Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kukubaliwa na Mungu Kunaongoza Kwenye Uzima wa Milele

Kukubaliwa na Mungu Kunaongoza Kwenye Uzima wa Milele

Kukubaliwa na Mungu Kunaongoza Kwenye Uzima wa Milele

“Wewe mwenyewe utambariki mtu yeyote aliye mwadilifu, Ee Yehova; kana kwamba kwa ngao kubwa, utawazunguka pande zote kwa kibali chako.”—ZAB. 5:12.

1, 2. Eliya alimwomba nini mjane mmoja aliyeishi huko Sarefathi, naye alimhakikishia nini?

MWANAMKE fulani na mwana wake walikuwa na njaa, na nabii wa Mungu pia alikuwa na njaa. Mjane huyo aliyeishi huko Sarefathi alipokuwa akijitayarisha kuwasha moto ili apike chakula, nabii Eliya alimwomba maji na mkate. Mjane huyo alikuwa tayari kumpa kitu cha kunywa, lakini hakuwa na chakula kingine isipokuwa “mkono mmoja tu wa unga katika mtungi mkubwa na mafuta kidogo katika mtungi mdogo.” Alihisi kwamba hakuwa na chakula chochote ambacho angempa nabii huyo na hata alimwambia hivyo.—1 Fal. 17:8-12.

2 Eliya alisisitiza hivi: “Ila tu unitayarishie kwanza keki ndogo ya mviringo kutokana na kile kilichopo, nawe uniletee hiyo, na unaweza kutayarisha kitu kwa ajili yako na mwana wako baadaye. Kwa maana Yehova Mungu wa Israeli, amesema hivi, ‘Ule mtungi mkubwa wa unga hautamalizika, na ule mtungi mdogo wa mafuta hautapungua.’”—1 Fal. 17:13, 14.

3. Ni jambo gani zito zaidi lililo mbele yetu?

3 Jambo ambalo mjane huyo alihitaji kuamua lilikuwa zito zaidi kuliko kuamua tu kile ambacho angefanya na chakula kidogo alichokuwa nacho. Je, angemtegemea Yehova amwokoe pamoja na mwana wake, au angetanguliza mahitaji yake ya kimwili badala ya kupata kibali cha Mungu na urafiki wake? Sisi sote tunakabili jambo kama hilo. Je, tutahangaikia zaidi kupata kibali cha Yehova kuliko kutafuta usalama wa kimwili? Tuna kila sababu ya kumtegemea na kumtumikia Mungu. Na kuna hatua ambazo tunaweza kuchukua ili kutafuta na kupata kibali chake.

‘Unastahili Kupokea Ibada’

4. Kwa nini Yehova anastahili kupokea ibada yetu?

4 Yehova ana haki ya kutazamia wanadamu wamtumikie kwa njia inayokubalika. Kikundi kimoja cha watumishi wake wa kimbingu kilithibitisha ukweli huo kwa umoja, kilisema: “Unastahili, Ee Yehova, naam, Mungu wetu, kupokea utukufu na heshima na nguvu, kwa sababu uliumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilikuwako navyo vikaumbwa.” (Ufu. 4:11) Yehova anastahili kupokea ibada yetu kwa kuwa yeye ndiye Muumba.

5. Kwa nini upendo wa Mungu unapaswa kutuchochea kumtumikia?

5 Sababu nyingine inayotufanya tumtumikie Yehova ni kwamba anatupenda kuliko mtu mwingine yeyote yule. Biblia inasema: “Mungu akamuumba mtu kwa mfano wake, kwa mfano wa Mungu alimuumba; mwanamume na mwanamke aliwaumba.” (Mwa. 1:27) Mwanadamu ana uhuru wa kuchagua, Mungu amemuumba akiwa na uwezo wa kufikiri na kufanya maamuzi. Yehova alitupatia uhai na hivyo akawa Baba wa wanadamu. (Luka 3:38) Kama anavyofanya baba yeyote mzuri, Yehova amefanya yote ili kuandaa mambo ambayo wana na mabinti wake wanahitaji ili wafurahie maisha. “Hulichomoza jua lake” na “hunyesha mvua,” ili Dunia yetu izae chakula kingi kwa ajili yetu katika mazingira yaliyo maridadi kabisa.—Mt. 5:45.

