Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Umeingia Katika Pumziko la Mungu?

Je, Umeingia Katika Pumziko la Mungu?

Je, Umeingia Katika Pumziko la Mungu?

“Neno la Mungu liko hai nalo lina nguvu.”—EBR. 4:12.

1. Tunaingia jinsi gani katika pumziko la Mungu leo, lakini kwa nini inaweza kuwa vigumu kutii?

KATIKA habari iliyotangulia, tuliona kwamba tunaweza kuingia katika pumziko la Mungu kwa kumtii na kufanya kazi pamoja na tengenezo lake ili kutimiza makusudi yake. Lakini nyakati fulani inaweza kuwa vigumu kutii. Kwa mfano, tunapojifunza kwamba Yehova anachukizwa na jambo fulani ambalo sisi tunapenda sana, huenda isiwe rahisi kutii haraka. Hilo linaonyesha kwamba tunahitaji kujifunza kuwa “tayari kutii.” (Yak. 3:17) Katika habari hii, tutachunguza hali fulani ambazo zinaweza kutujaribu na kuonyesha ikiwa tuko tayari kutii kutoka moyoni ili kutenda kulingana na kusudi la Mungu.

2, 3. Tunapaswa kufanya nini ili kuendelea kuwa wenye kutamanika machoni pa Yehova?

2 Je, uko tayari kutii unapojifunza katika Biblia kwamba unahitaji kufanya mabadiliko fulani katika maisha yako? Maandiko yanatuambia kwamba Mungu anataka kujikusanyia “vitu vyenye kutamanika vya mataifa yote.” (Hag. 2:7) Bila shaka, kabla ya kujifunza kweli za Biblia wengi wetu hatukuwa wenye kutamanika. Hata hivyo, kumpenda Mungu na Mwana wake mpendwa kulitulazimisha kufanya mabadiliko makubwa katika mtazamo na tabia zetu ili tuweze kumpendeza Mungu kikamili. Mwishowe, baada ya kusali sana na kujitahidi, siku yenye baraka ilifika na tulijitoa kwa ajili ya ubatizo wa Kikristo.—Soma Wakolosai 1:9, 10.

3 Hata hivyo, kupambana na hali yetu ya kutokamilika hakukumalizika baada ya ubatizo wetu. Mapambano yaliendelea na yataendelea kwa sababu bado sisi si wakamilifu. Lakini tunahakikishiwa kwamba tukiendelea kufanya bidii na kuazimia kuwa wenye kutamanika zaidi machoni pa Yehova Mungu, atabariki jitihada zetu.

Tunapohitaji Mashauri

4. Yehova anatumia njia gani tatu ili kutuonyesha kwamba tunahitaji kufanya mabadiliko?

4 Kabla ya kuanza kufanya mabadiliko katika maisha yetu, tunapaswa kujua ni mabadiliko gani ambayo tunahitaji kufanya. Yehova anatusaidia kufanya mabadiliko hayo katika njia tofauti-tofauti. Anaweza kutumia hotuba kwenye Jumba la Ufalme au habari fulani katika magazeti yetu ili kutuonyesha kwamba kuna jambo fulani lenye makosa katika matendo na kufikiri kwetu. Nyakati nyingine hatuelewi kwamba tunahitaji kufanya mabadiliko hata baada ya kusikia hotuba fulani au kusoma kitabu fulani, hivyo Yehova anaweza kumtumia ndugu au dada fulani katika kutaniko ili kuturekebisha kwa fadhili.—Soma Wagalatia 6:1.

5. Nyakati nyingine tunatenda jinsi gani mtu fulani anapoturekebisha, na kwa nini wachungaji Wakristo wanapaswa kuendelea katika jitihada zao za kutusaidia?

