Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unachukia Uasi-sheria?

Je, Unachukia Uasi-sheria?

Je, Unachukia Uasi-sheria?

“Nawe [Yesu] ukauchukia uasi-sheria.”—EBR. 1:9.

1. Yesu alifundisha nini kuhusu upendo?

AKIKAZIA kwamba upendo ni jambo la maana, Yesu Kristo aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Ninawapa ninyi amri mpya, kwamba mpendane; kama vile ambavyo nimewapenda ninyi, ninyi nanyi mpendane vivyo hivyo. Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.” (Yoh. 13:34, 35) Yesu aliwaamuru wafuasi wake waonyeshane upendo wa kujidhabihu. Upendo huo ndio ungewatambulisha. Yesu aliwahimiza hivi pia: “Endeleeni kuwapenda adui zenu na kusali kwa ajili ya wale wanaowatesa ninyi.”—Mt. 5:44.

2. Wafuasi wa Kristo wanapaswa kusitawisha chuki kuelekea nini?

2 Hata hivyo, zaidi ya kuwafundisha wanafunzi wake kuhusu upendo, Yesu aliwafundisha pia jambo ambalo walipaswa kuchukia. Ilisemwa hivi kumhusu Yesu: “Uliupenda uadilifu, nawe ukauchukia uasi-sheria [uovu].” (Ebr. 1:9; Zab. 45:7) Hilo linaonyesha kwamba hatupaswi tu kusitawisha upendo kwa ajili ya uadilifu bali pia ni lazima tusitawishe chuki kuelekea dhambi, au uasi-sheria. Ni vizuri kujua kwamba mtume Yohana alitaja hivi waziwazi: “Kila mtu aliye na mazoea ya kufanya dhambi anazoea pia kufanya uasi-sheria, na kwa hiyo dhambi ni uasi-sheria.”—1 Yoh. 3:4.

3. Kuhusiana na kuchukia uasi-sheria, habari hii itazungumzia mambo gani ya maisha?

3 Hivyo basi, tukiwa Wakristo tunapaswa kujiuliza hivi: ‘Je, ninachukia uasi-sheria?’ Acheni tuchunguze jinsi tunavyoweza kuonyesha kwamba tunachukia mabaya katika mambo manne yafuatayo ya maisha: (1) mtazamo wetu kuelekea kunywa pombe kupita kiasi, (2) maoni yetu kuhusu mambo ya uchawi, (3) maoni yetu kuhusu mwenendo mpotovu wa kingono, na (4) mtazamo wetu kuelekea watu wanaopenda uasi-sheria.

Usiwe Mtumwa wa Pombe

4. Kwa nini Yesu alikuwa na uhuru wa kusema alipotoa onyo kuhusu kunywa pombe kupita kiasi?

4 Katika pindi fulani, Yesu alikunywa divai, akitambua kwamba divai ni zawadi kutoka kwa Mungu. (Zab. 104:14, 15) Hata hivyo, hakutumia vibaya kamwe zawadi hiyo kwa kunywa kupita kiasi. (Met. 23:29-33) Hivyo basi, Yesu alikuwa na uhuru wa kusema alipotoa shauri kuhusu zoea hilo. (Soma Luka 21:34.) Kunywa pombe kupita kiasi kunaweza kuongoza kwenye dhambi nyingine nzito. Hivyo, mtume Paulo aliandika hivi: “Msiwe mkilewa divai, ambayo ina upotovu ndani yake, bali endeleeni kujazwa na roho.” (Efe. 5:18) Pia, aliwahimiza wanawake wenye umri mkubwa katika kutaniko wasiwe “watumwa wa divai nyingi sana.”—Tito 2:3.