6, 7. (a) Ni madhara gani ambayo Adamu aliwaletea wazao wake wote? (b) Dhabihu ya Kristo itawanufaisha jinsi gani wale wanaotafuta kibali cha Mungu?

6 Yehova pia ametuokoa kutokana na madhara mabaya sana ya dhambi. Adamu alipotenda dhambi alikuwa kama mchezaji wa kamari ambaye anaibia familia yake ili acheze mchezo huo. Alipomwasi Yehova, Adamu aliwaibia watoto wake tumaini lao la kupata furaha milele. Uchoyo wake uliwafanya wanadamu kuwa watumwa wa bwana mkatili, yaani, kutokamilika. Hivyo, wanadamu wote wanalazimika kuwa wagonjwa, kupatwa na huzuni, na mwishowe wanakufa. Ili mtumwa awe huru malipo yanahitaji kutolewa, na Yehova ametoa malipo ambayo yanaweza kutuokoa kutoka katika madhara hayo mabaya. (Soma Waroma 5:21.) Yesu Kristo alitenda kulingana na mapenzi ya Baba yake kwa kutoa “nafsi yake kuwa fidia badala ya wengi.” (Mt. 20:28) Hivi karibuni wale ambao wamekubaliwa na Mungu watapata faida kamili zinazotokana na malipo hayo ya fidia au dhabihu ya ukombozi.

7 Muumba wetu, Yehova, amefanya mengi zaidi kuliko mtu mwingine yeyote ili tuwe na maisha yenye furaha na kusudi. Tukipata kibali chake, tutaweza kuona jinsi atakavyoondoa madhara yote ambayo yameipata jamii ya wanadamu. Yehova ataendelea kumwonyesha kila mmoja wetu jinsi alivyo “mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.”—Ebr. 11:6.

“Watu Wako Watajitoa kwa Hiari”

8. Kisa cha Isaya kinatufundisha nini kuhusu kumtumikia Mungu?

8 Ili tukubaliwe na Mungu tunapaswa pia kutumia vizuri uhuru wetu wa kuchagua. Tunapaswa kufanya hivyo kwa sababu Yehova hamlazimishi mtu yeyote amtumikie. Katika siku za Isaya, Mungu aliuliza hivi: “Nitamtuma nani, na ni nani atakayeenda kwa ajili yetu?” Yehova alimheshimu nabii huyo kwa kutambua haki yake ya kuamua. Fikiria jinsi Isaya alivyofurahi alipojibu hivi: “Mimi hapa! Nitume mimi.”—Isa. 6:8.

9, 10. (a) Tunapaswa kumtumikia Mungu tukiwa na mtazamo gani? (b) Kwa nini inafaa tumtumikie Yehova kwa nafsi yote?

9 Wanadamu wana uhuru wa kuchagua kumtumikia Mungu au kutomtumikia. Yehova anataka tumtumikie kwa kupenda. (Soma Yoshua 24:15.) Mtu yeyote ambaye anakataa kumwabudu Mungu hawezi kumpendeza; na Mungu hakubali ibada ya wale ambao kwa kweli wanataka tu kuwafurahisha wanadamu wenzao. (Kol. 3:22) Ikiwa tunatoa utumishi mtakatifu “kwa kusitasita” na kuruhusu mambo ya ulimwengu yaingilie ibada yetu, hatuwezi kupata kibali cha Mungu. (Kut. 22:29) Yehova anajua kwamba ni jambo zuri kwetu kumtumikia kwa nafsi yote. Musa aliwahimiza Waisraeli wachague uzima ‘kwa kumpenda Yehova Mungu wao, kwa kuisikiliza sauti yake na kwa kushikamana naye.’—Kum. 30:19, 20.

