Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Fuatilia Amani

Fuatilia Amani

Fuatilia Amani

“Na tufuatilie mambo yanayofanya kuwe na amani.”—ROM. 14:19.

1, 2. Kwa nini Mashahidi wa Yehova wanafurahia amani kati yao?

NI VIGUMU kupata amani ya kweli katika ulimwengu wa leo. Hata watu ambao ni wa nchi moja na ambao wanazungumza lugha ileile, mara nyingi wanagawanyika kidini, kisiasa, na kijamii. Lakini watu Yehova wana umoja ingawa wametoka katika “mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha.”—Ufu. 7:9.

2 Hali ya amani ambayo kwa ujumla tunafurahia haijitokezi yenyewe tu. Tumepata hali hiyo hasa kwa sababu ‘tunafurahia amani pamoja na Mungu’ kupitia imani yetu katika Mwana wake, ambaye damu yake iliyomwagwa inafunika dhambi zetu. (Rom. 5:1; Efe. 1:7) Zaidi ya hayo, Mungu wa kweli anawapa roho takatifu watumishi wake washikamanifu, na amani ni sehemu ya tunda la roho hiyo. (Gal. 5:22) Sababu nyingine inayofanya tuwe na amani na umoja ni kwamba sisi “si sehemu ya ulimwengu.” (Yoh. 15:19) Hatuungi mkono upande wowote katika mambo ya kisiasa. Kwa kuwa ‘tumefua panga zetu kuwa majembe,’ hatushiriki vita katika nchi yetu au kati ya mataifa mbalimbali.—Isa. 2:4.

3. Amani tunayoweza kufurahia inatuwezesha kufanya nini, na nini kitakachozungumziwa katika habari hii?

3 Amani tunayoweza kufurahia kati yetu inatia ndani mengi zaidi ya kuepuka tu kuwaumiza ndugu zetu. Ingawa huenda kutaniko la Mashahidi wa Yehova ambalo tunashirikiana nalo lina watu kutoka katika makabila mengi na utamaduni mbalimbali, ‘tunapendana.’ (Yoh. 15:17) Amani yetu inatuwezesha ‘kuwatendea wote mema, na hasa wale ambao katika imani ni jamaa zetu.’ (Gal. 6:10) Tunapaswa kuthamini na kulinda paradiso yetu ya kiroho yenye amani. Hivyo basi, acheni tuchunguze jinsi tunavyoweza kufuatilia amani katika kutaniko.

Tunapojikwaa

4. Tunaweza kufanya nini ili kufuatilia amani tunapomkosea mtu fulani?

4 Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “Sisi sote hujikwaa mara nyingi. Ikiwa yeyote hajikwai katika neno, huyo ni mtu mkamilifu.” (Yak. 3:2) Hivyo, tunatazamia kwamba kutakuwa na kutoelewana na matatizo kati ya Wakristo. (Flp. 4:2, 3) Hata hivyo, matatizo kati ya watu binafsi yanaweza kutatuliwa bila kuvuruga amani ya kutaniko. Kwa mfano, fikiria shauri ambalo tunapaswa kufuata tunapotambua kwamba huenda tumemkasirisha mtu fulani.—Soma Mathayo 5:23, 24.

5. Tunaweza kufuatilia amani jinsi gani tunapokosewa?

5 Namna gani ikiwa tumekosewa kwa njia fulani ndogo? Je, tunapaswa kutazamia mtu aliyetukosea aje na kutuomba msamaha? Andiko la 1 Wakorintho 13:5 linasema hivi: “[Upendo] hauweki hesabu ya ubaya.” Tunapokosewa, tunafuatilia amani kwa kusamehe na kusahau, yaani, kwa ‘kutoweka hesabu ya ubaya.’ (Soma Wakolosai 3:13.) Hiyo ndiyo njia bora ya kutatua makosa madogo-madogo katika maisha ya kila siku, kwa sababu hilo linatusaidia kuwa na uhusiano wenye amani pamoja na waabudu wenzetu na kupata amani ya akili. Methali moja yenye hekima inasema hivi: ‘Ni jambo lenye kupendeza kupita kosa.’—Met. 19:11.

