Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Lo! Jinsi Kilivyo Kina cha Hekima ya Mungu!’

‘Lo! Jinsi Kilivyo Kina cha Hekima ya Mungu!’

‘Lo! Jinsi Kilivyo Kina cha Hekima ya Mungu!’

“Lo! Jinsi kilivyo kina cha utajiri wa Mungu na hekima na ujuzi! Jinsi hukumu zake zisivyochunguzika na njia zake zisivyotafutika!” —ROM. 11:33.

1. Wakristo waliobatizwa wana pendeleo gani kubwa zaidi?

NI PENDELEO gani kubwa zaidi ambalo umewahi kupewa? Kwanza kabisa, huenda ukafikiria mgawo fulani ambao umepewa au heshima ambayo umeonyeshwa. Hata hivyo, pendeleo kubwa zaidi ambalo Mungu wa pekee wa kweli, Yehova, ametupatia tukiwa Wakristo waliobatizwa ni kuwa na uhusiano wa karibu pamoja naye. Kwa sababu ya uhusiano huo tumepata nafasi ya ‘kujulikana naye.’—1 Kor. 8:3; Gal. 4:9.

2. Kwa nini ni pendeleo kubwa sana kumjua Yehova na kujulikana naye?

2 Kwa nini ni pendeleo kubwa kumjua Yehova na kujulikana naye? Si kwamba tu yeye ni Mtu mkuu zaidi katika ulimwengu wote bali pia anawalinda wale wanaompenda. Nabii Nahumu aliongozwa na roho ya Mungu kuandika hivi: “Yehova ni mwema, yeye ni ngome katika siku ya taabu. Naye hutambua wale wanaotafuta kimbilio kwake.” (Nah. 1:7; Zab. 1:6) Kwa kweli, ili kupata uzima wa milele ni lazima tumjue Mungu wa kweli na Mwana wake, Yesu Kristo.—Yoh. 17:3.

3. Kupata kumjua Mungu kunatia ndani nini?

3 Kumjua Mungu hakumaanishi kujua tu jina lake la kibinafsi. Ni lazima tumjue kama Rafiki, na kuelewa mambo anayopenda na yale asiyopenda. Njia muhimu ya kuonyesha kwamba tumemjua Mungu vizuri sana ni kuishi kulingana na ujuzi huo. (1 Yoh. 2:4) Lakini kuna jambo lingine ambalo tunahitaji ikiwa kwa kweli tunataka kumjua Yehova. Hatupaswi kujua tu yale ambayo amefanya bali pia tunapaswa kujua ni jinsi gani na kwa nini ametenda hivyo. Kadiri tunavyoelewa makusudi ya Yehova, ndivyo tunavyochochewa kustaajabia ‘kina cha hekima ya Mungu.’—Rom. 11:33.

Mungu Mwenye Kusudi

4, 5. (a) Neno “kusudi” linamaanisha nini kama linavyotumiwa katika Biblia? (b) Toa mfano unaoonyesha jinsi kusudi linavyoweza kutimizwa kwa njia zaidi ya moja.

4 Yehova ni Mungu mwenye kusudi, na Biblia inasema kuhusu ‘kusudi lake la milele.’ (Efe. 3:10, 11) Maneno hayo yanamaanisha nini hasa? Kama linavyotumiwa katika Biblia, neno “kusudi” linamaanisha mradi fulani hususa, au shabaha, ambayo inaweza kufikiwa kwa njia zaidi ya moja.

5 Kwa mfano: Huenda mtu akapenda kusafiri kwenda mahali fulani hususa. Hivyo, kufika mahali hapo kunaweza kuwa mradi, au kusudi lake. Huenda akahitaji kuamua mambo mbalimbali kuhusiana na aina ya usafiri na barabara ambayo anaweza kutumia. Anaposafiri kwenye barabara ambayo amechagua, huenda kwa ghafula akakumbana na hali mbaya ya hewa, msongamano wa magari, na vizuizi barabarani, na hivyo kumlazimisha atumie barabara nyingine. Hata hivyo, haidhuru ni marekebisho gani anayohitaji kufanya, bado atatimiza mradi wake anapofika mahali anapoenda.

