Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mashauri ya Hekima Kuhusu Useja na Ndoa

Mashauri ya Hekima Kuhusu Useja na Ndoa

Mashauri ya Hekima Kuhusu Useja na Ndoa

“Nasema jambo hili . . . ili niwasukume ninyi kwenye lile linalofaa na lile linalomaanisha kumhudumia Bwana daima bila kukengeushwa fikira.”—1 KOR. 7:35.

1, 2. Kwa nini mtu anapaswa kutafuta mashauri ya Biblia kuhusu useja na ndoa?

KUSHUGHULIKA na watu wa jinsia tofauti ni kati ya mambo machache maishani ambayo yanaleta furaha, mahangaiko, au kuvunja moyo. Kwa kuwa tunahitaji kupambana ifaavyo na hisia hizo tofauti-tofauti, hiyo ni sababu nzuri ya kutufanya tutafute mwongozo wa Mungu. Mkristo ambaye ametosheka kuwa mseja huenda akahisi kwamba familia au marafiki wake wanamsukuma aoe au aolewe. Huenda mwingine anapenda kuoa au kuolewa lakini bado hajapata mwenzi wa ndoa anayefaa. Wengine wanahitaji mwongozo ili kujitayarisha kutimiza madaraka ya mume au mke. Na Wakristo wote waseja na wale waliofunga ndoa wanajaribiwa kuhusiana na maadili yanayohusu ngono.

2 Hali hizo zinaweza kutufanya tupoteze furaha na pia msimamo wetu mzuri mbele za Yehova Mungu. Katika sura ya 7 ya barua yake ya kwanza kwa Wakorintho, Paulo alitoa mwongozo kuhusu useja na ndoa. Kusudi lake lilikuwa kuwachochea wasomaji wake kwenye “lile linalofaa na lile linalomaanisha kumhudumia Bwana daima bila kukengeushwa fikira.” (1 Kor. 7:35) Unapofikiria mashauri yake kuhusu mambo hayo ya maana, jitahidi kuona hali yako kuwa nafasi ya kumtumikia Yehova kikamili zaidi, iwe wewe ni mseja au umefunga ndoa.

Uamuzi Mzito wa Kibinafsi

3, 4. (a) Nyakati nyingine, ni matatizo gani yanayoweza kutokea ikiwa marafiki au watu wa ukoo wanamsukuma mtu afunge ndoa? (b) Shauri la Paulo linaweza kutusaidia jinsi gani kuwa na maoni yenye usawaziko kuhusu ndoa?

3 Kama Wayahudi wa karne ya kwanza, tamaduni nyingi leo zinakazia kwamba ni jambo la maana sana kufunga ndoa. Ikiwa kijana mwanamume au mwanamke anapita umri fulani bila kufunga ndoa, huenda marafiki na watu wa ukoo wenye kujali wakahisi kwamba wanapaswa kumpa mashauri fulani. Katika mazungumzo, huenda wakapendekeza kwamba atafute mwenzi wa ndoa kwa bidii zaidi. Huenda wakamdokezea kuhusu mtu fulani wa jinsia tofauti ambaye anaweza kuwa mwenzi mzuri wa ndoa. Wanaweza hata kutumia njia za werevu ili kuwakutanisha waseja wawili. Nyakati nyingine matendo hayo yanaweza kusababisha aibu, kuharibu urafiki, na kuumiza hisia.

4 Paulo hakuwasukuma kamwe wengine wafunge ndoa au wabaki waseja. (1 Kor. 7:7) Paulo alitosheka kumtumikia Yehova bila mke, lakini aliheshimu haki ya wengine ya kufurahia ndoa. Leo pia, kila Mkristo ana haki ya kujiamulia mwenyewe kufunga ndoa au kubaki mseja. Wengine hawapaswi kuwasukuma waseja wafunge ndoa au wasifunge ndoa.

Jinsi ya Kufanikiwa Ukiwa Mseja

5, 6. Kwa nini Paulo aliwatia moyo Wakristo wabaki waseja?

