Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kumtegemea Yehova Kikamili Kunatuchochea Kuwa na Uhakika

Kumtegemea Yehova Kikamili Kunatuchochea Kuwa na Uhakika

Kumtegemea Yehova Kikamili Kunatuchochea Kuwa na Uhakika

“Yehova mwenyewe atasikia ninapomwita.”—ZAB. 4:3.

1, 2. (a) Daudi alipatwa na hali gani iliyokuwa hatari sana? (b) Tutazungumzia zaburi gani?

MFALME DAUDI amekuwa akitawala Israeli kwa muda fulani, lakini sasa anapatwa na hali hatari sana. Absalomu, mwana wake mwenye hila amejitangaza kuwa mfalme, na Daudi amelazimika kuondoka Yerusalemu. Amesalitiwa pia na rafiki wa karibu sana, na sasa, akiwa pamoja na watu wachache washikamanifu, anatembea akilia na akiwa miguu wazi kwenye Mlima wa Mizeituni. Zaidi ya hayo, Shimei, ambaye ni mtu wa familia ya Mfalme Sauli, anamtupia Daudi mawe na mavumbi huku akimlaani.—2 Sam. 15:30, 31; 16:5-14.

2 Je, hali hiyo itamwingiza Daudi ndani ya Sheoli au kaburi akiwa na huzuni na aibu? Hapana, kwa sababu anamtegemea Yehova. Hilo linaonekana wazi katika Zaburi ya 3, ambayo ilitungwa na Daudi akieleza jinsi alivyokimbia. Aliandika pia Zaburi ya 4. Zaburi hizo mbili zinaonyesha usadikisho wa kwamba Mungu anasikia na kujibu sala. (Zab. 3:4; 4:3) Zaburi hizo zinatuhakikishia kwamba Yehova yuko pamoja na watumishi wake waaminifu mchana na usiku, na anawabariki kwa kuwategemeza na pia kwa kuwapa amani na hali ya usalama. (Zab. 3:5; 4:8) Kwa hiyo, acheni tuzungumzie zaburi hizo na kuona jinsi zinavyotuchochea kuwa na uhakika na kuendelea kumtegemea Mungu.

Wakati ‘Wengi Wanapoinuka Juu Yetu’

3. Kama inavyoonyeshwa katika Zaburi 3:1, 2, Daudi alikuwa katika hali gani?

3 Mjumbe mmoja anasema hivi: “Moyo wa watu wa Israeli umekuwa nyuma ya Absalomu.” (2 Sam. 15:13) Akishangaa Absalomu amefanikiwa jinsi gani kupata wafuasi wengi hivyo, Daudi anauliza: “Ee Yehova, kwa nini adui zangu wamekuwa wengi? Kwa nini wengi wanainuka dhidi yangu? Wengi wanasema juu ya nafsi yangu: ‘Hakuna wokovu kwa ajili yake kutoka kwa Mungu.’” (Zab. 3:1, 2) Waisraeli wengi wanafikiri kwamba Yehova hatamkomboa Daudi kutoka katika msiba ambao umesababishwa na Absalomu na wafuasi wake.

4, 5. (a) Daudi alikuwa na uhakika gani? (b) Maneno “Mwenye kuinua kichwa changu” yanamaanisha nini?

4 Lakini Daudi ana uhakika kwa sababu anamtegemea Mungu kabisa. Anaimba hivi: “Na bado wewe, Ee Yehova, ni ngao inayonizunguka, utukufu wangu na Mwenye kuinua kichwa changu.” (Zab. 3:3) Daudi ana uhakika kwamba Yehova atamlinda kama vile ngao inavyomlinda askari-jeshi. Ndiyo, mfalme huyo anayeendelea kuzeeka anakimbia, kichwa chake kikiwa kimefunikwa na kuinama chini kwa sababu ya aibu. Lakini Aliye Juu Zaidi atabadili hali ya Daudi na kumtukuza. Yehova atamsaidia kusimama wima, kuinua kichwa chake na kukiinua juu zaidi kwa mara nyingine tena. Daudi anaita akiwa na uhakika kwamba Mungu atamjibu. Je, unaonyesha kwamba unamtegemea Yehova kwa njia hiyo?

