Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Tunapaswa kuelewa jinsi gani hesabu inayoonyeshwa katika ripoti ya utumishi ya kila mwaka?

Kila mwaka tunatazamia kwa hamu ripoti ya utumishi inayochapishwa katika Kitabu cha Mwaka. Inasisimua kuona mambo ambayo watu wa Yehova wametimiza wakiwa kikundi katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme na kufundisha ulimwenguni pote. Lakini ili tufaidike kabisa na ripoti hiyo, tunahitaji kuelewa vizuri hesabu hiyo na vilevile kuwa na maoni yenye usawaziko kuihusu. Fikiria mifano michache.

Mwaka wa utumishi. Mwaka huo unaanza Septemba mpaka Agosti (Mwezi wa 8) mwaka unaofuata. Kitabu cha Mwaka kinakuwa na ripoti ya mwaka wa utumishi uliotangulia. Hivyo, Kitabu cha Mwaka—2011 kina ripoti ya mwaka wa utumishi wa 2010, ambao ulianza Septemba 1, 2009, mpaka Agosti 31, 2010.

Kilele cha wahubiri na wastani wa wahubiri. “Wahubiri” wanatia ndani Mashahidi wa Yehova waliobatizwa na pia wale ambao hawajabatizwa ambao wanastahili kuwa wahubiri wa Ufalme. “Kilele cha wahubiri” ni hesabu ya juu zaidi ya wahubiri wanaoripoti mwezi wowote katika mwaka wa utumishi na inaweza kutia ndani ripoti zilizochelewa ambazo hazikujumlishwa katika ripoti ya mwezi uliotangulia. Kwa hiyo, huenda wahubiri fulani wakahesabiwa mara mbili. Hata hivyo, kilele au hesabu ya juu zaidi haitii ndani idadi ya wahubiri ambao walishiriki katika huduma lakini wakasahau kutoa ripoti. Hilo linakazia kwa nini ni jambo la maana kwa kila mhubiri kutoa ripoti haraka kila mwezi. “Wastani wa wahubiri” ni hesabu ya wahubiri ambao wanaripoti muda wanaotumia katika huduma kila mwezi.

Jumla ya saa. Kulingana na Kitabu cha Mwaka—2011, Mashahidi wa Yehova walitumia saa zaidi ya bilioni 1.6 katika huduma ya shambani. Hata hivyo, hesabu hiyo haionyeshi saa zote tunazotumia katika ibada yetu, kwa sababu haijatia ndani wakati ambao tunatumia kwa kawaida katika shughuli kama vile ziara za uchungaji, kuhudhuria mikutano, na funzo la Biblia la kibinafsi na kutafakari.

Pesa zilizotumiwa. Katika mwaka wa utumishi wa 2010, Mashahidi wa Yehova walitumia dola zaidi ya milioni 155 za Marekani katika kuwatunza mapainia wa pekee, wamishonari, na waangalizi wanaosafiri katika migawo yao ya utumishi wa shambani. Hata hivyo, hesabu hiyo, haitii ndani gharama za kuchapisha vichapo vinavyotegemea Biblia ambavyo tunachapisha; wala haitii ndani pesa zilizotumiwa kuwatunza Wanabetheli zaidi ya 20,000 ambao wanajitolea kutumika katika ofisi za tawi ulimwenguni pote.

Waliokula mkate na kunywa divai wakati wa Ukumbusho. Hesabu hiyo inatia ndani wahubiri waliobatizwa ambao walikula mkate na kunywa divai wakati wa Ukumbusho ulimwenguni pote. Je, hesabu hiyo inaonyesha jumla ya watiwa-mafuta walio duniani? Si lazima iwe hivyo. Sababu mbalimbali kama vile, imani za kidini ambazo watu walikuwa nazo zamani au hata matatizo ya kiakili au kihisia, yanaweza kufanya wengine wafikiri kimakosa kwamba wana mwito wa kimbingu. Hivyo, hatuwezi kujua hesabu kamili ya watiwa-mafuta walio duniani; wala hatuhitaji kujua. Baraza Linaloongoza halina orodha ya watu wanaokula mkate na kunywa divai wakati wa ukumbusho, kwa kuwa hawana mpango wa kuwasiliana na watiwa-mafuta wote duniani. *

Jambo tunalojua ni kwamba kutakuwa na ‘watumwa fulani wa Mungu wetu’ waliotiwa mafuta duniani wakati pepo zenye kuharibu za dhiki kuu zitakapoachiliwa. (Ufu. 7:1-3) Kabla ya wakati huo, watiwa-mafuta wataongoza katika jambo ambalo linaonyeshwa vizuri na ripoti yetu ya utumishi ya kila mwaka—kazi kubwa zaidi ya kuhubiri na kufundisha katika historia ya wanadamu.

[Maelezo ya Chini]