Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Roho Takatifu Ilivyotumiwa Katika Kazi ya Uumbaji!

Jinsi Roho Takatifu Ilivyotumiwa Katika Kazi ya Uumbaji!

Jinsi Roho Takatifu Ilivyotumiwa Katika Kazi ya Uumbaji!

“Mbingu zilifanywa kwa neno la Yehova, nayo majeshi yake yote yalifanywa kwa roho ya kinywa chake.”—ZAB. 33:6.

1, 2. (a) Ujuzi wa mwanadamu kuhusu mbingu na dunia umeongezeka jinsi gani baada ya muda? (b) Ni swali gani ambalo linahitaji kujibiwa?

WAKATI Albert Einstein alipotangaza katika mwaka wa 1905 nadharia au fundisho lake la pekee kuhusu uwiano au ulinganifu wa vitu, yeye na wanasayansi wengine wengi waliamini kwamba ulimwengu ulikuwa na kundi moja tu la nyota, yaani, Kundi la Kilimia. Walikosea kama nini kuhusu ukubwa wa ulimwengu! Kwa sasa inafikiriwa kwamba mbingu zina makundi zaidi ya bilioni 100 ya nyota, mengine yana mabilioni ya nyota. Darubini zenye nguvu zaidi zinapoendelea kutumiwa duniani au kuwekwa angani kuizunguka dunia, idadi ya makundi ya nyota yanayogunduliwa inazidi kuongezeka.

2 Kama vile tu ambavyo watu hawakuwa na ujuzi mwingi wa kisayansi kuhusu mbingu mwaka wa 1905, vivyo hivyo hawakuwa na ujuzi mwingi kuhusu dunia. Ni kweli kwamba watu walioishi katika karne iliyopita walijua mambo mengi zaidi kuliko mababu zao. Hata hivyo, leo umaridadi na maajabu ya uhai na mifumo ya dunia inayoutegemeza uhai inaeleweka vizuri zaidi kuliko wakati huo. Na bila shaka tutajifunza mengi zaidi kuhusu dunia na mbingu katika miaka ijayo. Lakini ni vizuri hasa kujiuliza, Vitu vyote hivi vilitokea jinsi gani? Tunaweza kupata jibu la swali au ulizo hilo kwa sababu tu Muumba amelifunua kupitia Maandiko Matakatifu.

Muujiza wa Uumbaji

3, 4. Mungu aliumba ulimwengu mzima jinsi gani, na kazi zake zinamtukuza namna gani?

3 Mstari wa kwanza wa Biblia unaeleza jinsi ulimwengu wote ulivyotokea: “Hapo mwanzo Mungu aliumba mbingu na dunia.” (Mwa. 1:1) Yehova alipoanza kuumba hakukuwa na kitu chochote, alitumia roho yake takatifu, yaani, nguvu yake nyingi ya utendaji, ili kuumba mbingu, dunia, na kila kitu katika ulimwengu. Fundi anatumia mikono yake na vifaa vya kazi ili kutengeneza vitu, lakini Mungu anatuma roho yake takatifu ili kutimiza kazi zake kubwa.

4 Maandiko yanasema kwa njia ya mfano kwamba roho takatifu ni “kidole” cha Mungu. (Luka 11:20; Mt. 12:28) Na “kazi ya mikono yake”—ambayo Yehova aliumba kupitia roho yake takatifu—inamletea utukufu mwingi. Mtunga-zaburi Daudi aliimba hivi: “Mbingu zinatangaza utukufu wa Mungu, nalo anga linatangaza kazi ya mikono yake.” (Zab. 19:1) Kwa kweli, uumbaji ambao unaonekana unaonyesha waziwazi nguvu za ajabu za roho takatifu ya Mungu. (Rom. 1:20) Unafanya hivyo jinsi gani?

