Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Pokea Roho ya Mungu, Bali Si Roho ya Ulimwengu

Pokea Roho ya Mungu, Bali Si Roho ya Ulimwengu

Pokea Roho ya Mungu, Bali Si Roho ya Ulimwengu

“Sisi tulipokea, si roho ya ulimwengu, bali roho inayotoka kwa Mungu, ili tuyajue mambo ambayo Mungu ametupa sisi kwa fadhili.” —1 KOR. 2:12.

1, 2. (a) Ni katika maana gani Wakristo wa kweli wako katika vita? (b) Tutachunguza maswali au maulizo gani?

WAKRISTO wa kweli wako katika vita! Adui yetu ni mwenye nguvu sana, ni mjanja, na ni mpiganaji hodari. Ana silaha hatari sana ambayo ametumia ili kuwatiisha wanadamu wengi. Lakini hatuhitaji kujiona kuwa dhaifu sana au kuona kwamba hatuwezi kushinda vita hivyo. (Isa. 41:10) Tuna ulinzi ambao unaweza kushinda shambulizi lolote lile.

2 Vita vyetu si vya kimwili; ni vya kiroho. Adui yetu ni Shetani Ibilisi, na silaha kuu ambayo anatumia ni “roho ya ulimwengu.” (1 Kor. 2:12) Njia kuu ya kujilinda kutokana na mashambulizi yake ni kuwa na roho ya Mungu. Ili kuokoka vita hivyo na kubaki wenye nguvu kiroho, tunahitaji kuomba roho ya Mungu na kisha kuonyesha tunda la roho hiyo katika maisha yetu. (Gal. 5:22, 23) Hata hivyo, roho ya ulimwengu ni nini, na ilipata jinsi gani kuwa yenye uvutano mkubwa sana? Tunaweza kujua jinsi gani ikiwa roho ya ulimwengu ina uvutano juu yetu? Na tunaweza kujifunza nini kutoka kwa Yesu kuhusu kupokea roho ya Mungu na kuipinga roho ya ulimwengu?

Kwa Nini Roho ya Ulimwengu Imeenea Sana?

3. Roho ya ulimwengu ni nini?

3 Roho ya ulimwengu huu inatokana na Shetani, “mtawala wa ulimwengu,” na inapingana na roho takatifu ya Mungu. (Yoh. 12:31; 14:30; 1 Yoh. 5:19) Roho ya ulimwengu ni mwelekeo wenye nguvu zaidi ambao unawasukuma watu kutenda. Nguvu hiyo inayowachochea watu watende kwa njia fulani, inaongoza jamii ya wanadamu kupinga kusudi na mapenzi ya Mungu.

4, 5. Roho inayochochewa na Shetani ilienea sana jinsi gani?

4 Roho ambayo Shetani anachochea ilienea sana jinsi gani? Kwanza, Shetani alimdanganya Hawa katika bustani ya Edeni. Alimsadikisha Hawa kwamba angekuwa na maisha mazuri zaidi ikiwa hangemtegemea Mungu. (Mwa. 3:13) Alithibitika kuwa mwongo kama nini! (Yoh. 8:44) Kisha, kupitia mwanamke huyo, kwa ujanja Shetani alimshawishi Adamu ili avunje ushikamanifu wake kwa Yehova. Kwa sababu ya uamuzi wa Adamu, wanadamu waliuzwa chini ya dhambi, na hivyo wakarithi mwelekeo wa kufuata roho ya Shetani ya kutotii.—Soma Waefeso 2:1-3.

5 Shetani aliwashawishi pia malaika wengi, ambao walikuja kuwa roho waovu. (Ufu. 12:3, 4) Hali hiyo ya kutokuwa washikamanifu kwa Mungu ilianza muda mfupi kabla ya Gharika ya siku za Noa. Malaika hao waliamini kwamba wangefaidika kwa kuacha vyeo walivyopewa huko mbinguni na kuja duniani ili kutosheleza tamaa zao zisizo za asili bila kujali. (Yuda 6) Kwa msaada wa roho hao waovu, ambao hawawezi tena kuvaa miili ya kibinadamu, Shetani ‘anaipotosha dunia nzima inayokaliwa.’ (Ufu. 12:9) Inasikitisha kwamba wanadamu wengi hawaoni uvutano wa roho waovu.—2 Kor. 4:4.

