Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nimefurahia Kumtumikia Yehova

Nimefurahia Kumtumikia Yehova

Nimefurahia Kumtumikia Yehova

Limesimuliwa na Fred Rusk

Nilijionea mapema maishani ukweli wa maneno ya Daudi yaliyo katika Zaburi 27:10: “Hata ikiwa baba yangu na mama yangu wangeniacha, Yehova mwenyewe angenichukua.” Acheni nisimulie jinsi maneno hayo yalivyotimia maishani mwangu.

NILILELEWA kwenye shamba la pamba la babu yangu katika jimbo la Georgia, huko Marekani wakati wa ule Mshuko Mkubwa wa Kiuchumi katika miaka ya 1930. Baba yangu, ambaye alikuwa amevunjika moyo kabisa baada ya kifo cha mama yangu na ndugu yangu mchanga, aliniacha nikiishi na baba yake aliyekuwa mjane akahamia katika mji wa mbali sana ambako alipata kazi ya kuajiriwa. Baadaye, alijaribu kufanya mipango ili niende nikaishi naye, lakini mipango hiyo haikufanikiwa.

Binti wakubwa wa babu yangu walisimamia nyumba. Ingawa babu yangu hakuwa mtu wa kidini, mabinti wake walikuwa wafuasi wenye bidii wa dini ya Southern Baptist. Walinilazimisha kwenda kanisani kila Jumapili kwa kunitisha kwamba wangenipiga ikiwa singeenda kanisani kila Jumapili. Kwa hiyo, tangu nilipokuwa na umri mdogo, sikupenda dini. Hata hivyo, nilifurahia michezo na kwenda shuleni.

Ziara Ambayo Ilibadili Maisha Yangu

Alasiri moja katika mwaka wa 1941, nilipokuwa na umri wa miaka 15, mwanamume mmoja mzee pamoja na mke wake walikuja nyumbani kwetu. Nikaambiwa hivi: “Huyu ni mjomba wako Talmadge Rusk.” Sikuwahi kusikia habari zake lakini nilijua baadaye kwamba yeye na mke wake ni Mashahidi wa Yehova. Maelezo yake kuhusu kusudi la Mungu la wanadamu kuishi milele duniani yalikuwa tofauti sana na yale niliyosikia kanisani. Watu wengi katika familia yetu walikataa na hata walidharau mambo waliyosema. Hawakuruhusiwa tena kuja nyumbani kwetu. Hata hivyo, shangazi yangu Mary, ambaye ananizidi umri kwa miaka mitatu, alikubali Biblia pamoja na vitabu ambavyo viliifafanua Biblia.

Mary alisadiki haraka kwamba alikuwa amepata kweli ya Biblia, kisha akabatizwa mwaka wa 1942 na kuwa Shahidi wa Yehova. Pia, alikabili hali ambayo Yesu alitabiri, yaani: “Adui za mtu watakuwa watu wa nyumbani kwake mwenyewe.” (Mt. 10:34-36) Familia ilimpinga vikali. Dada mkubwa wa Mary, ambaye alikuwa na uvutano mkubwa katika mambo ya kijamii katika jimbo lao, alipanga njama na meya wa mji ili Mjomba Talmadge akamatwe. Alishtakiwa kwa kuuza vitu bila leseni (kuwa mchuuzi). Akafungwa gerezani.

Gazeti la mji wetu liliripoti kwamba meya, ambaye pia alikuwa hakimu, aliwaambia hivi watu waliokuwa katika mahakama ya mji: “Vitabu ambavyo mtu huyu anasambaza . . . ni hatari kama sumu.” Mjomba wangu alikata rufani na kushinda kesi, lakini alikaa gerezani kwa siku kumi.

