Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unakumbuka?

Je, Unakumbuka?

Je, Unakumbuka?

Je, umefurahia kusoma matoleo ya hivi karibuni ya Mnara wa Mlinzi? Ona kama unaweza kujibu maswali yafuatayo:

• Kwa nini tunaweza kuamini kwamba kulikuwa na bustani ya Edeni?

Biblia inaonyesha kwamba bustani ya Edeni ilikuwepo kikweli, na inaeleza mahali hususa ambapo ilipatikana. Mito miwili inayotajwa katika simulizi hilo bado ipo mpaka leo. Hadithi au hekaya hazielezi mambo kwa njia hiyo. Yesu, Shahidi mwenye kutegemeka zaidi, aliwataja Adamu na Hawa kuwa watu halisi.​—1/1, ukurasa wa 5-6, 9.

• Je, Mungu alijua kwamba Adamu na Hawa wangefanya dhambi?

Hapana. Yehova aliwapa akili na uhuru wa kuchagua, na hivyo wangeweza kumtii au kukosa kumtii. Ingawa Mungu ana uwezo wa kujua mambo mapema, nyakati nyingine anaamua kutotumia uwezo huo.​—1/1, ukurasa wa 13-15.

• Je, Wakristo wa kweli wanatumia jina la Mungu kama hirizi?

Watu fulani wanaona kitu au ishara fulani kuwa hirizi, kitu ambacho kinawalinda kimuujiza, lakini watu wa Mungu hawalioni jina lake kwa njia hiyo. Wanamwamini Yehova na wanajitahidi kufanya mapenzi yake, na hivyo kupata kimbilio katika jina lake. (Sef. 3:12, 13)​—1/15, ukurasa wa 5-6.

• Katika Israeli, ni nani waliofaidika na mpango wa kukusanya masalio?

Wote walifaidika. Mpango huo uliwachochea maskini wawe na bidii, kwa sababu walipaswa kukusanya masalio. Wengine walifaidika kwa kutiwa moyo wawe wakarimu na wategemee baraka za Mungu.​—2/1, ukurasa wa 15.

• Kwa nini Yehova alimkataa Mfalme Sauli?

Sauli alipaswa kumsubiri nabii wa Mungu atoe dhabihu, lakini mfalme huyo hakutii, na akatoa dhabihu hiyo yeye mwenyewe. Baadaye, hakutii amri ya kuwafagilia mbali maadui fulani.​—2/15, ukurasa wa 22-23.

• Tunaweza kuonyesha jinsi gani kwamba tunachukia uasi-sheria?

Tutaepuka kunywa pombe kupita kiasi, tutaepuka mazoea ya kuwasiliana na pepo, na kutii onyo la Yesu kuhusu maadili mapotovu. Kwa mfano, tutaepuka ponografia (picha au habari za ngono) na mawazo ambayo yanasababishwa na ponografia. (Mt. 5:27, 28) Pia, hatutashirikiana na watu waliotengwa na ushirika.​—2/15, ukurasa wa 29-32.

• Ni jambo gani ambalo linaonekana wazi kuhusu mizinga ya kale ya nyuki ambayo wataalamu wa vitu vya kale walipata katika nchi ya leo ya Israel?

Wachunguzi wa vitu vya kale walipata mizinga zaidi ya 30 ya nyuki, ambayo wasomi wanakadiria kwamba ilitokeza asali yenye uzito wa karibu nusu tani kila mwaka. Hilo linaonyesha kwamba kulikuwa na ufugaji wa nyuki katika nchi ambayo Mungu alikuwa amesema kwamba ‘ingetiririka maziwa na asali.’ (Kut. 3:8)​—3/1, ukurasa wa 15.

• Yeremia alikuwa jinsi gani kama mti “uliopandwa kando ya maji, unaopeleka mizizi yake kando ya maji”? (Yer. 17:7, 8)

Hakuacha kamwe kuzaa matunda; wala hakuacha wadhihaki wamfanye apunguze bidii yake. Badala yake, alishikamana na Mungu ambaye ni Chanzo cha maji yanayoendeleza uhai, na akachukua kwa uzito mambo ambayo alimwambia.​—3/15, ukurasa wa 14.

• Yesu alimaanisha nini alipomwambia Martha kwamba mambo machache ndiyo yanayohitajiwa, au jambo moja tu? (Luka 10:41, 42)

Hakuwa akisema kwamba Martha alipenda vitu vya kimwili kwa sababu alikuwa akitayarisha vyakula vya aina mbalimbali; wala hakuwa akisema kwamba kazi ya Martha ilikuwa ya bure. Badala yake, alikuwa akikazia mambo ambayo Martha alipaswa kutanguliza. Martha hakutumia nafasi hiyo ya pekee kutia nguvu imani yake.​—4/1, ukurasa wa 12-13.

• Ni mambo gani ambayo hayakuwa ya haki katika kesi ya Yesu?

Mahakama haikuwa na mashahidi wa kumtetea Yesu ili awekwe huru. Mashahidi wa uwongo waliletwa. Kesi ilisikilizwa usiku. Kesi ilianza na kumalizika kwa siku moja.​—4/1, ukurasa wa 20.