Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Yehova Anakujua?

Je, Yehova Anakujua?

Je, Yehova Anakujua?

“Yehova anawajua walio wake.”—2 Tim. 2:19.

1, 2. (a) Yesu alihangaikia jambo gani? (b) Tunapaswa kujiuliza maswali gani?

SIKU moja Farisayo fulani alimuuliza Yesu hivi: “Amri iliyo kuu katika ile Sheria ni gani?” Yesu akajibu hivi: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.” (Mt. 22:35-37) Yesu alimpenda sana Baba yake wa mbinguni na kwa kweli maisha yake yalionyesha hivyo. Yesu alihangaikia pia msimamo wake mbele za Yehova, na kuonyesha hivyo kupitia maisha yake ya uaminifu. Hivyo, kabla ya kifo chake, alisema kwamba Mungu alimjua kuwa mtu ambaye alitii kwa uaminifu sheria za Mungu. Hivyo, Yesu alikaa katika upendo wa Yehova.—Yoh. 15:10.

2 Watu wengi leo wanadai kwamba wanampenda Mungu. Bila shaka, sisi pia ni kati ya watu hao. Hata hivyo, maswali au maulizo ya maana ambayo tunapaswa kujiuliza ni haya: ‘Je, Mungu ananijua? Yehova ana maoni gani kunihusu? Je, watu wananiona kuwa mtu wa Yehova?’ (2 Tim. 2:19) Ni pendeleo kama nini kujua kwamba tunaweza kuwa na uhusiano wa karibu hivyo pamoja na Mwenye Enzi Kuu wa ulimwengu wote!

3. Kwa nini watu fulani wanakuwa na shaka kwamba wao ni watu wa Yehova, na ni nini kitakachowasaidia kuondoa mawazo kama hayo?

3 Hata hivyo, watu fulani ambao wanampenda Yehova wanaona ni vigumu kuamini kwamba Mungu anaweza kuwa na maoni yanayofaa kuwaelekea. Wengine wanahisi kuwa hawafai, kwa hiyo wanakuwa na shaka kwamba wao ni watu wa Yehova. Hata hivyo, tunaweza kuwa na furaha kama nini kwamba Mungu anaweza kutuona kwa njia tofauti! (1 Sam. 16:7) Mtume Paulo aliwaambia hivi Wakristo wenzake: “Ikiwa yeyote anampenda Mungu, huyo anajulikana naye.” (1 Kor. 8:3) Ikiwa unataka Mungu akujue ni lazima kwanza wewe umpende. Fikiria jambo hili: Kwa nini unasoma gazeti hili? Kwa nini unajitahidi kumtumikia Yehova kwa moyo, nafsi, akili, na nguvu zako zote? Ikiwa umejiweka wakfu kwa Mungu na kubatizwa, ni nini kilichokuchochea kuchukua hatua hizo? Biblia inasema kwamba Yehova, ambaye anachunguza mioyo, anawavuta watu wenye kutamanika. (Soma Hagai 2:7; Yohana 6:44.) Kwa hiyo, unaweza kusema kwamba unamtumikia Yehova kwa sababu alikuvuta. Hatawaacha kamwe wale ambao amewavuta ikiwa wataendelea kuwa waaminifu. Mungu anawaona kuwa wenye thamani sana, na anawapenda kwelikweli.—Zab. 94:14.

4. Kwa nini tunapaswa kuendelea kufikiria pendeleo letu la kujulikana na Mungu?

4 Baada ya Yehova kutuvuta kwake, tunapaswa kujitahidi kuendelea kukaa katika upendo wake. (Soma Yuda 20, 21.) Kumbuka Biblia inasema kwamba tunaweza kupeperushwa au kujiondoa kwa Mungu. (Ebr. 2:1; 3:12, 13) Kwa mfano, kabla tu ya kusema maneno yaliyo katika 2 Timotheo 2:19, mtume Paulo aliwataja Himenayo na Fileto. Ni wazi kwamba wakati fulani wanaume hao wawili walikuwa watu wa Yehova, lakini baadaye waliacha kweli. (2 Tim. 2:16-18) Kumbuka pia kwamba katika makutaniko ya Galatia, watu fulani ambao Mungu aliwajua hawakuendelea kukaa katika nuru ya kiroho ambayo walifurahia mwanzoni. (Gal. 4:9) Acheni tusipuuze kamwe msimamo wetu wenye thamani mbele za Mungu.