5. Wale wanaoamua kunywa pombe wanaweza kujiuliza maswali au maulizo gani?

5 Ikiwa utaamua kunywa pombe, unapaswa pia kujiuliza hivi: ‘Je, nina maoni kama ya Yesu kuhusu kunywa pombe kupita kiasi? Ikiwa ninahitaji kuwashauri wengine kuhusu jambo hilo, je, nina uhuru wa kusema? Je, ninakunywa pombe ili kuepuka mahangaiko au kupunguza mikazo ya maisha? Ninakunywa kiasi gani cha pombe kila juma? Ninatenda jinsi gani mtu fulani anaposema kwamba huenda ninakunywa pombe kupita kiasi? Je, ninajitetea au hata kumfungia mtu huyo kinyongo moyoni?’ Kujiachilia kuwa watumwa wa pombe kunaweza kuharibu uwezo wetu wa kufikiria mambo vizuri na kufanya maamuzi yenye hekima. Wafuasi wa Kristo wanajitahidi kulinda uwezo wao wa kufikiri.—Met. 3:21, 22.

Epuka Mazoea ya Uchawi

6, 7. (a) Yesu alishughulika jinsi gani na Shetani na roho waovu? (b) Kwa nini mazoea ya uchawi yameenea sana leo?

6 Alipokuwa duniani, Yesu alimpinga kabisa Shetani na roho waovu. Alishinda kabisa mashambulizi ya Shetani ya moja kwa moja yaliyokusudiwa kuvunja ushikamanifu wake. (Luka 4:1-13) Alitambua pia na kushinda majaribu mengine yasiyo ya waziwazi ambayo yalikusudiwa kubadili mawazo na matendo yake. (Mt. 16:21-23) Yesu aliwasaidia watu waliostahili ili watoke chini ya utawala wenye ukatili wa roho waovu.—Marko 5:2, 8, 12-15; 9:20, 25-27.

7 Baada ya Yesu kuwekwa rasmi kuwa Mfalme mwaka wa 1914, alisafisha mbingu na kuondoa uvutano wenye kuchafua wa Shetani na roho waovu. Matokeo ni kwamba—sasa kuliko wakati mwingine wowote—Shetani ameazimia ‘kuipotosha dunia nzima inayokaliwa.’ (Ufu. 12:9, 10) Hivyo, hatupaswi kushangaa kwamba mambo ya uchawi yameenea sana na watu wengi wanazidi kuvutiwa na mambo hayo. Ni hatua gani ambazo tunaweza kuchukua ili kujilinda?

8. Kila mmoja wetu anapaswa kujichunguza jinsi gani kuhusiana na vitumbuizo anavyochagua?

8 Biblia inaonya waziwazi kuhusu hatari zinazohusiana na kuwasiliana na pepo. (Soma Kumbukumbu la Torati 18:10-12.) Leo, Shetani na roho waovu wanapotosha fikira za watu kupitia sinema, vitabu, na michezo ya kompyuta inayowachochea watu wapende mazoea ya uchawi. Kwa hiyo, tunapochagua vitumbuizo, kila mmoja wetu anapaswa kujiuliza hivi: ‘Katika miezi iliyopita, je, nimechagua kutumbuizwa na sinema, vipindi vya televisheni, michezo ya kompyuta, vitabu, au vichekesho ambavyo vinahusisha mazoea ya uchawi? Je, ninaelewa kwamba ni jambo la maana kupinga uvutano wa mambo ya uchawi, au je, ninapuuza hatari hizo? Je, hata nimefikiria jinsi ambavyo huenda Yehova atahisi kuhusu vitumbuizo ninavyochagua? Ikiwa nimekaribisha uvutano huo wa kishetani, je, kumpenda Yehova na kanuni zake za uadilifu kutanichochea kufanya uamuzi thabiti na kukataa kabisa uvutano huo?’—Mdo. 19:19, 20.

