi wenyewe. Je, wewe pia unaweza ‘kupanuka’ katika kuwapenda wengine?

Kuwa Mseja Muda Wote wa Maisha

16. (a) Kwa nini Yesu alibaki mseja muda wote wa maisha yake? (b) Paulo alitumia jinsi gani kwa hekima useja wake?

16 Yesu hakuoa; alihitaji kujitayarisha kwa ajili ya huduma aliyopewa na kisha kuitimiza. Alisafiri sehemu mbalimbali, akitumika kuanzia mapema asubuhi mpaka usiku kabisa, na mwishowe alitoa uhai wake kuwa dhabihu. Useja wake ulikuwa na faida. Mtume Paulo alisafiri maelfu ya kilomita na alipata matatizo makubwa sana katika huduma. (2 Kor. 11:23-27) Ingawa huenda mwanzoni alikuwa ameoa, Paulo alichagua kubaki mseja baada ya kupewa mgawo wa kuwa mtume. (1 Kor. 7:7; 9:5) Yesu na Paulo waliwahimiza wengine waige mfano wao ikiwezekana kwa ajili ya huduma. Hata hivyo, hakuna yeyote kati yao aliyeagiza kwamba useja unapaswa kuwa takwa kwa wahudumu Wakristo.—1 Tim. 4:1-3.

17. Watu fulani leo wamefuata jinsi gani hatua za Yesu na Paulo, na kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova anawathamini wale wanaojidhabihu kwa njia hiyo?

17 Vivyo hivyo, watu fulani leo wamechagua wenyewe kubaki waseja ili waweze kutimiza vizuri zaidi huduma yao. Harold, aliyetajwa mwanzoni, amefurahia utumishi wa Betheli kwa miaka zaidi ya 56. Anasema hivi: “Kufikia wakati ambapo nilikuwa nimetumika Betheli kwa miaka kumi, nilikuwa nimeona wenzi wengi wa ndoa wakiondoka Betheli kwa sababu ya ugonjwa au ili kumtunza mzazi aliyezeeka. Wazazi wangu wote wawili walikuwa wamekufa. Lakini nilipenda Betheli sana hivi kwamba sikutaka kuhatarisha pendeleo hilo kwa kuoa.” Pia, miaka mingi iliyopita, Margaret, painia aliyetumika kwa muda mrefu alisema hivi: “Nilipata watu waliotaka kunioa, lakini sikuolewa kwa sababu ya utumishi wangu. Badala yake, nilitumia uhuru wangu mwingi nikiwa mseja kuongeza huduma yangu, na hilo limeniletea furaha nyingi.” Bila shaka, Yehova hatamsahau kamwe mtu yeyote anayejidhabihu bila uchoyo kwa njia hiyo kwa ajili ya ibada ya kweli.—Soma Isaya 56:4, 5.

Tumia Vizuri Kabisa Hali Zako

18. Wengine wanaweza kuwatia moyo na kuwategemeza jinsi gani Wakristo waseja?

18 Tunapaswa kuwapongeza kutoka moyoni na kuwatia moyo Wakristo wote ambao hawajafunga ndoa na ambao wanajitahidi kabisa kumtumikia Yehova. Tunampenda kila mmoja wao kwa sababu ya sifa zake na kwa sababu ya mambo mengi wanayofanya kutanikoni. Hawatahisi upweke kamwe ikiwa kwa kweli tutakuwa “ndugu au dada au mama au baba au watoto” wao wa kiroho.—Soma Marko 10:28-30.

19. Unaweza kufanya nini ili utumie vizuri kabisa useja wako?

19 Iwe wewe ni mseja kwa sababu umechagua mwenyewe kuwa mseja au kwa sababu tu ya hali, mifano ya watu wanaotajwa katika Maandiko na mifano ya watu leo na ikuhakikishie kwamba unaweza kuwa na maisha yenye furaha na mafanikio. Kuna zawadi fulani ambazo tunatazamia kwa hamu kupata, lakini kuna nyingine ambazo hatutazamii kamwe. Kuna zawadi fulani ambazo tunazithamini papo hapo, lakini nyingine tunazithamini tu baada ya muda kupita. Hivyo basi, mengi yanategemea mtazamo wetu. Unaweza kufanya nini ili utumie vizuri kabisa useja wako? Mkaribie Yehova zaidi, uwe na mengi ya kufanya katika utumishi wa Mungu, na upanuke katika upendo wako kwa wengine. Useja pia unaweza kuthawabisha kama ndoa tukiwa na maoni kama ya Mungu kuhusu useja na kutumia zawadi hiyo kwa hekima.

Je, Unakumbuka?

• Useja unaweza kuwa zawadi katika njia gani mbalimbali?

• Useja unaweza jinsi gani kuwa baraka wakati wa ujana?

• Wakristo waseja wana nafasi gani za kumkaribia Yehova zaidi na kupanuka katika upendo wao?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 18]

Je, unatumia vizuri kabisa nafasi ambazo unapata katika utumishi wa Mungu?