6. Yehova ameonyesha jinsi gani kwamba anabadilika kulingana na hali ili atimize kusudi lake?

6 Vivyo hivyo, Yehova ameonyesha kwamba anabadilika sana kulingana na hali ili kutimiza kusudi lake la milele. Akifikiria uhuru wa kuchagua wa viumbe wake wenye akili, anafanya marekebisho haraka kuhusu jinsi ya kutimiza kusudi lake. Kwa mfano, acheni tuchunguze jinsi Yehova anavyotimiza kusudi lake kuhusu Uzao ulioahidiwa. Mwanzoni, Yehova aliwaambia hivi wanadamu wawili wa kwanza: “Zaeni, muwe wengi, mjaze dunia na kuitiisha.” (Mwa. 1:28) Je, kusudi hilo lililotangazwa lilizuiwa na uasi uliotokea katika bustani ya Edeni? Bila shaka hapana! Yehova alichukua mara moja hatua ya kushughulika na hali hiyo mpya kwa kutumia “barabara” nyingine ili kutimiza kusudi lake. Alitabiri kutokea kwa “uzao” ambao ungeondoa madhara yaliyosababishwa na wale waasi.—Mwa. 3:15; Ebr. 2:14-17; 1 Yoh. 3:8.

7. Tunajifunza nini kutokana na maelezo ya Yehova kujihusu kama yalivyoandikwa katika andiko la Kutoka 3:14?

7 Uwezo wa Yehova wa kubadilika kulingana na hali mpya anapoendelea kutimiza kusudi lake unapatana na maelezo aliyotoa kujihusu yeye mwenyewe. Musa alipomweleza Yehova kuhusu mambo ambayo yangemzuia asitimize mgawo aliopewa, Yehova alimhakikishia kwa kusema: “‘Nitakuwa kile nitakachokuwa.’ Naye akaongeza kusema: ‘Hivi ndivyo utakavyowaambia wana wa Israeli, “Nitakuwa amenituma kwenu.”’” (Kut. 3:14) Ndiyo, Yehova ana uwezo wa kuwa chochote anachohitaji kuwa ili kutimiza kusudi lake kikamili! Hilo linaonyeshwa vizuri na mtume Paulo katika sura ya 11 ya kitabu cha Waroma. Katika sura hiyo Paulo anazungumza kuhusu mzeituni wa mfano. Kuchunguza mfano huo kutatusaidia kuthamini hata zaidi hekima ya Yehova yenye kina, iwe tuna tumaini la kwenda mbinguni au kupata uzima wa milele duniani.

Kusudi la Yehova Kuhusu Uzao Ulioahidiwa

8, 9. (a) Ni mambo gani manne ya hakika yatakayotusaidia kuelewa mfano wa mzeituni? (b) Ni jibu la swali gani ambalo linafunua jinsi Yehova anavyobadilika kulingana na hali ili kutimiza kusudi lake?

8 Kabla ya kuelewa mfano wa mzeituni, tunahitaji kujua mambo manne ya hakika kuhusu jinsi kusudi la Yehova lilivyoendelea kutimizwa kuhusiana na uzao ulioahidiwa. Kwanza, Yehova alimwahidi Abrahamu kwamba “mataifa yote ya dunia hakika [yangejibariki]” kupitia uzao wake, au wazao. (Mwa. 22:17, 18) Pili, taifa la Israeli ambalo lilitokana na Abrahamu lilipewa nafasi ya kutokeza “ufalme wa makuhani.” (Kut. 19:5, 6) Tatu, wakati Waisraeli wengi wa asili walipomkataa Masihi, Yehova alichukua hatua nyingine ili kutokeza “ufalme wa makuhani.” (Mt. 21:43; Rom. 9:27-29) Mwishowe, ingawa Yesu ndiye sehemu ya kwanza ya uzao wa Abrahamu, watu wengine wanapewa pendeleo la kuwa sehemu ya uzao huo.—Gal. 3:16, 29.

9 Kwa kutegemea mambo hayo manne ya hakika, tunajifunza katika kitabu cha Ufunuo kwamba jumla ya watu 144,000 watatawala pamoja na Yesu wakiwa wafalme na makuhani huko mbinguni. (Ufu. 14:1-4) Hao wanaitwa pia “wana wa Israeli.” (Ufu. 7:4-8) Lakini je, wale 144,000 wote ni Waisraeli wa asili, au Wayahudi? Jibu la swali hilo linafunua jinsi Yehova anavyobadilika kulingana na hali ili kutimiza kusudi lake. Acheni sasa tuone jinsi barua ya mtume Paulo kwa Waroma inavyotusaidia kupata jibu.