5. (a) Ni sifa gani ambazo Mungu anathamini? (b) Tutachunguza mifano gani?

5 Kuna sifa fulani ambazo Yehova anathamini sana. (Zab. 15:1-5; 1 Pet. 3:4) Watu fulani ambao Mungu aliwajua walikuwa na sifa ya imani na unyenyekevu. Acheni tuchunguze mifano ya wanaume wawili ili tuone jinsi sifa hizo zilivyofanya Yehova awapende. Tutachunguza pia kisa cha mwanamume fulani ambaye alifikiri kwamba Mungu anamjua lakini akawa na kiburi na baadaye akagundua kwamba Yehova alikuwa amemkataa. Tunaweza kujifunza masomo ya maana kutokana na mifano hiyo.

Baba ya Wale Walio na Imani

6. (a) Abrahamu alionyesha jinsi gani imani katika ahadi za Yehova? (b) Yehova alimjua Abrahamu jinsi gani?

6 Abrahamu ni mwanamume ambaye ‘alikuwa na imani katika Yehova.’ Kwa kweli, anaitwa “baba ya wale wote walio na imani.” (Mwa. 15:6; Rom. 4:11) Kwa imani, Abrahamu aliacha nyumba yake, marafiki wake, na mali zake na kwenda kwenye nchi ya mbali. (Mwa. 12:1-4; Ebr. 11:8-10) Bado imani ya Abrahamu ilikuwa yenye nguvu miaka mingi baadaye. Hilo lilionekana wazi wakati ilikuwa ni “kana kwamba alimtoa Isaka” mwana wake kwa kutii amri ya Yehova. (Ebr. 11:17-19) Abrahamu alionyesha imani katika ahadi za Yehova, hivyo, Mungu alimwona kuwa mtu wa pekee; kwa kweli alimjua Abrahamu. (Soma Mwanzo 18:19.) Yehova hakujua tu kwamba kulikuwa na mtu aliyeitwa Abrahamu; alimpenda sana Abrahamu kama rafiki.—Yak. 2:22, 23.

7. Ni jambo gani la maana tunalopaswa kujua kuhusu kutimizwa kwa ahadi za Yehova, na jambo hilo lilimsaidia Abrahamu jinsi gani?

7 Ni jambo la maana kujua kwamba wakati wa maisha yake, Abrahamu hakupokea urithi wa nchi ambayo alikuwa ameahidiwa. Pia, hakuona uzao wake ukiwa “kama chembe za mchanga zilizo kando ya bahari.” (Mwa. 22:17, 18) Ingawa ahadi hizo hazikutimizwa wakati wa maisha ya Abrahamu, alidumisha imani yenye nguvu katika Yehova. Alijua kwamba Mungu akisema jambo, ni kana kwamba tayari limetendeka. Ndiyo, Abrahamu aliishi kulingana na imani hiyo. (Soma Waebrania 11:13.) Je, Yehova anatujua kuwa watu wenye imani kama ya Abrahamu?

Tunaonyesha Kwamba Tuna Imani Tunapomngojea Yehova

8. Ni mambo gani yanayofaa ambayo wengi wanatamani kuona yakitimia?

8 Huenda tunatamani kuona mambo fulani yakitimia. Ni jambo la kawaida na linalofaa kutamani kufunga ndoa, kupata watoto, na kuwa na afya nzuri. Hata hivyo, huenda watu wengi wasipate jambo moja au mambo mengi ambayo wanatamani. Ikiwa ndivyo ilivyo kwetu, tunaweza kuonyesha imani yetu kupitia jinsi tunavyoshughulikia hali hiyo.

