Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Acheni Tushangilie Pamoja!

Acheni Tushangilie Pamoja!

Acheni Tushangilie Pamoja!

INAZIDI kuwa vigumu sana kupata shangwe na furaha. Inaonekana ni jambo lisilowezekana kwa watu wengi kuzungumza na wengine kuhusu mambo yanayotia moyo. Maisha ya leo, hasa katika majiji makubwa, yanawafanya watu wasichangamane na wengine na hivyo kujitenga.

Profesa wa elimu ya afya ya akili na tabia, Alberto Oliverio, anasema hivi: “Upweke ni hali ya kawaida sana na bila shaka, kuishi katika majengo makubwa yaliyozungukwa na kuta kunawafanya watu wajitenge. Katika hali nyingi, jambo hilo linafanya tumpuuze mfanyakazi mwenzetu, jirani yetu, au karani anayefanya kazi katika sehemu ya kulipia kwenye duka kubwa.” Mara nyingi kujitenga kwa aina hiyo kunafanya watu washuke moyo.

Hata hivyo, hali na mtazamo kati ya Wakristo ni tofauti. Mtume Paulo aliandika hivi: “Shangilieni sikuzote.” (1 The. 5:16) Kuna sababu nyingi zinazoweza kutufanya tufurahi na kushangilia pamoja. Tunamwabudu Mungu Aliye Juu Zaidi, Yehova; tunaelewa ujumbe wa kweli ya Biblia; tuna tumaini la kupata wokovu na uzima wa milele; na tunaweza pia kuwasaidia wengine kupata baraka hizohizo.—Zab. 106:4, 5; Yer. 15:16; Rom. 12:12.

Kushangilia na kushiriki furaha hiyo na wengine ni sifa zinazowatambulisha Wakristo wa kweli. Hivyo, haishangazi kwamba Paulo aliwaandikia Wafilipi hivi: “Mimi nafurahi na kushangilia pamoja nanyi nyote. Basi katika njia hiyohiyo ninyi wenyewe furahini pia na kushangilia pamoja nami.” (Flp. 2:17, 18) Katika maneno hayo machache tu Paulo anataja mara mbili kuhusu kuwa na furaha na kushangilia pamoja na wengine.

Bila shaka, Wakristo wanahitaji kuwa waangalifu ili kuepuka mwelekeo wowote wa kujitenga. Hakuna mtu anayejitenga na wengine anayeweza kushangilia na waamini wenzake. Basi tunaweza jinsi gani kufuata himizo la Paulo la ‘kuendelea kushangilia katika Bwana’ pamoja na ndugu zetu?—Flp. 3:1.

Shangilia Pamoja na Waamini Wenzako

Paulo alipoandika barua yake kwa Wafilipi, huenda alikuwa mfungwa huko Roma kwa sababu ya kazi yake ya kuhubiri. (Flp. 1:7; 4:22) Hata hivyo, kifungo hicho hakikupunguza shangwe yake kuelekea huduma. Badala yake, alifurahia kumtumikia Yehova kwa ukamili kadiri alivyoweza na ‘kumiminwa kama toleo la kinywaji.’ (Flp. 2:17) Mtazamo wa Paulo unaonyesha kuwa shangwe haitegemei hali za mtu. Ingawa alikuwa kifungoni, alisema: “Nitaendelea pia kushangilia.”—Flp. 1:18.

Paulo alikuwa ameanzisha kutaniko huko Filipi na aliwapenda sana ndugu zake katika kutaniko hilo. Alijua kwamba kuwaeleza wengine kuhusu shangwe aliyopata katika utumishi wake kwa Yehova kungewatia moyo pia. Hivyo, aliandika hivi: “Basi nataka mjue, akina ndugu, kwamba mambo yangu yamegeuka na kuwa yenye kuendeleza mbele habari njema badala ya kuwa kinyume, hivi kwamba vifungo vyangu vimejulikana kwa watu wote kwa kushirikiana na Kristo kati ya Walinzi wote wa Mfalme na wale wengine wote.” (Flp. 1:12, 13) Njia moja ambayo Paulo alifurahi na kushangilia pamoja na ndugu zake ilikuwa kuwaeleza jambo hilo lenye kutia moyo. Ni wazi kwamba Wafilipi pia walishangilia pamoja na Paulo. Hata hivyo, ili washangilie pamoja naye hawakupaswa kuvunjika moyo kwa sababu ya mambo ambayo Paulo alikuwa akikabili. Badala yake, walihitaji kuiga mfano wake. (Flp. 1:14; 3:17) Zaidi ya hayo, Wafilipi wangeendelea kumtaja Paulo katika sala zao na kumpa msaada na utegemezo wowote ambao wangeweza kutoa.—Flp. 1:19; 4:14-16.