“Ufalme wa Makuhani”

10. Taifa la Israeli lilikuwa na tumaini gani la pekee?

10 Kama ilivyotajwa mapema, taifa la Israeli ndilo lililokuwa na tumaini la pekee la kutoa washiriki ambao wangekuwa “ufalme wa makuhani na taifa takatifu.” (Soma Waroma 9:4, 5.) Lakini ni jambo gani lingetukia wakati ambapo Uzao ulioahidiwa ungefika? Je, taifa la Waisraeli wa asili lingetokeza hesabu kamili ya Waisraeli wa kiroho 144,000 ambao wangekuja kuwa sehemu ya pili ya uzao wa Abrahamu?

11, 12. (a) Kuchaguliwa kwa wale ambao wangekuwa Ufalme wa kimbingu kulianza wakati gani, na Wayahudi wengi walioishi wakati huo waliitikia jinsi gani? (b) Yehova alikamilisha jinsi gani “hesabu kamili” ya wale ambao wangekuja kuwa uzao wa Abrahamu?

11 Soma Waroma 11:7-10. Wakiwa taifa, Wayahudi wa karne ya kwanza walimkataa Yesu. Hivyo, watu wengine wakapata pia pendeleo la kutokeza uzao wa Abrahamu. Hata hivyo, wale ambao wangekuwa “ufalme wa makuhani” mbinguni walipoanza kuchaguliwa siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K., kulikuwa na Wayahudi fulani wenye mioyo minyoofu ambao walikubali mwaliko huo. Wakiwa maelfu machache, Wayahudi hao walikuwa kama “mabaki” tu wakilinganishwa na taifa lote la Wayahudi.—Rom. 11:5.

12 Hata hivyo, Yehova angekamilisha jinsi gani “hesabu kamili” ya wale ambao wangekuja kuwa uzao wa Abrahamu? (Rom. 11:12, 25) Ona jibu linalotolewa na mtume Paulo: “Si kwamba neno la Mungu lilikuwa limeshindwa. Kwa maana si wote wanaotokana na Israeli [wa asili] ni ‘Israeli’ kikweli. Wala si wote walio watoto [sehemu ya uzao wa Kiabrahamu] kwa sababu wao ni uzao [mzao] wa Abrahamu . . . Yaani, watoto kwa njia ya mwili si watoto wa Mungu kikweli, bali watoto kwa njia ya ahadi huhesabiwa kuwa ndio uzao.” (Rom. 9:6-8) Kwa hiyo, ukoo wa kimwili kutokana na Abrahamu halikuwa takwa pekee lililohitajiwa ili kusudi la Yehova kuhusu uzao litimizwe.

Mzeituni wa Mfano

13. Ni nini kinachofananishwa na (a) mzeituni, (b) mzizi wake, (c) shina lake, na (d) matawi yake?

13 Mtume Paulo anawalinganisha wale ambao wanakuwa sehemu ya uzao wa Abrahamu na matawi ya mzeituni wa mfano. * (Rom. 11:21) Mzeituni huo uliopandwa unafananisha kutimizwa kwa kusudi la Mungu kuhusiana na agano la Kiabrahamu. Mzizi wa mti huo ni mtakatifu na unafananisha Yehova akiwa yule ambaye anapatia Israeli wa kiroho uhai. (Isa. 10:20; Rom. 11:16) Shina linafananisha Yesu akiwa sehemu ya kwanza ya uzao wa Abrahamu. Matawi yote hayo kwa pamoja yanafananisha “hesabu kamili” ya wale ambao wanatiwa ndani ya sehemu ya pili ya uzao wa Abrahamu.

14, 15. Ni nani ‘waliokatwa’ kutoka kwenye mzeituni uliopandwa, na ni nani waliopandikizwa kwenye mzeituni huo?

14 Katika mfano wa mzeituni, Wayahudi wa asili ambao walimkataa Yesu wanalinganishwa na matawi ambayo “yalikatwa.” (Rom. 11:17) Hivyo, walipoteza nafasi ya kuwa sehemu ya uzao wa Abrahamu. Lakini ni nani ambao wangechukua mahali pao? Wayahudi wa asili ambao walijivunia kuwa wazao wa kimwili wa Abrahamu hawakufikiri kamwe kwamba watu wengine wangeweza kuchukua mahali pao. Lakini Yohana Mbatizaji alikuwa tayari amewaonya kwamba ikiwa Yehova angetaka, angeweza kumwinulia Abrahamu watoto kutoka katika mawe.—Luka 3:8.