Tii Onyo la Yesu Kuhusu Mwenendo Mpotovu Kingono

9. Mtu anaweza jinsi gani kusitawisha upendo kuelekea uasi-sheria?

9 Yesu alitetea viwango vya Yehova kuhusu maadili ya ngono. Alisema hivi: “Je, hamkusoma kwamba yeye aliyewaumba hao kutoka mwanzo aliwafanya mwanamume na mwanamke na kusema, ‘Kwa sababu hiyo mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake, na hao wawili watakuwa mwili mmoja’? Hivi kwamba wao si wawili tena, bali mwili mmoja. Kwa hiyo, kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe.” (Mt. 19:4-6) Yesu alijua kwamba mambo tunayotazama yanaweza kuwa na uvutano juu ya moyo wetu. Kwa hiyo, alisema hivi kwenye Mahubiri yake ya Mlimani: “Ninyi mlisikia kwamba ilisemwa, ‘Usifanye uzinzi.’ Lakini mimi ninawaambia ninyi kwamba kila mtu ambaye anaendelea kumtazama mwanamke na kumtamani tayari amefanya uzinzi pamoja naye moyoni mwake.” (Mt. 5:27, 28) Wale wanaopuuza onyo la Yesu kwa kweli wanasitawisha upendo kuelekea uasi-sheria.

10. Simulia jambo linaloonyesha kwamba mtu anaweza kuacha zoea la kutazama ponografia.

10 Shetani anawachochea watu kupenda mwenendo mpotovu wa kingono kupitia ponografia (picha au habari za ngono). Mfumo wa sasa wa mambo umejaa ponografia. Wale wanaotazama ponografia wanashindwa kuondoa katika akili zao mambo machafu ya ngono. Hata wanaweza kuwa na zoea la kutazama ponografia. Fikiria jambo lililompata Mkristo mmoja. Anasema hivi: “Nilitazama ponografia kisiri. Nilikuwa nikiwazia mambo yasiyo halisi ambayo nilifikiri kwamba hayakuhusiana na utumishi wangu kwa Yehova. Nilijua kwamba zoea hilo lilikuwa baya lakini nilijiambia kwamba bado Mungu anakubali utumishi wangu.” Ni nini kilichomfanya ndugu huyo abadili njia yake ya kufikiri? Anasema hivi: “Niliamua kuwaambia wazee kuhusu tatizo langu, ingawa hilo lilikuwa jambo gumu zaidi ambalo nimewahi kufanya.” Mwishowe ndugu huyo aliacha zoea hilo chafu. Anakubali hivi: “Baada ya kusafisha maisha yangu kwa kuacha dhambi hiyo, mwishowe nilihisi kwamba kwa kweli nilikuwa na dhamiri safi.” Ni lazima wale wanaochukia uasi-sheria wajifunze kuchukia ponografia.

11, 12. Tunaweza kuonyesha jinsi gani kwamba tunachukia uasi-sheria tunapochagua muziki?

11 Muziki na maneno yake yanaweza kuchochea sana hisia zetu na hivyo kuchochea moyo wetu wa mfano. Muziki ni zawadi kutoka kwa Mungu na tangu zamani umetumiwa katika ibada ya kweli. (Kut. 15:20, 21; Efe. 5:19) Lakini ulimwengu mwovu wa Shetani unawachochea watu kupenda muziki unaotukuza maadili mapotovu. (1 Yoh. 5:19) Unaweza kujua jinsi gani kwamba muziki unaosikiliza unakuchafua au hapana?

12 Kwanza, unaweza kujiuliza hivi: ‘Je, nyimbo ambazo ninasikiliza zinatukuza uuaji, uzinzi, uasherati, na kukufuru? Ikiwa ningemsomea mtu mwingine maneno ya nyimbo fulani ninazosikiliza, je, mtu huyo angeona kwamba ninachukia uasi-sheria, au je, maneno hayo yangeonyesha kwamba moyo wangu umechafuliwa?’ Hatuwezi kudai kwamba tunachukia uasi-sheria na wakati huohuo tunautukuza kupitia nyimbo. Yesu alisema kwamba “mambo yanayotoka katika kinywa hutoka moyoni, na mambo hayo humtia mtu unajisi. Kwa mfano, mawazo mabaya hutoka moyoni, mauaji, uzinzi, uasherati, wizi, ushuhuda wa uwongo, makufuru.”—Mt. 15:18, 19; linganisha na Yakobo 3:10, 11.

