Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Niliogopa Kifo—Sasa Ninangoja ‘Uzima kwa Wingi’

Niliogopa Kifo—Sasa Ninangoja ‘Uzima kwa Wingi’

Niliogopa Kifo—Sasa Ninangoja ‘Uzima kwa Wingi’

Limesimuliwa na Piero Gatti

SAUTI ya chini yenye kuvuma ilizidi kuongezeka hatua kwa hatua. Ilifuatwa na milio ya ving’ora vya kuwaonya watu wajifiche. Kisha kukawa na milipuko ya mabomu na uharibifu na mngurumo mkubwa sana ukasikika.

Hivyo ndivyo mambo yalivyokuwa huko Milan, Italia, mwaka wa 1943/1944. Nikiwa kijana mwanajeshi, nilifanya kazi katika mji huo, mara nyingi niliamrishwa niokote mabaki ya miili ya wanadamu yaliyozikwa katika vyumba vya kujificha kutokana na mabomu ambavyo vilikuwa vimelipuliwa, na watu walikuwa wamekwama ndani, huku miili yao ikiwa imepasuliwa vipande-vipande na haingeweza kutambulika. Na zaidi ya kuona watu wengine wakifa kando yangu, nyakati nyingine, mimi mwenyewe nilikaribia sana kufa. Katika pindi hizo nilisali, na kumwahidi Mungu kwamba ikiwa ningeokoka mauaji hayo, ningefanya mapenzi yake.

Niliacha Kuogopa Kifo

Nililelewa katika kijiji fulani kilicho umbali wa kilomita 10 hivi kutoka Como, Italia, karibu na mpaka wa Uswisi. Nikiwa na umri mdogo, nilikabiliana moja kwa moja na huzuni na kuogopa kifo. Homa ya Hispania iliua dada zangu wawili. Kisha mwaka wa 1930, nikiwa na umri wa miaka sita tu, mama yangu, Luigia, alikufa. Kwa kuwa nililelewa nikiwa Mkatoliki, nilifuata sheria za kidini na kuhudhuria Misa kila juma. Lakini miaka mingi baadaye nikiwa kwa kinyozi, si katika kanisa, ndipo nilipoacha kuogopa kifo.

Katika mwaka wa 1944, watu wengi sana walikuwa wakifa katika Vita vya Pili vya Ulimwengu. Nilikuwa mmoja kati ya makumi ya maelfu ya wanajeshi wa Italia ambao walikuwa wamekimbia kutoka katika eneo la vita na kwenda Uswisi, nchi ambayo haikuunga mkono upande wowote. Tulipofika tulipelekwa katika kambi mbalimbali za wakimbizi. Nilipelekwa katika kambi moja karibu na Steinach, kaskazini-mashariki mwa nchi hiyo. Tukiwa huko tulipewa uhuru wa kadiri fulani. Kinyozi wa huko Steinach alihitaji mtu wa kumsaidia kwa muda mahali pake pa kazi. Niliishi na kufanya kazi naye kwa mwezi mmoja tu, lakini muda huo ulitosha kunisaidia kukutana na mtu ambaye alibadili maisha yangu.

Mmoja wa watu waliokuwa wakija kunyolewa hapo ni Adolfo Tellini, Mwitaliano ambaye alikuwa akiishi huko Uswisi. Alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Sikuwa nimewahi kamwe kusikia kuhusu kikundi hicho, na hilo halikuwa jambo la kushangaza kwa kuwa wakati huo kulikuwa na Mashahidi wasiozidi 150 katika nchi yote ya Italia. Adolfo aliniambia kuhusu kweli nzuri ajabu za Biblia, na ahadi kuhusu amani na ‘uzima kwa wingi.’ (Yoh. 10:10; Ufu. 21:3, 4) Nilisisimuka sana nilipopata ujumbe kuhusu wakati ujao usio na vita na kifo. Niliporudi kwenye kambi ya wakimbizi, nilizungumza kuhusu tumaini hilo pamoja na kijana fulani kutoka Italia, Giuseppe Tubini, na yeye pia akapendezwa. Adolfo na Mashahidi wengine walikuwa wakitutembelea mara kwa mara katika kambi.