5 Daudi anaposema “Mwenye kuinua kichwa changu,” anaonyesha kwamba Yehova ndiye atakayempa msaada anaohitaji. Biblia Habari Njema inasema hivi: “Lakini wewe ee Mwenyezi-Mungu u ngao yangu kila upande; kwako napata fahari na ushindi wangu.” Kuhusu usemi “Mwenye kuinua kichwa changu,” kitabu kimoja cha marejeo kinasema hivi: “Mungu anapoinua . . . ‘kichwa’ cha mtu, Anamjaza mtu huyo tumaini na uhakika.” Akiwa amelazimishwa kuacha kiti cha ufalme cha Israeli, Daudi ana sababu ya kuvunjika moyo. Hata hivyo, ‘kuinuliwa kwa kichwa chake’ kutampa tena ujasiri, uhakika, na ataweza kumtegemea Mungu kikamili.

‘Yehova Atajibu!’

6. Kwa nini Daudi alisema kwamba sala zake zingejibiwa kutoka katika mlima mtakatifu wa Yehova?

6 Akimtegemea Yehova na akiwa na uhakika kabisa, Daudi anaendelea kusema: “Kwa sauti yangu nitamwita Yehova, naye atanijibu kutoka katika mlima wake mtakatifu.” (Zab. 3:4) Kulingana na maagizo ya Daudi, sanduku la agano, ambalo linafananisha kuwapo kwa Mungu, limepelekwa kwenye Mlima Sayuni. (Soma 2 Samweli 15:23-25.) Basi, kwa kufaa Daudi anasema kwamba sala zake zitajibiwa kutoka katika mlima mtakatifu wa Yehova.

7. Kwa nini Daudi hakuogopa hata kidogo?

7 Akiwa na uhakika kwamba sala yake kwa Mungu si ya bure, Daudi haogopi hata kidogo. Badala yake, anaimba hivi: “Nami nitajilaza nipate kulala usingizi; hakika nitaamka, kwa maana Yehova anaendelea kunitegemeza.” (Zab. 3:5) Hata usiku, wakati ambapo kuna hatari zaidi ya kushambuliwa kwa ghafula, Daudi haogopi kulala usingizi. Ana uhakika kwamba ataamka, kwa kuwa mambo yaliyompata mapema yamemfanya awe na uhakika kabisa kwamba anaweza kutegemea msaada wa Mungu ambao hauwezi kushindwa. Sisi pia tunaweza kufanya hivyo tukishikamana na “njia za Yehova” na tusipomwacha kamwe.—Soma 2 Samweli 22:21, 22.

8. Andiko la Zaburi 27:1-4 linaonyesha jinsi gani kwamba Daudi alimtegemea Mungu?

8 Zaburi nyingine ya Daudi inaonyesha kwamba ana uhakika katika Mungu na anamtegemea kikamili, Zaburi hiyo ina maneno haya yaliyoongozwa na roho ya Mungu: “Yehova ni nuru yangu na wokovu wangu. Nitamwogopa nani? Yehova ni ngome ya uhai wangu. Nitamhofu nani? . . . Hata kambi ijapopiga hema dhidi yangu, moyo wangu hautaogopa. . . . Nimemwomba Yehova jambo moja—ndilo nitakalolitafuta, kwamba nipate kukaa katika nyumba ya Yehova siku zote za maisha yangu, ili kuuona uzuri wa Yehova na kulitazama kwa uthamini hekalu lake.” (Zab. 27:1-4) Ikiwa wewe pia unahisi vivyo hivyo na hali zako zinakuruhusu, utakusanyika kwa ukawaida pamoja na waabudu wenzako wa Yehova.—Ebr. 10:23-25.

9, 10. Ingawa Daudi alisema maneno yaliyo katika Zaburi 3:6, 7, kwa nini unaweza kusema kwamba hakuwa na roho ya kulipiza kisasi?

9 Ingawa Daudi anakabili udanganyifu wa Absalomu na ukosefu wa ushikamanifu wa watu wengine wengi sana, anaimba hivi: “Sitaogopa maelfu kumi ya watu ambao wamejipanga dhidi yangu kunizunguka pande zote. Usimame, Ee Yehova! Uniokoe, Ee Mungu wangu! Kwa maana utawapiga adui zangu wote kwenye taya. Utayavunja meno ya waovu.”Zab. 3:6, 7.

