Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mkutano wa Kihistoria

Mkutano wa Kihistoria

Mkutano wa Kihistoria

“BAADA ya mkutano huu kwisha, utasema, ‘Kwa kweli mkutano huu wa kitheokrasi wa kila mwaka ulikuwa wa kihistoria!’” Kwa maneno hayo, Stephen Lett ambaye ni mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova aliwachochea wahudhuriaji wengi waliokuwapo watazamie kwa hamu mkutano huo. Walikuwa wamekusanyika kwa ajili ya mkutano wa kila mwaka wa 126 wa Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania, uliofanywa Oktoba 2, 2010, katika Jumba la Kusanyiko la Mashahidi wa Yehova huko Jersey City, New Jersey, Marekani. Ni mambo gani makuu ambayo yalizungumziwa katika pindi hiyo ya kihistoria?

Katika hotuba ya kwanza ambayo ilitolewa na Ndugu Lett, alizungumzia kwa njia yenye kusisimua kuhusu gari la kimbingu la Yehova linalotajwa katika kitabu cha Biblia cha Ezekieli. Gari hilo kubwa, na lenye utukufu linafananisha tengenezo la Mungu, ambalo linaongozwa kikamili na Yehova. Ndugu Lett alisema kwamba sehemu ya kimbingu ya tengenezo hilo, ambayo inafanyizwa na viumbe wa roho, inasonga kwa kasi sana—kwa kasi kama mawazo ya Yehova. Vivyo hivyo, sehemu ya kidunia ya tengenezo la Yehova Mungu inasonga mbele. Ndugu Lett alitaja marekebisho fulani yenye kusisimua katika sehemu inayoonekana ya tengenezo la Mungu ambayo yamefanywa katika miaka ya karibuni.

Kwa mfano, ofisi fulani za tawi zinaunganishwa pamoja, na hilo litawawezesha wengi ambao walikuwa wakitumikia Betheli katika nchi hizo wakazie fikira kazi ya kuhubiri. Ndugu Lett aliwahimiza wahudhuriaji waendelee kusali kwamba washiriki wa Baraza Linaloongoza, wakiwa wawakilishi wa jamii ya mtumwa, waendelee si kuwa tu waaminifu bali pia wawe na hekima, au busara.—Mt. 24:45-47.

Ripoti na Mahojiano Yenye Kutia Moyo

Tab Honsberger, ambaye ni mshiriki wa Halmashauri ya Tawi nchini Haiti, alitoa ripoti yenye kugusa moyo kuhusu mambo yaliyotukia baada ya tetemeko la ardhi lililotokea Januari 12, 2010 (12/1/2010), ambalo lilisababisha vifo vya watu 300,000 hivi katika nchi hiyo. Alisema viongozi wa kidini wamekuwa wakiwaambia watu kwamba Mungu aliwalinda watu wazuri na kuwaadhibu wale waliokufa kwa sababu hawakuwa na imani. Hata hivyo, maelfu ya wahalifu waliofungwa gerezani walitoroka wakati kuta za gereza zilipoangushwa na tetemeko. Hivyo, wakaaji wengi wa Haiti wenye mioyo minyoofu wanapata faraja kwa kujifunza ukweli kuhusu kwa nini nyakati zetu zina matatizo mengi sana. Ndugu Honsberger alitaja maneno ya ndugu mmoja mwaminifu nchini Haiti ambaye alimpoteza mke wake katika msiba huo, alisema hivi: “Bado ninaendelea kulia mpaka leo. Sijui nitaendelea kuomboleza kwa muda gani, lakini ninashangilia kwa sababu ya upendo kutoka kwa tengenezo la Yehova. Nina tumaini, na nimeazimia kuwaambia wengine kulihusu.”

