Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Mwatilie Maanani Wale Wanaofanya Kazi kwa Bidii Kati Yenu”

“Mwatilie Maanani Wale Wanaofanya Kazi kwa Bidii Kati Yenu”

“Mwatilie Maanani Wale Wanaofanya Kazi kwa Bidii Kati Yenu”

“Mwatilie maanani wale wanaofanya kazi kwa bidii kati yenu na kuwasimamia ninyi katika Bwana na kuwaonya ninyi.”—1 THE. 5:12.

1, 2. (a) Kutaniko la Thesalonike lilikuwa katika hali gani Paulo alipowaandikia barua yake ya kwanza? (b) Paulo aliwatia moyo Wathesalonike wafanye nini?

JIWAZIE ukiwa mshiriki wa kutaniko la Thesalonike katika karne ya kwanza, ambalo ni moja kati ya makutaniko ya mapema zaidi kuanzishwa huko Ulaya. Mtume Paulo alitumia wakati mwingi kuwajenga akina ndugu huko. Huenda aliweka rasmi wanaume wazee waongoze, kama ilivyokuwa katika makutaniko mengine. (Mdo. 14:23) Lakini baada ya kutaniko hilo kuanzishwa, Wayahudi walikusanya umati wa watu ili kuwafukuza Paulo na Sila katika jiji hilo. Huenda Wakristo waliobaki walihisi upweke, labda hata waliogopa.

2 Ni wazi kwamba baada ya kuondoka Thesalonike, Paulo alihangaikia hali ya kutaniko hilo changa. Alijaribu kurudi huko, lakini “Shetani aliizuia” njia yake. Hivyo, alimtuma Timotheo ili kulitia moyo kutaniko hilo. (1 The. 2:18; 3:2) Timotheo alipoleta ripoti nzuri, Paulo alichochewa kuwaandikia Wathesalonike barua. Kati ya mambo mengine, Paulo aliwatia moyo ‘wawatilie maanani wale wanaowasimamia.’—Soma 1 Wathesalonike 5:12, 13.

3. Wakristo wa Thesalonike walikuwa na sababu gani nzuri za kuwafikiria wanaume wazee kwa njia inayozidi ile ya kawaida?

3 Ndugu waliokuwa wakiongoza kati ya Wakristo wa Thesalonike hawakuwa na uzoefu kama wa Paulo na wasafiri wenzake; wala hawakuwa na urithi wa utajiri wa kiroho ambao wazee wa Yerusalemu walikuwa nao. Kwa vyovyote vile, mwaka mmoja haukuwa umepita tangu kutaniko hilo kuanzishwa! Hata hivyo, washiriki wa kutaniko walikuwa na sababu nzuri ya kuwathamini wanaume wao wazee waliokuwa ‘wakifanya kazi kwa bidii’ na ‘kulisimamia’ kutaniko na “kuwaonya” ndugu. Kwa kweli, walikuwa na sababu nzuri ya “kuwafikiria [wazee hao] kwa njia inayozidi ile ya kawaida katika upendo.” Ombi hilo lilifuatwa na shauri hili la Paulo: “Iweni wenye kufanya amani mtu na mwenzake.” Kama ungekuwa huko Thesalonike, je, ungeonyesha kwamba unathamini kutoka moyoni kazi ya wazee? Una maoni gani kuhusu “zawadi katika wanadamu” ambazo Mungu kupitia Kristo amelipatia kutaniko lenu?—Efe. 4:8.

“Wanaofanya Kazi kwa Bidii”

4, 5. Kwa nini wanaume wazee katika siku za Paulo walipaswa kujitahidi sana ili kulifundisha kutaniko, na kwa nini wanapaswa kufanya hivyo leo?