9, 10. (a) Watu fulani wamejaribu kutosheleza tamaa zao jinsi gani? (b) Unahisi namna gani kuhusu kutimizwa kwa ahadi za Mungu?

9 Ni jambo lisilo la hekima kama nini kujaribu kutosheleza tamaa hizo kwa njia ambayo ni kinyume na hekima ya Mungu. Hilo linaweza kuharibu hali yetu ya kiroho. Kwa mfano, wengine wamechagua matibabu ambayo yanapingana na mashauri ya Yehova. Wengine wamechagua kazi ya kuajiriwa ambayo inafanya wawe mbali na familia zao au wakose mikutano ya kutaniko. Au namna gani kuhusu kusitawisha uhusiano wa kimapenzi na mtu ambaye si mwamini? Mkristo akichukua hatua kama hiyo, je, kweli anajitahidi kujulikana na Yehova? Yehova angehisi namna gani ikiwa Abrahamu angekosa kuonyesha subira kuhusiana na kutimizwa kwa ahadi ambazo Mungu alimpa? Namna gani ikiwa Abrahamu angechukua hatua ya kuishi tena maisha ya starehe na kujifanyia jina maarufu badala ya kumngojea Yehova? (Linganisha na Mwanzo 11:4.) Je, Yehova angeendelea kumjua kwa njia inayofaa?

10 Ni mambo gani ambayo unatamani sana kuona yakitimizwa? Je, una imani yenye nguvu vya kutosha kumngojea Yehova, ambaye ameahidi kutosheleza tamaa zako zinazofaa? (Zab. 145:16) Kama ilivyokuwa katika kisa cha Abrahamu, huenda ahadi fulani za Mungu zisitimie haraka kama tunavyotaka. Lakini bado Yehova anathamini tunapositawisha imani kama ya Abrahamu na kutenda kulingana nayo. Bila shaka, kufanya hivyo ni kwa faida yetu.—Ebr. 11:6.

Tofauti Kati ya Unyenyekevu na Kiburi

11. Huenda Kora alifurahia mapendeleo gani, na hilo linaonyesha nini kuhusu mtazamo wake kumwelekea Mungu?

11 Musa na Kora wanatofautiana sana inapohusu kuheshimu mpango wa Yehova na maamuzi yake. Matendo yao yanatusaidia kuelewa maoni ya Yehova kuwahusu. Kora alikuwa Mlawi Mkohathi, na alifurahia mapendeleo mengi, ambayo inaelekea yalitia ndani kuona Yehova akikomboa taifa la Israeli kupitia Bahari Nyekundu, kuunga mkono hatua ya Yehova ya kuwahukumu Waisraeli waliokosa kutii kwenye Mlima Sinai, na kushiriki katika kusafirisha sanduku la agano. (Kut. 32:26-29; Hes. 3:30, 31) Inaonekana kwamba alikuwa mshikamanifu kwa Yehova kwa miaka mingi na hivyo aliheshimiwa na watu wengi katika kambi ya Waisraeli.

12. Kama inavyoonyeshwa na picha kwenye ukurasa wa 28, kiburi kilikuwa na matokeo gani juu ya uhusiano wa Kora na Mungu?

12 Hata hivyo, taifa la Israeli lilipokuwa njiani kuelekea kwenye Nchi ya Ahadi, Kora aliona mambo ambayo alifikiri kwamba yalikuwa makosa katika mpango wa Mungu. Kisha, wanaume wengine 250 walioongoza katika taifa hilo wakajiunga na Kora katika kujaribu kufanya marekebisho. Ni lazima iwe kwamba Kora na wale watu wengine walihisi kwamba uhusiano wao pamoja na Yehova hauwezi kuharibika. Walimwambia Musa hivi: “Imetosha, kwa sababu kusanyiko lote, wote hao ni watakatifu na Yehova yuko katikati yao.” (Hes. 16:1-3) Walikuwa na uhakika kupita kiasi na mtazamo wenye kiburi kama nini! Musa aliwaambia hivi: “Yehova atajulisha ni nani aliye wake.” (Soma Hesabu 16:5.) Kufikia mwisho wa siku iliyofuata, Kora na wote waliokuwa wamemuunga mkono katika kuasi walikuwa wamekufa.—Hes. 16:31-35.