Je, Roho ya Ulimwengu Ina Uvutano Juu Yako?

6. Roho ya ulimwengu inaweza kuwa na uvutano juu yetu kwa njia gani tu?

6 Watu wengi hawaoni uvutano wa Shetani, lakini Wakristo wa kweli hawana sababu za kutojua mbinu za Shetani. (2 Kor. 2:11) Kwa kweli, roho ya ulimwengu haiwezi kuwa na uvutano juu yetu isipokuwa tu tuiruhusu kufanya hivyo. Acheni tuchunguze maswali manne ambayo yatafunua ikiwa tunaongozwa na roho ya Mungu au roho ya ulimwengu.

7. Taja njia moja ambayo Shetani anatumia kujaribu kututenga mbali na Yehova.

7 Vitumbuizo ambavyo ninachagua vinafunua nini kunihusu? (Soma Yakobo 3:14-18.) Shetani anajaribu kututenga mbali na Mungu kwa kuchochea mioyo yetu ipende jeuri. Ibilisi anajua kwamba Yehova anamchukia yeyote anayependa jeuri. (Zab. 11:5) Kwa hiyo, Shetani anajaribu kutumia vitabu, sinema, muziki, na michezo ya kompyuta kuchochea tamaa za mwili, na kuna michezo mingine kati ya hiyo ambayo inawachochea wachezaji kuiga ukatili na mwenendo mpotovu kiadili. Shetani hajali ikiwa sehemu moja ya moyo wetu inapenda mambo yaliyo sawa na sehemu nyingine inapenda mambo mabaya, ambayo anawachochea watu kutenda.—Zab. 97:10.

8, 9. Ni maswali gani kuhusu vitumbuizo ambayo tunapaswa kujiuliza?

8 Kwa upande mwingine, roho ya Mungu inawachochea wale wanaoipokea kuwa safi kiadili, wenye amani, na wenye kujaa huruma. Ni vizuri tujiulize, ‘Je, vitumbuizo ninavyochagua vinanisaidia kusitawisha sifa nzuri ndani yangu?’ Hekima kutoka juu si “ya kinafiki.” Wale ambao wanaongozwa na roho ya Mungu hawahubiri kwamba majirani wao wawe safi kiadili na wenye amani huku wao wenyewe wakifurahia kutazama kwa siri ndani ya nyumba zao mambo mabaya sana ya kijeuri na mambo mapotovu kiadili.

9 Yehova anatazamia watu wajitoe kwake kikamili. Hata hivyo, Shetani, anataka tendo moja tu la ibada, kama alivyotaka Yesu afanye. (Luka 4:7, 8) Tunaweza kujiuliza hivi: ‘Je, vitumbuizo ninavyochagua vinanisaidia kujitoa kikamili kwa Mungu? Je, vitumbuizo ninavyochagua vinafanya iwe vigumu zaidi au rahisi zaidi kwangu kuipinga roho ya ulimwengu? Je, ninapaswa kufanya marekebisho yoyote kuhusu vitumbuizo ambavyo nitachagua wakati ujao?’

10, 11. (a) Roho ya ulimwengu inawachochea watu wawe na mtazamo gani kuhusu vitu vya kimwili? (b) Neno lililoongozwa na roho ya Mungu linawahimiza watu wawe na mtazamo gani?