Mark Sanderson, ambaye sasa ni mshiriki wa familia ya Betheli ya Brooklyn, alitoa ripoti kuhusu Ufilipino. Zamani alikuwa mshiriki wa Halmashauri ya Tawi huko Ufilipino na alifurahi alipokuwa akizungumza kuhusu vilele 32 vyenye kufuatana vya hesabu ya wahubiri wa Ufalme katika nchi hiyo na jinsi idadi ya mafunzo ya Biblia inavyozidi kwa mbali idadi ya wahubiri. Alisimulia kuhusu ndugu anayeitwa Miguel ambaye mjukuu wake aliuawa. Miguel alijitahidi kabisa ili kuhakikisha kwamba mtu aliyemuua mjukuu wake ameshtakiwa na kufungwa gerezani. Baadaye, alipokuwa akihubiri gerezani, Miguel alikutana na yule muuaji. Ingawa Miguel alikuwa na wasiwasi, alizungumza naye kwa upole na kwa fadhili. Mwishowe alijifunza na mtu huyo, ambaye alikubali kweli na akaja kumpenda Yehova. Na sasa amebatizwa. Miguel ndiye rafiki yake wa karibu na anajitahidi kumsaidia ndugu huyo mpya kuachiliwa mapema kutoka gerezani. *

Kisha programu ilikuwa na kipindi cha mahojiano ambacho kiliongozwa na Mark Noumair, mwalimu katika Idara ya Shule za Kitheokrasi. Alihoji wenzi sita wa ndoa—Alex na Sarah Reinmueller, David na Krista Schafer, na Robert na Ketra Ciranko. Alex Reinmueller, ambaye ni msaidizi wa Halmashauri ya Utangazaji, alieleza jinsi alivyofanya ukweli uwe mali yake alipokuwa akipainia huko Kanada akiwa na umri wa miaka 15 tu, mara nyingi akihubiri peke yake. Alipoulizwa kuhusu watu waliomchochea sana akiwa Betheli, Ndugu Reinmueller alitaja wanaume watatu waaminifu, na kueleza jinsi kila mmoja wao alivyomsaidia kukomaa kiroho. Mke wake Sarah, alizungumza kuhusu urafiki wake pamoja na dada fulani ambaye alivumilia miaka mingi katika magereza nchini China kwa sababu ya imani yake. Sarah alisema kwamba amejifunza kumtegemea Yehova kupitia sala ya kibinafsi.

David Schafer, msaidizi wa Halmashauri ya Ufundishaji, alimsifu mama yake kwa sababu ya imani yake yenye nguvu na akaeleza kuhusu ndugu ambao walifanya kazi ya kukata miti na kumsaidia kuwa painia msaidizi alipokuwa kijana. Mke wake, Krista, alizungumza kwa shauku kuhusu jinsi alivyochochewa na washiriki wenye umri mkubwa wa familia ya Betheli ambao walithibitika kuwa ‘waaminifu katika lililo dogo zaidi,’ kama Yesu alivyopendekeza.—Luka 16:10.

Robert Ciranko, msaidizi wa Halmashauri ya Uandikaji, alisimulia kuhusu babu na nyanya yake wa upande wa mama na pia wa upande wa baba, ambao walikuwa wahamiaji kutoka Hungaria na ambao walikuwa Wakristo watiwa-mafuta. Akiwa mvulana, alifurahi sana alipohudhuria makusanyiko makubwa katika miaka ya 1950 na kujifunza kwamba tengenezo la Yehova lilikuwa kubwa zaidi kuliko kutaniko lao. Mke wake, Ketra, alisimulia jinsi alivyojifunza kuhusu ushikamanifu alipokuwa akitumika akiwa painia katika kutaniko ambalo lilikuwa na waasi-imani na matatizo mengine. Alivumilia na mwishowe akapewa mgawo wa kutumika akiwa painia wa pekee katika kutaniko ambalo lilikuwa na umoja, na aliguswa moyo sana na umoja huo.

Kisha, Manfred Tonak akatoa ripoti kuhusu Ethiopia. Historia ya nchi hiyo ilianza nyakati za Biblia, na sasa imebarikiwa kwa kuwa na wahubiri zaidi ya 9,000 wa habari njema. Wengi wao wanaishi katika au karibu na mji mkuu, Addis Ababa. Hivyo, maeneo ya mashambani yanahitaji kuhubiriwa zaidi. Ili kutimiza uhitaji huo, Mashahidi Waethiopia wanaoishi katika nchi nyingine walialikwa kutembelea nchi hiyo ili kuhubiri katika maeneo fulani ya mashambani. Wengi wao walikuja, wakawatia moyo Mashahidi wenyeji, na wakapata watu waliowasikiliza.

