Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Kutii Ni Bora Kuliko Dhabihu”

“Kutii Ni Bora Kuliko Dhabihu”

“Kutii Ni Bora Kuliko Dhabihu”

SAULI ndiye aliyekuwa mfalme wa kwanza wa taifa la kale la Israeli. Ingawa Sauli alichaguliwa na Mungu wa kweli, mwishowe alikosa kutii.

Sauli alifanya makosa gani? Je, angeweza kuyaepuka? Tunaweza kufaidika jinsi gani kwa kuchunguza mfano wake?

Yehova Atangaza Mfalme Aliyemchagua

Kabla ya Sauli kuwa mfalme, nabii Samweli alikuwa akitumika akiwa mwakilishi wa Mungu katika Israeli. Sasa Samweli alikuwa amezeeka, na watoto wake hawakuwa waaminifu. Wakati huohuo, taifa hilo lilikuwa likitishwa na maadui. Wanaume wazee wa Israeli walipomwomba Samweli aweke rasmi mfalme juu yao ili awahukumu na kuwaongoza katika vita, Yehova alimwambia nabii huyo amtie mafuta Sauli ili awe kiongozi kisha akasema: “Atawaokoa watu wangu kutoka mkononi mwa Wafilisti.”—1 Sam. 8:4-7, 20; 9:16.

Sauli alikuwa ‘kijana mwenye sura nzuri.’ Hata hivyo, hakuchaguliwa kuwa mfalme kwa sababu tu ya sura yake. Alikuwa pia mnyenyekevu. Kwa mfano, Sauli alimuuliza Samweli hivi: “Je, mimi si Mbenyamini wa kutoka katika kabila dogo zaidi kati ya makabila ya Israeli, na je, familia yangu si dhaifu zaidi kati ya familia zote za kabila la Benyamini? Basi kwa nini umeniambia jambo kama hili?” Sauli alikuwa na maoni yenye kiasi juu yake mwenyewe na familia yake, hata ingawa baba yake, Kishi, alikuwa “mtu mwenye nguvu ya mali.”—1 Sam. 9:1, 2, 21.

Fikiria pia jinsi Sauli alivyotenda wakati Samweli alipowatangazia watu yule aliyechaguliwa na Yehova kuwa mfalme wa Israeli. Kwanza, Samweli alimtia mafuta Sauli faraghani na kumwambia hivi: “Jifanyie lile ambalo mkono wako unaweza, kwa sababu Mungu wa kweli yupo pamoja nawe.” Baada ya hapo, nabii Samweli akawakusanya watu ili awatangazie yule aliyechaguliwa na Yehova kuwa mfalme. Hata hivyo, Sauli alipotangazwa, hakupatikana. Sauli alijificha kwa sababu alikuwa mwenye haya. Yehova alifunua mahali ambapo Sauli alikuwa amejificha, na Sauli akatangazwa kuwa mfalme.—1 Sam. 10:7, 20-24.

Katika Uwanja wa Vita

Muda si muda, Sauli alithibitisha kwamba mtu yeyote ambaye huenda alifikiri kwamba hastahili alikosea. Waamoni walipotisha kushambulia mji wa Waisraeli, “roho ya Mungu ikaanza kutenda kazi juu ya Sauli.” Aliamuru mashujaa wa vita wa taifa la Israeli wakusanyike pamoja, akawapanga, na kuwaongoza kupata ushindi. Lakini Sauli alimsifu Mungu kwa kuwaletea ushindi huo, akisema: “Leo Yehova ametimiza wokovu katika Israeli.”—1 Sam. 11:1-13.