Nguvu za Mungu Zisizo na Mipaka

5. Toa mfano unaoonyesha nguvu za uumbaji za roho takatifu ya Yehova.

5 Ulimwengu wetu mkubwa isivyowazika unathibitisha kwamba nishati na nguvu za Yehova hazina mipaka. (Soma Isaya 40:26.) Leo, wanasayansi wanajua kwamba vitu fulani vinaweza kugeuzwa kuwa nishati au nguvu, na nishati inaweza kugeuzwa kuwa kitu. Jua letu, ambalo ni nyota, ni mfano wa kitu kinachoweza kugeuzwa kuwa nishati au nguvu. Kila sekunde, jua linageuza tani milioni nne hivi za vitu vya asili vilivyomo ili kutokeza mwangaza wa jua, joto, na aina nyingine za nishati au nguvu. Kiasi kidogo sana cha nguvu hizo ambacho kinatufikia kinatosha kutegemeza uhai duniani. Bila shaka, nishati na nguvu nyingi zaidi zilihitajiwa ili kuumba si jua tu bali pia mabilioni yote ya nyota. Yehova ana nguvu nyingi sana kuliko nguvu zilizohitajiwa kuumba vitu hivyo.

6, 7. (a) Kwa nini tunaweza kusema kwamba Mungu ametumia roho yake takatifu kwa njia yenye utaratibu? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba ulimwengu wote haukujitokeza wenyewe tu?

6 Kuna mambo mengi yanayotuonyesha kwamba Mungu alitumia roho yake takatifu kwa njia yenye utaratibu sana. Kwa mfano: Tuseme una sanduku ambalo lina mipira ya rangi tofauti-tofauti. Unalitikisa sanduku hilo na kuichanganya kabisa mipira hiyo. Kisha, unaimwaga mipira yote chini. Je, ungetazamia mipira ya rangi moja ijikusanye pamoja, yaani, mipira ya bluu iwe pamoja, ya manjano vivyo hivyo, na kadhalika? Bila shaka hapana! Kwa kawaida, matendo yanayofanywa bila mpango hayatokezi utaratibu, wala mpangilio mzuri. Ukweli huo umekubaliwa kuwa sheria ya msingi ya asili. *

7 Hata hivyo, tunapoinua macho yetu juu na kutazama mbinguni kwa darubini, tunaona nini? Tunaona mfumo mkubwa na wenye mpangilio wa hali ya juu kabisa wa nyota, makundi ya nyota, na sayari, na vitu vyote hivyo vinazunguka kwa usahihi mkubwa. Utaratibu huo haungeweza kujitokeza wenyewe tu bila mpango au kwa vitu kugongana vyenyewe angani kwa aksidenti. Kwa hiyo, tunapaswa kujiuliza, Ni nguvu gani zilizotumiwa mwanzoni ili kutokeza ulimwengu wetu wote wenye utaratibu? Sisi wanadamu hatuna uwezo wa kutambua nguvu hizo kupitia uchunguzi wa kisayansi na utafiti peke yake. Hata hivyo, Biblia inafunua kwamba nguvu hizo ni roho takatifu ya Mungu, nguvu zenye uwezo mkubwa zaidi katika ulimwengu wote. Mtunga-zaburi aliimba hivi: “Mbingu zilifanywa kwa neno la Yehova, nayo majeshi yake yote yalifanywa kwa roho ya kinywa chake.” (Zab. 33:6) Na kwa macho yetu, tunaweza kuona tu sehemu ndogo sana ya “majeshi” hayo ya nyota tunapochunguza anga wakati wa usiku!

Roho Takatifu na Dunia

8. Kwa kweli, tunajua mengi kadiri gani kuhusu kazi za Yehova?

8 Mambo tunayoelewa sasa kuhusu uumbaji ni machache sana yakilinganishwa na mambo yote yaliyopo ya kujifunza. Tunajua mambo machache sana kuhusu kazi za uumbaji za Mungu, kama mwanamume mwaminifu Ayubu alivyosema: “Tazama! Hizo ndizo kingo za njia zake, nao ni mnong’ono ulioje wa jambo lililosikiwa juu yake!” (Ayu. 26:14) Karne nyingi baadaye, Mfalme Sulemani ambaye alichunguza kwa makini sana uumbaji wa Yehova, alisema hivi: “[Mungu] amefanya kila kitu kiwe chenye kupendeza kwa wakati wake. Tena wakati usio na kipimo ameuweka ndani ya moyo wao, ili mwanadamu asiweze kugundua kazi ambazo Mungu wa kweli amefanya tangu mwanzo mpaka mwisho.”—Mhu. 3:11; 8:17.

