Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Walimpata Masihi!

Walimpata Masihi!

Walimpata Masihi!

“Tumempata Masihi.”—YOH. 1:41.

1. Ni nini kilichomfanya Andrea aseme: “Tumempata Masihi”?

YOHANA MBATIZAJI amesimama pamoja na wawili kati ya wanafunzi wake. Yesu anapokaribia, Yohana anasema hivi kwa sauti kubwa: “Ona, Mwana-Kondoo wa Mungu!” Papo hapo, Andrea na yule mwanafunzi mwingine wanamfuata Yesu na kukaa naye siku nzima. Baadaye, Andrea anampata ndugu yake, Simoni Petro, na kumpeleka kwa Yesu baada ya kusema hivi kwa msisimko: “Tumempata Masihi.”—Yoh. 1:35-41.

2. Tutafaidika jinsi gani tunapoendelea kuchunguza unabii mbalimbali kumhusu Masihi?

2 Kadiri wakati unavyopita, Andrea, Petro, na wengine watakuwa na nafasi nyingi za kujifunza kwa undani Maandiko na watasema kwa uhakika kabisa kwamba Yesu wa Nazareti ndiye Masihi aliyeahidiwa. Imani yetu katika Neno la Mungu na Mtiwa-Mafuta wake itatiwa nguvu tunapoendelea kuchunguza unabii mbalimbali kumhusu Masihi.

“Tazama! Mfalme Wako Anakuja”

3. Ni unabii gani ambao ulitimia Yesu alipoingia Yerusalemu kwa ushindi?

3 Masihi angeingia Yerusalemu kwa ushindi. Unabii wa Zekaria ulisema hivi: “Shangilia sana, Ee binti Sayuni. Piga kelele za ushindi, Ee binti Yerusalemu. Tazama! mfalme wako anakuja kwako. Yeye ni mwadilifu, ndiyo, ameokolewa; ni mnyenyekevu, naye amepanda juu ya punda, juu ya mnyama mkomavu, mwana wa punda-jike.” (Zek. 9:9) Mtunga-zaburi aliandika hivi: “Na abarikiwe Yeye anayekuja katika jina la Yehova.” (Zab. 118:26) Yesu hakuuambia umati jambo la kufanya. Hata hivyo, umati huo ulipaaza sauti kwa ghafula na kwa shangwe nyingi sana na hivyo kutimiza unabii huo. Unaposoma simulizi hilo, wazia tukio hilo na usikie sauti za furaha za umati huo.—Soma Mathayo 21:4-9.

4. Eleza jinsi andiko la Zaburi 118:22, 23 lilivyotimia.

4 Yesu ni mwenye thamani machoni pa Mungu, lakini watu wengi wangemkataa ingawa angetimiza mengi akiwa Masihi. Kama ilivyotabiriwa, Yesu ‘alidharauliwa na kuhesabiwa kuwa asiye na maana’ na watu ambao hawakuamini uthibitisho. (Isa. 53:3; Marko 9:12) Hata hivyo, Mungu alimwongoza kwa roho takatifu mtunga-zaburi kusema hivi: “Jiwe ambalo wajenzi walilikataa limekuwa jiwe kuu la pembeni. Hili limetokana na Yehova mwenyewe.” (Zab. 118:22, 23) Pindi moja, Yesu alizungumzia unabii huo alipokuwa akiongea na wapinzani wake wa kidini, na Petro alisema kwamba Kristo alitimiza unabii huo. (Marko 12:10, 11; Mdo. 4:8-11) Yesu akaja kuwa “jiwe la pembeni la msingi” la kutaniko la Kikristo. Ingawa watu wasiomwogopa Mungu walimkataa, yeye ni ‘mchaguliwa na mwenye thamani kwa Mungu.’—1 Pet. 2:4-6.

Alisalitiwa na Kuachwa!

5, 6. Ni jambo gani lililotabiriwa na kutimia kuhusu kusalitiwa kwa Masihi?