5 Si jambo rahisi kukubali shauri kutoka kwa mwanadamu mwenzetu asiye mkamilifu, hata shauri hilo likitolewa kwa busara na kwa njia ya upendo kadiri gani. Hata hivyo, kama andiko la Wagalatia 6:1 linavyoonyesha, Yehova anawaamuru wale walio na sifa za kustahili za kiroho ‘wajaribu’ kuturekebisha, wakifanya hivyo “katika roho ya upole.” Tukikubali msaada wao, tutakuwa wenye kutamanika hata zaidi machoni pa Mungu. Bila shaka, katika sala zetu, mara nyingi tunakubali kwamba sisi si wakamilifu. Hata hivyo, mtu fulani anapotuonyesha udhaifu wetu, mwelekeo wetu ni kujaribu kujitetea, kupunguza uzito wa tatizo hilo, kutilia shaka nia ya mtu anayetushauri, au kunung’unika juu ya namna shauri hilo lilivyotolewa. (2 Fal. 5:11) Na ikiwa shauri hilo linagusa jambo fulani ambalo hatupendi watu wazungumzie, kama vile matendo ya mshiriki fulani wa familia yetu, jinsi tunavyovaa na kujipamba, usafi wetu, au aina fulani ya vitumbuizo ambavyo tunapenda lakini vinamchukiza Yehova, tunaweza kukasirika na kumhuzunisha yule anayejaribu kutusaidia! Lakini baada ya kutulia, kwa kawaida tunakubali kwamba shauri hilo lilifaa.

6. Neno la Mungu linafunua jinsi gani “fikira na makusudio ya moyo”?

6 Andiko la msingi la habari hii linatukumbusha kwamba neno la Mungu “lina nguvu.” Ndiyo, neno la Mungu lina nguvu za kubadili maisha. Biblia ilitusaidia kufanya mabadiliko tuliyohitaji kufanya kabla ya kubatizwa. Katika barua yake kwa Waebrania, Paulo pia anaandika kwamba neno la Mungu “huchoma hata kufikia kugawanya nafsi na roho, na viungo na urojorojo wake, nalo linaweza kutambua fikira na makusudio ya moyo.” (Ebr. 4:12) Kwa maneno mengine, tunapoelewa vizuri kusudi la Mungu kwa ajili yetu, namna tunavyoitikia kusudi hilo kunaonyesha jinsi tulivyo kwa ndani kabisa. Je, nyakati nyingine kuna tofauti kati ya jinsi tunavyoonekana kwa nje (“nafsi”) na jinsi tulivyo kikweli kwa ndani (“roho”)? (Soma Mathayo 23:27, 28.) Chunguza jinsi ambavyo ungetenda katika hali zinazofuata.

Endelea Kusonga Mbele Pamoja na Tengenezo la Yehova

7, 8. (a) Huenda Wakristo fulani Waebrania walichochewa na nini kuendelea kufuata mazoea fulani ya Sheria ya Musa? (b) Kwa nini tunaweza kusema kwamba walikuwa wakitenda kinyume na kusudi la Yehova?

7 Wengi wetu tunajua vizuri maneno ya andiko la Methali 4:18: “Njia ya waadilifu ni kama nuru inayong’aa, inayozidi kuongezeka mpaka mchana mkamilifu.” Hilo linamaanisha kwamba mwenendo wetu na uelewaji wetu wa kusudi la Mungu utakuwa mzuri zaidi kadiri siku zinavyopita.

8 Kama tulivyozungumzia katika habari iliyotangulia, baada ya kifo cha Yesu ilikuwa vigumu kwa Wakristo wengi Wayahudi kuacha kufuata Sheria ya Musa. (Mdo. 21:20) Ingawa Paulo alieleza kwa ustadi kwamba Wakristo hawakuwa tena chini ya Sheria, wengine walikataa wazo hilo la Paulo lililoongozwa na roho ya Mungu. (Kol. 2:13-15) Labda walihisi kwamba ikiwa wangeendelea kufuata sehemu fulani za Sheria, wangeepuka kuteswa. Kwa vyovyote vile, Paulo aliwaandikia Wakristo Waebrania na kuwaeleza waziwazi kwamba hawangeingia katika pumziko la Mungu kama wangeendelea kukataa kufanya kazi kupatana na kusudi la Mungu linalofunuliwa hatua kwa hatua. * (Ebr. 4:1, 2, 6; soma Waebrania 4:11.) Ili wakubaliwe na Yehova, wangelazimika kutambua ukweli wa kwamba alikuwa akiongoza watu wake katika njia tofauti.