Sauli alikuwa na sifa nyingi nzuri na Mungu alimbariki. Pia, alikiri kwamba Yehova ana nguvu. Hata hivyo, Waisraeli na mfalme wao wangeendelea kufanikiwa ikiwa wangefanya jambo moja la maana sana. Samweli aliwaambia watu wa Israeli hivi: “Mkimwogopa Yehova na kumtumikia na kuitii sauti yake kwelikweli, nanyi msipoliasi agizo la Yehova, ninyi pamoja na mfalme atakayetawala juu yenu mtakuwa wafuasi wa Yehova, Mungu wenu.” Waisraeli wangeweza kuwa na uhakika gani ikiwa wangekuwa waaminifu kwa Mungu? Samweli alisema, “Yehova hatawaacha watu wake kwa ajili ya jina lake kuu, kwa sababu Yehova ameamua mwenyewe kuwafanya ninyi kuwa watu wake.”—1 Sam. 12:14, 22.

Kutii kulikuwa jambo la maana sana ili kupata kibali cha Mungu, na bado ni jambo la maana sana leo. Watumishi wa Yehova wanapotii amri zake, anawabariki. Lakini namna gani wasipomtii Yehova?

“Umetenda Kipumbavu”

Shambulizi lililofuata la Sauli juu ya Wafilisti liliwachochea Wafilisti kuchukua hatua kali sana. Jeshi lenye “watu wengi kama chembe za mchanga kando ya bahari” liliinuka ili kupigana na Sauli. “Watu wa Israeli wakaona kwamba wako katika shida kali, kwa sababu watu walikuwa wamebanwa sana; na watu wakajificha katika mapango na mashimo na miamba na ngome na mashimo ya maji.” (1 Sam. 13:5, 6) Sauli angefanya nini?

Samweli alikuwa amemwambia Sauli akutane naye huko Gilgali, ambako nabii huyo angetoa dhabihu. Sauli alingoja, lakini Samweli alichelewa kufika, na jeshi la Sauli lilikuwa likitawanyika. Kwa hiyo, Sauli akajichukulia daraka la kutoa dhabihu. Mara tu alipofanya hivyo, Samweli akafika. Baada ya kusikia jambo ambalo Sauli alikuwa amefanya, Samweli alimwambia hivi: “Umetenda kipumbavu. Hukuishika amri ya Yehova Mungu wako ambayo alikuamuru, kwa sababu, kama ungeishika, Yehova angeufanya ufalme wako juu ya Israeli kuwa imara mpaka wakati usio na kipimo. Lakini sasa ufalme wako hautadumu. Yehova atajitafutia mtu anayekubalika kwa moyo wake; na Yehova atamweka kuwa kiongozi juu ya watu wake, kwa sababu wewe hukushika yale aliyokuamuru Yehova.”—1 Sam. 10:8; 13:8, 13, 14.

Kwa sababu ya kukosa imani, Sauli aliamua kwa kimbelembele kutotii amri ya Mungu ya kumngojea Samweli aje kutoa dhabihu. Sauli alitenda kwa njia tofauti kama nini na Gideoni, ambaye alikuwa kiongozi wa majeshi ya Waisraeli hapo zamani! Yehova alimwagiza Gideoni apunguze jeshi lake kutoka watu 32,000 mpaka 300, na Gideoni alitii. Kwa nini? Kwa sababu alikuwa na imani katika Yehova. Kwa msaada wa Mungu, aliwashinda wavamizi 135,000. (Amu. 7:1-7, 17-22; 8:10) Yehova angemsaidia Sauli pia. Hata hivyo, kwa sababu Sauli hakutii, Wafilisti walipora Israeli.—1 Sam. 13:17, 18.

Tunapopata matatizo, tunafanya maamuzi jinsi gani? Wale ambao hawana imani huenda wakaona kwamba ni jambo linalofaa kupuuza kanuni za Mungu. Wakati Samweli hakuwapo, huenda Sauli alifikiri kwamba jambo alilofanya lilikuwa la hekima. Hata hivyo, wale ambao wameazimia kupata kibali cha Mungu, wanaona kwamba jambo pekee linalofaa ni kufuata kanuni za Kimaandiko ambazo zinahusu maamuzi wanayokabili.