4 Baada ya kuwatuma Paulo na Sila kwenda Beroya, wanaume wazee huko Thesalonike walikuwa ‘wakifanya kazi kwa bidii’ jinsi gani? Kwa kumwiga Paulo, hakuna shaka kwamba walifundisha kutaniko kwa kutumia Maandiko. Huenda ukajiuliza, ‘Je, Wakristo huko Thesalonike walithamini sana Neno la Mungu?’ Kwa vyovyote vile, Biblia inasema kwamba Waberoya walikuwa “wasikivu kuliko wale wa Thesalonike, . . . wakiyachunguza Maandiko kwa uangalifu kila siku.” (Mdo. 17:11) Hata hivyo, ulinganifu huo ulihusu Wayahudi Wathesalonike kwa ujumla, bali si Wakristo. Wale waliogeuka na kuwa waamini ‘walilikubali neno la Mungu, si kama neno la wanadamu, bali kama neno la Mungu.’ (1 The. 2:13) Ni wazi kwamba wanaume wazee walijitahidi sana kuwalisha kiroho watu hao.

5 Leo, jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara inalitayarishia kundi la Mungu ‘chakula kwa wakati unaofaa.’ (Mt. 24:45) Chini ya mwongozo wa mtumwa huyo, wazee wanafanya kazi kwa bidii ili kuwalisha ndugu zao kiroho. Huenda washiriki wa kutaniko wakawa na vitabu vingi vinavyozungumzia Biblia, na huenda vifaa kama vile Fahirisi na Watchtower Library kwenye CD-ROM vikapatikana katika lugha fulani. Ili kutosheleza mahitaji ya kiroho ya kutaniko, wazee wanatumia saa nyingi kutayarisha sehemu za mikutano ili watoe habari walizogawiwa kwa njia yenye kujenga. Je, umewahi kuwazia ni muda gani ambao wazee wanatumia ili kutayarisha sehemu zao za mikutano ya kutaniko, makusanyiko ya pekee, ya mzunguko, na ya wilaya?

6, 7. (a) Wanaume wazee huko Thesalonike waliiga mfano gani wa Paulo? (b) Kwa nini inaweza kuwa vigumu leo kwa wazee kumwiga Paulo?

6 Wanaume wazee huko Thesalonike walikumbuka mfano mzuri ambao Paulo aliwawekea katika kulichunga kundi. Hakufanya kazi ya uchungaji kidesturi au ili kutimiza wajibu tu. Lakini kama tulivyozungumzia katika habari iliyotangulia, Paulo ‘alikuwa mpole kama mama mwenye kunyonyesha anavyowatunza kwa upendo watoto wake mwenyewe.’ (Soma 1 Wathesalonike 2:7, 8.) Alikuwa tayari ‘kuwapa hata nafsi yake mwenyewe’! Walipokuwa wakifanya kazi ya uchungaji, wanaume hao wazee walipaswa kumwiga Paulo.

7 Wachungaji Wakristo leo wanamwiga Paulo kwa kulipenda na kulithamini sana kundi. Kiasili, huenda kondoo wengine wasiwe wenye shauku na wenye urafiki. Hata hivyo, wazee wanajitahidi kuonyesha ufahamu na ‘kupata mema’ ndani ya kondoo. (Met. 16:20) Ni kweli kwamba, kwa kuwa mzee ni mtu asiye mkamilifu, huenda akajitahidi sana ili kuwa na maoni mazuri kuhusu kila kondoo. Hata hivyo, anapojikaza kadiri ya uwezo wake ili kuwa mpole kwa wote, je, hapaswi kupongezwa kwa juhudi zake za kuwa mchungaji mwema chini ya Kristo?

8, 9. Taja njia fulani ambazo wazee wanaonyesha leo kwamba ‘wanaendelea kuzilinda nafsi zetu.’

8 Sisi sote tuna sababu nzuri ya ‘kujinyenyekeza’ kwa wazee. Kama Paulo alivyoandika, ‘wanaendelea kuzilinda nafsi zetu.’ (Ebr. 13:17) Maneno hayo yanatukumbusha mchungaji halisi anayejinyima usingizi ili kulinda kundi lake. Vivyo hivyo, huenda leo wazee wakajinyima usingizi wanaposhughulikia mahitaji ya wale ambao wana matatizo ya kiafya au kihisia au kiroho. Kwa mfano, ndugu wanaotumika katika Halmashauri za Uhusiano na Hospitali wanaamshwa kutoka katika usingizi ili kusaidia wakati kunapokuwa na matatizo ya kitiba. Hata hivyo, tunathamini kama nini utumishi wao tunapopambana na hali kama hiyo!