10 Mfalme Daudi, wa taifa la kale la Israeli, alimwimbia hivi Yehova: “Watu wako watajitoa kwa hiari katika siku ya jeshi lako. Katika fahari za utakatifu, kutoka tumbo la uzazi la mapambazuko, una kundi lako la vijana kama matone ya umande.” (Zab. 110:3) Watu wengi leo wanatafuta kwanza usalama wa kifedha na raha. Hata hivyo, wale wanaompenda Yehova wanatanguliza utumishi wao mtakatifu badala ya kitu kingine chochote. Bidii yao ya kuhubiri habari njema inaonyesha mambo ambayo wanatanguliza. Wana uhakika kabisa katika uwezo wa Yehova wa kuandaa mahitaji yao ya kila siku.—Mt. 6:33, 34.

Dhabihu Zinazokubaliwa na Mungu

11. Waisraeli walitazamia kupata faida gani kwa kumtolea Yehova dhabihu?

11 Chini ya agano la Sheria, watu wa Mungu walitoa dhabihu zinazokubalika ili wapate kibali chake. Andiko la Mambo ya Walawi 19:5 linasema hivi: “Ikiwa mtamtolea Yehova dhabihu ya ushirika, mtaitoa ili mjipatie kibali.” Tunasoma hivi katika kitabu hichohicho cha Biblia: “Ikiwa mtatoa dhabihu ya shukrani kwa Yehova, mtaitoa ili kupata kibali kwa ajili yenu.” (Law. 22:29) Waisraeli walipotoa dhabihu zinazofaa za wanyama juu ya madhabahu ya Yehova, moshi uliopanda juu ulikuwa kama “harufu ya kumtuliza” Mungu wa kweli. (Law. 1:9, 13) Yehova alitulizwa na kuburudishwa na wonyesho huo wa upendo kutoka kwa watu wake. (Mwa. 8:21) Katika matakwa hayo ya Sheria, tunapata kanuni inayotuhusu leo. Wale wanaomtolea Yehova dhabihu zinazokubalika wanapata kibali chake. Ni dhabihu gani ambazo anakubali? Fikiria mambo haya mawili katika maisha: mwenendo wetu na usemi wetu.

12. Ni mazoea gani ambayo yangefanya ‘kutoa miili yetu kuwa dhabihu’ kuwe chukizo kwa Mungu?

12 Mtume Paulo aliandika hivi katika barua yake kwa Waroma: “Mtoe miili yenu iwe dhabihu iliyo hai, takatifu, yenye kukubalika kwa Mungu, utumishi mtakatifu pamoja na nguvu zenu za kufikiri.” (Rom. 12:1) Ili kupata kibali cha Mungu mtu anahitaji kuhakikisha kwamba mwili wake unakubaliwa na Mungu. Ikiwa mtu angejichafua kwa kuvuta sigara, kutafuna miraa, kutumia dawa za kulevya, au kunywa pombe kupita kiasi, dhabihu hiyo haingekuwa na thamani. (2 Kor. 7:1) Zaidi ya hayo, kwa kuwa yule “aliye na mazoea ya kufanya uasherati anautendea dhambi mwili wake mwenyewe,” mwenendo mpotovu wa aina yoyote unafanya dhabihu yake kuwa chukizo kwa Yehova. (1 Kor. 6:18) Ili kumpendeza Mungu, mtu anapaswa ‘kuwa mtakatifu katika mwenendo wake wote.’—1 Pet. 1:14-16.

13. Kwa nini ni jambo linalofaa tumsifu Yehova?

13 Dhabihu nyingine ambayo Yehova anapendezwa nayo ni nguvu yetu ya usemi. Wale wanaompenda Yehova wanasema sikuzote mambo mazuri kumhusu mbele ya watu wote na katika nyumba zao. (Soma Zaburi 34:1-3.) Soma Zaburi ya 148-150, na uone ni mara ngapi zaburi hizo tatu zinatutia moyo kumsifu Yehova. Kwa kweli, “sifa ni jambo linalofaa kwa wanyoofu.” (Zab. 33:1) Na Kielelezo chetu, Yesu Kristo, alikazia umuhimu wa kumsifu Mungu kwa kuhubiri habari njema.—Luka 4:18, 43, 44.

14, 15. Hosea aliwahimiza Waisraeli watoe dhabihu gani, na Yehova alijibu jinsi gani?