Adolfo alinipeleka Arbon, karibu kilomita 10 kutoka Steinach, ambako kikundi kidogo cha Mashahidi kilikuwa kikifanya mikutano katika Kiitaliano. Nilichangamka sana kwa sababu ya mambo niliyosikia hivi kwamba juma lililofuata nilitembea mpaka huko. Baadaye, nilihudhuria kusanyiko la Mashahidi katika jumba la kusanyiko huko Zurich. Niliguswa moyo sana hasa na picha za slaidi za kambi za mauaji, zilizoonyesha marundo ya maiti za watu. Nilikuja kujua kwamba Mashahidi wengi Wajerumani walikuwa wameuawa kwa sababu ya imani yao. Katika kusanyiko hilo nilikutana na Maria Pizzato. Kwa sababu ya utendaji wake mbalimbali akiwa Shahidi, alikuwa amefungwa gerezani kwa miaka 11 na serikali ya Kifashisti ya Italia.

Vita vilipokwisha, nilirudi Italia na kujiunga na kutaniko dogo lililokuwa huko Como. Sikuwa nimejifunza vizuri Biblia, lakini nilijua waziwazi kweli za msingi. Maria Pizzato alikuwa pia katika kutaniko hilo. Alinieleza kwamba Wakristo wanapaswa kubatizwa na akaniomba nimtembelee Marcello Martinelli, ambaye alikuwa akiishi huko Castione Andevenno, katika jimbo la Sondrio. Marcello alikuwa ndugu mtiwa-mafuta mwaminifu ambaye alikuwa amefungwa gerezani kwa miaka 11 na utawala wa kidikteta. Niliendesha baiskeli kilomita 80 ili kumtembelea.

Marcello alitumia Biblia kunieleza kuhusu matakwa ya kubatizwa, baada ya hapo tukasali na kwenda kwenye mto Adda, ambako nilibatizwa. Ilikuwa Septemba mwaka wa 1946. Ilikuwa siku ya pekee sana. Nilikuwa nimesisimuka sana kuhusu uamuzi wangu wa kumtumikia Yehova na sasa nilikuwa na tumaini la wakati ujao lenye nguvu hivi kwamba jioni ilipofika, hata sikutambua kwamba nilikuwa nimeendesha baiskeli umbali wa kilomita 160 siku hiyo!

Mei 1947, baada ya vita, kusanyiko la kwanza nchini Italia lilifanyiwa huko Milan. Karibu watu 700 walihudhuria, kutia ndani wengi ambao walikuwa wameishi wakati wa mateso ya Wafashisti. Jambo fulani ambalo si la kawaida lilitukia katika kusanyiko hilo. Giuseppe Tubini, ambaye nilikuwa nimemhubiria katika kambi ya wakimbizi, alitoa hotuba ya ubatizo na akabatizwa baada ya kutoa hotuba hiyo!

Katika kusanyiko hilo, nilipata pendeleo la kukutana na Ndugu Nathan Knorr, kutoka Betheli ya Brooklyn. Alinitia moyo mimi na Giuseppe tutumie maisha yetu katika utumishi wa Mungu. Niliamua kwamba ningeanza utumishi wa wakati wote baada ya mwezi mmoja. Nilipofika nyumbani, niliiambia familia yangu kuhusu uamuzi wangu, na wote walijaribu kunishawishi nibadili uamuzi huo. Lakini nilikuwa nimeazimia. Hivyo, mwezi mmoja baadaye nikaanza utumishi wangu katika Betheli huko Milan. Kulikuwa na wamishonari wanne katika Betheli hiyo: Giuseppe (Joseph) Romano na mke wake, Angelina; Carlo Benanti na mke wake, Costanza. Mshiriki wa tano wa familia hiyo alikuwa Giuseppe Tubini, ambaye alikuwa tu amejiunga nao, na mimi nilikuwa mtu wa sita.

Baada ya kukaa Betheli kwa mwezi mmoja, niliwekwa rasmi kuwa mwangalizi wa mzunguko, mwangalizi wa kwanza Mwitaliano aliyezaliwa katika nchi hiyo. Ndugu George Fredianelli, mmishonari wa kwanza ambaye alikuja Italia kutoka Marekani mwaka wa 1946, tayari alikuwa akifanya kazi ya kusafiri. Alinizoeza kwa majuma machache, kisha nikaanza kufanya kazi hiyo nikiwa peke yangu. Ninakumbuka hasa kutaniko la kwanza ambalo nilitembelea, Faenza. Hebu fikiria jambo hili! Kufikia wakati huo, sikuwa nimewahi kamwe kutoa hotuba katika kutaniko lolote! Hata hivyo, niliwatia moyo wale waliohudhuria, kutia ndani vijana wengi, wafikirie kuingia katika huduma ya wakati wote. Baadaye, vijana fulani kati ya hao walipokea migawo ya kushughulikia madaraka makubwa katika eneo la Kiitaliano.