15 Basi, Yehova alifanya nini ili kutimiza kusudi lake? Paulo anaeleza kwamba matawi kutoka kwenye mzeituni wa mwituni yalipandikizwa kwenye mzeituni uliopandwa ili kuchukua mahali pa yale matawi yaliyokatwa. (Soma Waroma 11:17, 18.) Hivyo, Wakristo watiwa-mafuta wa mataifa, kama Wakristo fulani katika kutaniko la Roma, walipandikizwa kwa njia ya mfano kwenye mzeituni huo wa mfano. Katika njia hiyo walikuja kuwa sehemu ya uzao wa Abrahamu. Mwanzoni, walikuwa kama matawi ya mzeituni wa mwituni, kwa sababu hawakuwa na nafasi yoyote ya kuwa sehemu ya agano hilo la pekee. Lakini Yehova aliwafungulia njia ili wawe Wayahudi wa kiroho.—Rom. 2:28, 29.

16. Mtume Petro alieleza jinsi gani kuanzishwa kwa taifa jipya la kiroho?

16 Mtume Petro anaeleza hali hiyo kwa njia hii: “Kwa hiyo, yeye [Yesu Kristo] ni mwenye thamani kwenu ninyi [Waisraeli wa kiroho, kutia ndani Wakristo wa Mataifa], kwa kuwa ninyi ni waamini; lakini kwa wale wasioamini, ‘jiwe lilelile ambalo wajenzi walilikataa limekuwa jiwe kuu la pembeni,’ na ‘jiwe la kukwaza na mwamba wa kuangusha.’ . . . Lakini ninyi ni ‘jamii iliyochaguliwa, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa kuwa mali ya pekee, ili mtangaze kotekote sifa bora’ zake yeye aliyewaita ninyi kutoka katika giza kuingia katika nuru yake ya ajabu. Kwa kuwa wakati mmoja ninyi mlikuwa si watu, lakini sasa ninyi ni watu wa Mungu; mlikuwa wale ambao hawakuwa wameonyeshwa rehema, lakini sasa ninyi ni wale ambao wameonyeshwa rehema.”—1 Pet. 2:7-10.

17. Jambo ambalo Yehova alifanya lilikuwa “kinyume cha asili” jinsi gani?

17 Yehova alifanya jambo ambalo wengi hawakutazamia kabisa. Paulo anaeleza yale yaliyotukia kuwa “kinyume cha asili.” (Rom. 11:24) Hilo lilitukia jinsi gani? Kwa kweli, lingeonekana kuwa jambo lisilo la kawaida, hata lisilo la asili, kupandikiza tawi la mwituni kwenye mti uliopandwa, lakini hivyo ndivyo wakulima fulani walivyofanya katika karne ya kwanza. * Kwa njia hiyohiyo, Yehova alifanya jambo fulani lisilo la kawaida. Kwa maoni ya Wayahudi, Watu wa Mataifa hawangeweza kuzaa matunda yenye kukubalika. Hata hivyo, Yehova aliwafanya watu hao wa mataifa kuwa sehemu ya “taifa” ambalo lilizaa matunda ya Ufalme. (Mt. 21:43) Kuanzia mwaka wa 36 W.K., wakati Kornelio, Mtu wa kwanza wa Mataifa asiyetahiriwa alipogeuzwa imani na kutiwa mafuta, mlango ulifunguliwa kwa watu wasio Wayahudi ambao hawakuwa wametahiriwa kupandikizwa kwenye mzeituni huo wa mfano.—Mdo. 10:44-48. *

18. Wayahudi wa asili walikuwa na nafasi gani baada ya mwaka wa 36 W.K.?

18 Je, hilo linamaanisha kwamba baada ya mwaka wa 36 W.K., Wayahudi wa asili hawakuwa tena na nafasi ya kuwa sehemu ya uzao wa Abrahamu? Hapana. Paulo anaeleza: “Wao pia [Wayahudi wa asili], ikiwa hawatadumu katika ukosefu wao wa imani, watapandikizwa; kwa maana Mungu anaweza kuwapandikiza tena. Kwa maana ikiwa wewe ulikatwa kutoka kwenye mzeituni ulio wa asili ya mwituni na kupandikizwa kinyume cha asili katika mzeituni wa bustanini, si afadhali zaidi kwamba hawa walio wa asili wapandikizwe katika mzeituni wao wenyewe!” *Rom. 11:23, 24.