Jinsi Shangazi Mary Alivyonisaidia

Mary alinieleza kuhusu imani yake mpya, na pia alianza kuwahubiria majirani. Niliambatana naye alipoenda kuongoza funzo la Biblia kwa mwanamume ambaye alikuwa amekubali kitabu Ulimwengu Mpya (cha Kiingereza). * Mke wake alisema kwamba mume wake alikisoma usiku mzima bila kulala. Ingawa sikutaka kujihusisha haraka na jambo lolote la kidini, mambo niliyokuwa nikijifunza yalinivutia. Hata hivyo, si mafundisho ya Biblia hasa yaliyonisadikisha kwamba Mashahidi ni watu wa Mungu. Nilisadiki nilipoona jinsi walivyokuwa wakipingwa.

Kwa mfano, siku moja mimi na Mary tulipokuwa tukirudi nyumbani baada ya kupalilia nyanya, tuligundua kwamba dada zake walikuwa wameteketeza vitabu vyake, pamoja na kinanda cha gramafoni na sahani za santuri zenye ujumbe wa Biblia. Nilikasirika sana lakini shangazi yangu alinishutumu. “Utashukuru baadaye kwa sababu ya jambo tulilofanya.”

Mary alifukuzwa nyumbani mwaka wa 1943 kwa sababu alikataa kuacha imani yake mpya na kuacha kuwahubiria majirani. Kufikia wakati huo, nilisisimuka kujifunza kwamba Mungu ana jina, Yehova, na pia ni Mungu mwenye upendo, mwenye huruma, na hateketezi watu katika moto wa mateso. Pia nilijifunza kwamba Yehova ana tengenezo lenye upendo, ingawa bado sikuwa nimehudhuria mkutano.

Baadaye, nilipokuwa nikifyeka nyasi, gari fulani lilikuja polepole nilipokuwa na mmoja kati ya wanaume wawili waliokuwa katika gari hilo akaniuliza ikiwa mimi ni Fred. Nilipogundua kwamba walikuwa Mashahidi, nilisema, “Acheni niingie ndani ya gari, ili twende mahali salama kuzungumza.” Mary alipanga ili wanitembelee. Mmoja wa wanaume hao alikuwa Shield Toutjian, mhudumu anayesafiri ambaye alinitia moyo na kunipa mwongozo wa kiroho nilipouhitaji sana. Sasa familia ilianza kunipinga kwa sababu nilitetea mafundisho ya Mashahidi wa Yehova.

Mary aliniandikia barua akiwa Virginia, ambako alihamia, akaniambia kwamba ikiwa nilikuwa nimeazimia kumtumikia Yehova, ningeweza kwenda kuishi naye. Mara moja, niliamua kwenda. Ijumaa moja jioni, mnamo Oktoba (Mwezi wa 10) 1943, niliweka vitu vichache muhimu ndani ya sanduku na kulifunga juu ya mti fulani mbali kidogo kutoka nyumbani. Jumamosi (Siku ya Posho), nilichukua sanduku hilo, nikapitia nyuma ya nyumba ya jirani bila kuonekana, kisha nikapanda gari ambalo lilikuwa likielekea mjini. Nilipofika katika mji wa Roanoke, nilimkuta Mary akiishi katika nyumba ya Edna Fowlkes.

Kukua Kiroho, Kubatizwa, na Kwenda Betheli

Edna alikuwa Shahidi mtiwa-mafuta mwenye huruma, alikuwa kama Lydia anayetajwa katika Biblia. Edna alikodi nyumba kubwa na alikuwa akiishi na Shangazi Mary, pamoja na mke wa ndugu ya Edna, na vilevile binti zake wawili. Wasichana hao—Gladys na Grace Gregory—baadaye walikuja kuwa wamishonari. Sasa Gladys ana umri wa miaka 90 na kitu, na bado anatumikia kwa uaminifu katika ofisi ya tawi ya Japani.

Nilipokuwa nikiishi katika nyumba ya Edna, nilihudhuria mikutano kwa ukawaida na kuzoezwa katika huduma. Njaa yangu ya kiroho iliyokuwa ikiongezeka ilitoshelezwa nilipopata uhuru wa kujifunza Neno la Mungu na kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Mnamo Juni 14, 1944 (14/6/1944), nilibatizwa. Mary, na Grace na dada yake Gladys Gregory walianza upainia na kukubali mgawo kaskazini mwa Virginia. Walisaidia sana kuanzisha kutaniko huko Leesburg. Mwanzoni mwa mwaka wa 1946, nilianza kufanya upainia katika jimbo jirani. Katika majira ya kiangazi tulisafiri pamoja kwenda katika kusanyiko la kimataifa lisilosahaulika ambalo lilifanywa huko Cleveland, Ohio, Agosti 4-11.