9. Tunapaswa kuwa na mtazamo gani wakati marekebisho yanapofanywa kuhusu uelewaji wetu wa Maandiko?

9 Katika nyakati zetu, kumekuwa na marekebisho katika uelewaji wetu wa mafundisho fulani ya Biblia. Jambo hilo halipaswi kutuvuruga; badala yake linapaswa kutuchochea kuitumaini zaidi jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara. Wakati washiriki wanaowakilisha “mtumwa” wanapotambua kwamba maoni yetu kuhusu kweli fulani za Biblia yanahitaji kufafanuliwa au kurekebishwa, hawasiti kufanya marekebisho. Washiriki wa jamii ya mtumwa wanataka sana kutenda kupatana na kusudi la Mungu linalofunuliwa hatua kwa hatua na hawaogopi kuchambuliwa kwa sababu ya kurekebisha mafundisho fulani. Wewe unaitikia jinsi gani wakati marekebisho yanapofanywa kuhusu uelewaji wetu wa Maandiko?—Soma Luka 5:39.

10, 11. Ni mambo gani tunayoweza kujifunza kutokana na jinsi watu fulani walivyotenda wakati njia mpya za kuhubiri habari njema zilipoanzishwa?

10 Acheni tuzungumzie mfano mwingine. Karibu miaka mia moja hivi iliyopita, Wanafunzi fulani wa Biblia ambao walitoa hotuba nzuri sana walifikiri kwamba kutoa hotuba ilikuwa njia bora zaidi ya kuhubiri. Walipenda sana kutoa hotuba mbele ya watu wengi, na wengine wao walifurahia sana kusifiwa na wasikilizaji wao. Lakini baadaye, watu wa Yehova walielewa wazi zaidi kwamba Yehova alitaka watu wake wafanye mengi zaidi ya kutoa tu hotuba za watu wote. Aliwataka wahubiri nyumba kwa nyumba na kuhubiri kwa njia nyingine mbalimbali. Wengine kati ya wasemaji hao wazuri hawakutaka kufanya hivyo. Kwa nje, walionekana kuwa wanaume wa kiroho ambao walijitoa kabisa kwa Bwana. Hata hivyo, walipoonyeshwa wazi kusudi la Mungu kuhusu kazi ya kuhubiri, mawazo yao, nia yao, na makusudi yao ya ndani kabisa yalionekana wazi. Yehova alihisi namna gani kuwahusu? Hakuwabariki. Waliacha tengenezo.—Mt. 10:1-6; Mdo. 5:42; 20:20.

11 Ilikuwa pia vigumu kwa wanafunzi wengi wa Biblia waliobaki washikamanifu kwa tengenezo kuhubiri nyumba kwa nyumba, hasa mwanzoni. Lakini walitii. Baada ya muda, ilikuwa rahisi kwao kuhubiri nyumba kwa nyumba, na Yehova aliwabariki sana. Wewe unafanya nini unapoombwa ushiriki katika njia fulani ya kuhubiri ambayo haikupendezi? Je, uko tayari kujaribu njia hiyo mpya ya kuhubiri?

Mtu Tunayempenda Anapomwacha Yehova

12, 13. (a) Ni nini kusudi la Yehova la kuamuru wakosaji wasiotubu watengwe na ushirika? (b) Ni jaribu gani ambalo wazazi fulani Wakristo wanakabili, na ni nini kinachofanya jaribu hilo liwe gumu?

12 Bila shaka sote tunakubaliana na kanuni ya kwamba ni lazima tuwe safi kimwili, kiadili, na kiroho ili kumpendeza Mungu. (Soma Tito 2:14.) Hata hivyo, nyakati fulani ushikamanifu wetu kwa sehemu hiyo ya kusudi la Mungu unaweza kujaribiwa kabisa. Kwa mfano, tuseme kwamba mwana pekee wa wenzi wa ndoa Wakristo ambao ni mfano mzuri anaacha kweli. Kwa kuwa anapendelea zaidi “kufurahia dhambi kwa muda” kuliko uhusiano wake pamoja na Yehova na pamoja na wazazi wake wanaomwogopa Mungu, kijana huyo anatengwa na ushirika.—Ebr. 11:25.