Uwe na Maoni Kama ya Yesu Kuhusu Wale Wanaopenda Uasi-Sheria

13. Yesu alikuwa na maoni gani kuhusu wale ambao hawakutaka kuacha mwenendo wa dhambi?

13 Yesu alisema kwamba alikuja kuwaita watenda-dhambi, au watu wanaopenda uasi-sheria, ili watubu. (Luka 5:30-32) Hata hivyo, aliwaona jinsi gani wale ambao hawakutaka kuacha mwenendo wao wa dhambi? Yesu alitoa maonyo makali kuhusu kukubali kushawishiwa na watu kama hao. (Mt. 23:15, 23-26) Pia, alisema hivi waziwazi: “Si kila mtu anayeniambia, ‘Bwana, Bwana,’ atakayeingia katika ufalme wa mbinguni, bali yule anayefanya mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni ndiye atakayeingia. Wengi wataniambia siku hiyo [Mungu atakapoleta hukumu], ‘Bwana, Bwana, hatukutoa unabii katika jina lako, na kufukuza roho waovu katika jina lako, na kufanya matendo mengi yenye nguvu katika jina lako?’” Hata hivyo, atawakataa wale wanaozoea kufanya uasi-sheria bila kutubu, na atawaambia hivi: “Ondokeni kwangu.” (Mt. 7:21-23) Kwa nini watahukumiwa kwa njia hiyo? Kwa sababu watu hao hawamheshimu Mungu na wanawaumiza wengine kwa sababu ya mazoea yao ya uasi-sheria.

14. Kwa nini watenda-dhambi wasiotubu wanaondolewa katika kutaniko?

14 Neno la Mungu linaamuru kwamba watenda-dhambi wasiotubu waondolewe katika kutaniko. (Soma 1 Wakorintho 5:9-13.) Ni jambo la maana kufanya hivyo kwa sababu tatu hivi: (1) ili kufanya jina la Yehova libaki bila lawama, (2) ili kulinda kutaniko lisichafuliwe, na (3) ili kumsaidia mtenda-dhambi atubu ikiwezekana.

15. Ikiwa tunataka kuendelea kuwa washikamanifu kwa Yehova tunapaswa kujiuliza maswali gani mazito?

15 Je, tuna maoni kama ya Yesu kuhusu watu ambao wameazimia kuendelea kutenda uasi-sheria? Tunahitaji kufikiria maswali haya: ‘Je, ninapaswa kuchagua kushirikiana kwa ukawaida na mtu ambaye ametengwa au ambaye amejitenga na ushirika wa kutaniko la Kikristo? Namna gani ikiwa ni mtu wa ukoo wa karibu ambaye sasa haishi nyumbani?’ Hali kama hiyo inaweza kujaribu kwelikweli upendo wetu wa uadilifu na ushikamanifu wetu kwa Mungu. *

16, 17. Mama mmoja Mkristo alipatwa na hali gani ngumu, na ni nini kilichomsaidia kuunga mkono mpango wa kuwatenga na ushirika watenda-dhambi wasiotubu?

16 Fikiria jambo lililoonwa kuhusu dada mmoja ambaye mwana wake ni mtu mzima na ambaye wakati mmoja alimpenda Yehova. Hata hivyo, baadaye maishani mwana huyo aliamua kuendelea kufanya uasi-sheria bila kutubu. Kwa hiyo, akatengwa na ushirika wa kutaniko. Dada yetu alimpenda Yehova, lakini pia alimpenda mwana wake na ilikuwa vigumu sana kwake kufuata agizo la Kimaandiko la kuepuka kushirikiana naye.

17 Ungempa dada huyo mashauri gani? Mzee mmoja wa kutaniko alimsaidia kutambua kwamba Yehova alielewa uchungu aliokuwa akihisi. Ndugu huyo alimwomba afikirie uchungu ambao bila shaka Yehova alihisi wakati wanawe fulani wa kimalaika walipoasi. Mzee huyo alizungumza naye na kumwonyesha kwamba ingawa Yehova anajua jinsi hali hiyo inavyoleta uchungu, anataka watenda-dhambi wasiotubu watengwe na ushirika. Dada huyo alithamini kwa moyo wote vikumbusho hivyo na akaunga mkono kwa ushikamanifu mpango wa kutenga na ushirika. * Ushikamanifu kama huo unafanya moyo wa Yehova ufurahi.—Met. 27:11.