13, 14. Musa alionyesha jinsi gani kwamba alikuwa mnyenyekevu?

13 Kwa upande mwingine, Musa alikuwa “mpole zaidi kuliko watu wote waliokuwa juu ya uso wa nchi.” (Hes. 12:3) Alionyesha upole na unyenyekevu wake kwa kuazimia kufuata mwongozo wa Yehova. (Kut. 7:6; 40:16) Hakuna jambo linaloonyesha kwamba Musa alitilia shaka mara nyingi njia ya Yehova ya kufanya mambo au akakasirika kwa sababu ya kulazimika kufuata maagizo ambayo Yehova alitoa. Kwa mfano, Yehova alitoa amri na maagizo madogo-madogo ambayo yangetumiwa kujenga maskani, kama vile rangi ya uzi na hesabu ya vitanzi ambavyo vingetumiwa kutengeneza vitambaa vya mahema. (Kut. 26:1-6) Ikiwa mwanadamu ambaye ni mwangalizi katika tengenezo la Yehova anakupatia maagizo ambayo yanaonekana kuwa na mambo mengi kupita kiasi, huenda nyakati fulani ukavunjika moyo. Hata hivyo, Yehova ni mwangalizi mkamilifu, ambaye anawapa wengine mapendeleo kwa ukarimu na anawaamini watumishi wake. Anapotoa maagizo mengi, anafanya hivyo akiwa na sababu nzuri. Hata hivyo, ona kwamba Musa hakumkasirikia Yehova kwa sababu ya kumpa maagizo mengi, kana kwamba Yehova alimdharau au kumzuia asitumie uwezo wake wa kufikiri au kumnyima uhuru. Badala yake, Musa alihakikisha kwamba wafanyakazi “walifanya vivyo hivyo” katika kufuata miongozo ya Mungu. (Kut. 39:32) Alionyesha unyenyekevu kama nini! Musa alitambua kwamba ilikuwa kazi ya Yehova na kwamba alikuwa tu chombo cha kutumiwa kufanya kazi hiyo.

14 Unyenyekevu wa Musa ulionekana pia alipopambana na hali zisizofaa ambazo zilimhusu kibinafsi. Pindi moja, Musa alishindwa kujizuia na hivyo akakosa kumtakasa Mungu alipokuwa akishughulika na watu waliokuwa wakilalamika. Matokeo ni kwamba Yehova alimwambia Musa kuwa hangewaingiza watu hao katika Nchi ya Ahadi. (Hes. 20:2-12) Musa na Haruni, ndugu yake, walikuwa wamevumilia malalamiko ya Waisraeli kwa miaka mingi. Kisha, kwa sababu Musa alikosea katika pindi hiyo moja, hangeona utimizo wa jambo ambalo alikuwa ametazamia kwa muda mrefu sana! Musa alitenda jinsi gani? Ingawa jambo hilo lilimvunja moyo, Musa alikubali uamuzi wa Yehova kwa unyenyekevu. Alijua kwamba Yehova ni Mungu mwadilifu ambaye hana ukosefu wa haki. (Kum. 3:25-27; 32:4) Unapomfikiria Musa, je, huoni kwamba Yehova alimjua?—Soma Hesabu 33:12, 13.