10 Nina mtazamo gani kuelekea vitu vya kimwili? (Soma Luka 18:24-30.) Roho ya ulimwengu inachochea “tamaa ya macho” kwa kuwatia watu moyo kuwa na pupa na kupenda vitu vya kimwili. (1 Yoh. 2:16) Imewachochea watu wengi kuazimia kuwa matajiri. (1 Tim. 6:9, 10) Roho hiyo inataka tuamini kwamba kujirundikia vitu vya kimwili kutatupatia usalama wa kudumu. (Met. 18:11) Hata hivyo, tukiruhusu kupenda pesa kuwe na nguvu zaidi kuliko upendo wetu kwa Mungu, Shetani atakuwa ameshinda. Tunapaswa kujiuliza hivi: ‘Je, ninakazia utafutaji wa vitu vya kimwili na raha katika maisha yangu?’

11 Tofauti na hilo, Neno lililoongozwa na roho ya Mungu linatutia moyo kuwa na maoni yenye usawaziko kuhusu pesa na kufanya kazi kwa bidii ili kutosheleza mahitaji yetu wenyewe ya kimwili na ya familia yetu. (1 Tim. 5:8) Roho ya Mungu inawasaidia wale wanaoipata kuiga utu wa ukarimu wa Yehova. Watu kama hao wanajulikana kuwa watoaji, si wapokeaji. Wanawathamini watu zaidi kuliko vitu vya kimwili na wanashiriki nao kwa furaha kile walicho nacho ikiwa wanaweza kufanya hivyo. (Met. 3:27, 28) Na hawaruhusu kamwe kufuatia pesa kuchukue mahali pa utumishi wao kwa Mungu.

12, 13. Tofauti na roho ya ulimwengu, roho ya Mungu inaweza kuwa na uvutano mzuri juu yetu jinsi gani?

12 Utu wangu unaonyesha roho gani? (Soma Wakolosai 3:8-10, 13.) Roho ya ulimwengu inaendeleza matendo ya mwili. (Gal. 5:19-21) Kwa kweli, tunaweza kujua ni roho gani inayotuongoza wakati mambo si mazuri, kama vile wakati ndugu au dada Mkristo anapotupuuza, anapotukasirisha, au hata anapotutendea dhambi, bali si wakati mambo yanapokuwa mazuri. Zaidi ya hayo, roho inayotuongoza inaweza kuonekana waziwazi tunapokuwa peke yetu ndani ya nyumba zetu. Huenda tunahitaji kujichunguza wenyewe. Jiulize mwenyewe hivi: ‘Kwa muda wa miezi sita iliyopita, je, utu wangu umezidi kuwa kama wa Kristo au nimerudia tena tabia fulani mbaya za usemi na mwenendo?’

13 Roho ya Mungu inaweza kutusaidia ‘kuvua utu wa zamani pamoja na mazoea yake’ na kuvaa “utu mpya.” Hilo litatusaidia kuwa wenye fadhili na wenye upendo zaidi. Tutakuwa na mwelekeo wa kusameheana kwa kupenda, hata ikiwa inaonekana kwamba tuna sababu nzuri ya kulalamika. Tukitendewa kwa ukosefu wa haki hatutafoka kwa “uchungu wote wenye uovu na hasira na ghadhabu na kupiga kelele na matukano.” Badala yake, tutajitahidi sana kuwa wenye “huruma nyororo.”—Efe. 4:31, 32.

14. Watu wengi katika ulimwengu wana maoni gani kuhusu Neno la Mungu?

14 Je, ninaheshimu na kupenda viwango vya maadili vya Biblia? (Soma Methali 3:5, 6.) Roho ya ulimwengu inawachochea watu kuasi Neno la Mungu. Wale wanaoongozwa na roho hiyo wanapuuza sehemu za Biblia ambazo haziwapendezi, badala yake wanapendelea falsafa na mapokeo ya wanadamu. (2 Tim. 4:3, 4) Wengine wanalipuuza kabisa Neno la Mungu. Watu kama hao wanatilia shaka umuhimu na usahihi wa Biblia, na hivyo kuwa wenye hekima machoni pao wenyewe. Wanapunguza uzito wa viwango safi vya Biblia kuhusu uzinzi, ulawiti, na talaka. Wanafundisha kwamba “wema ni ubaya na ubaya ni wema.” (Isa. 5:20) Je, roho hiyo imekuwa na uvutano juu yetu? Je, tunategemea hekima ya wanadamu, kutia ndani mawazo yetu wenyewe, tunapopambana na matatizo? Au je, tunajitahidi kufuata mashauri ya Biblia?