6. Tunapaswa kufanya nini ikiwa ni vigumu sana kwetu kupuuza kosa tulilotendewa?

6 Namna gani tukiona kwamba ni vigumu sana kupuuza kosa fulani? Bila shaka, si jambo la hekima kuwaeleza watu wengi iwezekanavyo kuhusu kosa hilo. Porojo kama hiyo inavuruga tu amani ya kutaniko. Tunapaswa kufanya nini ili kusuluhisha tatizo hilo kwa amani? Andiko la Mathayo 18:15 linasema hivi: “Ndugu yako akitenda dhambi, nenda ufunue kosa lake kati yako na yeye peke yake. Akikusikiliza, umempata ndugu yako.” Ingawa andiko la Mathayo 18:15-17 linahusu dhambi nzito, kwa kufuata kanuni inayotajwa kwenye mstari wa 15, tunapaswa kuzungumza kwa fadhili na mtu aliyetukosea akiwa peke yake na kujaribu kurudisha uhusiano wenye amani pamoja naye. *

7. Kwa nini tunapaswa kutatua matatizo upesi?

7 Mtume Paulo aliandika hivi: “Iweni na ghadhabu, lakini msitende dhambi; jua lisitue mkiwa katika hali ya kuchokozeka, wala msimpe Ibilisi nafasi.” (Efe. 4:26, 27) Yesu alisema: “Uwe tayari kusuluhisha mambo upesi pamoja na mtu anayekushtaki mahakamani.” (Mt. 5:25) Hivyo, ili kufuatilia amani tunapaswa kusuluhisha matatizo upesi. Kwa nini? Kwa sababu kufanya hivyo kunazuia matatizo kuwa makubwa zaidi kama vile kidonda kinavyooza kisipotibiwa. Acheni tusiruhusu kiburi, wivu, au kupenda sana pesa kutuzuie kutatua matatizo mara tu yanapotokea.—Yak. 4:1-6.

Tatizo Linapohusu Watu Wengi

8, 9. (a) Kulikuwa na maoni gani yaliyotofautiana katika kutaniko la karne ya kwanza huko Roma? (b) Ni shauri gani ambalo Paulo aliwapa Wakristo Waroma kuhusu mabishano yao?

8 Nyakati nyingine matatizo katika kutaniko yanahusisha watu wengi. Ndivyo ilivyokuwa kwa Wakristo fulani huko Roma ambao Paulo aliwaandikia barua iliyoongozwa na roho ya Mungu. Kulikuwa na mabishano kati ya Wakristo Wayahudi na Wakristo wasio Wayahudi. Inaonekana kwamba Wakristo fulani katika kutaniko hilo walikuwa wakiwadharau wale ambao walikuwa na dhamiri dhaifu, au wale ambao walikuwa na dhamiri zenye nguvu. Watu hao walikuwa wakiwahukumu wengine kuhusu mambo ya kibinafsi kabisa. Paulo alitoa mashauri gani kwa kutaniko hilo?—Rom. 14:1-6.

9 Paulo aliwashauri wote waliohusika. Aliwaambia wale ambao walielewa kwamba hawako chini ya Sheria ya Musa wasiwadharau ndugu zao. (Rom. 14:2, 10) Mtazamo kama huo ungewakwaza waamini ambao bado walichukia kula vyakula ambavyo vilikatazwa na Sheria. Paulo aliwashauri hivi: ‘Acheni kuibomoa kazi ya Mungu kwa ajili ya chakula tu. Ni vema kutokula nyama au kunywa divai au kufanya jambo lolote ambalo ndugu yako anakwazika juu yake.’ (Rom. 14:14, 15, 20, 21) Kwa upande mwingine, Paulo aliwashauri Wakristo waliokuwa na dhamiri dhaifu zaidi wasiwahukumu wale waliokuwa na maoni tofauti na yao na kuwaona kuwa wasio waaminifu. (Rom. 14:13) Aliwaambia hivi: “Kila mtu hapo kati yenu asijifikirie mwenyewe zaidi kuliko ilivyo lazima kufikiri.” (Rom. 12:3) Baada ya kuwashauri wote waliohusika katika mabishano hayo, Paulo aliandika hivi: “Hivyo, basi, na tufuatilie mambo yanayofanya kuwe na amani na mambo ambayo ni ya kujengana.”—Rom. 14:19.

10. Kama ilivyokuwa katika kutaniko la karne ya kwanza huko Roma, tunahitaji kufanya nini leo ili kutatua matatizo?

10 Tunaweza kuwa na hakika kwamba kutaniko la Roma lilifuata mashauri ya Paulo na kufanya marekebisho yaliyohitajiwa. Matatizo yanapotokea kati ya Wakristo leo, je, hatupaswi vivyo hivyo kuyatatua kwa fadhili kwa kutafuta kwa unyenyekevu mashauri ya Kimaandiko na kuyafuata? Kama ilivyokuwa huko Roma, leo wale ambao wamekosana huenda wakahitaji kufanya marekebisho ili ‘kudumisha amani kati ya mtu na mwenzake.’—Marko 9:50.

Tunapoombwa Kusaidia

11. Kwa nini mzee anapaswa kuwa mwangalifu Mkristo fulani anapotaka kuzungumza naye kuhusu tatizo kati yake na Mkristo mwenzake?