5 Ilitabiriwa kwamba Masihi angesalitiwa na rafiki mwenye hila. Daudi alitabiri hivi: “Mtu mwenye kuwa na amani nami, ambaye nimemtegemea, ambaye alikuwa akila mkate wangu, amekiinua kisigino chake dhidi yangu.” (Zab. 41:9) Mtu ambaye alikula mkate pamoja na mwingine alionwa kuwa rafiki yake. (Mwa. 31:54) Hivyo, Yuda Iskariote alipomsaliti Yesu, alitenda kwa njia ya hila kabisa. Yesu alionyesha kwamba unabii wa Daudi ulitimia alipozungumza kuhusu msaliti wake na kuwaambia mitume wake hivi: “Mimi sisemi juu yenu nyote; ninawajua wale ambao nimewachagua. Lakini ni ili Andiko lipate kutimizwa, ‘Yule aliyekuwa akila mkate wangu amekiinua kisigino chake dhidi yangu.’”—Yoh. 13:18.

6 Mtu ambaye angemsaliti Masihi angepokea vipande 30 vya fedha, yaani, bei ya mtumwa! Akitumia unabii wa Zekaria 11:12, 13, Mathayo alionyesha kwamba Yesu alisalitiwa kwa kiasi hicho kidogo cha fedha. Lakini kwa nini Mathayo alisema kwamba jambo hilo lilikuwa limetabiriwa “kupitia nabii Yeremia”? Katika siku za Mathayo, huenda kitabu cha Yeremia kilikuwa cha kwanza katika kikundi cha vitabu vya Biblia ambavyo vilitia ndani Zekaria. (Linganisha na Luka 24:44.) Yuda hakutumia kamwe pesa alizopata kwa hila, kwa kuwa alizitupa ndani ya hekalu na kwenda kujinyonga.—Mt. 26:14-16; 27:3-10.

7. Unabii wa Zekaria 13:7 ulitimia jinsi gani?

7 Hata wanafunzi wa Masihi wangetawanyika. Zekaria aliandika hivi: “Mpige mchungaji, na wale wa kundi watawanyike.” (Zek. 13:7) Katika Nisani 14, mwaka wa 33 W.K., Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Ninyi nyote mtakwazika kuhusiana nami usiku huu, kwa maana imeandikwa, ‘Nitampiga mchungaji, nao kondoo wa kundi watatawanyika huku na huku.’” Na hivyo ndivyo ilivyokuwa, kwa sababu Mathayo aliripoti kwamba “wanafunzi wote wakamwacha [Yesu] na kukimbia.”—Mt. 26:31, 56.

Alishtakiwa na Kupigwa

8. Unabii wa Isaya 53:8 ulitimia chini ya hali gani?

8 Masihi angeshtakiwa na kuhukumiwa. (Soma Isaya 53:8.) Asubuhi ya Nisani 14, washiriki wote wa Sanhedrini walikutana, wakaamuru Yesu afungwe mikono, na kumpeleka kwa Gavana Mroma Pontio Pilato. Alimuuliza Yesu maswali lakini hakumpata na hatia yoyote. Hata hivyo, Pilato alipotaka kumwachilia Yesu, watu walipaaza sauti hivi: “Mtundike mtini!” na wakaomba Baraba aliyekuwa mhalifu aachiliwe. Akitaka kuupendeza umati huo, Pilato alimwachilia Baraba, akaamuru Yesu apigwe mijeledi, na kumtoa ili atundikwe mtini.—Marko 15:1-15.

9. Ni jambo gani lililotukia katika siku za Yesu ambalo lilitabiriwa katika Zaburi 35:11?

9 Mashahidi wa uwongo wangetoa ushahidi wa uwongo kumhusu Masihi. Mtunga-zaburi Daudi alisema hivi: “Mashahidi wenye jeuri husimama; huniuliza mambo nisiyojua.” (Zab. 35:11) Kama unabii ulivyosema, “wakuu wa makuhani na Sanhedrini nzima walikuwa wakitafuta ushahidi wa uwongo juu ya Yesu ili wamuue.” (Mt. 26:59) Kwa kweli, “wengi walikuwa wakitoa ushahidi wa uwongo juu yake, lakini ushuhuda wao haukupatana.” (Marko 14:56) Maadui wa Yesu wenye hasira ambao walitaka auawe hawakujali ushahidi wa uwongo uliotolewa kumhusu.