15. Badala ya kutegemea hekima yetu wenyewe, tunapaswa kufanya nini?

15 Roho ya Mungu inatuchochea kuiheshimu Biblia. Kama mtunga-zaburi, tunaliona neno la Mungu kuwa taa ya miguu yetu na nuru ya barabara yetu. (Zab. 119:105) Badala ya kutegemea hekima yetu wenyewe, tunategemea kwa uhakika Neno la Mungu lililoandikwa ili kutusaidia kutofautisha kati ya lililo sawa na lililo kosa. Tunajifunza si kuiheshimu tu Biblia bali pia kupenda sheria ya Mungu.—Zab. 119:97.

Jifunze Kutokana na Mfano wa Yesu

16. Ni mambo gani yanayohusika katika kuwa na “akili ya Kristo”?

16 Ili kupokea roho ya Mungu, ni lazima tusitawishe ndani yetu “akili ya Kristo.” (1 Kor. 2:16) Ili kuwa na “mtazamo uleule wa akili ambao Kristo Yesu alikuwa nao” tunahitaji kujua jinsi alivyofikiri na kutenda na kisha kumwiga. (Rom. 15:5; 1 Pet. 2:21) Fikiria njia fulani ambazo tunaweza kufanya hivyo.

17, 18. (a) Tunajifunza nini kutoka kwa Yesu kuhusu sala? (b) Kwa nini tunapaswa ‘kuendelea kuomba’?

17 Sali ili upewe roho ya Mungu. Kabla ya kupambana na majaribu, Yesu alisali ili roho ya Mungu imsaidie. (Luka 22:40, 41) Sisi pia tunahitaji kumwomba Mungu atupatie roho yake takatifu. Yehova anawapa kwa ukarimu wote na kwa kupenda wale wanaomwomba kwa imani roho hiyo. (Luka 11:13) Yesu alisema hivi: “Endeleeni kuomba, nanyi mtapewa; endeleeni kutafuta, nanyi mtapata; endeleeni kupiga hodi, nanyi mtafunguliwa. Kwa maana kila mtu anayeomba hupokea, na kila mtu anayetafuta hupata, na kila mtu anayepiga hodi atafunguliwa.”—Mt. 7:7, 8.

18 Unapotafuta roho ya Yehova na msaada wake, usiache haraka kuomba ili upewe roho hiyo. Huenda tukahitaji kusali mara nyingi zaidi na kwa muda mrefu. Nyakati nyingine, Yehova anaacha wale wanaomwomba waonyeshe hangaiko lao kubwa na unyoofu wa imani yao kabla ya kujibu sala zao. *

19. Sikuzote Yesu alifanya nini, na kwa nini tunapaswa kumwiga?

19 Mtii Yehova kikamili. Sikuzote Yesu alifanya mambo yaliyompendeza Baba yake. Katika pindi moja, Yesu alikuwa na mwelekeo tofauti na Baba yake kuhusu kushughulikia hali fulani. Hata hivyo, akiwa na uhakika, Yesu alimwambia Baba yake hivi: “Acha, si mapenzi yangu, bali yako yatendeke.” (Luka 22:42) Jiulize mwenyewe, ‘Je, ninamtii Mungu hata wakati kufanya hivyo si rahisi?’ Kumtii Mungu ni jambo la maana ili kupata uzima. Tunapaswa kumtii kikamili akiwa Mtengenezaji wetu, Chanzo na Mtegemezaji wa uhai wetu. (Zab. 95:6, 7) Hakuna jambo linaloweza kuchukua nafasi ya utii. Hatuwezi kupata kibali cha Mungu bila utii.