Tunahitaji Unyenyekevu ili Tujitiishe kwa Yehova

15. Tunaweza kujifunza nini kutokana na jinsi Kora alivyotenda kwa kiburi?

15 Maoni yetu kuhusu marekebisho katika kutaniko la Kikristo la ulimwenguni pote na maamuzi yanayofanywa na wale wanaoongoza katika kutaniko hilo yanaamua jinsi Yehova anavyotuona. Kora na wenzake walijitenga na Mungu kwa sababu ya kujiamini kupita kiasi, kuwa na kiburi, na kukosa imani. Ingawa Kora aliona kwamba Musa ambaye alikuwa amezeeka ndiye aliyekuwa akifanya maamuzi siku baada ya siku, kwa kweli ni Yehova aliyekuwa akiliongoza taifa hilo. Kora hakuona jambo hilo la hakika na hivyo akakosa kuonyesha ushikamanifu kwa wale waliokuwa wakitumiwa na Mungu. Lingekuwa jambo la hekima zaidi kwa Kora kumngojea Yehova amsaidie kuelewa mambo vizuri zaidi au kumngojea afanye marekebisho ikiwa kwa kweli yalihitajika. Hivyo, mwishowe Kora aliharibu rekodi yake ya kutumikia kwa uaminifu kwa sababu ya kutenda kwa kiburi!

16. Kuiga mfano wa Musa wa kuwa wanyenyekevu kunaweza kuwa na matokeo gani kuhusu jinsi Yehova anavyotujua?

16 Simulizi hilo linatoa onyo kali kwa wazee na wengine kutanikoni leo. Tunahitaji kuwa wanyenyekevu ili tumngojee Yehova na kufuata mwongozo wa wale waliowekwa rasmi kuongoza. Je, tunaonyesha kwamba sisi ni wanyenyekevu na wenye tabia pole kama Musa alivyokuwa? Je, tunatambua mamlaka ya wale wanaoongoza kati yetu na kutii miongozo tunayopokea? Je, tunaweza kuepuka kuongozwa na hisia zetu za kibinafsi tunapovunjika moyo? Ikiwa ndivyo, Yehova atatujua sisi pia kwa njia inayofaa. Unyenyekevu na ujitiisho wetu utamfanya Yehova atupende.

Yehova Anawajua Watu Wake

17, 18. Ni nini kinachoweza kutusaidia kuendelea kujulikana kuwa watu wa Yehova?

17 Ni jambo lenye faida kufikiria mfano wa wale ambao Yehova aliwavuta na kuwajua kwa njia inayofaa. Abrahamu na Musa hawakuwa wakamilifu na walikuwa na kasoro kama sisi. Hata hivyo, Yehova aliwajua au kuwaona kuwa watu wake. Lakini mfano wa Kora unaonyesha kwamba tunaweza kujiondoa kwa Yehova na hivyo tukose kukubaliwa naye. Ni vizuri kila mmoja wetu ajiulize mwenyewe hivi: ‘Yehova ana maoni gani kunihusu? Ninaweza kujifunza nini kutokana na mifano hiyo ya Biblia?’

18 Unaweza kufarijiwa sana kujua kwamba Yehova anawaona watu waaminifu ambao amewavuta kwake, kuwa ni watu wake. Endelea kusitawisha imani, unyenyekevu, na sifa nyingine ambazo zitafanya Mungu wetu akupende zaidi. Bila shaka, kujulikana na Yehova ni pendeleo lenye thamani ambalo linafanya tutosheke maishani sasa, na litatuletea baraka nzuri ajabu wakati ujao.—Zab. 37:18.

Je, Unakumbuka?

• Ni msimamo gani wenye thamani ambao unaweza kufurahia mbele za Yehova?

• Unaweza kuiga jinsi gani imani ya Abrahamu?

• Ni mambo gani ambayo tunajifunza kutokana na Kora na Musa?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 26]

Je, tunaamini kama Abrahamu kwamba Yehova atatimiza kikamili ahadi zake?

[Picha katika ukurasa wa 28]

Kora hakuwa tayari kutii mwongozo kwa unyenyekevu

[Picha katika ukurasa wa 29]

Je, Yehova anakujua kuwa mtu ambaye ananyenyekea na kutii miongozo?