Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Wafariji Wote Wanaoomboleza’

‘Wafariji Wote Wanaoomboleza’

‘Wafariji Wote Wanaoomboleza’

“Yehova amenitia mafuta . . . kuwafariji wote wanaoomboleza.”—ISA. 61:1, 2.

1. Yesu alifanya nini kwa ajili ya watu waliokuwa wakiomboleza, na kwa nini?

YESU KRISTO alisema hivi: “Chakula changu ni mimi kufanya mapenzi yake aliyenituma na kuimaliza kazi yake.” (Yoh. 4:34) Alipokuwa akitimiza mgawo aliopewa na Mungu, Yesu alionyesha sifa nzuri sana za Baba yake. Moja ya sifa hizo ni upendo mkubwa wa Yehova kuelekea watu. (1 Yoh. 4:7-10) Mtume Paulo alitaja njia moja ambayo Yehova anaonyesha upendo huo alipomwita Yehova, “Mungu wa faraja yote.” (2 Kor. 1:3) Yesu alionyesha upendo kama huo alipotimiza mambo yaliyotabiriwa katika unabii wa Isaya. (Soma Isaya 61:1, 2.) Yesu alisoma maneno ya unabii huo katika sinagogi huko Nazareti na akasema kwamba yeye mwenyewe ametimiza maneno ya unabii huo. (Luka 4:16-21) Wakati wa huduma yake yote, Yesu aliwafariji watu kwa upendo, na hivyo akawatia moyo na kuwapa amani ya akili.

2, 3. Kwa nini wafuasi wa Kristo wanahitaji kumwiga kwa kuwafariji wengine?

2 Wafuasi wote wa Yesu wanahitaji kumwiga kwa kuwafariji wale wanaoomboleza. (1 Kor. 11:1) Paulo alisema: “Endeleeni kufarijiana na kujengana.” (1 The. 5:11) Tunahitaji kuwafariji wengine hasa, kwa sababu sasa wanadamu wanakabili “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Tim. 3:1) Watu wengi wenye mioyo minyoofu ulimwenguni pote wanaishi miongoni mwa watu wanaosema na kufanya mambo ambayo yanasababisha maumivu, uchungu moyoni, na huzuni.

3 Kama unabii wa Biblia ulivyotabiri, katika siku hizi za mwisho za mfumo huu mwovu wa mambo, watu wengi ni “wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, wenye kujidai, wenye majivuno, wakufuru, wasiotii wazazi, wasio na shukrani, wasio washikamanifu, wasio na upendo wa asili, wasiotaka makubaliano yoyote, wachongezi, wasiojizuia, wakali, wasiopenda wema, wasaliti, wenye vichwa vigumu, wenye kujivuna kwa kiburi, wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu.” Mitazamo kama hiyo sasa ni mibaya zaidi kuliko wakati mwingine wowote ule, kwa sababu ‘watu waovu na wajanja wameendelea kutoka ubaya mpaka ubaya zaidi.’—2 Tim. 3:2-4, 13.

4. Hali za ulimwengu zimekuwa namna gani katika nyakati zetu?

4 Mambo yote hayo hayapaswi kutushangaza, kwa sababu Neno la Mungu linaonyesha wazi kwamba “ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.” (1 Yoh. 5:19) “Ulimwengu mzima” unatia ndani sehemu ya kisiasa, kidini, na kibiashara, na pia njia ambazo Shetani anatumia ili kusambaza mawazo yake. Hakuna shaka yoyote kwamba Shetani Ibilisi ndiye “mtawala wa ulimwengu” na “mungu wa mfumo huu wa mambo.” (Yoh. 14:30; 2 Kor. 4:4) Hali zinazidi kuwa mbaya duniani pote kwa sababu Shetani sasa ana hasira kali, akijua kwamba ni kipindi kifupi tu cha wakati kinachobaki kabla Yehova hajamwangamiza. (Ufu. 12:12) Inafariji kama nini kujua kwamba hivi karibuni Mungu hatamruhusu Shetani na mfumo wake mwovu kuendelea, na suala ambalo Shetani alitokeza kuhusu enzi kuu ya Yehova litatatuliwa!—Mwa., sura ya 3; Ayu., sura ya 2.