Katika kusanyiko hilo, Nathan Knorr, ambaye alikuwa akiongoza katika tengenezo, alieleza kuhusu mipango ya kupanua Betheli ya Brooklyn. Kazi hiyo ingetia ndani kujenga majengo mapya ya makazi na kiwanda kingine cha uchapishaji. Ndugu wengi vijana walihitajiwa. Niliamua kwamba nilitaka kumtumikia Yehova katika Betheli. Hivyo, nilipeleka ombi langu, na baada ya miezi michache, mnamo Desemba 1, 1946, nilienda Betheli.

Baada ya mwaka mmoja hivi, mwangalizi wa kiwanda cha uchapishaji, Max Larson, alikuja kuniona katika ofisi yangu katika Idara ya Barua. Alinijulisha kwamba nimepata mgawo katika Idara ya Utumishi. Katika mgawo huo, nilijifunza mengi kuhusu kutumia kanuni za Biblia na utendaji wa tengenezo la Mungu, hasa nilipokuwa nikifanya kazi na T. J. (Bud) Sullivan, mwangalizi wa idara hiyo.

Baba yangu alinitembelea mara kadhaa Betheli. Baadaye maishani alipendezwa na mambo ya kidini. Mara ya mwisho aliponitembelea, katika mwaka wa 1965, alisema hivi: “Unaweza kuja kunitembelea, lakini sitakuja tena kamwe kukutembelea hapa.” Nilimtembelea mara chache kabla hajafa. Alikuwa na hakika kwamba angeenda mbinguni. Ninatumaini kwamba yuko katika kumbukumbu la Yehova, na ikiwa ndivyo ilivyo, basi wakati wa ufufuo hatakuwa mahali ambapo alifikiri kwamba angekuwa, bali atakuwa hapa duniani akiwa na tumaini la kuishi milele katika Paradiso iliyorudishwa.

Makusanyiko na Miradi Mingine ya Ujenzi Isiyosahaulika

Sikuzote makusanyiko yalinisaidia kupiga hatua muhimu za ukuzi wa kiroho. Makusanyiko ya kimataifa kama lile lililofanywa katika Uwanja wa Yankee huko New York katika miaka ya 1950 yalinisaidia sana kukua kiroho. Katika mwaka wa 1958, watu 253,922 kutoka katika nchi 123 walijaa katika Uwanja wa Yankee pamoja na ule wa Polo Grounds wakati wa kipindi kimoja cha kusanyiko. Sitasahau kamwe jambo fulani ambalo lilitokea katika kusanyiko hilo. Nilipokuwa nikisaidia katika ofisi ya kusanyiko, Ndugu Knorr alikuja haraka kuniona. Akasema hivi: “Fred, nilisahau kumtuma ndugu fulani awahutubie mapainia wote ambao wamekusanyika sasa katika jumba fulani la chakula tulilokodi hapa karibu. Je, unaweza kukimbia huko na kuwatolea hotuba nzuri kuhusu jambo lolote unalofikiria?” Nilisali sana kabla ya kufika huko nikihemahema.

Idadi ya makutaniko ilipoongezeka sana katika New York City katika miaka ya 1950 na 1960, hakukuwa na majengo ya kutosha ya kukodi ili yatumiwe kama Majumba ya Ufalme. Kwa hiyo, kuanzia mwaka wa 1970 mpaka 1990, majengo matatu yalinunuliwa na kurekebishwa huko Manhattan ili tuwe na mahali panapofaa pa kufanyia mikutano. Nilikuwa mwenyekiti wa halmashauri za ujenzi wa majengo hayo na ninakumbuka mambo mengi mazuri yanayoonyesha jinsi Yehova alivyoyabariki sana makutaniko yaliyoshirikiana kutoa michango na kukamilisha majengo hayo ambayo yanaendelea kutumiwa vizuri yakiwa vitovu vya ibada ya kweli.