Nilikuwa nimeanza maisha yenye kusisimua nikiwa mwangalizi anayesafiri. Yalikuwa maisha yenye mambo mengi ya kusisimua, matatizo, na shangwe, na wakati huo ndugu na dada wapendwa walinionyesha upendo mkubwa.

Hali ya Kidini Nchini Italia Baada ya Vita

Acheni niwaambie jambo fulani kuhusu hali ya kidini nchini Italia wakati huo. Kanisa Katoliki lilikuwa na ushawishi mkubwa usiopingwa na yeyote. Ingawa katiba mpya ilianza kutumika mwaka wa 1948, sheria za Wafashisti zilizowazuia Mashahidi kuhubiri kwa uhuru ziliondolewa mwaka wa 1956. Mara nyingi makusanyiko ya mzunguko yalivurugwa kwa sababu ya uchochezi wa makasisi. Lakini nyakati nyingine jitihada za makasisi zilishindwa kabisa, na ndivyo ilivyotukia mwaka wa 1948 huko Sulmona, mji mdogo ulio katikati ya Italia.

Kusanyiko hilo lilikuwa likifanywa katika jumba la sinema. Jumapili (Siku ya Yenga) asubuhi, nilikuwa mwenyekiti, na Giuseppe Romano ndiye aliyetoa hotuba ya watu wote. Siku hizo watu wengi sana walihudhuria. Wakati ambapo hata hakukuwa na wahubiri 500 katika nchi yote, watu 2,000 walijaa katika jumba hilo. Baada ya hotuba, kijana mmoja ambaye alikuwa amezoezwa na makasisi wawili ambao walikuwa katika umati, alipanda jukwaani. Akiwa na lengo la kuleta mvurugo, alianza kupiga mayowe kwa sauti ya juu kabisa. Mara moja nikamwambia hivi: “Ikiwa una jambo la kusema, kodi jumba, kisha useme jambo unalotaka kusema.” Umati haukupendezwa na jambo alilofanya na wakapaaza sauti na kumkemea. Hapo ndipo kijana huyo aliporuka kutoka jukwaani na kutoweka.

Kusafiri kulikuwa jambo gumu sana siku hizo. Nyakati nyingine nilitembea kutoka kutaniko moja mpaka lingine, au niliendesha baiskeli yangu, au nilisafiri kwa mabasi yaliyozeeka ambayo yalikuwa yamejaa watu, au kwa garimoshi. Nyakati nyingine nililala katika chumba cha kulishia wanyama au chumba cha vifaa vya kazi. Vita vilikuwa vimetoka tu kumalizika na Waitaliano wengi walikuwa maskini. Kulikuwa na ndugu wachache na waliishi maisha ya hali ya chini. Hata hivyo, maisha ya kumtumikia Yehova yalikuwa mazuri ajabu.

Kuzoezwa Katika Shule ya Gileadi

Mwaka wa 1950, mimi na Giuseppe Tubini, tulialikwa kuhudhuria darasa la 16 la shule ya wamishonari ya Gileadi. Tangu mwanzoni nilijua kwamba ingekuwa vigumu kwangu kujifunza Kiingereza. Nilijikaza kabisa lakini ilikuwa vigumu sana. Tulipaswa kusoma Biblia nzima katika Kiingereza. Ili nitimize jambo hilo, nyakati nyingine sikula chakula cha mchana ili nijizoeze kusoma kwa sauti. Mwishowe, wakati wangu wa kutoa hotuba ulifika. Ninakumbuka vizuri sana maelezo ambayo mwalimu alitoa, “Ishara zako za mwili na shauku ni bora kabisa, lakini Kiingereza chako hakieleweki hata kidogo!” Hata hivyo, nilifanikiwa kumaliza mazoezi hayo. Baada ya hapo mimi na Giuseppe tulipewa mgawo wa kurudi Italia. Baada ya kuzoezwa zaidi, tungeweza sasa kuwatumikia akina ndugu kwa njia nzuri zaidi.