Je, tunaonyesha roho ileile ya shangwe kama Paulo alivyofanya? Je, tunajitahidi kuona mambo mazuri katika hali zetu maishani na katika huduma yetu ya Kikristo? Tunaposhirikiana na ndugu zetu, ni vizuri kushangilia kuhusu kazi ya kutoa ushahidi. Hatupaswi kungojea mpaka tupate jambo lililoonwa lenye kusisimua ili tufanye hivyo. Huenda tuliweza kumchochea mtu fulani apendezwe na ujumbe wa Ufalme kwa kutumia utangulizi fulani wenye matokeo mazuri au kwa kutoa hoja nzuri. Labda tulikuwa na mazungumzo mazuri na mwenye nyumba kuhusu andiko fulani la Biblia. Au huenda watu katika eneo walitambua kuwa sisi ni Mashahidi wa Yehova, na jambo hilo pekee likatoa ushahidi mzuri. Kusimulia mambo kama hayo ni njia ya kushangilia pamoja na wengine.

Watu wengi wa Yehova wamejidhabihu na wanaendelea kujidhabihu ili kutimiza kazi ya kuhubiri. Mapainia, waangalizi wanaosafiri, Wanabetheli, wamishonari, na watumishi wa kimataifa wanajidhabihu kabisa katika utumishi wa wakati wote na wanashangilia wanapofanya hivyo. Je, tunafurahi na kushangilia pamoja nao? Basi, acheni tuonyeshe kwamba tunawathamini ‘wafanyakazi hao wenzetu wapendwa kwa ajili ya ufalme wa Mungu.’ (Kol. 4:11) Tunapokuwa pamoja kwenye mikutano ya kutaniko au makusanyiko makubwa ya Kikristo, tunaweza kuwatia moyo kwa uchangamfu. Tunaweza pia kuiga bidii yao. Tunaweza kutafuta “nafasi” ya kusikiliza mambo waliyoona na mambo yenye kujenga kwa kuwakaribisha nyumbani mwetu, na labda kula nao chakula.—Flp. 4:10.

Shangilia Pamoja na Wale Wanaokabili Majaribu

Kuvumilia mateso na kushinda majaribu kulitia nguvu azimio la Paulo la kuendelea kubaki mwaminifu kwa Yehova. (Kol. 1:24; Yak. 1:2, 3) Kujua kwamba akina ndugu huko Filipi huenda wangekabili majaribu kama yake na kwamba wangetiwa moyo na uvumilivu wake kulimpa sababu ya kufurahi na kushangilia pamoja nao. Hivyo, aliandika hivi: “Ninyi mlipewa pendeleo kwa ajili ya Kristo, si muwe tu na imani katika yeye, bali pia mteseke kwa ajili yake. Kwa maana ninyi mna pambano lilelile kama mlivyoona kunihusu mimi na kama mnavyosikia sasa kunihusu mimi.”—Flp. 1:29, 30.

Vivyo hivyo leo, Wakristo wanapingwa kwa sababu ya kazi yao ya kutoa ushahidi. Nyakati nyingine wanapingwa kwa kutendewa kijeuri, lakini mara nyingi upinzani huo si wa moja kwa moja. Mateso hayo yanaweza kuwa ni mashtaka ya uwongo kutoka kwa waasi-imani, kuchukiwa na watu wa familia, kudhihakiwa na wafanyakazi au wanafunzi wenzetu. Yesu alionya kwamba majaribu hayo hayapaswi kutushangaza wala kutuvunja moyo. Badala yake, ni sababu ya kushangilia. Alisema hivi: “Wenye furaha ni ninyi wakati watu wanapowashutumu na kuwatesa na kusema kwa uwongo kila namna ya jambo baya juu yenu kwa ajili yangu. Shangilieni na kuruka kwa shangwe, kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni.”—Mt. 5:11, 12.

Hatupaswi kutishwa au kuogopa tunaposikia kwamba ndugu zetu wanateswa vikali katika nchi fulani. Badala yake, tunapaswa kushangilia kwa sababu ya uvumilivu wao. Tunaweza kusali kwa ajili yao na kumwomba Yehova atie nguvu imani yao ili waendelee kuvumilia. (Flp. 1:3, 4) Ingawa tunaweza kufanya machache kwa ajili ya ndugu hao wapendwa, tunaweza kuwasaidia sana ndugu walio katika kutaniko letu ambao wanakabili majaribu. Tunaweza kupendezwa nao na kuwategemeza. Tunaweza kutafuta nafasi mbalimbali za kushangilia pamoja nao kwa kuwaalika mara kwa mara ili wajiunge nasi wakati wa jioni ya Ibada yetu ya Familia, kuhubiri nao, na kutumia wakati pamoja nao katika tafrija.

Tuna sababu nyingi za kushangilia pamoja! Acheni tupinge roho ya kujitenga ya ulimwengu huu na kuendelea kushiriki shangwe yetu pamoja na ndugu zetu. Tukifanya hivyo, hatutachangia tu upendo na umoja wa kutaniko bali pia tutafurahia undugu wa Kikristo kwa ukamili. (Flp. 2:1, 2) Ndiyo, ‘shangilia sikuzote katika Bwana,’ kwa kuwa Paulo anatuhimiza hivi: “Mara nyingine tena nitasema, Shangilieni!”—Flp. 4:4.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 6]

Globe: Courtesy of Replogle Globes