5 Jambo la maana kuhusu maneno ya Paulo kwa Wakorintho ni kwamba alikuwa na maoni yanayofaa kuelekea useja. (Soma 1 Wakorintho 7:8.) Ingawa Paulo hakuoa, hakujiona kuwa bora kuliko wale ambao walikuwa wamefunga ndoa, kama wanavyofanya makasisi waseja wa dini zinazodai kuwa za Kikristo. Badala yake, mtume Paulo alikazia faida ambayo wahudumu wengi wa habari njema ambao ni waseja wanafurahia. Ni faida gani hiyo?

6 Mara nyingi Mkristo mseja anaweza kukubali migawo ambayo huenda mtu aliyefunga ndoa hawezi kukubali katika utumishi wa Yehova. Paulo alipata pendeleo la pekee akiwa “mtume kwa mataifa.” (Rom. 11:13) Soma Matendo sura ya 13 mpaka 20, na uambatane naye pamoja na wamishonari wenzake wanapoenda kuhubiri katika maeneo mapya na kuanzisha makutaniko katika sehemu mbalimbali. Katika utumishi wake, Paulo alivumilia matatizo ambayo watu wengi hawatawahi kamwe kupatwa nayo. (2 Kor. 11:23-27, 32, 33) Lakini shangwe aliyopata kwa kuwasaidia watu wengi wawe wanafunzi ilikuwa kubwa kuliko matatizo yaliyompata. (1 The. 1:2-7, 9; 2:19) Je, angeweza kutimiza mambo yote aliyotimiza ikiwa angekuwa ameoa au kuwa na familia? Labda hangeweza.

7. Toa mfano wa Mashahidi waseja ambao wametumia hali yao ya useja kuendeleza kazi ya Ufalme.

7 Wakristo wengi waseja wanatumia hali yao ya useja kutimiza mengi katika kazi ya Ufalme. Sara na Limbania, ambao ni mapainia waseja huko Bolivia, walihamia katika kijiji ambacho hakikuwa kimehubiriwa kwa miaka mingi. Je, ukosefu wa umeme ungekuwa tatizo kwao? Walisema hivi: “Hakuna redio au televisheni, hivyo watu hawakengeushwi wasifanye jambo wanalopenda kufanya wanapostarehe, yaani, kusoma.” Wanakijiji fulani waliwaonyesha mapainia hao vitabu mbalimbali vya Mashahidi wa Yehova ambavyo walikuwa bado wanasoma lakini vitabu hivyo havichapishwi tena. Dada hao walipata watu wanaopendezwa katika karibu kila nyumba, hivi kwamba hawakuweza kuwatembelea watu wote katika eneo hilo. Mwanamke mmoja mzee aliwaambia hivi: “Lazima mwisho uwe umekaribia kwa sababu Mashahidi wa Yehova wametufikia hatimaye.” Baada ya muda mfupi, watu fulani katika kijiji hicho walianza kuhudhuria mikutano ya kutaniko.

8, 9. (a) Kwa nini Paulo alisema kwamba ni vizuri mtu amtumikie Mungu akiwa mseja? (b) Kuna faida gani za kuwa Mkristo mseja?

8 Bila shaka, Wakristo waliofunga ndoa pia wanapata matokeo mazuri wanapohubiri habari njema katika maeneo magumu. Lakini migawo fulani ambayo waseja wanaweza kukubali huenda ikawa migumu kwa Wakristo waliofunga ndoa au walio na watoto. Paulo alifikiria nafasi nzuri aliyokuwa nayo ya kueneza habari njema katika makutaniko yaliyokuwa katika eneo lao. Alitaka wote wawe na shangwe kama yeye. Ndiyo sababu Paulo alisema kwamba ni vizuri mtu amtumikie Yehova akiwa mseja.

9 Dada mmoja mseja kutoka Marekani ambaye ni painia aliandika hivi: “Watu fulani wanaamini kwamba waseja hawawezi kupata furaha. Lakini nimeona kwamba furaha ya kudumu inategemea uhusiano wa mtu pamoja na Yehova. Ingawa maisha ya useja ni ya kujidhabihu, ni zawadi nzuri ajabu ukiitumia vizuri.” Aliandika hivi kuhusu kupata furaha: “Badala ya kumzuia mtu kupata furaha, useja unaweza kumsaidia kupata furaha. Ninajua kwamba Yehova anawapenda kwa wororo watu wote, waseja na waliofunga ndoa.” Sasa dada huyo anatumikia kwa furaha katika nchi ambayo ina uhitaji mkubwa zaidi wa wahubiri wa Ufalme. Ikiwa wewe ni mseja, je, unaweza kutumia uhuru wako kuongeza wakati unaoshiriki katika kazi ya kuwafundisha wengine kweli? Ukifanya hivyo, Wewe pia unaweza kujionea kwamba useja ni zawadi yenye thamani sana kutoka kwa Yehova.