10 Daudi hana roho ya kulipiza kisasi. Ikiwa adui zake ‘wangepigwa kwenye taya au mfupa wa kidevu,’ Mungu ndiye angefanya hivyo. Mfalme Daudi amejiandikia nakala yake mwenyewe ya Sheria na anajua kwamba katika Sheria hiyo Yehova anatangaza hivi: “Kisasi ni changu, na malipo.” (Kum. 17:14, 15, 18; 32:35) Pia, ni daraka la Mungu ‘kuvunja meno ya waovu.’ Kuvunja meno yao kunamaanisha kuwamaliza nguvu kabisa ili wasiwe na uwezo wa kusababisha madhara. Yehova anawajua watu waovu kwa sababu yeye “huona jinsi moyo ulivyo.” (1 Sam. 16:7) Tunathamini kama nini kwamba Mungu anatupatia imani na nguvu za kumpinga Shetani, ambaye ni mwovu kuliko wote, na ambaye hivi karibuni atatupwa ndani ya abiso kama simba anayenguruma ambaye hana meno na ambaye anastahili tu kuharibiwa!—1 Pet. 5:8, 9; Ufu. 20:1, 2, 7-10.

“Wokovu Ni wa Yehova”

11. Kwa nini tunapaswa kusali kwa ajili ya waamini wenzetu?

11 Daudi anatambua kwamba Yehova peke yake ndiye anayeweza kuleta ukombozi ambao anauhitaji sana. Lakini mtunga-zaburi huyo hajifikirii yeye mwenyewe tu. Namna gani watu wa Yehova kwa ujumla ambao wana kibali chake? Kwa kufaa, Daudi anamalizia wimbo wake ulioongozwa na roho ya Mungu kwa maneno haya: “Wokovu ni wa Yehova. Baraka yako iko juu ya watu wako.” (Zab. 3:8) Ni kweli kwamba Daudi ana matatizo makubwa sana, lakini anawakumbuka watu wa Yehova kwa ujumla na ana hakika kwamba Mungu atawabariki. Je, sisi pia hatupaswi kuwakumbuka waabudu wenzetu? Acheni tuwakumbuke katika sala zetu, na kumwomba Yehova awape roho yake takatifu ili wawe na ujasiri na watende kwa uhakika wanapotangaza habari njema.—Efe. 6:17-20.

12, 13. Ni nini kilichompata Absalomu, na Daudi alitenda jinsi gani?

12 Absalomu anakufa kifo cha aibu—onyo kwa wote ambao wanawatendea wengine vibaya, hasa watiwa-mafuta wa Mungu, kama vile Daudi. (Soma Methali 3:31-35.) Vita vinatokea, na majeshi ya Absalomu yanashindwa. Absalomu anakimbia akiwa amepanda nyumbu, mnyama anayefanana na punda, wakati nywele zake nyingi zinaposhikwa na tawi la mti mkubwa. Ananing’inia juu ya mti huo akiwa hai, lakini hawezi kufanya lolote, kisha Yoabu anamuua Absalomu kwa kuchoma mikuki mitatu midogo ndani ya moyo wake.—2 Sam. 18:6-17.

13 Je, Daudi anashangilia anapopata habari kuhusu jambo ambalo limempata mwana wake? Hapana. Badala yake, anatembea huku na huku, akiomboleza, na kulia hivi kwa sauti: “Mwanangu Absalomu, mwanangu, mwanangu Absalomu! Laiti mimi mwenyewe ningekufa badala yako, Absalomu mwanangu, mwanangu!” (2 Sam. 18:24-33) Ni maneno ya Yoabu tu ndiyo yanayomwondolea Daudi huzuni ambayo ilikuwa karibu kumlemea kabisa. Ni mwisho wenye kuhuzunisha kama nini kwa Absalomu, ambaye aliruhusu tamaa ya kichoyo ya kutaka makuu imwongoze kupigana na baba yake mwenyewe—mtiwa-mafuta wa Yehova—na hivyo akajiletea msiba yeye mwenyewe!—2 Sam. 19:1-8; Met. 12:21; 24:21, 22.

Daudi Anaonyesha Tena Anamtegemea Mungu

14. Tunaweza kusema nini kuhusu kutungwa kwa Zaburi ya 4?

14 Kama Zaburi ya 3, Zaburi ya 4 ni sala ya Daudi inayotoka moyoni ambayo inaonyesha kwamba alimtegemea Yehova kikamili. (Zab. 3:4; 4:3) Labda Daudi alitunga wimbo huo ili kumshukuru Mungu na kuonyesha kwamba alikuwa amepata kitulizo baada ya mapinduzi ya Absalomu kukosa kufanikiwa. Au huenda zaburi hiyo iliandikwa kwa ajili ya Walawi ambao walikuwa waimbaji. Kwa vyovyote vile, kutafakari kuhusu zaburi hiyo kunaweza kututia nguvu ili tuendelee kumtegemea Yehova.