11 Namna gani ikiwa Mkristo anataka kuzungumza na mzee kuhusu tatizo kati yake na mtu wa ukoo au na mwamini mwenzake? Andiko la Methali 21:13 linasema hivi: “Yeyote anayeziba sikio lake asisikie kilio cha kulalamika cha mtu wa hali ya chini, yeye mwenyewe ataita wala hatajibiwa.” Bila shaka, mzee ‘hataziba sikio lake.’ Hata hivyo, methali nyingine inaonya hivi: “Ajiteteaye kwanza huonekana msema kweli, mpaka hapo mpinzani wake atakapoanza kumhoji.” (Met. 18:17, Biblia Habari Njema) Mzee anapaswa kusikiliza kwa fadhili, lakini anahitaji kuwa mwangalifu ili asimuunge mkono mtu anayeripoti kosa. Baada ya kusikiliza jambo hilo, inaelekea atamuuliza mtu aliyekosewa kama amezungumza na mtu aliyemkosea. Mzee anaweza pia kutaja hatua za Kimaandiko ambazo mtu aliyekosewa anaweza kuchukua ili kufuatilia amani.

12. Taja mifano inayoonyesha hatari ya kuchukua hatua haraka baada ya kusikia malalamiko.

12 Mifano mitatu katika Biblia inakazia hatari ya kuchukua hatua haraka baada ya kusikiliza upande mmoja tu katika ubishi. Potifa alimwamini mke wake alipomwambia kwamba Yosefu alijaribu kumlala kinguvu. Akiwa na hasira isiyo ya haki, Potifa aliagiza Yosefu atupwe gerezani. (Mwa. 39:19, 20) Mfalme Daudi alimwamini Siba aliyesema kwamba bwana wake, Mefiboshethi, alikuwa amejiunga na maadui wa Daudi. Daudi akajibu hivi haraka: “Tazama! Mali yote ya Mefiboshethi ni yako.” (2 Sam. 16:4; 19:25-27) Mfalme Artashasta aliambiwa kwamba Wayahudi walikuwa wakijenga upya kuta za Yerusalemu na walikuwa karibu kuasi utawala au Milki ya Uajemi. Mfalme huyo aliamini ripoti hiyo ya uwongo na akaagiza kwamba kazi yote ya kujenga upya ikomeshwe huko Yerusalemu. Matokeo ni kwamba Wayahudi waliacha kujenga hekalu la Mungu. (Ezra 4:11-13, 23, 24) Wazee Wakristo wanafuata kwa hekima shauri la Paulo kwa Timotheo la kuepuka kufanya maamuzi haraka-haraka.—Soma 1 Timotheo 5:21.

13, 14. (a) Sisi sote hatuwezi kujua nini kuhusu ubishi kati ya watu wengine? (b) Ni nini kinachoweza kuwasaidia wazee kufanya maamuzi yanayofaa kuhusu waamini wenzao?

13 Hata baada ya kuwasikiliza wote waliohusika katika ubishi, ni jambo la maana kutambua kwamba “yeyote akifikiri amejipatia ujuzi juu ya kitu fulani, bado hajakijua kama vile anavyopaswa kukijua.” (1 Kor. 8:2) Je, kweli tunajua mambo yote yaliyosababisha tatizo hilo? Je, tunaweza kuelewa kikamili hali za watu waliohusika? Wazee wanapoombwa kufanya uamuzi, ni jambo la maana kama nini kutokubali kudanganywa na habari za uwongo, mbinu za ujanja, au uvumi! Yesu Kristo, Mwamuzi aliyechaguliwa na Mungu, anahukumu kwa uadilifu. Yesu ‘hahukumu kulingana na sura inayoonekana kwa macho yake tu, wala kukaripia kulingana tu na jambo lililosikiwa na masikio yake.’ (Isa. 11:3, 4) Badala yake, Yesu anaongozwa na roho ya Yehova. Vivyo hivyo, wazee Wakristo wanapaswa kuongozwa na roho takatifu ya Mungu.

14 Kabla ya kufanya maamuzi yanayohusu waamini wenzao, wazee wanahitaji kusali ili kupata msaada wa roho ya Yehova na kutegemea mwongozo wa roho hiyo kwa kuchunguza Neno la Mungu na vichapo vya jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara.—Mt. 24:45.

Ni Lazima Tuwe na Amani Pamoja na Mungu

15. Ni wakati gani tunapopaswa kuripoti kuhusu dhambi nzito ambayo tumejua?

15 Tukiwa Wakristo, tunahimizwa tufuatilie amani. Hata hivyo, Biblia inasema hivi pia: “Hekima inayotoka juu kwanza kabisa ni safi kiadili, kisha yenye kufanya amani.” (Yak. 3:17) Tunapaswa kwanza kuwa safi kiadili kisha tufanye amani, yaani, kufuata viwango safi vya Mungu kuhusu maadili na kutimiza matakwa yake ya uadilifu. Mkristo akijua kwamba mwamini mwenzake amefanya dhambi nzito, anapaswa kumtia moyo aungame dhambi hiyo mbele ya wazee. (1 Kor. 6:9, 10; Yak. 5:14-16) Ikiwa mtu aliyetenda dhambi hachukui hatua hiyo, Mkristo ambaye amejua kuhusu dhambi hiyo anapaswa kuwaambia wazee. Mkristo akiamua kimakosa kunyamaza kwa sababu anataka kuendelea kuwa na amani pamoja na yule mtenda-dhambi, yeye pia anashiriki katika dhambi hiyo.—Law. 5:1; soma Methali 29:24.