9 Wazee wa Halmashauri za Ujenzi za Mkoa na halmashauri za kutoa misaada wanafanya kazi kwa bidii ili kuwasaidia akina ndugu. Tunapaswa kuwaunga mkono kwa moyo wote! Fikiria kazi ya kutoa misaada iliyofanywa baada ya upepo mkali au Kimbunga kinachoitwa Nargis kuipiga nchi ya Myanmar katika mwaka wa 2008. Ili kufikia Kutaniko la Bothingone katika eneo la Irrawaddy Delta lililoharibiwa sana, kikundi cha kutoa misaada kilisafiri kupitia eneo lililoharibiwa sana lenye kujaa maiti. Ndugu wa eneo hilo walipoona kwamba kikundi cha kwanza cha kutoa misaada ambacho kilifika Bothingone kilitia ndani mwangalizi wao wa zamani wa mzunguko, walipaaza sauti hivi: “Tazama! Ni mwangalizi wetu wa mzunguko! Yehova ametuokoa!” Je, unathamini kazi ya bidii inayofanywa na wazee mchana na usiku? Wazee fulani wanawekwa rasmi kutumikia katika halmashauri za pekee ili kushughulikia matatizo mazito ya kihukumu. Wazee hao hawajigambi kuhusu mambo ambayo wanatimiza; hata hivyo, wale wanaofaidika na utumishi wao wanathamini sana kazi yao.—Mt. 6:2-4.

10. Ni kazi gani zisizojulikana sana ambazo wazee wanafanya?

10 Leo pia, wazee wengi wanashughulikia kazi inayohusu maandishi ya kutaniko. Kwa mfano, mratibu wa baraza la wazee anatayarisha ratiba au programu kwa ajili ya mikutano ya kila juma. Mwandishi wa kutaniko anajumlisha ripoti za utumishi wa shambani za kila mwezi na kila mwaka. Mwangalizi wa shule anatayarisha kwa uangalifu ratiba ya shule. Baada ya kila miezi mitatu, hesabu ya kutaniko inakaguliwa. Wazee wanasoma barua kutoka kwenye ofisi ya tawi na wanafuata mwongozo ambao unasaidia kudumisha “umoja katika imani.” (Efe. 4:3, 13) Kupitia juhudi za wazee hao wenye bidii, ‘mambo yote yanatendeka kwa adabu na kwa mpango.’—1 Kor. 14:40.

“Kuwasimamia Ninyi”

11, 12. Ni nani wanaosimamia kutaniko, na hilo linatia ndani nini?

11 Paulo alisema kwamba wanaume wazee wenye bidii huko Thesalonike ‘walisimamia’ kutaniko. Katika lugha ya asili, neno hilo linamaanisha “kusimama mbele” na linaweza kutafsiriwa kuwa “kuelekeza; kuongoza kati ya.” (1 The. 5:12) Paulo alisema pia kwamba wazee hao ‘wanafanya kazi kwa bidii.’ Hakuwa akizungumza kuhusu ‘mwangalizi mmoja msimamizi,’ bali kuhusu wanaume wote wazee katika kutaniko. Leo, wazee wengi wanasimama mbele ya kutaniko na kuongoza mikutano. Marekebisho ya hivi karibuni ya kutumia maneno “mratibu wa baraza la wazee” yanatusaidia kuwaona wazee wote kuwa washiriki wa baraza lenye umoja.