Habari Njema Inahubiriwa Duniani Pote

5. Unabii kuhusu kazi ya kuhubiri unatimizwa jinsi gani katika siku hizi za mwisho?

5 Katika kipindi hiki kigumu cha historia ya wanadamu, mambo ambayo Yesu alitabiri yanatimia. Alisema hivi: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mt. 24:14) Kazi hiyo ya kutoa ushahidi duniani pote kuhusu Ufalme wa Mungu inazidi kufanywa kwa kiwango kikubwa zaidi. Leo, zaidi ya Mashahidi wa Yehova 7,500,000, wanaoshirikiana na makutaniko zaidi ya 107,000 duniani pote, wanahubiri kuhusu Ufalme wa Mungu, ambao ulikuwa kichwa kikuu cha mahubiri na mafundisho ya Yesu. (Mt. 4:17) Kwa sababu ya kazi yetu ya kuhubiri leo, watu wanaoomboleza wanapata faraja kubwa. Katika kipindi cha miaka miwili iliyopita, jumla ya watu 570,601 walibatizwa na kuwa Mashahidi wa Yehova.

6. Una maoni gani kuhusu ukuzi wa kazi yetu ya kuhubiri?

6 Mashahidi wa Yehova sasa wanatafsiri na kusambaza machapisho yanayotegemea Biblia katika lugha zaidi ya 500 na hilo linaonyesha kwamba kazi ya kuhubiri inafanywa kwa kiwango kikubwa sana. Kazi kama hiyo haijawahi kamwe kufanywa katika historia yote ya wanadamu! Kwa kweli, kuwapo kwa sehemu ya kidunia ya tengenezo la Yehova, kazi ambayo inatimiza, na ukuzi wake, ni mambo yenye kushangaza sana. Bila mwongozo na msaada wa roho takatifu yenye nguvu ya Mungu, jambo kama hilo halingewezekana katika ulimwengu huu ulio chini ya uvutano wa Shetani. Kwa kuwa habari njema inahubiriwa duniani pote, watu wanaokubali ujumbe wa Ufalme wanaweza pia kupata faraja inayotokana na Maandiko kama watu wa Yehova.

Kuwafariji Waabudu Wenzetu

7. (a) Kwa nini hatuwezi kumtazamia Yehova aondoe sasa hali zote zenye kuhuzunisha? (b) Tunajua jinsi gani kwamba tunaweza kuvumilia mateso na dhiki?

7 Katika ulimwengu huu ambao umejaa uovu na mateso, tuna hakika kwamba tutapatwa na hali fulani zenye kuhuzunisha. Hatuwezi kumtazamia Mungu aondoe mambo yote yanayotukosesha furaha au kutuletea huzuni kabla hajauharibu mfumo huu wa mambo. Tunapongoja siku hiyo, mateso yaliyotabiriwa yatajaribu utimilifu wetu kwa Yehova na yataonyesha ikiwa tunaunga mkono enzi yake kuu ya ulimwengu wote. (2 Tim. 3:12) Hata hivyo, kwa msaada na faraja kutoka kwa Baba yetu wa mbinguni, tunaweza kuwa kama Wakristo watiwa-mafuta katika jiji la kale la Thesalonike, ambao walipambana na mateso na dhiki kwa uvumilivu na imani.—Soma 2 Wathesalonike 1:3-5.

8. Kuna uthibitisho gani wa Kimaandiko unaoonyesha kwamba Yehova anawafariji watumishi wake?

8 Hapana shaka kwamba Yehova anawapa watumishi wake faraja wanayohitaji. Kwa mfano, Malkia Yezebeli aliyekuwa mwovu alipotisha kumuua nabii Eliya, nabii huyo aliogopa sana na kukimbia na hata alisema kwamba ni heri afe. Lakini badala ya kumkemea Eliya, Yehova alimfariji na kumpa ujasiri ili atimize kazi yake akiwa nabii. (1 Fal. 19:1-21) Jinsi Yehova alivyolisaidia kutaniko la Kikristo katika karne ya kwanza inathibitisha pia kwamba Yehova anawafariji watu wake. Kwa mfano, tunasoma kwamba wakati fulani ‘kutaniko kotekote katika Yudea na Galilaya na Samaria liliingia katika kipindi cha amani, likajengwa.’ Zaidi ya hayo, “lilipokuwa likitembea katika kumwogopa Yehova na katika faraja ya roho takatifu likaendelea kuongezeka.” (Mdo. 9:31) Tunashukuru kama nini kwamba sisi pia tuna “faraja ya roho takatifu”!

9. Kwa nini kujifunza kumhusu Yesu kunaweza kutufariji?

9 Tukiwa Wakristo, tumefarijiwa kwa kujifunza kumhusu Yesu Kristo na kwa kufuata mfano wake. Yesu alisema: “Njooni kwangu, nyote mnaotaabika na kulemewa na mizigo, nami nitawaburudisha ninyi. Chukueni nira yangu na mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mwenye tabia-pole na mnyenyekevu moyoni, nanyi mtapata burudisho kwa ajili ya nafsi zenu. Kwa maana nira yangu ni laini na mzigo wangu ni mwepesi.” (Mt. 11:28-30) Kujifunza kuhusu jinsi Yesu alivyowatendea watu kwa fadhili na upendo na kisha kuiga mfano wake mzuri, kunaweza kutusaidia sana kupata kitulizo kutokana na mikazo ambayo huenda ikatupata.