13 Wazazi wanavunjika moyo kabisa! Bila shaka, kuhusu kutengwa na ushirika, wanajua kwamba Biblia inasema “mwache kuchangamana katika ushirika pamoja na mtu yeyote anayeitwa ndugu ambaye ni mwasherati au mtu mwenye pupa au mwabudu-sanamu au mtukanaji au mlevi au mnyang’anyi, hata msile chakula pamoja na mtu wa namna hiyo.” (1 Kor. 5:11, 13) Wanatambua pia kwamba maneno “mtu yeyote” katika mstari huo yanatia ndani washiriki wa familia ambao hawaishi nyumbani. Lakini wazazi hao wanampenda sana mwana wao! Hisia zenye nguvu zinaweza kufanya wafikiri hivi: ‘Tunaweza kumsaidia kijana wetu jinsi gani amrudie Yehova tukikatisha kabisa uhusiano wetu pamoja naye? Je, hatuwezi kumsaidia zaidi kwa kuendelea kushirikiana naye kwa ukawaida?’ *

14, 15. Wazazi wa watoto waliotengwa na ushirika wanapaswa kufanya uamuzi gani hasa?

14 Tunahuzunika pamoja na wazazi hao. Hata hivyo, mwana wao alipaswa kufanya uamuzi, na aliamua kufuatia mwenendo usio wa Kikristo badala ya kuendelea kufurahia kushirikiana kwa ukaribu pamoja na wazazi wake na waamini wenzake. Kwa upande mwingine, wazazi wake hawangeweza kumwamulia jambo la kufanya. Haishangazi kwamba wanaumia sana moyoni!

15 Lakini wazazi hao wapendwa watafanya nini? Je, watatii mwongozo wa Yehova ulio wazi? Au je, watapunguza uzito wa mwongozo huo kwa kufikiri kwamba wanaweza kuendelea kushirikiana kwa ukawaida na mwana wao aliyetengwa na ushirika na kusema kwamba hayo ni “mambo ya lazima ya familia”? Wanapofanya uamuzi wao, hawapaswi kamwe kusahau jinsi Yehova anavyohisi kuhusu yale wanayofanya. Kusudi lake ni kwamba tengenezo liendelee kuwa safi na, ikiwezekana, kuwachochea wakosaji kurudiwa na fahamu zao. Wazazi Wakristo wanaweza jinsi gani kuunga mkono kusudi hilo?

16, 17. Tunaweza kujifunza nini kwa kutafakari juu ya mfano wa Haruni?

16 Haruni, ndugu ya Musa, alikuwa katika hali ngumu kwa sababu ya mambo ambayo wawili kati ya watoto wake wa kiume walifanya. Fikiria jinsi ambavyo huenda alihisi vijana wake wawili Nadabu na Abihu walipotoa moto haramu mbele za Yehova naye Akawaua mara moja. Bila shaka, wanaume hao walipokufa uhusiano wowote ambao wangekuwa nao pamoja na wazazi wao ulikoma. Lakini kulikuwa na jambo lingine zaidi ya hilo. Yehova alimwamuru hivi Haruni na watoto wake wa kiume waaminifu: “Msiache vichwa vyenu vikose kuwa nadhifu, wala msiyararue mavazi yenu [kwa kuomboleza], msije mkafa wala [Yehova] asije akalikasirikia kusanyiko lote.” (Law. 10:1-6) Ujumbe uko wazi. Ni lazima upendo wetu kwa Yehova uwe wenye nguvu zaidi kuliko upendo wetu kwa washiriki wa familia ambao si waaminifu.

17 Leo, Yehova hawaangamizi papo hapo wale wanaovunja sheria zake. Kwa upendo, anawapa nafasi ya kutubu kutokana na matendo yao yasiyo ya uadilifu. Hata hivyo, Yehova atahisi namna gani ikiwa wazazi wa mkosaji asiyetubu wanaendelea kumjaribu Yehova kwa kushirikiana isivyo lazima na mwana au binti yao aliyetengwa na ushirika?

18, 19. Ni baraka gani ambazo washiriki wa familia wanaweza kupata kwa kufuata maagizo ya Yehova kuhusu watu waliotengwa na ushirika?