18, 19. (a) Tukikatisha uhusiano na mtu anayeendelea na matendo ya uasi-sheria tunaonyesha kwamba tunachukia nini? (b) Matokeo yanaweza kuwa nini tukiwa washikamanifu kwa Yehova na mpango wake?

18 Ikiwa unapambana na hali kama hiyo, tafadhali kumbuka kwamba Yehova anakusikitikia. Unapokatisha uhusiano pamoja na mtu ambaye ametengwa au kujitenga na ushirika, unaonyesha kwamba unachukia mtazamo na matendo yaliyoongoza kwenye hali hiyo. Hata hivyo, unaonyesha pia kwamba unampenda mtenda-dhambi huyo na ungependa afanye jambo ambalo litamletea faida. Ukiwa mshikamanifu kwa Yehova kuna uwezekano mkubwa kwamba mtu aliyetiwa nidhamu atatubu na kumrudia Yehova.

19 Mtu fulani ambaye alikuwa ametengwa na ushirika na baadaye akarudishwa katika kutaniko aliandika hivi: “Ninafurahi kwamba Yehova anawapenda sana watu wake hivi kwamba anahakikisha tengenezo lake linabaki likiwa safi. Hatua ambayo huenda watu wa nje wakaona kwamba ni kali, kwa kweli inafaa na ni hatua ya upendo.” Je, unafikiri kwamba mtu huyo angesaidiwa kufikia uamuzi huo ikiwa washiriki wa kutaniko, kutia ndani familia yake, wangeendelea kuzungumza naye kwa ukawaida alipokuwa ametengwa na ushirika? Tunapounga mkono mpango wa Kimaandiko wa kutenga na ushirika tunaonyesha wazi kwamba tunapenda uadilifu na tunatambua kuwa Yehova ana haki ya kuweka viwango vya mwenendo.

“Chukieni Yaliyo Mabaya”

20, 21. Kwa nini ni jambo la maana kujifunza kuchukia uasi-sheria?

20 Mtume Petro anaonya hivi: “Tunzeni akili zenu, iweni wenye kulinda.” Kwa nini? Kwa sababu “adui yenu, Ibilisi, anatembea huku na huku kama simba anayenguruma, akitafuta kummeza mtu.” (1 Pet. 5:8) Je, mtu huyo atakuwa ni wewe? Hilo linategemea sana jinsi unavyojifunza kuchukia uasi-sheria.

21 Si jambo rahisi kusitawisha chuki kuelekea mambo mabaya. Tunazaliwa katika dhambi, na tunaishi katika ulimwengu ambao unatuchochea kufuata tamaa za mwili. (1 Yoh. 2:15-17) Hata hivyo, kwa kumwiga Yesu Kristo na kusitawisha upendo mwingi sana kwa ajili ya Yehova Mungu, tunaweza kufanikiwa kusitawisha chuki kuelekea uasi-sheria. Acheni tuazimie ‘kuchukia yaliyo mabaya,’ tukiwa na hakika kabisa kwamba Yehova ‘anawalinda washikamanifu wake; anawakomboa kutoka katika mkono wa waovu.’—Zab. 97:10.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 15 Ili upate habari zaidi kuhusu jambo hilo, ona gazeti la Mnara wa Mlinzi la Januari 1, 1982 (1/1/1982), ukurasa wa 18-24.

^ fu. 17 Ona pia gazeti la Mnara wa Mlinzi la Januari 15, 2007, ukurasa wa 17-20.

Ungesema Nini?

• Ni nini kitakachotusaidia kuchunguza mtazamo wetu kuelekea pombe?

• Tunaweza kuchukua hatua gani ili kujilinda na mazoea ya uchawi?

• Kwa nini ponografia ni hatari?

• Tunaonyesha jinsi gani kwamba tunachukia uasi-sheria wakati mtu tunayempenda anapotengwa na ushirika?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 29]

Unapaswa kufikiria mambo gani ukiamua kunywa pombe?

[Picha katika ukurasa wa 30]

Jihadhari na uvutano wa kishetani katika vitumbuizo

[Picha katika ukurasa wa 31]

Mtu anayetazama ponografia anasitawisha upendo kuelekea nini?