9, 10. Mungu alitumia nguvu gani wakati alipoiumba dunia, na ni mambo gani yaliyotukia katika siku za kwanza tatu za uumbaji?

9 Hata hivyo, Yehova amefunua mambo ya maana kuhusu kazi zake. Kwa mfano, Maandiko yanatuambia kwamba roho ya Mungu ilikuwa ikitenda juu ya dunia miaka mingi sana iliyopita. (Soma Mwanzo 1:2.) Wakati huo, hakukuwa na nchi kavu na nuru, na inaelekea kwamba hakukuwa na hewa ya kupumua juu ya uso wa dunia.

10 Biblia inaendelea kueleza yale ambayo Mungu alifanya katika siku za uumbaji zilizofuatana. Hizo si siku za saa 24 lakini ni vipindi virefu vya wakati. Katika siku ya kwanza ya uumbaji, Yehova alifanya nuru ianze kuonekana kwenye uso wa dunia. Kazi hiyo ilikamilika wakati mwezi na jua vilipoanza kuonekana wazi duniani. (Mwa. 1:3, 14) Katika siku ya pili, anga lilianza kufanyizwa. (Mwa. 1:6) Sasa, dunia ikawa na maji, nuru, na hewa lakini bado hakukuwa na nchi kavu. Mwanzoni mwa siku ya tatu ya uumbaji, Yehova alitumia roho yake takatifu kutokeza nchi, labda alitumia nguvu nyingi zilizo ndani ya dunia kusukuma mabara au nchi zitokee juu ya bahari. (Mwa. 1:9) Katika siku hiyo ya tatu na katika vipindi vya baadaye vya uumbaji, kulikuwa na matukio mengine yenye kustaajabisha.

Roho Takatifu na Viumbe Hai

11. Utata, usawaziko, na umaridadi wa mimea na wanyama walio hai unafunua nini?

11 Roho ya Mungu ilitokeza pia mimea na wanyama wenye utaratibu wa hali ya juu sana. Katika siku ya tatu mpaka siku ya sita ya uumbaji, Mungu alitumia roho yake takatifu kuumba mimea na wanyama wenye kustaajabisha wa aina mbalimbali. (Mwa. 1:11, 20-25) Hivyo, mimea na wanyama wengi walio hai wanaonyesha utata, usawaziko, na umaridadi unaofunua ubunifu wa hali ya juu zaidi.

12. (a) DNA au ADN inatimiza kazi gani? (b) Tunapaswa kujifunza nini kutokana na kazi inayoendelea kwa mafanikio ya DNA au ADN?

12 Fikiria DNA au ADN (deoksiribonyukilia asidi), moja ya kemikali zinazopitisha tabia za viumbe kutoka kizazi kimoja mpaka kizazi kingine. Viumbe vyote vilivyo hai duniani, kutia ndani viumbe vidogo sana, majani, tembo, nyangumi wa rangi ya bluu, na wanadamu, wanazaana kwa kutumia DNA au ADN. Ingawa viumbe vilivyo duniani vinatofautiana sana, sheria ya urithi inayoongoza tabia nyingi za urithi haibadiliki na imedumisha tofauti zilizopo kati ya aina za msingi za viumbe tangu zamani. Kwa hiyo, kulingana na kusudi la Yehova Mungu, viumbe mbalimbali duniani vinaendelea kutimiza kazi zake katika mfumo wenye kustaajabisha sana wa uhai. (Zab. 139:16) Mpangilio huo mzuri sana na wenye utaratibu unathibitisha zaidi kwamba uumbaji ni kazi ya “kidole” cha Mungu, au roho takatifu.