Waseja Ambao Wanatamani Kufunga Ndoa

10, 11. Yehova anawategemeza jinsi gani wale ambao wangependa kuoa au kuolewa lakini hawajapata mwenzi wa ndoa anayefaa?

10 Baada ya kukaa kwa muda fulani wakiwa waseja, watumishi wengi waaminifu wa Yehova wanaamua kutafuta mwenzi wa ndoa. Kwa kuwa wanatambua kwamba wanahitaji mwongozo, wanamwomba Yehova awasaidie kupata mwenzi wa ndoa anayefaa.—Soma 1 Wakorintho 7:36.

11 Ikiwa unatumaini kuoa au kuolewa na mtu aliye na tamaa kama yako ya kumtumikia Yehova kwa nafsi yote, mwambie Yehova jambo hilo katika sala. (Flp. 4:6, 7) Hata ukilazimika kungoja kwa muda mrefu kadiri gani, usivunjike moyo. Mtumaini Mungu wetu mwenye upendo akiwa Msaidizi wako, naye atakutegemeza kihisia kulingana na uhitaji wako.—Ebr. 13:6.

12. Kwa nini Mkristo anapaswa kuwa mwangalifu anapoombwa uchumba?

12 Mkristo mseja ambaye anatamani kufunga ndoa anaweza kuombwa uchumba na mtu ambaye hana hali nzuri sana ya kiroho au hata mtu asiye mwamini. Ukijikuta katika hali hiyo, kumbuka kwamba maumivu yanayosababishwa na kumchagua mwenzi asiyefaa wa ndoa yanaweza kuwa mabaya zaidi kuliko maumivu yanayosababishwa na tamaa ya kuoa au kuolewa ambayo mtu anahisi akiwa mseja. Na mara tu baada ya kufunga ndoa na kuapa kukaa pamoja katika hali nzuri au mbaya, umefungwa kwa mwenzi wako wa ndoa muda wote wa maisha yako. (1 Kor. 7:27) Usihangaike kupita kiasi na kufanya uamuzi wa kufunga ndoa ambao utakufanya ujute baadaye.—Soma 1 Wakorintho 7:39.

Jitayarishe Kukabiliana na Hali Halisi ya Maisha ya Ndoa

13-15. Wakati wa uchumba, watu wanaotaka kufunga ndoa wanapaswa kuzungumzia mambo gani ambayo yanaweza kusababisha dhiki katika ndoa?

13 Ingawa Paulo alisema ni vizuri zaidi kumtumikia Yehova tukiwa waseja, hakuwadharau wale ambao waliamua kuoa au kuolewa. Badala yake, shauri lake lililoongozwa na roho ya Mungu linawasaidia wenzi wa ndoa kukabiliana na hali halisi ya maisha ya ndoa na kufanya kifungo chao kidumu.

14 Wenzi fulani wa ndoa wanahitaji kubadili matarajio yao ya wakati ujao. Watu wawili wanapochumbiana, huenda wakafikiri kwamba upendo wao ni wa pekee, si wa kawaida, na kwamba daima wataishi kwa raha katika ndoa. Wanaanza maisha yao ya ndoa wakichochewa na hisia hizo za raha huku wakiamini kwamba hakuna kitu chochote ambacho kinaweza kamwe kuharibu furaha yao. Mawazo kama hayo si ya kweli. Hisia za mapenzi katika maisha ya ndoa zinafurahisha sana, lakini hisia hizo peke yake hazimtayarishi bwana na bibi-arusi kukabiliana na dhiki ambayo iko katika kila ndoa.—Soma 1 Wakorintho 7:28. *