Sehemu moja ya pekee katika programu hiyo ilikuwa mfululizo kuhusu Mashahidi wa Yehova nchini Urusi na mapambano yao ya kutambuliwa kisheria. Aulis Bergdahl, ambaye ni mshiriki wa Halmashauri ya Tawi nchini Urusi alizungumzia historia ya mateso ya Mashahidi nchini Urusi, na hasa katika jiji la Moscow. Philip Brumley ambaye anafanya kazi katika Idara ya Sheria katika ofisi ya tawi ya Marekani alieleza kuhusu mambo yenye kusisimua katika miezi ya hivi karibuni wakati Mahakama ya Ulaya ya Haki za Binadamu (ECHR) iliposikiliza mashtaka tisa yaliyotolewa kuhusu Mashahidi wa Yehova. Waamuzi wote wa Mahakama hiyo waliamua kwamba hakukuwa na shtaka lolote kati ya mashtaka hayo ambalo lilikuwa la kweli, na mara nyingi walitoa sababu zao kwa makini ili kupinga mashtaka yaliyotolewa. Ingawa bado tunangoja kuona matokeo, Ndugu Brumley alizungumza akiwa na matumaini kwamba uamuzi wa Mahakama hiyo utakuwa na matokeo makubwa juu ya kesi zinazoendelea katika nchi nyingine.

Baada ya habari hizo zenye kusisimua, Ndugu Lett alitangaza kwamba Mahakama ya ECHR ilikuwa imekubali kusikiliza kesi ya muda mrefu kati ya serikali ya Ufaransa na Mashahidi wa Yehova inayohusu kulipa kodi. Mahakama hiyo ambayo inaheshimiwa sana inakubali kesi chache sana ambazo zinaletwa huko. Kufikia sasa, mahakama ya ECHR imeshughulikia jumla ya kesi 39 ambazo zinawahusu Mashahidi wa Yehova, na kati ya kesi hizo imewaunga mkono Mashahidi katika kesi 37. Ndugu Lett aliwatia moyo watu wote wa Mungu wasali kwa Yehova Mungu kuhusu kesi inayoendelea.

Ripoti ya mwisho ilitolewa na Richard Morlan, ambaye ni mwalimu katika Shule ya Wazee wa Kutaniko. Alizungumza kwa shauku kuhusu shule hiyo na akataja maelezo ya shukrani kutoka kwa wazee ambao tayari wamehudhuria.

Hotuba Nyingine za Washiriki wa Baraza Linaloongoza

Guy Pierce, mshiriki wa Baraza Linaloongoza alitoa hotuba yenye kugusa moyo ambayo ilikazia andiko la mwaka wa 2011, ‘Pata kimbilio katika jina la Yehova.’ (Sef. 3:12) Alisema kwamba ingawa huu ni wakati wenye furaha kwa njia nyingi kwa watu wa Yehova, ni wakati hatari pia, kipindi chenye kutisha. Siku kuu ya Yehova iko karibu; ingawa hivyo, watu wanaendelea kutafuta kimbilio katika dini ya uwongo, mashirika ya kisiasa, utajiri wa kimwili, kujaribu kukwepa matatizo, na kadhalika. Ili kupata kimbilio la kweli, tunahitaji kuliitia jina la Yehova, na hilo linatia ndani kumjua, kumheshimu sana, na kumtumaini Yule anayewakilishwa na jina hilo, na kumpenda kwa vyote tulivyo navyo.

Kisha, David Splane, mshiriki wa Baraza Linaloongoza akatoa hotuba yenye uzito na yenye kuchochea fikira yenye kichwa “Je, Umeingia Katika Pumziko la Mungu?” Alisema kwamba pumziko la Mungu halimaanishi hali ya kutotenda, kwa kuwa Yehova na Mwana wake ‘wameendelea kufanya kazi’ katika kipindi chote cha siku hiyo ya mfano ya pumziko ili kutimiza kwa mafanikio kusudi la Mungu kwa ajili ya vitu alivyoumba kuhusiana na dunia. (Yoh. 5:17) Hivyo basi, tunaweza jinsi gani kuingia katika pumziko la Mungu? Jibu linatia ndani kuepuka dhambi na kuepuka kujifanya waadilifu. Tunahitaji kuwa na imani na kuishi tukikumbuka kusudi la Mungu, na kufanya yote tunayoweza ili kuunga mkono kusudi hilo. Nyakati nyingine, inaweza kuwa vigumu sana kufanya hivyo, lakini tunapaswa kukubali mashauri na kuunga mkono mwongozo kutoka kwa tengenezo la Yehova. Ndugu Splane aliwasihi wale waliohudhuria wafanye yote wanayoweza ili kuingia katika pumziko la Mungu.