12 ‘Kusimamia’ kutaniko kunatia ndani mengi zaidi kuliko kufundisha tu. Neno hilohilo linatumiwa katika 1 Timotheo 3:4. Paulo alisema kwamba mwangalizi anapaswa kuwa “mwanamume anayeisimamia nyumba yake mwenyewe kwa njia nzuri, mwenye watoto wanaojitiisha pamoja na kuchukua mambo kwa uzito wote.” Ni wazi kwamba hapa neno “anayeisimamia” linatia ndani si kufundisha tu watoto wake bali pia kuongoza katika familia na kuwa na “watoto wanaojitiisha.” Ndiyo, wazee wanaongoza katika kutaniko, wakiwasaidia wote kujitiisha au kujinyenyekeza kwa Yehova.—1 Tim. 3:5.

13. Kwa nini inaweza kuchukua wakati kufikia uamuzi kwenye mkutano wa wazee?

13 Ili kusimamia kundi vizuri, wazee wanazungumza pamoja jinsi ya kushughulikia mahitaji ya kutaniko. Huenda ikawa rahisi kwa mzee mmoja kufanya maamuzi yote. Hata hivyo, kwa kufuata mfano wa baraza linaloongoza la karne ya kwanza, mabaraza ya wazee leo yanazungumzia mambo kwa uhuru, huku yakifuata mwongozo wa Maandiko. Kusudi lao ni kufuata kanuni za Kimaandiko ili kushughulikia mahitaji ya kutaniko lao. Inakuwa rahisi kufanya hivyo ikiwa kila mzee anajitayarisha kwa ajili ya mikutano ya wazee, kuchunguza Maandiko na miongozo inayotoka kwa jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara. Bila shaka, kufanya hivyo kunachukua wakati. Wanapokuwa na maoni yanayotofautiana, kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza wakati baraza linaloongoza lilipokuwa likizungumza kuhusu suala la kutahiriwa, huenda walihitaji kutumia wakati zaidi na kufanya utafiti ili kufikia uamuzi wa pamoja ambao unategemea Maandiko.—Mdo. 15:2, 6, 7, 12-14, 28.

14. Je, unathamini kwamba baraza la wazee linafanya kazi pamoja kwa umoja? Kwa nini unahisi hivyo?

14 Ni nini kinachoweza kutokea ikiwa mzee mmoja anasisitiza kwamba maoni yake yafuatwe au anajaribu kuwashawishi wengine wafuate maoni yake? Au namna gani ikiwa mtu anapanda mbegu za migawanyiko, kama Diotrefe alivyofanya katika karne ya kwanza? (3 Yoh. 9, 10) Bila shaka, kutaniko lote litaumia. Ikiwa Shetani alijaribu kulivuruga kutaniko katika karne ya kwanza, tunaweza kuwa na hakika kwamba anataka kuvuruga amani ya kutaniko leo. Anaweza kuchochea mielekeo yetu ya kibinadamu yenye uchoyo, kama vile tamaa ya kutaka ukubwa. Kwa hiyo, wazee wanapaswa kusitawisha sifa ya unyenyekevu na kufanya kazi pamoja wakiwa baraza lenye umoja. Tunathamini kama nini unyenyekevu wa wazee ambao wanashirikiana wakiwa baraza!

“Kuwaonya Ninyi”

15. Wazee wanachochewa na nini wanapomwonya ndugu au dada fulani?

15 Kisha Paulo alikazia kazi ngumu lakini ya maana ya wanaume wazee: kuonya kundi. Katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, ni Paulo peke yake aliyetumia neno la Kigiriki linalotafsiriwa “kuonya.” Linaweza kumaanisha shauri kali lakini halionyeshi uadui. (Mdo. 20:31; 2 The. 3:15) Kwa mfano, Paulo aliwaandikia Wakorintho hivi: “Ninaandika mambo haya, si ili kuwaaibisha ninyi, bali kuwaonya kama watoto wangu wapendwa.” (1 Kor. 4:14) Alitoa onyo hilo kwa sababu aliwahangaikia wengine kwa upendo.

16. Wazee wanapaswa kukumbuka nini wanapowaonya wengine?

16 Wazee wanakumbuka kwamba ni jambo la maana kufikiria jinsi wanavyowaonya wengine. Wanajikaza kumwiga Paulo kwa kuwa wenye fadhili, wenye upendo, na wenye kusaidia. (Soma 1 Wathesalonike 2:11, 12.) Bila shaka, wazee ‘wanalishika imara neno la uaminifu ili waweze kuhimiza kwa fundisho lenye afya.’—Tito 1:5-9.