18 Watu wengi ambao wakati fulani walikuwa wametengwa na ushirika, sasa wanakubali waziwazi kwamba msimamo imara wa marafiki wao na washiriki wa familia zao uliwasaidia kurudiwa na fahamu. Kwa mfano, mwanamke mmoja aliwaambia wazee wakati wa kurudishwa kwake kwamba jambo moja lililomsaidia kubadili njia yake ya maisha “ni jinsi ndugu yake wa kimwili alivyotenda kwa kuheshimu mpango wa kutenga na ushirika.” Mwanamke huyo alisema kwamba “kilichomsaidia kutaka kurudi ni kwamba ndugu yake alishikamana kwa uaminifu na miongozo ya Kimaandiko.”

19 Basi, tunahitaji kufanya nini? Tunahitaji kupambana na mwelekeo wa mioyo yetu isiyo mikamilifu wa kuasi mashauri ya Kimaandiko. Tunapaswa kusadiki kabisa kwamba njia ya Mungu ya kushughulikia matatizo yetu sikuzote ni bora kabisa kwetu.

“Neno la Mungu Liko Hai”

20. Tunaweza kuelewa andiko la Waebrania 4:12 katika njia gani mbili? (Ona maelezo ya chini.)

20 Paulo alipoandika kwamba “neno la Mungu liko hai,” hakuwa akizungumzia hasa Neno la Mungu lililoandikwa, yaani, Biblia. * Mistari mingine katika sura hiyo inaonyesha kwamba alikuwa akizungumza kuhusu ahadi za Mungu. Paulo alikuwa akisema kwamba sikuzote Mungu anatimiza ahadi zake. Yehova alionyesha ukweli wa jambo hilo kupitia nabii Isaya kwa kusema: “Neno langu . . . halitarudi kwangu bila matokeo, bali . . . litafanikiwa katika yale ambayo nimelituma.” (Isa. 55:11) Hivyo, tunahitaji kuwa wenye subira ikiwa mambo hayafanyiki haraka kama tunavyotazamia. Tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova ‘anaendelea kufanya kazi’ ili kutimiza kabisa kwa mafanikio kusudi lake.—Yoh. 5:17.

21. Andiko la Waebrania 4:12 linaweza jinsi gani kuwatia moyo washiriki waaminifu waliozeeka wa “umati mkubwa”?

21 Washiriki waaminifu waliozeeka wa “umati mkubwa” wamemtumikia Yehova kwa makumi ya miaka. (Ufu. 7:9) Wengi wao hawakutazamia kwamba wangezeeka katika mfumo huu wa mambo. Hata hivyo, hawavunjiki moyo. (Zab. 92:14) Wanajua kwamba ahadi za Mungu ni za kweli, ziko hai, na Yehova anafanya kazi ili kuzitimiza. Kwa kuwa Mungu anathamini kutoka moyoni kusudi lake, tunamfanya ashangilie tunapoonyesha kwamba kusudi hilo ni la maana kwetu pia. Katika siku hii ya saba ya pumziko, hakuna jambo ambalo litamzuia Yehova kukamilisha kusudi lake. Na anajua kwamba watu wake, wakiwa kikundi, wataendelea kutenda kupatana na kusudi lake. Namna gani wewe? Je, wewe binafsi umeingia katika pumziko la Mungu?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Viongozi wengi kati ya Wayahudi walifuata kwa uangalifu sana Sheria ya Musa, lakini Masihi alipofika, walishindwa kumtambua. Hawakutenda kulingana na kusudi la Mungu lenye kuendelea.

^ fu. 20 Leo, Mungu anazungumza nasi kupitia Neno lake lililoandikwa, Biblia, ambalo lina nguvu ya kubadili maisha yetu. Kwa hiyo, yale tunayosoma katika Waebrania 4:12 ni kweli pia kuhusu Biblia.

Usikose Lile Kusudi

• Tunahitaji kufanya nini ili tuingie katika pumziko la Mungu leo?

• Kuna uhusiano gani kati ya kusudi la Mungu na sisi kuwa tayari kukubali mashauri ya Kimaandiko?

• Ni katika hali gani inaweza kuwa vigumu kutii mwongozo wa Kimaandiko, lakini kwa nini ni jambo la maana sana kwetu kutii?

• Tunaweza kuelewa andiko la Waebrania 4:12 katika njia gani mbili?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 31]

Wazazi wanavunjika moyo kabisa!