Mabadiliko Maishani

Siku moja mwaka wa 1957, nilipokuwa nikitembea kwenda kazini kupitia bustani iliyokuwa katikati ya Makao ya Betheli na kiwanda cha uchapishaji, mvua ilianza kunyesha. Nilimwona mwanabetheli mpya msichana akitembea mbele yangu. Msichana huyo alikuwa mrembo na mwenye nywele za rangi ya manjano. Hakuwa na mwavuli, basi nilijitolea kujifunika naye mwavuli wangu. Hivyo ndivyo nilivyokutana na Marjorie, na tangu tulipofanya arusi mwaka wa 1960, tumekuwa tukitembea pamoja kwa furaha katika utumishi wa Yehova, wakati wa mvua na wa jua pia. Tulisherehekea mwaka wa 50 wa ndoa yetu mnamo Septemba (Mwezi wa 9) 2010.

Kabla ya tu ya kufungua mizigo yetu baada ya fungate, Ndugu Knorr aliniambia kwamba nilikuwa nimepata mgawo wa kuwa mwalimu katika Shule ya Gileadi. Hilo lilikuwa pendeleo la pekee kama nini! Kuanzia mwaka 1961 mpaka 1965, madarasa matano ya muda mrefu zaidi yalifanywa kwa ajili ya wafanyakazi wa ofisi za tawi ili kuwazoeza kwa njia ya pekee kusimamia ofisi za tawi. Katika majira ya mvua ya mwaka wa 1965, madarasa yalianza tena kufanywa kwa muda wa miezi mitano, na yalianza tena kuwazoeza wamishonari.

Katika mwaka wa 1972, nilihamishwa kutoka katika Shule ya Gileadi na kupelekwa katika Idara ya Kushughulikia Maswali ya Wasomaji, ambamo nilitumikia nikiwa mwangalizi. Kufanya utafiti ili kujibu maswali na kutatua matatizo mbalimbali kumenisaidia kuelewa vizuri zaidi mafundisho ya Neno la Mungu na kujua kutumia kanuni bora za Mungu wetu katika kuwasaidia wengine.

Kisha, mwaka wa 1987, nilipewa mgawo wa kwenda katika idara mpya inayoitwa Huduma za Habari za Kihospitali. Mikutano ilipangwa ili kuwafundisha wazee wa Halmashauri za Uhusiano na Hospitali kuwafikia madaktari, mahakimu, na wafanyakazi wa kijamii ili kuzungumza nao juu ya msimamo wetu wa Kimaandiko kuhusu damu. Tatizo kubwa lilikuwa kwamba madaktari walikuwa wakiwatia damu watoto wetu bila ruhusa ya wazazi wao, na mara nyingi walifanya hivyo kwa amri ya mahakama.

Madaktari walipopewa mapendekezo kuhusu matibabu mengine yasiyohusisha damu, kwa kawaida walisema kwamba hakuna matibabu ya aina hiyo au ni ghali mno. Kwa kawaida, nilimwambia hivi daktari-mpasuaji aliyesema hivyo: “Tafadhali nyoosha mkono wako.” Baada ya kuunyoosha, nilimwambia hivi: “Wajua, una mojawapo ya njia bora zaidi za kumtibu mgonjwa bila kutumia damu.” Kumpa pongezi hiyo kulimkumbusha jambo alilojua vizuri sana, kwamba angeweza kuzuia damu nyingi isivuje kwa kutumia kwa makini kisu cha upasuaji.

Katika muda wa miaka 20 ambayo imepita, Yehova amebariki sana jitihada hizo za kuwaelimisha madaktari na mahakimu. Mitazamo yao ilibadilika sana walipoelewa vizuri zaidi msimamo wetu. Walijifunza kwamba utafiti wa kimatibabu unathibitisha kwamba matibabu yasiyohusisha damu yana matokeo mazuri na kwamba mgonjwa anaweza kupelekwa kwa madaktari na pia hospitali nyingi ambazo zinaheshimu msimamo wetu.