16. Tunaweza kujifunza nini kutokana na kisa cha Yehu alipokutana na Mfalme Yehoramu?

16 Simulizi moja kuhusu Yehu linaonyesha kwamba ni jambo la maana zaidi kuunga mkono uadilifu wa Mungu badala ya kuwa na amani pamoja na mtu aliyetenda dhambi. Mungu alimtuma Yehu kutekeleza hukumu Yake juu ya nyumba ya Mfalme Ahabu. Mfalme Yehoramu aliyekuwa mwovu, na aliyekuwa mwana wa Ahabu na Yezebeli, alipanda gari lake ili kukutana na Yehu na akasema hivi: “Je, kuna amani, Yehu?” Yehu alijibu namna gani? Alisema hivi: “Kunaweza kuwa na amani gani wakati kungali na uasherati wa Yezebeli mama yako na ulozi wake mwingi?” (2 Fal. 9:22) Kisha, Yehu akatoa upinde wake na kumpiga Yehoramu mshale ambao uliingia ndani ya moyo. Kama vile tu Yehu alivyochukua hatua, wazee hawapaswi kuruhusu watu wanaozoea kufanya dhambi kimakusudi bila kutubu waendelee kuwa katika kutaniko ili tu kuwe na amani. Wanawaondoa watenda-dhambi wasiotubu ili kutaniko liendelee kufurahia amani pamoja na Mungu.—1 Kor. 5:1, 2, 11-13.

17. Wakristo wote wanahusika jinsi gani katika kufuatilia amani?

17 Matatizo mengi kati ya akina ndugu hayahusishi dhambi nzito zinazohitaji kushughulikiwa kihukumu na wazee. Hivyo, ni vizuri kufunika makosa ya wengine kwa upendo. Neno la Mungu linasema hivi: “Anayefunika makosa anatafuta upendo, naye anayeendelea kuongea juu ya jambo anawatenganisha watu wanaofahamiana.” (Met. 17:9) Kufuata maneno hayo kutatusaidia kudumisha amani katika kutaniko na kuendelea kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Yehova.—Mt. 6:14, 15.

Kufuatilia Amani Kunaleta Baraka

18, 19. Ni baraka gani ambazo tunapata kwa kufuatilia amani?

18 Tunapata baraka nyingi tunapofuatilia “mambo yanayofanya kuwe na amani.” Tunafurahia uhusiano wa karibu pamoja na Yehova tunapoiga njia zake, na tunachangia umoja na amani katika paradiso yetu ya kiroho. Kufuatilia amani ndani ya kutaniko kunatusaida pia kuona njia ambazo tunaweza kufuatilia amani pamoja na watu tunaowahubiria “habari njema ya amani.” (Efe. 6:15) Tunakuwa tayari zaidi ‘kuwa wapole kwa wote, tukiendelea kujizuia chini ya uovu.’—2 Tim. 2:24.

19 Kumbuka pia kwamba kutakuwa na “ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” (Mdo. 24:15) Watu watakapofufuliwa duniani, mamilioni ya watu wenye malezi, tabia, na nyutu mbalimbali watakuwa hai tena, yaani, wote waliokufa tangu “kuwekwa msingi wa ulimwengu”! (Luka 11:50, 51) Kwa kweli, litakuwa pendeleo kubwa kuwafundisha njia za amani watu watakaofufuliwa. Mazoezi tunayopata sasa tukiwa watu wanaofanya amani yatatusaidia sana wakati huo!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Ili kupata mwongozo wa Kimaandiko kuhusu kushughulikia dhambi nzito kama vile uchongezi na upunjaji, ona Mnara wa Mlinzi wa Oktoba 15, 1999, ukurasa wa 17-22.

Umejifunza Nini?

• Tunaweza jinsi gani kufuatilia amani ikiwa tumemkosea mtu fulani?

• Tunapaswa kufanya nini ili kufuatilia amani tunapokosewa?

• Kwa nini si jambo la hekima kuunga mkono upande mmoja katika ubishi?

• Eleza kwa nini tunapaswa kuunga mkono uadilifu wa Mungu badala ya kuwa na amani pamoja na mtu aliyetenda dhambi.

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 29]

Yehova anawapenda wale wanaowasamehe wengine kutoka moyoni