Yehova Amkataa Sauli

Wakati wa kampeni ya kupambana na Waamaleki, Sauli alikuwa na hatia kwa sababu alifanya kosa lingine zito. Mungu aliwashutumu Waamaleki kwa sababu ya kuwashambulia Waisraeli bila sababu walipokuwa wakitoka Misri. (Kut. 17:8; Kum. 25:17, 18) Zaidi ya hayo, Waamaleki walijiunga na wengine katika nyakati za Waamuzi ili kuwashambulia tena watu waliochaguliwa na Mungu. (Amu. 3:12, 13; 6:1-3, 33) Kwa hiyo, Yehova aliwatoza Waamaleki hesabu naye akamwamuru Sauli atekeleze hukumu juu yao.—1 Sam. 15:1-3.

Badala ya kutii amri ya Yehova ya kuwafagilia mbali Waamaleki hao wenye uadui na kuharibu mali yao, Sauli alimkamata mfalme wao na kuchukua wanyama wao waliokuwa bora. Ni nini kilichotokea Samweli alipomuuliza Sauli kuhusu jambo hilo? Sauli alijaribu kuwalaumu wengine kwa kusema: “Watu waliwahurumia wanyama walio bora zaidi wa kundi na mifugo, kwa kusudi la kutoa dhabihu kwa Yehova.” Iwe kwa kweli Sauli alikusudia kutoa wanyama hao dhabihu au hapana, hakutii. Sauli hakuwa tena ‘mdogo machoni pake mwenyewe.’ Hivyo, nabii wa Mungu alisema kwamba Sauli alikosa kumtii Mungu. Kisha Samweli akasema: “Je, Yehova hupendezwa sana na matoleo ya kuteketezwa na dhabihu kuliko kuitii sauti ya Yehova? Tazama! Kutii ni bora kuliko dhabihu . . . Kwa kuwa umelikataa neno la Yehova, basi yeye pia amekukataa wewe usiwe mfalme.”—1 Sam. 15:15, 17, 22, 23.

Yehova alipoondoa baraka na roho yake takatifu kutoka juu ya Sauli, “roho mbaya” ilianza kumtawala mfalme huyo wa kwanza wa Israeli. Sauli alianza kumwonea wivu na kumtilia shaka Daudi, mwanamume ambaye Yehova angemfanya kuwa mfalme baadaye. Sauli alijaribu mara nyingi kumuua Daudi. Sauli alipoona kwamba “Yehova alikuwa pamoja na Daudi,” Biblia inasema, “Sauli akawa adui ya Daudi sikuzote.” Sauli alijaribu kumwinda na hata aliagiza makuhani 85 na watu wengine wauawe. Haishangazi kwamba Yehova alimwacha Sauli!—1 Sam. 16:14; 18:11, 25, 28, 29; 19:10, 11; 20:32, 33; 22:16-19.

Wafilisti waliposhambulia Israeli tena, Sauli aliamua kuwasiliana na pepo akijaribu kutafuta msaada lakini hakufanikiwa. Siku iliyofuata, aliumizwa vibaya sana katika vita, na akajiua. (1 Sam. 28:4-8; 31:3, 4) Maandiko yanasema hivi kuhusu mfalme wa kwanza wa Israeli ambaye hakutii: “Sauli akafa kwa sababu alikosa uaminifu kwa kutenda bila imani juu ya Yehova kuhusu lile neno la Yehova ambalo hakuwa ameshika na pia kwa sababu ya kuuliza kutoka kwa mwenye kuwasiliana na pepo. Naye hakuuliza kutoka kwa Yehova.”—1 Nya. 10:13, 14.

Mfano mbaya wa Sauli unaonyesha waziwazi kwamba kumtii Yehova ni bora kuliko kumtolea dhabihu yoyote. Mtume Yohana aliandika hivi: “Kumpenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake; na bado amri zake si mzigo mzito.” (1 Yoh. 5:3) Tusipuuze kamwe ukweli huu wa msingi: Ili tuwe na urafiki wa kudumu pamoja na Mungu ni lazima tumtii yeye.

[Picha katika ukurasa wa 21]

Sauli alikuwa kiongozi mnyenyekevu alipoanza kutawala

[Picha katika ukurasa wa 23]

Kwa nini Samweli alimwambia Sauli kwamba “kutii ni bora kuliko dhabihu”?