Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unaweza Kuwa Kama Finehasi Unapokabili Hali Ngumu?

Je, Unaweza Kuwa Kama Finehasi Unapokabili Hali Ngumu?

Je, Unaweza Kuwa Kama Finehasi Unapokabili Hali Ngumu?

NI PENDELEO kubwa kutumika ukiwa mzee wa kutaniko. Hata hivyo, Neno la Mungu linaonyesha kwamba wazee wanakabili hali ngumu. Nyakati fulani, wanalazimika kushughulikia kesi zinazohusu dhambi na kutoa ‘hukumu kwa ajili ya Yehova.’ (2 Nya. 19:6) Au mzee anaweza kupokea mgawo ambao anahisi kwamba hawezi kuutimiza, kama vile Musa alivyohisi, ambaye aliomba hivi kwa unyenyekevu kuhusu mgawo wake: “Mimi ni nani hata niende kwa Farao?”—Kut. 3: 11.

Maandiko, ambayo yaliandikwa kwa mwongozo wa nguvu ileile ya utendaji ambayo inawaweka rasmi wazee, yana mifano ya waangalizi ambao walikabiliana na hali ngumu kwa mafanikio. Finehasi alikuwa mwana wa Eleazari na pia mjukuu wa Haruni na hivyo alikuwa na haki ya kuwa kuhani mkuu. Matukio matatu katika maisha yake yanaonyesha kwamba leo wazee wanapaswa kukabiliana na hali ngumu kwa ujasiri, ufahamu, na kumtegemea Yehova.

“Akainuka Mara Moja”

Waisraeli walipokuwa wamepiga kambi kwenye Nchi Tambarare za Moabu, Finehasi alikuwa kijana. Biblia inasema hivi: “Watu wakaanza kufanya uasherati na binti za Moabu. . . . Nao watu wakaanza kula na kuinamia miungu yao.” (Hes. 25:1, 2) Yehova aliwaadhibu waovu kwa tauni iliyosababisha kifo. Je, unaweza kuwazia jinsi ripoti hiyo ya uovu na tauni iliyosababishwa na uovu huo ilivyomkasirisha Finehasi?

Simulizi hilo linaendelea kusema hivi: “Tazama! mwanamume mmoja kati ya wana wa Israeli akaja, naye alikuwa akimleta mwanamke Mmidiani karibu na ndugu zake, mbele ya macho ya Musa na mbele ya macho ya kusanyiko lote la wana wa Israeli, walipokuwa wakilia kwenye mwingilio wa hema la mkutano.” (Hes. 25:6) Kuhani Finehasi angefanya nini? Alikuwa kijana, na Mwisraeli aliyekuwa akitenda uovu alikuwa mkuu ambaye aliongoza ibada kati ya watu.—Hes. 25:14.

Lakini Finehasi alimwogopa Yehova, si wanadamu. Alipowaona watu hao wawili, mara moja akachukua mkuki mkononi na kumfuata yule mwanamume ndani ya hema na kuwachoma mkuki wote wawili. Yehova alikuwa na maoni gani kuhusu ujasiri wa Finehasi na jinsi alivyochukua hatua na kutenda? Mara moja Yehova akakomesha ile tauni na kumthawabisha Finehasi kwa kufanya agano pamoja naye ili ukuhani ubaki katika ukoo wake “mpaka wakati usio na kipimo.”—Hes. 25:7-13.

Bila shaka, leo wazee Wakristo hawatendi kwa ujeuri. Lakini kama Finehasi, ni lazima wazee wawe tayari kuchukua hatua na kutenda kwa ujasiri. Kwa mfano, Guilherme alikuwa ametumikia akiwa mzee kwa miezi michache tu alipoombwa ashiriki kwenye halmashauri ya hukumu. Yule aliyetenda kosa ni mzee ambaye alikuwa amemsaidia Guilherme alipokuwa na umri mdogo zaidi. Guilherme anasema hivi: “Nilikuwa na wasiwasi kuhusu kusikiliza kesi hiyo. Nilishindwa kulala wakati wa usiku. Nilifikiria sana njia za kushughulikia kesi hiyo bila kuruhusu hisia zangu zinipofushe kiroho. Nilisali kwa siku nyingi na kufanya utafiti katika vichapo vya Biblia.” Hilo lilimsaidia kupata ujasiri aliohitaji ili kushughulikia hali hiyo ngumu na kumsaidia kiroho ndugu aliyekosea.—1 Tim. 4:11, 12.