20. Maisha ya Yesu yalionyesha nini, na tunaweza kumwiga jinsi gani?

20 Ijue Biblia vizuri. Yesu alitaja Maandiko alipokuwa akipinga mashambulizi ya moja kwa moja ya Shetani juu ya imani yake. (Luka 4:1-13) Alipokuwa akikabiliana na wapinzani wake wa kidini, Yesu alitumia Neno la Mungu kuwa mamlaka yake. (Mt. 15:3-6) Maisha yote ya Yesu yalionyesha kwamba alijua na kutimiza sheria ya Mungu. (Mt. 5:17) Sisi pia tunataka kuendelea kulisha akili zetu Neno la Mungu lenye kutia imani nguvu. (Flp. 4:8, 9) Huenda ikawa vigumu kwa wengi wetu kupata wakati kwa ajili ya funzo la kibinafsi na la familia. Hata hivyo, badala ya kutafuta wakati, huenda tukahitaji kununua wakati.—Efe. 5:15-17.

21. Ni mpango gani ambao tunaweza kutumia ili kutusaidia kujua Neno la Mungu vizuri zaidi na kulifuata?

21 “Mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ametusaidia kuwa na wakati wa funzo la kibinafsi na funzo la familia kwa kupanga ili tuwe na jioni ya Ibada ya Familia kila juma. (Mt. 24:45) Je, unatumia kwa hekima mpango huo? Ili kukusaidia kupata akili ya Kristo, katika pindi zako za funzo la kibinafsi, je, unaweza pia kuamua kuchunguza hatua kwa hatua mambo ambayo Yesu alifundisha kuhusu habari mbalimbali unazotaka kujua? Unaweza kutumia Fahirisi ya vichapo ili kupata vichwa vya mazungumzo vya habari unayotaka kujifunza. Kwa mfano, tangu mwaka wa 2008 mpaka 2010, toleo la watu wote la gazeti hili lilikuwa na mfululizo wa makala 12 wenye kichwa “Tunayojifunza Kutoka kwa Yesu.” Huenda ukataka kutumia habari hizo kuwa msingi wa funzo. Kuanzia mwaka wa 2006, gazeti la Amkeni! limekuwa na sehemu yenye kichwa “Ungejibuje?” Sehemu hiyo yenye maswali imekusudiwa kukusaidia kupanua na kuongeza kina cha ujuzi wako kuhusu Neno la Mungu. Kwa nini msitie ndani ya programu yenu ya Ibada ya Familia habari kutoka katika sehemu kama hizo mara kwa mara?

Tunaweza Kuushinda Ulimwengu

22, 23. Ni lazima tufanye nini ili tuushinde ulimwengu?

22 Ili kuongozwa na roho ya Mungu, ni lazima tuipinge roho ya ulimwengu. Si jambo rahisi kuipinga roho hiyo. Huenda tukahitaji kupambana sana, kufanya pigano kali. (Yuda 3) Lakini tunaweza kushinda! Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Ulimwenguni mna dhiki, lakini jipeni moyo! Mimi nimeushinda ulimwengu.”—Yoh. 16:33.

23 Sisi pia tunaweza kuushinda ulimwengu tukiipinga roho ya ulimwengu na kufanya yote tunayoweza ili kuipokea roho ya Mungu. Kwa kweli, “ikiwa Mungu yuko upande wetu, ni nani atakayekuwa dhidi yetu?” (Rom. 8:31) Tukiipokea roho ya Mungu na kufuata mwongozo wake ambao unaonyeshwa katika Biblia, tutapata uradhi, amani, furaha, na tutakuwa na uhakika kwamba tutapata uzima wa milele katika ulimwengu mpya ambao unakaribia.

[Maelezo ya Chini]

Je, Unakumbuka?

• Kwa nini roho ya ulimwengu imeenea sana?

• Ni maswali gani manne ambayo tunapaswa kujiuliza?

• Ni mambo gani matatu tunayojifunza kutoka kwa Yesu kuhusu kuipokea roho ya Mungu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 8]

Malaika fulani walikuja kuwa roho waovu jinsi gani?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Shetani anatumia roho ya ulimwengu kuwaongoza watu, lakini tunaweza kuepuka kabisa uvutano wake