Hotuba ya mwisho ambayo ilitolewa na Anthony Morris, mshiriki wa Baraza Linaloongoza, ilikuwa na kichwa “Tunangojea Nini?” Akizungumza kwa hisi ya uharaka na uchangamfu kama wa baba, Ndugu Morris aliwakumbusha wahudhuriaji mambo yaliyotabiriwa ambayo bado hayajatukia, matukio ambayo watu wote waaminifu wanangojea kwa hamu. Matukio hayo yanatia ndani tangazo la “Amani na usalama!” na kuharibiwa kwa dini ya uwongo. (1 The. 5:2, 3; Ufu. 17:15-17) Ndugu Morris alitoa onyo kwamba tusiseme, “Lazima hii iwe ni Har–Magedoni,” tunapoona matukio katika vyombo vya habari ambayo hayatimizi unabii kama huo. Aliwatia moyo wasikilizaji wawe na mtazamo wa shangwe, wa subira, na wa kungojea ambao unatajwa katika Mika 7:7. Hata hivyo, wakati huohuo aliwahimiza wote “waungane mkono” na Baraza Linaloongoza, wakae karibu-karibu kama vile wanajeshi wanavyofanya wanapoingia kwenye uwanja wa mapigano makali. Alisema hivi: “Mioyo yenu na iwe na nguvu, ninyi nyote mnaomngojea Yehova.”—Zab. 31:24.

Kwa kumalizia, kulikuwa na matangazo ya kihistoria yenye kusisimua. Geoffrey Jackson, mshiriki wa Baraza Linaloongoza alitangaza kuhusu mipango ya kujaribiwa kwa toleo la funzo la Mnara wa Mlinzi katika Kiingereza rahisi, kwa ajili ya wasomaji ambao hawajui sana Kiingereza. Kisha, Stephen Lett akatangaza kwamba Baraza Linaloongoza litafanya mipango ili waangalizi wa wilaya na wake zao wafanyiwe ziara za uchungaji nchini Marekani. Kisha alitangaza kwamba kuanzia sasa Shule ya Mazoezi ya Kihuduma itaitwa Shule ya Biblia ya Ndugu Waseja. Hivi karibuni kutakuwa pia na Shule ya Biblia ya Wenzi wa Ndoa Wakristo. Shule hiyo itawapa wenzi wa ndoa mazoezi ya ziada ili watumike zaidi katika tengenezo la Yehova. Ndugu Lett alitangaza pia kwamba Shule ya Waangalizi Wanaosafiri na Wake Zao na Shule ya Washiriki wa Halmashauri ya Tawi na Wake Zao zitapanuliwa na kuwa madarasa mawili kila mwaka huko Patterson, na wale ambao tayari wamehudhuria watapata nafasi ya kuhudhuria tena shule hizo.

Programu hiyo ilimalizika kwa njia yenye kugusa moyo wakati John E. Barr mwenye umri wa miaka 97, na ambaye ni mshiriki wa muda mrefu wa Baraza Linaloongoza, alipotoa sala kwa unyenyekevu na kwa unyoofu. * Kila mtu alibaki akijiambia kwamba kwa kweli hiyo ilikuwa siku ya kihistoria.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Ona Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova cha 2011, ukurasa wa 62-63.

^ fu. 20 Ndugu Barr alikufa Desemba 4, 2010 (4/12/2010), akiwa na tumaini la kwenda mbinguni.

[Blabu katika ukurasa wa 19]

Wote waliohudhuria walifurahia kipindi cha mahojiano

[Blabu katika ukurasa wa 20]

Yehova amebariki kazi ya kuhubiri nchini Ethiopia