17, 18. Unapaswa kukumbuka nini unapoonywa na mzee fulani?

17 Bila shaka, wazee si wakamilifu na wanaweza kusema mambo ambayo yatawafanya wajute baadaye. (1 Fal. 8:46; Yak. 3:8) Pia, wazee wanajua kwamba kwa kawaida kuwashauri ndugu na dada wa kiroho si jambo ‘lenye kuleta shangwe, bali lenye kuhuzunisha.’ (Ebr. 12:11) Hivyo, mzee anapomfikia mtu fulani ili kumwonya, inaelekea anafanya hivyo baada ya kusali na kufikiria sana jambo hilo. Ikiwa umeonywa, je, unathamini kwamba mzee huyo anakuhangaikia kwa upendo?

18 Tuseme una tatizo la kiafya ambalo madaktari hawalielewi. Kisha, daktari mmoja anatambua vizuri tatizo lako, lakini unaona ni vigumu kukubali matokeo ya uchunguzi wake. Je, utamkasirikia daktari huyo? Hapana! Hata ikiwa atapendekeza ufanyiwe upasuaji, inaelekea kwamba utakubali matibabu hayo, huku ukiamini kwamba yatakusaidia. Labda uliumia moyoni kwa sababu ya namna ambavyo daktari huyo alikujulisha habari hiyo, lakini je, ungeacha hilo likuzuie kufanya uamuzi unaofaa? Sivyo kabisa. Vivyo hivyo, usiruhusu njia inayotumiwa kukuonya ikuzuie kuwasikiliza wale ambao huenda Yehova na Yesu wanatumia ili kukujulisha jinsi unavyoweza kufanya maendeleo kiroho au kulinda uhusiano wako pamoja na Yehova.

Thamini Uandalizi wa Yehova wa Kuwa na Wazee

19, 20. Unaweza kuonyesha jinsi gani kwamba unathamini “zawadi katika wanadamu”?

19 Ungefanya nini ikiwa ungepokea zawadi ambayo imetayarishwa hasa kwa ajili yako? Je, ungeonyesha kwamba unaithamini kwa kuitumia? Yehova kupitia Yesu Kristo amekupa wewe “zawadi katika wanadamu.” Njia moja unayoweza kuonyesha kwamba unathamini zawadi hizo ni kusikiliza kwa makini hotuba zinazotolewa na wazee na kujitahidi kufuata mambo wanayosema. Unaweza pia kuonyesha kwamba unathamini zawadi hizo kwa kutoa maelezo yenye kujenga katika mikutano. Unga mkono kazi ambayo wazee wanaongoza, kama vile kazi ya kuhubiri. Ikiwa umefaidika na mashauri ambayo umepokea kutoka kwa mzee fulani, kwa nini usimwambie hivyo? Zaidi ya hayo, kwa nini usionyeshe kwamba unathamini familia za wazee? Kumbuka kwamba ili mzee afanye kazi kwa bidii katika kutaniko, familia yake inajinyima wakati wa kuwa pamoja naye.

20 Ndiyo, tuna sababu nyingi za kuonyesha kwamba tunawathamini wazee ambao wanafanya kazi kwa bidii kati yetu, wanaotusimamia, na wanaotuonya. ‘Zawadi hizo katika wanadamu’ kwa kweli ni uandalizi wenye upendo kutoka kwa Yehova!

Je, Unakumbuka?

• Wakristo wa huko Thesalonike walikuwa na sababu gani za kuwathamini wale wanaoongoza kati yao?

• Wazee wa kutaniko lenu wanafanya kazi kwa bidii jinsi gani kwa ajili yenu?

• Unafaidika jinsi gani kutokana na wazee wanaokusimamia?

• Unapaswa kukumbuka nini unapoonywa na mzee?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 27]

Je, unathamini jinsi wazee wanavyolichunga kutaniko katika njia mbalimbali?