15 Baada tu ya kufunga ndoa, wenzi wengi wanashangaa au hata wanavunjika moyo wanapokosana kwa sababu ya mambo ya maana. Huenda wenzi hao wawili wakajikuta wakikosana kuhusu jinsi wanavyopaswa kutumia pesa au muda wa mapumziko, kuhusu mahali pa kuishi, na pia mara ambazo wanapaswa kuwatembelea wakwe zao. Na kila mmoja wao ana kasoro za utu ambazo zinaweza kumuudhi mwenzi wake. Wakati wa uchumba, ni rahisi kutoona mambo hayo kuwa mazito, lakini baadaye yanaweza kusababisha mkazo mkubwa katika ndoa. Kabla ya kufunga ndoa, ni vizuri watu hao wawili watatue mambo yanayofanya wakosane.

16. Kwa nini watu wanaochumbiana wanapaswa kukubaliana kuhusu jinsi ya kupambana na matatizo katika maisha ya ndoa?

16 Ili wafanikiwe na kuwa na furaha, ni lazima watu wanaochumbiana washughulikie pamoja matatizo yao. Wanapaswa kukubaliana kuhusu jinsi ya kuwatia watoto nidhamu na jinsi ya kuwatunza wazazi waliozeeka. Wenzi wa ndoa hawapaswi kuruhusu mikazo inayosababishwa na matatizo ya familia iwatenganishe. Kwa kufuata mashauri ya Biblia, watatatua matatizo mengi, watavumilia matatizo ambayo hawawezi kutatua, na kuishi pamoja kwa furaha.—1 Kor. 7:10, 11.

17. Wenzi wa ndoa wanapaswa kutazamia kwamba ‘watahangaikia mambo gani ya ulimwengu’?

17 Katika andiko la 1 Wakorintho 7:32-34 (Soma), Paulo anataja hali nyingine ambayo inatokea katika ndoa. Watu waliofunga ndoa wanalazimika ‘kuhangaikia mambo ya ulimwengu,’ kama vile chakula, mavazi, makao, na mambo mengine ambayo si ya kiroho. Kwa nini? Huenda ndugu alitumia nguvu na wakati wake mwingi katika huduma alipokuwa mseja. Lakini akiwa mume, anatambua kwamba ni lazima atumie sehemu fulani ya wakati na nguvu hizo kumtunza mke wake na hivyo kupata kibali chake. Mke naye anafanya vivyo hivyo kuelekea mume wake. Kwa hekima yake, Yehova anatambua kwamba tunahitaji kufanya hivyo. Anajua kwamba mara nyingi ili ndoa ifanikiwe ni lazima mume na mke watumie kiasi fulani cha wakati na nguvu ambazo walitumia katika utumishi Wake wakiwa waseja ili kuboresha ndoa yao.

18. Huenda wengine wakahitaji kufanya marekebisho gani kuhusu kushirikiana na marafiki baada ya kufunga ndoa?

18 Lakini kuna mengi zaidi ya kujifunza. Ikiwa wenzi wa ndoa wanalazimika kutumia nguvu na kiasi fulani cha wakati ambacho walitumia katika utumishi wa Mungu ili kutunzana, je, hawapaswi kutumia vivyo hivyo nguvu na wakati ambao wakiwa waseja, walitumia kuwa pamoja na marafiki wao? Mke atahisi jinsi gani ikiwa mume wake bado anaendelea kujishughulisha katika michezo pamoja na marafiki wake? Au huenda mume akahisi jinsi gani ikiwa mke atatumia wakati mwingi sana katika michezo pamoja na marafiki wake? Muda si muda, huenda mwenzi aliyepuuzwa akahisi upweke, akakosa furaha, na kuhisi kwamba hapendwi. Wale wanaofunga ndoa wanaweza kuepuka hali hiyo kwa kufanya yote wanayoweza kutia nguvu kifungo chao wakiwa mume na mke.—Efe. 5:31.

Yehova Anataka Tuwe na Maadili Safi

19, 20. (a) Kwa nini watu waliofunga ndoa wanaweza kushawishiwa kutumbukia katika upotovu wa maadili? (b) Wenzi wa ndoa wanaweza kujikuta katika hatari gani wakikaa mbali na wenzi wao kwa muda mrefu?