Wazee wanaweka mfano mzuri katika kuonyesha imani na ushikamanifu wanapotenda kwa ujasiri na kuchukua hatua hali zinapowalazimisha kufanya hivyo katika kutaniko. Bila shaka, Wakristo wengine pia wanahitaji kutenda kwa ujasiri, kwa kuripoti makosa mazito ambayo huenda wanajua. Vivyo hivyo, tunahitaji kuwa washikamanifu ili kukatisha uhusiano na rafiki au mtu wa ukoo ambaye ametengwa na ushirika.—1 Kor. 5:11-13.

Ufahamu Unazuia Mzozano

Finehasi hakuwa na ujasiri kwa sababu tu ya msukumo wa ujana. Fikiria jinsi alivyoonyesha ufahamu na kutenda kwa hekima na busara aliposikia ripoti nyingine. Makabila ya Rubeni na Gadi na nusu ya kabila la Manase yalikuwa yamejenga madhabahu karibu na Mto Yordani. Waisraeli wengine walifikiri kwamba madhabahu hiyo ilikuwa ya ibada ya uwongo na wakajitayarisha kuchukua hatua ya kijeshi.—Yos. 22:11, 12.

Finehasi alitenda jinsi gani? Finehasi pamoja na wakuu Waisraeli, walizungumzia kwa busara jambo hilo pamoja na wale waliokuwa wamejenga madhabahu hiyo. Makabila yaliyoshtakiwa yalifafanua jambo hilo, na kueleza kwamba kwa kweli ilikuwa madhabahu kwa ajili ya “utumishi wa Yehova.” Hivyo, wakaepuka mzozano.—Yos. 22:13-34.

Mkristo anaposikia shtaka au jambo lisilofaa kumhusu mtumishi mwenzake wa Yehova, ni jambo la hekima kama nini kumwiga Finehasi! Ufahamu unatuzuia kukasirika au kusema mambo yasiyofaa kuhusu ndugu zetu.—Met. 19:11.

Ufahamu unaweza kuwasaidia jinsi gani wazee kutenda kama Finehasi? Jaime ambaye amekuwa mzee kwa miaka zaidi ya kumi anasema hivi: “Mhubiri anapoanza kuzungumza kuhusu tatizo la kibinafsi kati yake na mtu mwingine, mara moja ninamwomba Yehova anisaidie ili nisiunge mkono upande wowote badala yake nitoe mwongozo wa Kimaandiko. Siku moja, dada fulani alizungumza nami juu ya tatizo la kibinafsi kuhusu jinsi ndugu mmoja mwenye madaraka katika kutaniko lingine alivyomtendea. Kwa kuwa ndugu huyo alikuwa rafiki yangu, ingekuwa rahisi kwangu kumtetea. Badala yake, nilizungumza na dada huyo kuhusu kanuni fulani za Biblia. Kwanza kabisa, alikubali kuzungumza na ndugu huyo yeye mwenyewe. (Mt. 5:23, 24) Amani haikupatikana mara moja. Hivyo nilimwomba afikirie kanuni nyingine za Kimaandiko. Aliamua kusali tena kuhusu hali hiyo na kujitahidi kusamehe.”

Matokeo yalikuwa nini? Jaime anakumbuka hivi: “Miezi michache baadaye, dada huyo alizungumza nami. Alisema kwamba baada ya muda, yule ndugu alisikitika kwa sababu ya mambo aliyosema. Ndugu huyo alifanya mpango wa kuhubiri pamoja na dada huyo na akamweleza kwamba anamthamini. Wakatatua tatizo walilokuwa nalo. Je, kweli ningetatua jambo hilo kwa njia nzuri hivyo ikiwa ningejiingiza katika mabishano hayo, na labda ionekane ninapendelea upande fulani?” Biblia inatoa shauri hili: “Usiende kwa haraka kufanya kesi.” (Met. 25:8) Wazee wenye ufahamu wanawatia moyo kwa hekima Wakristo ambao wana matatizo kati yao wafuate kanuni za Kimaandiko ili kupata na kuendeleza amani.