“Israeli Wote Wataokolewa”

19, 20. Yehova anatimiza nini kama inavyoonyeshwa na mzeituni wa mfano?

19 Ndiyo, kusudi la Yehova kuhusu “Israeli wa Mungu” linatimizwa kwa njia ya ajabu sana. (Gal. 6:16) Kama Paulo alivyosema, “Israeli wote wataokolewa.” (Rom. 11:26) Kwa wakati wa Yehova uliowekwa, “Israeli wote,” yaani, hesabu kamili ya Waisraeli wa kiroho, watatumika wakiwa wafalme na makuhani mbinguni. Hakuna kitu kinachoweza kuzuia kusudi la Yehova lisitimie!

20 Kama ilivyotabiriwa, uzao wa Abrahamu, yaani, Yesu Kristo pamoja na wale 144,000, utaleta baraka nyingi kwa “watu wa mataifa.” (Rom. 11:12; Mwa. 22:18) Kwa njia hiyo, watu wote wa Mungu wanafaidika kutokana na mpango huo. Kwa kweli, tunapotafakari kuhusu kutimizwa kwa kusudi la Yehova la milele, tunastaajabishwa na “kina cha utajiri wa Mungu na hekima na ujuzi.”—Rom. 11:33.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 13 Bila shaka, hakuna mzeituni ambao unafananisha kikundi fulani halisi cha watu au kikundi cha mfano. Ingawa Waisraeli wa asili walitokeza wafalme na makuhani, taifa hilo halikuwa ufalme wa makuhani. Wafalme katika Israeli walikatazwa na sheria wasiwe makuhani. Kwa hiyo, Waisraeli wa asili hawakutumika wakiwa mzeituni halisi. Paulo anaonyesha jinsi kusudi la Mungu la kutokeza “ufalme wa makuhani” linavyotimizwa kuhusiana na Israeli wa kiroho. Habari hii inarekebisha maelezo yaliyochapishwa katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Januari 15, 1984, ukurasa wa 7-12.

^ fu. 17 Nafasi ambayo Wayahudi wa asili walikuwa wamepewa ya kuwa sehemu ya taifa jipya la kiroho ilifikia mwisho baada ya miaka mitatu na nusu kwisha. Unabii kuhusu majuma 70 ya miaka ulitabiri matukio hayo.—Dan. 9: 27.

^ fu. 18 Kiambishi au neno la Kigiriki linalotafsiriwa “bustani” katika andiko la Waroma 11:24 linatokana na neno linalomaanisha “-zuri, bora sana” au “kitu kinachofaana vizuri na makusudi yake.” Kiambishi hicho kinatumiwa hasa kuhusu vitu ambavyo vinatimiza kusudi ambalo vilitengenezwa vitimize.

Je, Unakumbuka?

• Tunajifunza nini kumhusu Yehova kutokana na jinsi anavyotimiza kusudi lake?

• Katika Waroma sura ya 11, ni nini kinachofananishwa na . . .

mzeituni?

mzizi wake?

shina lake?

matawi yake?

• Kwa nini utaratibu wa kupandikiza ulikuwa “kinyume cha asili”?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku/​Picha katika ukurasa wa 24]

 Kwa Nini Matawi ya Mzeituni wa Mwituni Yalipandikizwa?

▪ Lucius Junius Moderatus Columella alikuwa askari-jeshi Mroma na mkulima aliyeishi katika karne ya kwanza W.K. Anajulikana sana kwa sababu ya vitabu 12 alivyoandika kuhusu maisha ya mashambani na ukulima.

Katika kitabu chake cha tano, anataja methali hii ya zamani: “Anayelima shamba la mizeituni, analiomba matunda; anayelitilia mbolea, analisihi limpe matunda; na yule anayekata matawi yake, analilazimisha lizae matunda.”

Baada ya kueleza kuhusu miti inayositawi na bado haizai matunda, anapendekeza utaratibu ufuatao: “Ni mpango mzuri kutoboa miti hiyo kwa kifaa kama vile msumari na kuingiza ndani kabisa ya shimo hilo tawi dogo la kijani kibichi lililochukuliwa kutoka kwenye mzeituni wa mwituni; matokeo ni kwamba mti huo, kwa kuwa umetiwa au kupachikwa mche wenye kuzaa, unazaa zaidi.”

[Picha katika ukurasa wa 23]

Je, unaelewa mfano wa mzeituni wa mfano?