10, 11. Ni nani katika kutaniko wanaoweza kuwafariji wengine?

10 Wakristo wenzetu wanaweza pia kutufariji. Kwa mfano, fikiria jinsi wazee katika kutaniko wanavyoweza kuwasaidia wale wanaopambana na hali zenye kuhuzunisha. Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi: “Je, kuna yeyote mgonjwa [kiroho] kati yenu? Na awaite kwake wanaume wazee wa kutaniko, nao wasali juu yake.” Kutakuwa na matokeo gani? “Sala ya imani itamponya huyo asiyejisikia vizuri, na Yehova atamwinua. Pia, ikiwa amefanya dhambi, atasamehewa.” (Yak. 5:14, 15) Washiriki wengine wa kutaniko wanaweza pia kutufariji.

11 Mara nyingi wanawake wanaona ni rahisi zaidi kuzungumza na wanawake wengine kuhusu matatizo yao. Dada wenye umri mkubwa zaidi na wenye uzoefu zaidi wanaweza hasa kuwapa dada wachanga mashauri mengi mazuri. Wanawake hao Wakristo wakomavu wenye umri mkubwa zaidi huenda wamekwisha kupatwa na hali kama hizo katika maisha yao. Sifa yao ya huruma na sifa nyingine za kike zinaweza kuwa msaada mkubwa sana. (Soma Tito 2:3-5.) Bila shaka, wazee na wengine wanaweza na wanapaswa ‘kusema kwa kuzifariji nafsi zilizohuzunika’ miongoni mwetu. (1 The. 5:14, 15) Na ni vizuri kukumbuka kwamba Mungu “hutufariji katika dhiki yetu yote, ili tuweze kuwafariji wale walio katika namna yoyote ya dhiki.”—2 Kor. 1:4.

12. Kwa nini ni muhimu kuhudhuria mikutano ya Kikristo?

12 Njia muhimu zaidi ya kufarijiwa ni kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Mazungumzo ya Biblia tunayosikia katika mikutano hiyo yanatutia moyo. Tunasoma kwamba Yuda na Sila ‘waliwatia moyo akina ndugu kwa hotuba nyingi na kuwatia nguvu.’ (Mdo. 15:32) Kabla na baada ya mikutano yetu, washiriki wa kutaniko wanakuwa na mazungumzo yenye kujenga kati yao. Hivyo, hata ikiwa tunateseka kwa sababu ya hali fulani yenye kuhuzunisha, tusijitenge, kwa sababu kujitenga hakutafanya mambo yawe mazuri. (Met. 18:1) Badala yake, ni vema tufuate shauri hili la mtume Paulo lililoongozwa na roho ya Mungu: “Acheni tufikiriane ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri, bila kuacha kukusanyika pamoja sisi wenyewe, kama vile wengine walivyo na desturi, bali tutiane moyo, na kufanya hivyo zaidi kwa kadiri mnavyoona siku ile kuwa inakaribia.”—Ebr. 10:24, 25.

Pata Faraja Kutokana na Neno la Mungu

13, 14. Eleza jinsi Maandiko yanavyoweza kutufariji.

13 Iwe sisi ni Wakristo waliobatizwa au tumeanza tu kujifunza hivi karibuni kumhusu Mungu na makusudi yake, tunaweza kupata faraja kubwa katika Neno la Mungu lililoandikwa. Paulo aliandika hivi: “Mambo yote yaliyoandikwa zamani yaliandikwa ili kutufundisha sisi, ili kupitia uvumilivu wetu na kupitia faraja kutokana na Maandiko tuwe na tumaini.” (Rom. 15:4) Maandiko Matakatifu yanaweza kutufariji na kutufanya tuwe na ‘uwezo kamili, tukiwa na vifaa kamili kwa ajili ya kila kazi njema.’ (2 Tim. 3:16, 17) Kujua ukweli kuhusu makusudi ya Mungu na kuwa na tumaini la kweli la wakati ujao, bila shaka kutatufariji sana. Kwa hiyo, acheni tutumie kikamili Neno la Mungu na machapisho yanayotegemea Biblia ambayo yanaweza kutufariji na kutunufaisha kwa njia nyingi.