19 Watumishi wa Yehova wameazimia kuendelea kuwa na maadili safi. Wengine wao wanaamua kufunga ndoa ili waepuke upotovu wa maadili. Hata hivyo, kufunga ndoa tu hakumlindi mtu asitumbukie katika uchafu wa kingono. Katika nyakati za Biblia, jiji lenye kuta liliwalinda tu watu waliobaki ndani yake. Ikiwa mtu angetoka nje ya lango la jiji wakati wanyang’anyi na wavamizi walipokuwa wakitembea huku na huku, angeweza kuibiwa au kuuawa. Vivyo hivyo, watu waliofunga ndoa wanaweza kulindwa kutokana na upotovu wa maadili ikiwa tu watatii sheria na mipaka ambayo Mwanzilishi wa ndoa ameweka kwa ajili ya waliofunga ndoa.

20 Paulo alieleza kuhusu mipaka hiyo katika andiko la 1 Wakorintho 7:2-5. Mke ana haki ya kuwa na mahusiano ya ngono na mume wake peke yake; vivyo hivyo mume ana haki ya kuwa na mahusiano hayo na mke wake. Kila mmoja anatazamiwa kumpa mwenzi wake “haki” ya ndoa, au mahusiano ya kingono ambayo mtu aliyefunga ndoa ana haki ya kupata. Hata hivyo, waume na wake fulani wanakaa mbali na wenzi wao kwa muda mrefu, huku kila mmoja wao akienda likizo peke yake au akikaa mbali na mwenzi wake kwa sababu ya kazi ya kimwili, na hivyo wananyimana “haki” ya ndoa. Wazia msiba unaoweza kutokea ikiwa mtu anashawishiwa na Shetani kufanya uzinzi kwa sababu ya “kukosa kujizuia.” Yehova anabariki vichwa vya familia ambao wanaziandalia familia zao mahitaji ya kimwili bila kuhatarisha ndoa zao.—Zab. 37:25.

Faida za Kutii Mashauri ya Biblia

21. (a) Kwa nini ni vigumu kufanya uamuzi wa kuwa mseja au kufunga ndoa? (b) Kwa nini mashauri yaliyo katika 1 Wakorintho sura ya 7 yana faida?

21 Maamuzi kuhusu useja na ndoa ni kati ya maamuzi magumu zaidi ambayo mtu anaweza kufanya. Ukiamua kufunga ndoa au kubaki mseja, bado utakabili matatizo kwa sababu kila mtu si mkamilifu. Na hata ingawa Yehova anawabariki watu wake, nyakati nyingine watakatishwa tamaa na mambo yanayotukia katika maisha yao. Ukifuata mashauri ya hekima yaliyo katika 1 Wakorintho 7, unaweza kupunguza matatizo kama hayo. Ukifanya hivyo, utakuwa ‘umefanya vema’ machoni pa Yehova, uwe mseja au uwe umefunga ndoa. (Soma 1 Wakorintho 7:37, 38.) Kupata kibali cha Mungu ndio mradi mkubwa zaidi ambao unaweza kufikia. Ukiwa na kibali cha Mungu, utaendelea kusonga mbele kuelekea uzima katika ulimwengu wake mpya. Katika ulimwengu huo, wanaume na wanawake hawatakuwa na mikazo na matatizo ambayo ni ya kawaida leo.

[Maelezo ya Chini]

Je, Unaweza Kujibu?

• Kwa nini mtu yeyote hapaswi kumsukuma mwingine afunge ndoa?

• Ni njia gani nzuri zaidi unayoweza kutumia wakati wako kumtumikia Yehova ukiwa mseja?

• Watu wanaochumbiana wanaweza jinsi gani kujitayarisha kupambana na matatizo katika ndoa?

• Kwa nini kufunga ndoa tu hakumlindi mtu asitumbukie katika upotovu wa maadili katika ngono?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 14]

Wakristo waseja ambao wanatumia wakati wao kuongeza huduma yao wanapata shangwe

[Picha katika ukurasa wa 16]

Huenda wengine wakahitaji kufanya marekebisho gani baada ya kufunga ndoa?