10. Eleza jinsi unabii wa Isaya 53:7 ulivyotimia.

10 Masihi angekaa kimya mbele ya wale waliomshtaki. Isaya alikuwa ametabiri hivi: “Alikazwa sana, naye alijiachilia ateswe; ingawa hivyo hakufungua kinywa chake. Alikuwa akiletwa kama kondoo machinjioni; na kama kondoo-jike ambaye amekuwa bubu mbele ya wakataji-manyoya wake, yeye pia hakufungua kinywa chake.” (Isa. 53:7) Yesu “alipokuwa akishtakiwa na wakuu wa makuhani na wanaume wazee, hakujibu.” Pilato akamuuliza: “Je, husikii ni mambo mangapi wanashuhudia juu yako?” Hata hivyo, Yesu “hakumjibu, hata neno moja, hivi kwamba gavana akastaajabu sana.” (Mt. 27:12-14) Yesu hakuwatukana wale waliokuwa wakimshtaki.—Rom. 12:17-21; 1 Pet. 2:23.

11. Unabii wa Isaya 50:6 na Mika 5:1 ulitimia jinsi gani?

11 Isaya alitabiri kwamba Masihi angepigwa. Nabii huyo aliandika: “Mgongo wangu niliwapa washambuliaji, na mashavu yangu nikawapa wale wenye kung’oa nywele. Uso wangu sikuuficha kutoka kwa mambo yenye kufedhehesha na mate.” (Isa. 50:6) Mika alitabiri hivi: “Watalipiga kwa fimbo shavu la mwamuzi wa Israeli.” (Mika 5:1) Akithibitisha kwamba unabii huo ulitimia, Marko, mwandikaji wa Injili alisema: “Wengine wakaanza kumtemea [Yesu] mate na kuufunika uso wake wote na kumpiga ngumi na kumwambia: ‘Toa unabii!’ Na, wakimpiga makofi usoni, watumishi wa mahakama wakamchukua.” Marko anasema kwamba askari-jeshi “wakawa wakimpiga kichwani kwa utete na kumtemea mate na kumsujudia [kwa dhihaka] wakiwa wamepiga magoti.” (Marko 14:65; 15:19) Bila shaka, Yesu hakutenda kosa lolote ambalo lingefanya astahili kutendewa hivyo.

Mwaminifu Mpaka Kifo

12. Unabii wa Zaburi 22:16 na Isaya 53:12 ulimhusu Yesu jinsi gani?

12 Unabii ulitabiri jinsi ambavyo Masihi angetundikwa mtini. Mtunga-zaburi Daudi alisema hivi: “Kusanyiko la watenda-maovu limenizunguka. Wako kwenye mikono yangu na miguu yangu kama simba.” (Zab. 22:16) Akiripoti tukio ambalo wasomaji wa Biblia wanajua vizuri, Marko, mwandikaji wa Injili anasema: “Sasa ilikuwa saa tatu [karibu saa tatu asubuhi], nao wakamtundika mtini.” (Marko 15:25) Pia, ilikuwa imetabiriwa kwamba Masihi angehesabiwa pamoja na watenda-dhambi. Isaya aliandika hivi: “Aliimwaga nafsi yake mpaka kufa, naye alihesabiwa pamoja na wakosaji.” (Isa. 53:12) Na kama ilivyotabiriwa, “wanyang’anyi wawili wakatundikwa mtini pamoja [na Yesu], mmoja upande wake wa kuume na mwingine upande wake wa kushoto.”—Mt. 27:38.