14 Tunapohubiri kwa bidii tunaonyesha kwamba tunampenda Yehova na tunatamani kupata kibali chake. Kwa mfano, fikiria jinsi nabii Hosea alivyowahimiza Waisraeli waliofuata ibada ya uwongo na hivyo wakapoteza kibali cha Mungu. (Hos. 13:1-3) Hosea aliwaambia wasihi hivi: “[Yehova] samehe kosa letu; na ukubali lililo jema, nasi tutatoa ng’ombe-dume wachanga wa midomo yetu.”—Hos. 14:1, 2.

15 Ng’ombe-dume alikuwa mnyama wa bei ghali zaidi ambaye Mwisraeli angemtolea Yehova. Kwa hiyo, “ng’ombe-dume wachanga wa midomo yetu” ni maneno manyoofu, yaliyofikiriwa vizuri ambayo yalisemwa ili kumsifu Mungu wa kweli. Yehova aliwajibu jinsi gani wale waliotoa dhabihu kama hizo? Alisema: “Nitawapenda kwa kupenda kwangu mwenyewe.” (Hos. 14:4) Yehova aliwasamehe wale waliotoa dhabihu kama hizo za sifa, akawakubali, naye akawa rafiki yao.

16, 17. Imani katika Mungu inapomchochea mtu kuhubiri habari njema, Yehova anahisi jinsi gani kuhusu sifa ambayo mtu huyo anamtolea?

16 Sikuzote kumsifu Yehova mbele ya watu wote kumekuwa sehemu ya maana ya ibada ya kweli. Kumtukuza Mungu wa kweli kulikuwa jambo la maana sana kwa mtunga-zaburi hivi kwamba alimsihi Mungu: “Tafadhali furahia matoleo ya hiari ya kinywa changu, Ee Yehova.” (Zab. 119:108) Namna gani leo? Akizungumza kuhusu umati mkubwa wa watu katika wakati wetu, Isaya alitabiri hivi: “Watatangaza sifa za Yehova. . . . Wakiwa na kibali [zawadi zao] watakuja juu ya madhabahu [ya Mungu].” (Isa. 60:6, 7) Katika utimizo wa unabii huo, mamilioni ya watu leo wanamtolea Mungu “dhabihu ya sifa, yaani, tunda la midomo ambayo hulifanyia jina lake tangazo la hadharani.”—Ebr. 13:15.

17 Namna gani wewe? Je, unamtolea Mungu dhabihu zinazokubalika? Ikiwa sivyo, je, utafanya mabadiliko yanayohitajiwa na kuanza kumsifu Yehova mbele ya watu wote? Imani inapokuchochea kuanza kuhubiri habari njema, toleo lako ‘litampendeza Yehova kuliko ng’ombe-dume.’ (Soma Zaburi 69:30, 31.) Uwe na hakika kwamba “harufu ya kutuliza” ya dhabihu yako ya sifa itamfikia Yehova na utapata kibali chake. (Eze. 20:41) Halafu utapata shangwe isiyo na kifani.

‘Yehova Mwenyewe Atambariki Mtu Yeyote Aliye Mwadilifu’

18, 19. (a) Watu wengi wana maoni gani leo kuhusu kumtumikia Mungu? (b) Kupoteza kibali cha Mungu kunasababisha nini?

18 Leo, watu wengi wanakata kauli ileile kama walivyofanya watu fulani katika siku za Malaki: “Ni bure kabisa kumtumikia Mungu; na tumepata faida gani kwa kushika wajibu wake?” (Mal. 3:14, An American Translation) Wakiongozwa na tamaa ya vitu vya kimwili, wanaona kuwa kusudi la Mungu haliwezi kutimizwa na kwamba sheria zake zimepitwa na wakati. Watu hao wanaona kwamba kuhubiri habari njema ni kupoteza wakati na kuwasumbua watu.