Tangu mwaka wa 1996, mimi na Marjorie tumekuwa tukimtumikia katika Kituo cha Elimu cha Watchtower huko Patterson, New York, umbali wa kilomita 110 hivi upande wa kaskazini wa Brooklyn. Katika kituo hicho nilifanya kazi kwa muda mfupi katika Idara ya Utumishi na kisha kwa kipindi fulani nikashiriki katika kuwafundisha waangalizi wa ofisi za tawi na waangalizi wanaosafiri. Katika miaka 12 iliyopita, nimetumikia tena nikiwa mwangalizi wa Idara ya Kushughulikia Maswali ya Wasomaji, ambayo imehamishwa kutoka Brooklyn mpaka Patterson.

Matatizo ya Uzeeni

Imekuwa vigumu zaidi kutimiza mapendeleo yangu ya utumishi Betheli kwa sababu nina umri wa miaka 80 na kitu. Nimepambana na kansa kwa miaka zaidi ya kumi. Ninajihisi kama Hezekia, ambaye Yehova alimwongezea siku za maisha yake. (Isa. 38:5) Afya ya mke wangu pia inazidi kuwa mbaya, na tunajitahidi pamoja kukabiliana na ugonjwa wake wa Alzheimer. Marjorie amekuwa mtumishi stadi wa Yehova, mwalimu wa vijana, msaidizi mwaminifu na mwenzi mshikamanifu kwangu. Sikuzote amekuwa mwanafunzi mwenye bidii na mwalimu bora wa Biblia, na watoto wengi wa kiroho wanaendelea kuwasiliana nasi.

Shangazi yangu Mary alikufa mnamo Machi (Mwezi wa 3) 2010 akiwa na umri wa miaka 87. Alikuwa mwalimu stadi wa Neno la Mungu na aliwasaidia wengine kujiunga na ibada ya kweli. Alifanya huduma ya wakati wote kwa miaka mingi. Ninamshukuru sana kwa sababu ya kunisaidia kujifunza kweli ya Neno la Mungu na kuwa kama yeye, mtumishi wa Mungu wetu mwenye upendo, Yehova. Mary amezikwa kando ya mume wake, ambaye zamani alitumika akiwa mmishonari katika nchi ya Israel. Nina hakika kwamba wako katika kumbukumbu la Yehova wakingojea ufufuo.

Ninapofikiria miaka zaidi ya 67 ambayo nimemtumikia Yehova, ninashukuru kwa sababu ya baraka nyingi ambazo nimepata. Nimefurahia kufanya mapenzi ya Yehova! Kwa kuwa nimetegemea fadhili zake zisizostahiliwa, nina tumaini hakika la kufurahia ahadi hii ya Mwanaye: “Kila mtu ambaye ameacha nyumba au ndugu au dada au baba au mama au watoto au mashamba kwa ajili ya jina langu atapokea mara nyingi zaidi naye atarithi uzima wa milele.”Mt. 19:29.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 11 Kilichapishwa mwaka wa 1942 lakini sasa hakichapishwi tena.

[Picha katika ukurasa wa 19]

Nikiwa katika shamba la pamba la babu yangu huko Georgia, Marekani, mwaka wa 1928

[Picha katika ukurasa wa 19]

Shangazi Mary na Mjomba Talmadge

[Picha katika ukurasa wa 20]

Mary, Gladys, na Grace

[Picha katika ukurasa wa 20]

Nikibatizwa, Juni 14, 1944

[Picha katika ukurasa wa 20]

Nikiwa katika Idara ya Utumishi Betheli

[Picha katika ukurasa wa 21]

Nikiwa na Mary katika kusanyiko la kimataifa la mwaka wa 1958 katika Uwanja wa Yankee

[Picha katika ukurasa wa 21]

Nikiwa na Marjorie siku yetu ya arusi

[Picha katika ukurasa wa 21]

Tukiwa pamoja mwaka wa 2008