13. Unabii wa Zaburi 22:7, 8 ulitimia jinsi gani kuhusiana na Yesu?

13 Daudi alitabiri kwamba Masihi angetukanwa. (Soma Zaburi 22:7, 8.) Yesu alitukanwa akiwa kwenye mti wa mateso, kwa kuwa Mathayo anaripoti hivi: “Wapita-njia wakaanza kumtukana, wakitikisa vichwa vyao na kusema: ‘Ewe uliyetaka kuliangusha hekalu na kulijenga kwa siku tatu, jiokoe mwenyewe! Ikiwa wewe ni mwana wa Mungu, shuka kutoka kwenye mti wa mateso!’” Vivyo hivyo, wakuu wa makuhani, waandishi, na wanaume wazee walimcheka na kusema: “Aliwaokoa wengine; yeye mwenyewe hawezi kujiokoa! Yeye ni Mfalme wa Israeli; acheni sasa ashuke kutoka kwenye mti wa mateso nasi tutamwamini. Ameweka tegemeo lake katika Mungu; acheni Yeye sasa amwokoe ikiwa Yeye anamtaka, kwa maana alisema, ‘Mimi ni Mwana wa Mungu.’” (Mt. 27:39-43) Hata hivyo, Yesu alivumilia mateso hayo yote kwa heshima. Alituwekea mfano mzuri kama nini!

14, 15. Eleza jinsi unabii ulivyotimia kuhusu mavazi ya Masihi na jinsi alivyopewa siki.

14 Mavazi ya Masihi yangepigiwa kura. Mtunga-zaburi aliandika hivi: “Wanagawana mavazi yangu, nao wanalipigia kura vazi langu.” (Zab. 22:18) Hilo ndilo jambo lililotukia, kwa kuwa “[askari-jeshi Waroma] walipokuwa wamemtundika [Yesu] mtini wakagawa mavazi yake ya nje kwa kupiga kura.”—Mt. 27:35; soma Yohana 19:23, 24.

15 Masihi angepewa siki na nyongo. Mtunga-zaburi alisema: “Walinipa mmea wenye sumu kuwa chakula, na kwa ajili ya kiu yangu wakajaribu kuninywesha siki.” (Zab. 69:21) Mathayo anatuambia hivi: “Wakampa [Yesu] divai iliyochanganywa na nyongo anywe; lakini, baada ya kuionja, akakataa kuinywa.” Baadaye, “mmoja wao akakimbia mara moja, akachukua sifongo akailowesha kwenye divai kali akaiweka juu ya utete na kuanza kumnywesha.”—Mt. 27:34, 48.

16. Eleza jinsi unabii wa Zaburi 22:1 ulivyotimia.

16 Ingeonekana kwamba Mungu amemwacha Masihi. (Soma Zaburi 22:1.) Kulingana na unabii huo, “saa tisa [karibu saa tisa mchana] Yesu akapaaza kilio kwa sauti kubwa: ‘Eli, Eli, lama sabakthani?’ maneno ambayo yanapotafsiriwa humaanisha: ‘Mungu wangu, Mungu wangu, kwa nini umeniacha?’” (Marko 15:34) Yesu hakuwa amepoteza imani katika Baba yake wa mbinguni. Mungu alimwacha Yesu mikononi mwa maadui wake kwa kuondoa ulinzi Wake ili utimilifu wa Kristo ujaribiwe kikamili. Na Yesu alipopaaza kilio, alitimiza unabii wa Zaburi 22:1.

17. Maneno ya Zekaria 12:10 na Zaburi 34:20 yalitimia jinsi gani?

17 Masihi angechomwa, lakini mifupa yake haingevunjwa. Wakaaji wa Yerusalemu ‘wangemtazama Yule waliyemchoma.’ (Zek. 12:10) Na andiko la Zaburi 34:20 linasema: “[Mungu] anailinda mifupa yote ya mtu huyo; hakuna hata mmoja uliovunjwa.” Akithibitisha maneno hayo, mtume Yohana aliandika hivi: “Mmoja wa hao askari-jeshi akauchoma ubavu wake [wa Yesu] kwa mkuki, na mara moja damu na maji vikatoka. Na [Yohana] ambaye ameona hilo ametoa ushahidi, nao ushahidi wake ni wa kweli . . . Mambo haya yalitendeka kusudi andiko litimizwe: ‘Hakuna mfupa wake hata mmoja utakaovunjwa.’ Na tena, andiko tofauti linasema: ‘Watamtazama Yule waliyemchoma.’”—Yoh. 19:33-37.