15. Kwa nini tunaweza kusali kwa Yehova kupitia Mwana wake tukiwa na uhakika?

15 Daudi anaonyesha tena kwamba anamtegemea Mungu kikamili na ana hakika kuwa Mungu anasikia na kujibu sala. Anaimba hivi: “Ninapoita, unijibu, Ee Mungu wangu mwadilifu. Katika taabu unifanyie nafasi pana. Nionyeshe kibali na kuisikia sala yangu.” (Zab. 4:1) Tunaweza kuwa na uhakika kama huo ikiwa tunazoea kutenda uadilifu. Tukijua kwamba Yehova, ‘Mungu mwadilifu’ anawabariki watu wake walio wanyoofu, tunaweza kusali kwake kwa uhakika kupitia Mwana wake tukiwa na imani katika fidia au dhabihu ya ukombozi ya Yesu. (Yoh. 3:16, 36) Hilo linatuletea amani nyingi kama nini!

16. Kwa nini huenda Daudi alivunjika moyo?

16 Nyakati nyingine, huenda tukapatwa na hali yenye kuvunja moyo ambayo inafanya tukose uhakika. Huenda Daudi alipatwa na hali kama hiyo kwa muda, kwa sababu anaimba hivi: “Enyi wana wa watu, utukufu wangu utatukanwa mpaka wakati gani, huku mkiendelea kupenda mambo ya upuuzi, huku mkiendelea kutafuta uwongo?” (Zab. 4:2) Inaelekea maneno “wana wa watu” yanamaanisha wanadamu wasio na kibali cha Mungu. Maadui wa Daudi ‘walipenda mambo ya upuuzi.’ Biblia ya New International Version inatafsiri mstari huo hivi: “Mtapenda mambo ya uwongo mpaka wakati gani na kutafuta miungu ya uwongo?” Hata tukivunjika moyo kwa sababu ya mambo ambayo wengine wanafanya, acheni tuendelee kusali kwa bidii na kuonyesha kwamba tunamtegemea kikamili yule Mungu wa pekee wa kweli.

17. Eleza jinsi tunavyoweza kutenda kulingana na Zaburi 4:3.

17 Maneno yafuatayo yanaonyesha wazi kwamba Daudi alimtegemea Mungu: “Basi jueni kwamba hakika Yehova atamtendea mshikamanifu wake kwa njia ya pekee; Yehova mwenyewe atasikia ninapomwita.” (Zab. 4:3) Tunahitaji kuwa na ujasiri na kumtegemea Yehova kikamili ili tuendelee kuwa washikamanifu kwake. Kwa mfano, sifa hizo zinahitajiwa na familia ya Kikristo wakati mshiriki wa familia hiyo anapotengwa na ushirika kwa sababu anakosa kutubu. Mungu anawabariki wale wanaoshikamana naye na njia zake. Kisha, kuwa washikamanifu na kumtegemea Yehova kikamili kunaleta shangwe kati ya watu wake.—Zab. 84:11, 12.

18. Kulingana na Zaburi 4:4, tunapaswa kufanya nini ikiwa mtu anasema au kututendea isivyofaa?

18 Namna gani mtu akisema au kufanya jambo ambalo linatukasirisha? Tunaweza kuendelea kuwa na shangwe ikiwa tutafanya jambo ambalo Daudi anasema: “Fadhaikeni, lakini msitende dhambi. Semeni moyoni mwenu, kitandani mwenu, na kunyamaza.” (Zab. 4:4) Ikiwa mtu anasema au kututendea isivyofaa, acheni tusitende dhambi kwa kulipiza kisasi. (Rom. 12:17-19) Tunaweza kusema moyoni mwetu mambo yanayotuumiza tukiwa katika kitanda chetu. Tukisali kuhusu jambo hilo, huenda tukaliona kwa njia tofauti na kuchochewa kusamehe kwa upendo. (1 Pet. 4:8) Kuhusiana na jambo hilo, mtume Paulo anatoa shauri lifuatalo ambalo inaonekana linategemea Zaburi 4:4: “Iweni na ghadhabu, lakini msitende dhambi; jua lisitue mkiwa katika hali ya kuchokozeka, wala msimpe Ibilisi nafasi.”—Efe. 4:26, 27.