Upeo wa Uumbaji Duniani

13. Mungu alimuumba mtu jinsi gani?

13 Baada ya miaka mingi sana kupita Mungu alipoumba vitu vingi visivyohesabika vilivyo hai na visivyo hai, dunia haikuwa tena “bila umbo, na ukiwa.” Hata hivyo, Yehova hakuwa amemaliza kutumia roho yake katika kazi ya uumbaji. Sasa alikusudia kuumba kiumbe chake bora zaidi duniani. Mwishoni mwa siku ya sita ya uumbaji, Mungu alimuumba mtu. Yehova alifanya hivyo jinsi gani? Alifanya hivyo kwa kutumia roho yake takatifu na vitu vya asili vilivyo duniani.—Mwa. 2:7.

14. Wanadamu wanatofautiana na wanyama katika njia gani kubwa?

14 Andiko la Mwanzo 1:27 linasema hivi: “Mungu akamuumba mtu kwa mfano wake, kwa mfano wa Mungu alimuumba; mwanamume na mwanamke aliwaumba.” Kuumbwa kwa mfano wa Mungu kunamaanisha kwamba Yehova alituumba tukiwa na uwezo wa kuonyesha upendo, kutumia uhuru wa kuchagua, na hata kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Muumba wetu. Kwa hiyo, ubongo wetu ni tofauti kabisa na ubongo wa wanyama. Yehova aliumba ubongo wa mwanadamu kwa njia ambayo inatuwezesha hasa kufurahia kuendelea kujifunza milele kumhusu yeye na kazi zake.

15. Adamu na Hawa walikuwa na tarajio gani?

15 Mwanzoni mwa maisha ya wanadamu, Mungu alimpa Adamu na mke wake, Hawa, dunia na kazi zote za ajabu zilizomo ili waichunguze na kufurahia maisha. (Mwa. 1:28) Yehova aliwapa chakula kingi na makao ya paradiso. Walikuwa na pendeleo la kuishi milele na kuwa wazazi wenye upendo wa mabilioni ya wazao wao wakamilifu. Hata hivyo, mambo yalibadilika.

Kuthamini Daraka la Roho Takatifu

16. Ingawa wanadamu wa kwanza waliasi, tuna tumaini gani?

16 Badala ya kumtii kwa shukrani Muumba wao, kwa uchoyo Adamu na Hawa waliasi. Wanadamu wote wasio wakamilifu wametokana nao na hivyo wanateseka. Lakini Biblia inaeleza jinsi Mungu atakavyokomesha madhara yote yaliyosababishwa na dhambi ya wazazi wetu wa kwanza. Maandiko pia yanaonyesha kwamba Yehova atatimiza kusudi lake la kwanza. Dunia itakuwa paradiso iliyojaa watu wenye furaha, afya nzuri, na watakaopata baraka ya uzima wa milele. (Mwa. 3:15) Ili tuendelee kuwa na imani katika tumaini hilo lenye kutia moyo, tunahitaji msaada wa roho takatifu ya Mungu.

17. Tunapaswa kuepuka mawazo gani?

17 Tunapaswa kusali ili kumwomba Yehova roho takatifu. (Luka 11:13) Kufanya hivyo kutatusaidia kuutia nguvu usadikisho wetu wa kwamba uumbaji ni kazi ya mikono ya Mungu. Leo, imani ya kwamba hakuna Mungu na propaganda za mageuzi ambazo zinategemea uwongo usio na msingi zinazidi kuongezeka. Hatupaswi kuruhusu mawazo hayo mengi yenye makosa yatuvuruge au kutuogopesha. Ni lazima Wakristo wote wajitayarishe kupinga mafundisho hayo na kutokubali kusongwa na watu wanaoyafuata.—Soma Wakolosai 2:8.

18. Tunapotafakari juu ya mwanzo wa ulimwengu na wanadamu, kwa nini ni jambo lisilopatana na akili kusema kwamba hakuna Muumba mwenye akili?