Alimuuliza Yehova

Finehasi alikuwa na pendeleo la kutumika akiwa kuhani kwa ajili ya watu wa Mungu waliochaguliwa. Kama ilivyotajwa, alikuwa na ufahamu na ujasiri usio wa kawaida hata alipokuwa kijana. Hata hivyo, alifanikiwa kushughulikia hali ngumu kwa sababu alimtegemea Yehova.

Baada ya wanaume wa Gibea wa kabila la Benyamini kumlala kinguvu na kumuua suria wa Mlawi fulani, yale makabila mengine yaliamua kwenda kupigana na Wabenyamini. (Amu. 20:1-11) Kabla ya kupigana, walisali kwa Yehova ili awasaidie, lakini wakashindwa mara mbili, na kupata hasara kubwa. (Amu. 20:14-25) Je, wangekata kauli kwamba sala zao hazikujibiwa? Je, kweli Yehova alitaka kuona wakichukua hatua kwa sababu ya kosa ambalo lilikuwa limefanywa?

Akiwa na uhakika kabisa, Finehasi, ambaye sasa alikuwa kuhani mkuu wa Israeli, alichukua hatua tena. Alisali hivi: “Je, niende tena kupigana na wana wa Benyamini ndugu yangu, au je, nisiende?” Yehova alijibu kwa kuyawezesha makabila mengine ya Israeli kuwashinda Wabenyamini, na kuteketeza Gibea kabisa.—Amu. 20:27-48.

Tunajifunza nini kutokana na kisa hicho? Matatizo fulani yanaweza kuendelea katika kutaniko ingawa wazee wanajitahidi na kumwomba Mungu awasaidie. Jambo kama hilo linapotokea, wazee wanapaswa kukumbuka maneno haya ya Yesu: “Endeleeni kuomba [au kusali], nanyi mtapewa; endeleeni kutafuta, nanyi mtapata; endeleeni kupiga hodi, nanyi mtafunguliwa.” (Luka 11:9) Hata inapoonekana kwamba sala hazijibiwi haraka, wazee wanaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atajibu kwa wakati wake.

Kwa mfano, kutaniko fulani huko Ireland lilihitaji sana Jumba la Ufalme lakini halikupata kibali cha ofisa wa mipango ya ujenzi katika eneo lao. Ofisa huyo alipinga mapendekezo yote ya mipango ya ujenzi kwenye eneo ambalo akina ndugu walitazamia kujenga. Ilionekana kwamba yule tu ambaye angewapa kibali hicho ni ofisa mkuu wa mipango ya ujenzi katika nchi yote. Je, sala ingesaidia kama ilivyosaidia katika siku za Finehasi?

Mzee mmoja katika kutaniko hilo anasema hivi: “Baada ya kutoa dua na kusali sana, tulienda kwenye ofisi kuu ya mipango ya ujenzi. Niliambiwa kwamba huenda ingechukua majuma mengi kabla ya kukutana na ofisa mkuu. Hata hivyo, tulifanikiwa kukutana naye kwa dakika tano. Baada ya kuona mipango ya ujenzi iliyochorwa upya, mara moja alitupatia ruhusa ya kuanza ujenzi, na kuanzia wakati huo na kuendelea ofisa wa ujenzi wa eneo letu akajitolea kutusaidia. Tukio hilo lilitusaidia kuthamini uwezo wa sala.” Ndiyo, Yehova atajibu sala za unyoofu za wazee wanaomtegemea.

Finehasi alikuwa na daraka zito katika Israeli la kale; hata hivyo, alifanikiwa kukabiliana na hali ngumu kwa sababu alitenda kwa ujasiri, ufahamu, na kumtegemea Mungu. Na Finehasi alipata kibali cha Yehova kwa sababu alijitahidi kulitunza kutaniko la Mungu. Miaka 1,000 hivi baadaye, Ezra aliongozwa na roho takatifu kuandika hivi: “Finehasi mwana wa Eleazari ndiye aliyekuwa kiongozi juu yao hapo zamani. Yehova alikuwa pamoja naye.” (1 Nya. 9:20) Na iwe hivyo kwa wale wanaoongoza kati ya watu wa Mungu leo, na iwe hivyo pia kwa Wakristo wote wanaomtumikia kwa ushikamanifu.