Mwaka wa 1955, nilimwoa Lidia, ambaye nilikuwa nimetoa hotuba yake ya ubatizo miaka saba iliyopita. Baba yake, Domenico, alikuwa ndugu mpendwa ambaye alikuwa amefanikiwa kuwasaidia watoto wake wote saba kukubali kweli, hata ingawa alikuwa ameteswa na serikali ya Wafashisti na kupelekwa uhamishoni kwa miaka mitatu. Lidia pia alipigana kabisa kwa ajili ya kweli. Alishtakiwa mara tatu mahakamani kabla ya haki yetu ya kisheria ya kuhubiri nyumba kwa nyumba kukubaliwa. Miaka sita baada ya kufunga ndoa, mwana wetu wa kwanza, Beniamino, alizaliwa. Mwaka wa 1972, tulipata mwana mwingine, Marco. Ninafurahi kwamba wote wawili na pia familia zao wanamtumikia Yehova kwa bidii.

Kuendelea Kuwa na Bidii Katika Utumishi wa Yehova

Katika maisha yangu yenye furaha ya kuwatumikia wengine, nimejionea mambo mengi mazuri ambayo bado ninayakumbuka. Kwa mfano, mwanzoni mwa miaka ya 1980, baba-mkwe wangu alimwandikia barua Sandro Pertini, ambaye alikuwa rais wa Italia wakati huo. Wakati wa utawala wa kidikteta wa Wafashisti, wote wawili walikuwa wamepelekwa uhamishoni kwenye kisiwa cha Ventotene, ambako watu walioonwa kuwa maadui wa serikali walifungwa. Baba-mkwe wangu aliomba kumhoji rais akiwa na nia ya kumhubiria. Ombi lake lilipokubaliwa, nilienda pamoja naye, na tulikaribishwa kwa uchangamfu, jambo ambalo hatukuwa tumezoea. Rais alimsalimu baba-mkwe wangu kwa shauku kwa kumkumbatia. Kisha tukazungumza kuhusu imani yetu na tukampa vitabu fulani.

Mwaka wa 1991, baada ya kutumika nikiwa mwangalizi anayesafiri kwa miaka 44, niliacha kazi ya kuzunguka, baada ya kutembelea makutaniko kotekote nchini Italia. Kwa miaka minne iliyofuata, nilitumika nikiwa mwangalizi wa Jumba la Kusanyiko mpaka nilipolazimika kupunguza utendaji wangu kwa sababu ya ugonjwa hatari. Hata hivyo, kwa sababu ya fadhili zisizostahiliwa za Yehova, bado niko katika utumishi wa wakati wote. Ninajitahidi kabisa kuhubiri na kufundisha habari njema, na sasa ninaongoza mafunzo fulani ya Biblia. Bado ndugu wanasema kwamba ninatoa hotuba kwa shauku “nyingi sana.” Ninamshukuru Yehova kwamba ingawa nimezeeka, nguvu zangu hazijapungua.

Nilipokuwa kijana niliogopa sana kifo, lakini baada ya kupata ujuzi sahihi wa Biblia nimekuwa na tumaini hakika la kupata uzima wa milele ambao Yesu aliuita ‘uzima kwa wingi.’ (Yoh. 10:10) Hilo ndilo jambo ambalo ninatazamia kwa sasa, maisha yaliyojaa amani, usalama, na furaha, pamoja na baraka nyingi za Yehova. Sifa zote na zimwendee Muumba wetu mwenye upendo, ambaye tuna pendeleo la kuitwa kwa jina lake.—Zab. 83:18.

[Ramani katika ukurasa wa 22, 23]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

USWISI

BERN

Zurich

Arbon

Steinach

ITALIA

ROME

Como

Milan

Mto Adda

Castione Andevenno

Faenza

Sulmona

Ventotene

[Picha katika ukurasa wa 22]

Tukiwa safarini kwenda Gileadi

[Picha katika ukurasa wa 22]

Nikiwa pamoja na Giuseppe katika Shule ya Gileadi

[Picha katika ukurasa wa 23]

Siku yetu ya harusi

[Picha katika ukurasa wa 23]

Mke wangu mpendwa amekuwa pamoja nami kwa miaka zaidi ya 55