18 Bila shaka, kuchunguza kwa unyoofu uthibitisho unaounga mkono uumbaji kutatia nguvu imani yetu katika Biblia na katika Mungu. Watu wengi wanapotafakari juu ya mwanzo wa ulimwengu na wanadamu, hawakubali wazo la kwamba nguvu fulani ambazo hazipatikani katika ulimwengu zilihusika. Hata hivyo, ikiwa tungezungumzia mambo hayo tukiwa na maoni kama hayo, hatungekuwa tukipima uthibitisho wote kwa haki. Zaidi ya hayo, tungekuwa tukipuuza uumbaji mbalimbali wenye utaratibu na wenye kusudi ambao unaonekana waziwazi na ‘ambao hauna hesabu.’ (Ayu. 9:10; Zab. 104:25) Tukiwa Wakristo, tuna hakika kwamba nguvu ya utendaji iliyohusika katika uumbaji ni roho takatifu iliyoongozwa na Yehova kwa akili.

Roho Takatifu na Imani Yetu Katika Mungu

19. Ni nini kinachotuhakikishia kwamba Mungu yupo na roho yake takatifu inafanya kazi?

19 Hatuhitaji kujua mambo yote kuhusu uumbaji ili tumwamini Mungu na pia kumpenda na kumheshimu sana. Kama ilivyo katika urafiki wa kibinadamu, kumwamini Yehova hakutegemei tu mambo yaliyothibitishwa. Kama vile tu uhusiano kati ya marafiki unavyokua wanapoendelea kujuana vizuri, imani yetu katika Mungu inaongezeka tunapojifunza mengi kumhusu. Kwa kweli, tunakuwa na hakika zaidi kwamba yupo anapojibu sala zetu na tunaona faida za kufuata kanuni zake katika maisha yetu. Tunamkaribia zaidi Yehova tunapoona uthibitisho unaoongezeka wa kwamba anaongoza hatua zetu, anatulinda, anabariki jitihada zetu katika utumishi wake, na anatupatia vitu tunavyohitaji. Mambo yote hayo yanatuhakikishia kabisa kwamba Mungu yupo na roho yake takatifu inafanya kazi.

20. (a) Kwa nini Mungu aliumba ulimwengu na mwanadamu? (b) Matokeo yatakuwa nini ikiwa tutaendelea kufuata mwongozo wa roho takatifu ya Mungu?

20 Biblia ni mfano mzuri sana unaoonyesha jinsi Yehova anavyotumia nguvu yake ya utendaji kwa sababu waandikaji wa Biblia “walisema yaliyotoka kwa Mungu kama walivyoongozwa na roho takatifu.” (2 Pet. 1:21) Kujifunza Maandiko kwa makini kunaweza kujenga imani yetu katika Mungu akiwa Muumba wa vitu vyote. (Ufu. 4:11) Yehova aliamua kuwa Muumba ili aonyeshe sifa yake yenye kuvutia sana ya upendo. (1 Yoh. 4:8) Kwa hiyo, acheni tufanye yote tunayoweza ili kuwasaidia wengine wajifunze kumhusu Baba na Rafiki yetu wa mbinguni mwenye upendo. Ikiwa kila mmoja wetu ataendelea kuongozwa na roho ya Mungu, tutapata pendeleo la kujifunza milele kumhusu. (Gal. 5:16, 25) Basi, kila mmoja wetu na aendelee kujifunza kumhusu Yehova na kazi zake kuu na kutafakari katika maisha yetu kuhusu upendo usio na mipaka ambao alionyesha alipotumia roho yake takatifu kuumba mbingu, dunia, na wanadamu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Ona ukurasa wa 24 na 25 wa kitabu Je, Kuna Muumba Anayekujali?

Je, Unaweza Kueleza?

• Kuwapo kwa mbingu na dunia kunatufundisha nini kuhusu jinsi Mungu anavyotumia roho takatifu?

• Kwa kuwa tumeumbwa kwa mfano wa Mungu, tuna nafasi gani?

• Kwa nini tunahitaji kuchunguza uthibitisho wa uumbaji?

• Uhusiano wetu pamoja na Yehova unaweza kukua katika njia gani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 7]

Utaratibu ambao tunaona katika ulimwengu wote unatufundisha nini kuhusu uumbaji?

[Hisani]

Stars: Anglo-Australian Observatory/David Malin Images

[Picha katika ukurasa wa 8]

DNA au ADN inahusika jinsi gani katika vitu hivi vyote?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Je, umejitayarisha kuitetea imani yako?