19. Andiko la Zaburi 4:5 linaweza kutusaidia jinsi gani kuhusiana na dhabihu zetu za kiroho?

19 Akikazia kwa nini tunahitaji kumtegemea Mungu, Daudi anaimba hivi: “Toeni dhabihu za uadilifu, na kumtumaini Yehova.” (Zab. 4:5) Dhabihu zilizotolewa na Waisraeli zilikuwa na thamani ikiwa tu walizitoa wakiwa na nia inayofaa. (Isa. 1:11-17) Ili dhabihu zetu za kiroho zikubaliwe na Mungu, ni lazima sisi pia tuwe na nia inayofaa na tumtegemee kikamili.—Soma Methali 3:5, 6; Waebrania 13:15, 16.

20. Ni nini kinachofananishwa na ‘nuru ya uso wa Yehova?’

20 Daudi anaendelea kusema: “Kuna wengi wanaosema: ‘Ni nani atakayetuonyesha mema?’ Inua nuru ya uso wako juu yetu, Ee Yehova.” (Zab. 4:6) ‘Nuru ya uso wa Yehova’ inafananisha kibali cha Mungu. (Zab. 89:15) Kwa hiyo, Daudi anaposali: “Inua nuru ya uso wako juu yetu,” anamaanisha ‘tuonyeshe kibali.’ Kwa kuwa tunamtegemea Yehova, tuna kibali chake na shangwe nyingi tunapoendelea kufanya mapenzi yake tukiwa na uhakika.

21. Tunaweza kuwa na uhakika wa kupata nini ikiwa tutashiriki kikamili katika kazi ya mavuno ya kiroho inayofanywa leo?

21 Akitazamia shangwe inayotoka kwa Mungu ambayo inapita shangwe ya wakati wa mavuno, Daudi anamwimbia Yehova hivi: “Hakika wewe utaupa moyo wangu shangwe iliyo kubwa kuliko wakati ambapo nafaka yao na divai yao mpya imejaa.” (Zab. 4:7) Tunaweza kuwa na hakika kwamba tutapata shangwe moyoni ikiwa tutashiriki kikamili katika kazi ya mavuno ya kiroho inayofanywa leo. (Luka 10:2) Tunapoongozwa na ‘taifa lenye watu wengi’ la watiwa-mafuta, tunashangilia sasa tunapoona hesabu ya ‘wafanyakazi wa mavuno’ ikiendelea kuongezeka. (Isa. 9:3) Je, unashiriki kikamili katika kazi hiyo ya kuvuna inayoleta shangwe?

Songa Mbele kwa Uhakika na Kumtegemea Mungu Kikamili

22. Kulingana na Zaburi 4:8, Waisraeli walifurahia hali gani walipofuata Sheria za Mungu?

22 Daudi anamalizia zaburi hii kwa maneno haya: “Katika amani nitajilaza na kulala usingizi, kwa maana wewe peke yako, Ee Yehova, hunifanya nikae kwa usalama.” (Zab. 4:8) Waisraeli walipofuata Sheria ya Yehova, walifurahia amani pamoja naye na wakajihisi wakiwa salama. Kwa mfano, chini ya utawala wa Sulemani ‘Yuda na Israeli walikaa salama.’ (1 Fal. 4:25) Wale waliomtegemea Mungu walifurahia amani hata mataifa jirani yalipowaonyesha uadui. Kama Daudi, tunalala usingizi tukiwa salama kwa sababu Mungu anatufanya tuhisi tukiwa salama.

23. Tutafurahia hali gani ikiwa tutamtegemea Mungu kikamili?

23 Acheni tusonge mbele katika utumishi wa Yehova tukiwa na uhakika. Acheni pia tusali tukiwa na imani na hivyo tufurahie “amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote.” (Flp. 4:6, 7) Kufanya hivyo kunatuletea shangwe nyingi sana. Na bila shaka tunaweza kukabili wakati ujao tukiwa na uhakika ikiwa tutaendelea kumtegemea Yehova kikamili.

Ungesema Nini?

• Daudi alipatwa na matatizo gani kwa sababu ya Absalomu?

Zaburi ya 3 inatuchochea jinsi gani kuwa na uhakika?

Zaburi ya 4 inaweza kutusaidia jinsi gani kumtegemea Yehova hata zaidi?

• Tunaweza kufaidika jinsi gani kwa kumtegemea Mungu kikamili?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 29]

Hata alipokimbia kwa sababu ya Absalomu, Daudi alikuwa na uhakika katika Yehova

[Picha katika ukurasa wa 32]

Je, unamtegemea Yehova kikamili?