Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Ninapaswa kufanya nini nikiwa na swali kuhusu jambo fulani katika Biblia au ninapohitaji mashauri kuhusu tatizo la kibinafsi?

Andiko la Methali 2:1-5 linamhimiza kila mmoja wetu ‘aendelee kuutafuta’ uelewaji na utambuzi kana kwamba anatafuta “hazina zilizofichika.” Hilo linaonyesha kwamba tunapaswa kujitahidi kabisa kufanya utafiti kuhusu maswali yetu ya Biblia na kutafuta suluhisho kwa matatizo yetu. Tunaweza kufanya hivyo jinsi gani?

Katika ukurasa wa 33 mpaka wa 38, kitabu Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi kinazungumza kuhusu “Jinsi ya Kufanya Utafiti” kwa kutumia vifaa ambavyo tumeandaliwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mt. 24:45) Ukurasa wa 36 unaeleza jinsi ya kutumia Fahirisi. Na katika kila Fahirisi kuna sehemu yenye kichwa, fahirisi ya habari na sehemu yenye kichwa, fahirisi ya maandiko. Sehemu hizo zinafanya iwe rahisi kutafuta habari kwa kutumia maneno makuu au mistari ya Biblia. Na chini ya sehemu hizo utapata orodha ya marejeo ambayo unaweza kusoma. Uwe na subira unapotafuta jibu au mwongozo fulani ambao unahitaji. Kumbuka kwamba unatafuta “hazina zilizofichika,” na wakati na jitihada zinahitajiwa ili kuzipata.

Bila shaka, kuna habari fulani na maandiko ambayo hayajazungumziwa moja kwa moja katika vitabu vyetu. Na hata ikiwa tumezungumzia andiko fulani la Biblia, huenda hatujazungumzia swali hususa ambalo unatafuta jibu lake. Pia, masimulizi fulani ya Biblia yanatokeza maswali kwa sababu Maandiko hayataji mambo yote kwa undani. Hivyo, hatuwezi kupata jibu la moja kwa moja kwa kila swali ambalo linaulizwa. Katika hali kama hiyo, tunapaswa kuepuka kukisia kuhusu mambo ambayo hayawezi kujibiwa, kama sivyo tutaanza kuzozana kuhusu “maswali ya utafiti badala ya kugawa kitu chochote kutoka kwa Mungu kuhusiana na imani.” (1 Tim. 1:4; 2 Tim. 2:23; Tito 3:9) Iwe ni ofisi ya tawi, au makao makuu ya ulimwenguni pote, haiwezi kuchanganua na kujibu maswali yote kama hayo ambayo hayajazungumziwa katika vitabu vyetu. Tunaweza kutosheka kwamba Biblia inatupatia habari za kutosha ili kutuongoza maishani lakini pia haielezi kwa undani kila jambo na hivyo tunahitaji kuonyesha imani yenye nguvu katika Mungu ambaye ni Mtungaji wake.—Ona ukurasa wa 185 mpaka 187 wa kitabu Mkaribie Yehova.

Namna gani ikiwa umejitahidi kadiri unavyoweza kutafuta habari fulani ambayo inakuhusu wewe binafsi lakini bado hujapata mwongozo au suluhisho unalohitaji? Jihisi huru kuzungumza na mwamini mwenzako mkomavu, labda mzee wa kutaniko lenu. Wana ujuzi mwingi wa Biblia na pia uzoefu katika maisha ya Kikristo. Msaada wao wenye usawaziko utakufaa hasa ikiwa unahitaji mashauri kuhusu tatizo au uamuzi wa kibinafsi kwa kuwa wanakujua na wako karibu nawe na wanaelewa hali zako. Na usisahau kamwe kusali kwa Yehova na kumweleza waziwazi mahangaiko yako na umwombe aongoze fikira zako kupitia roho yake takatifu, “kwa maana Yehova mwenyewe anatoa hekima . . . na utambuzi.”—Met. 2:6; Luka 11:13.