14 Yesu alituwekea mfano mzuri kwa kutumia Maandiko ili kuwafundisha na kuwafariji wengine. Kwa mfano, baada ya ufufuo wake, Yesu aliwatokea wawili kati ya wanafunzi wake naye ‘akawafungulia kikamili Maandiko.’ Alipokuwa akizungumza nao, mioyo yao iliguswa sana. (Luka 24:32) Mtume Paulo aliendelea kufuata mfano bora wa Yesu kwa ‘kujadiliana na watu kwa kutumia Maandiko.’ Huko Beroya, wasikilizaji wake “walilipokea neno kwa hamu kubwa zaidi ya akili, wakiyachunguza Maandiko kwa uangalifu kila siku.” (Mdo. 17:2, 10, 11) Kwa hiyo, ni jambo linalofaa kama nini kwamba tuisome Biblia kila siku, tufaidike kwa kuisoma na pia kwa kusoma machapisho ya Kikristo ambayo yanakusudiwa kutufariji na kutupatia tumaini katika nyakati hizi zenye msukosuko!

Njia Zaidi za Kuwafariji Wengine

15, 16. Ni mambo gani tunayoweza kufanya ili kuwasaidia na kuwafariji Wakristo wenzetu?

15 Tunaweza kuwasaidia na hivyo kuwafariji Wakristo wenzetu katika njia mbalimbali. Kwa mfano, tunaweza kuwasaidia waliozeeka au waamini wenzetu walio wagonjwa kwa kuwanunulia vitu dukani au sokoni. Tunaweza kuwasaidia wengine kwa kuwafanyia kazi za nyumbani, na hivyo kuonyesha kwamba tunapendezwa nao. (Flp. 2:4) Labda tunaweza kuwapongeza waabudu wenzetu kwa sababu ya sifa zao nzuri, kama vile upendo, uwezo wao wa kufanya mambo, ujasiri, na imani.

16 Jambo moja tunaloweza kufanya ili kuwafariji waliozeeka ni kuwatembelea na kuwasikiliza wanapotusimulia mambo waliyopitia maishani na baraka ambazo wamepata katika utumishi wa Yehova. Kwa kweli, hilo linaweza kututia moyo na kutufariji sana! Tunaweza kusoma Biblia au machapisho yetu yanayotegemea Biblia pamoja na wale ambao tunatembelea. Labda tunaweza kusoma pamoja nao makala itakayozungumziwa juma hilo katika Funzo la Mnara wa Mlinzi au habari ambayo itazungumziwa wakati wa Funzo la Biblia la Kutaniko juma hilo. Tunaweza kutazama pamoja nao DVD inayohusu habari fulani ya Kimaandiko. Na tunaweza pia kuwasomea au kuwasimulia mambo fulani yaliyoonwa yenye kutia moyo kutoka katika machapisho yetu.

17, 18. Tukiwa watumishi washikamanifu wa Yehova, kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba atatusaidia na kutufariji?

17 Tukiona kwamba mwabudu mwenzetu wa Yehova anahitaji faraja, tunaweza kumtaja katika sala zetu za kibinafsi. (Rom. 15:30; Kol. 4:12) Sisi wenyewe tunapopambana na matatizo ya maisha na kujitahidi kuwafariji wengine, tunaweza kuwa na imani na usadikisho kama ule wa mtunga-zaburi aliyeimba: “Mtupie Yehova mzigo wako, naye mwenyewe atakutegemeza. Hatamwacha kamwe mwadilifu atikisike.” (Zab. 55:22) Kwa kweli, tukiwa watumishi wake washikamanifu, sikuzote Yehova atatufariji na kutusaidia.

18 Mungu aliwaambia hivi waabudu wake wa nyakati za kale: “Mimi—mimi mwenyewe ndiye Yule anayewafariji ninyi.” (Isa. 51:12) Yehova atatufanyia vivyo hivyo na atabariki matendo na maneno yetu mazuri tunapowafariji wale wanaoomboleza. Iwe tunatumaini kuishi mbinguni au duniani, kila mmoja wetu anaweza kufarijiwa na maneno yafuatayo ambayo Paulo aliwaandikia Wakristo wenzake watiwa-mafuta: “Bwana wetu Yesu Kristo mwenyewe na Mungu Baba yetu, aliyetupenda na kutupa sisi faraja ya milele na tumaini jema kwa njia ya fadhili zisizostahiliwa, na aifariji mioyo yenu na kuwaimarisha ninyi katika kila tendo na neno jema.”—2 The. 2:16, 17.

Je, Unakumbuka?

• Kazi yetu ya kuwafariji wale wanaoomboleza imeenea kadiri gani?

• Ni mambo gani tunayoweza kufanya ili kuwafariji wengine?

• Kuna uthibitisho gani wa Kimaandiko unaoonyesha kwamba Yehova anawafariji watu wake?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 28]

Je, unashiriki kuwafariji wale wanaoomboleza?

[Picha katika ukurasa wa 30]

Vijana na pia waliozeeka wanaweza kuwatia moyo wengine