19 Mawazo kama hayo yalianza katika bustani ya Edeni. Shetani ndiye aliyemshawishi Hawa apuuze thamani halisi ya maisha mazuri ajabu ambayo Yehova alimpa na hivyo Hawa akadharau kibali cha Mungu. Leo, Shetani anajitahidi sana kuwashawishi watu waamini kwamba mtu hawezi kupata faida yoyote kwa kufanya mapenzi ya Mungu. Hata hivyo, Hawa na mume wake waligundua kwamba kupoteza kibali cha Mungu kulimaanisha kupoteza uhai wao. Wale ambao sasa wanafuata mfano wao mbaya, hivi karibuni watatambua ukweli huo kwa uchungu.—Mwa. 3:1-7, 17-19.

20, 21. (a) Mjane aliyeishi huko Sarefathi alifanya nini, na mambo yalimwendea namna gani? (b) Tunapaswa kumwiga mjane huyo jinsi gani na kwa nini?

20 Fikiria tofauti iliyopo kati ya mwisho wenye kuhuzunisha wa Adamu na Hawa na matokeo ya simulizi lililotajwa mapema kuhusu Eliya na mjane aliyeishi huko Sarefathi. Baada ya kusikiliza maneno ya Eliya yenye kutia moyo, mwanamke huyo alianza kuoka mkate naye akampa kwanza nabii huyo kipande cha mkate. Kisha, Yehova akatimiza ahadi aliyotoa kupitia Eliya. Simulizi hilo linasema hivi: “Mwanamke yule akaendelea kula, yeye pamoja na Eliya na nyumba ya yule mwanamke, kwa siku nyingi. Ule mtungi mkubwa wa unga haukumalizika, wala ule mtungi mdogo wa mafuta haukupungua, kulingana na neno la Yehova alilokuwa amesema kupitia Eliya.”—1 Fal. 17:15, 16.

21 Ni watu wachache sana kati ya mabilioni ya watu wanaoishi leo wanaoweza kufanya jambo ambalo mjane huyo aliyeishi huko Sarefathi alifanya. Alimtegemea kabisa Mungu wa wokovu, naye Mungu hakumwacha bila msaada. Simulizi hilo na masimulizi mengine ya Biblia yanaonyesha kwamba tunapaswa kumtegemea Yehova. (Soma Yoshua 21:43-45; 23:14.) Maisha ya Mashahidi wa Yehova leo yanathibitisha zaidi kwamba Mungu hatawaacha kamwe watu walio na kibali chake.—Zab. 34:6, 7, 17-19. *

22. Kwa nini tunapaswa kutafuta haraka kibali cha Mungu bila kuchelewa?

22 Siku ya Mungu ya hukumu “juu ya wale wote wanaokaa juu ya uso wa dunia yote” inakaribia sana. (Luka 21:34, 35) Hatutaiepuka siku hiyo. Hakuna utajiri au vitu vya kimwili vinavyoweza kulinganishwa na pendeleo la kumsikia Hakimu aliyewekwa rasmi na Mungu akisema: “Njooni, ninyi ambao mmebarikiwa na Baba yangu, urithini ufalme uliotayarishwa kwa ajili yenu.” (Mt. 25:34) Ndiyo, ‘Yehova mwenyewe atambariki mtu yeyote aliye mwadilifu, kana kwamba kwa ngao kubwa, atawazunguka pande zote kwa kibali chake.’ (Zab. 5:12) Je, hatupaswi kutafuta kibali cha Mungu?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 21 Ona gazeti la Mnara wa Mlinzi la Machi 15, 2005, (15/3/2005), ukurasa wa 13, fungu la 15; Agosti 1, 1997, (1/8/1997), ukurasa wa 20-25.

Je, Unakumbuka?

• Kwa nini Yehova anastahili kupokea ibada yetu ya kutoka moyoni?

• Yehova anakubali dhabihu gani leo?

• Maneno “ng’ombe-dume wachanga wa midomo yetu” yanamaanisha nini, na kwa nini tunapaswa kumtolea Yehova ng’ombe-dume hao?

• Kwa nini tunapaswa kutafuta kibali cha Mungu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 13]

Nabii wa Mungu alimwomba mama mmoja maskini aamue jambo gani zito?

[Picha katika ukurasa wa 15]

Tunapata faida gani kwa sababu ya kumtolea Yehova dhabihu ya sifa?

[Picha katika ukurasa wa 17]

Hutakatishwa tamaa kamwe ukimtegemea Yehova kikweli