18. Yesu alizikwa pamoja na matajiri jinsi gani?

18 Masihi angezikwa pamoja na matajiri. (Soma Isaya 53:5, 8, 9.) Baadaye Nisani 14 wakati wa mchana, “mtu mmoja tajiri wa Arimathea, anayeitwa Yosefu,” alimwomba Pilato mwili wa Yesu, na ombi lake likakubaliwa. Simulizi la Mathayo linaongezea hivi: “Yosefu akauchukua mwili huo, akaufunga katika kitani safi kizuri, na kuulaza katika kaburi lake jipya, alilokuwa amechimba katika mwamba. Na, baada ya kuviringisha jiwe kubwa kwenye mlango wa lile kaburi, akaondoka.”—Mt. 27:57-60.

Msifu Mfalme wa Kimasihi!

19. Unabii wa Zaburi 16:10 ulitimia jinsi gani?

19 Masihi angefufuliwa. Daudi aliandika hivi: “[Yehova] hutaiacha nafsi yangu katika Kaburi.” (Zab. 16:10) Fikiria jinsi wanawake waliokuja kwenye kaburi ambamo mwili wa Yesu ulikuwa umelazwa walivyoshangaa. Walimkuta malaika aliyejivika mwili wa kibinadamu, akawaambia hivi: “Acheni kufadhaika. Mnamtafuta Yesu Mnazareti, aliyetundikwa mtini. Alifufuliwa, hayupo hapa. Tazameni! Mahali walipomlaza.” (Marko 16:6) Siku ya Pentekoste ya mwaka 33 W.K., mtume Petro aliuambia hivi umati uliokusanyika Yerusalemu: “[Daudi] aliona kimbele na kusema kuhusu ufufuo wa Kristo, kwamba hakuachwa katika Kaburi wala mwili wake haukuona uharibifu.” (Mdo. 2:29-31) Mungu hakuruhusu mwili wa nyama wa Mwana wake mpendwa uoze. Zaidi ya hayo, Yesu alifufuliwa kimuujiza na kupewa mwili wa roho!—1 Pet. 3:18.

20. Unabii kuhusu utawala wa Masihi ulitimia jinsi gani?

20 Kama ilivyotabiriwa, Mungu alitangaza kwamba Yesu ni Mwana wake. (Soma Zaburi 2:7; Mathayo 3:17.) Pia, umati wa watu ulimsifu Yesu na Ufalme ambao ungekuja, na kwa shangwe tunawahubiria watu kumhusu na kuhusu utawala wake uliobarikiwa. (Marko 11:7-10) Hivi karibuni, Kristo atawaharibu maadui wake ‘atakapopanda kwa kutetea kweli, unyenyekevu, na uadilifu.’ (Zab. 2:8, 9; 45:1-6) Ufalme wake utaleta amani na ufanisi duniani pote. (Zab. 72:1, 3, 12, 16; Isa. 9:6, 7) Tuna pendeleo kubwa sana la kutangaza kweli hizo tukiwa Mashahidi wa Yehova, ambaye Mwana wake mpendwa anatawala sasa mbinguni akiwa Mfalme wa Kimasihi!

Ungesema Nini?

• Yesu alisalitiwa na kuachwa jinsi gani?

• Taja mambo fulani yaliyotabiriwa kuhusu Yesu Kristo kutundikwa mtini.

• Kwa nini unasadiki kwamba Yesu ndiye Masihi aliyeahidiwa?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 13]

Yesu alipoingia Yerusalemu kwa ushindi alitimiza unabii gani?

[Picha katika ukurasa wa 15]

Yesu alikufa kwa ajili ya dhambi zetu, lakini sasa anatawala akiwa Mfalme wa Kimasihi