Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Je, inawezekana kujua saa kamili ambayo Yesu Kristo alitundikwa mtini?

Swali hilo linatokea kwa sababu ya kile kinachoonekana kuwa kupingana kati ya masimulizi yaliyoongozwa na roho ya Mungu kuhusu kifo cha Yesu kama yalivyoandikwa na mwandikaji wa Injili Marko na pia mtume Yohana. Marko anasema hivi: “Sasa ilikuwa saa tatu, nao [askari-jeshi] wakamtundika mtini.” (Marko 15:25) Kulingana na Yohana, ‘ilikuwa karibu saa sita’ wakati Pilato alipomtoa Yesu kwa Wayahudi ili atundikwe mtini. (Yoh. 19:14-16) Wafafanuzi wa Biblia wametoa maelezo mbalimbali ili kujaribu kupatanisha masimulizi hayo ambayo yanaonekana kuwa yanapingana. Hata hivyo, hakuna habari za kutosha za Kimaandiko zinazoeleza tofauti kati ya masimulizi hayo mawili. Lakini, kuchunguza jinsi watu walivyohesabu wakati katika nyakati hizo za kale kunaweza kusaidia.

Katika karne ya kwanza ya Wakati wetu wa Kawaida, Wayahudi waligawanya siku katika saa 12, wakihesabu kuanzia jua linapochomoza. (Yoh. 11:9) Kwa hiyo, “saa tatu” ilianza saa mbili kamili asubuhi hadi saa tatu kamili asubuhi na “saa sita” ilianza saa tano asubuhi hadi saa sita mchana. Bila shaka, jua lilichomoza na kutua nyakati tofauti-tofauti katika mwaka mzima. Kwa hiyo, urefu wa kipindi cha mchana ulibadilika kulingana na majira. Zaidi ya hayo, watu walijua ni saa ngapi kwa kutazama tu mahali jua lilipokuwa. Hivyo, watu walikadiria tu wakati. Kwa ujumla, Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yanazungumza kuhusu matukio yaliyotukia saa tatu, saa sita, au saa tisa—mara nyingi ikimaanisha karibu na wakati huo. (Mt. 20:3, 5; Mdo. 10:3, 9, 30) Kutaja kihususa zaidi, maneno kama vile “saa saba,” yalisemwa ikiwa tu wakati ulikuwa muhimu katika habari iliyokuwa ikisimuliwa.—Yoh. 4:52.

Masimulizi ya Injili yanapatana kuhusiana na wakati wa matukio ya siku ya mwisho ya Yesu duniani. Vitabu vyote vinne vya Injili vinaonyesha kwamba makuhani na wanaume wazee walikutana baada ya mapambazuko na baadaye wakampeleka Yesu kwa Gavana Mroma Pontio Pilato. (Mt. 27:1; Marko 15:1; Luka 22:66; Yoh. 18:28) Mathayo, Marko, na Luka wote wanasema kwamba kuanzia saa sita, Yesu alipokuwa tayari ametundikwa juu ya mti, kukawa na giza juu ya nchi “mpaka saa tisa.”—Mt. 27:45, 46; Marko 15:33, 34; Luka 23:44.

Jambo moja kuu ambalo huenda likawa la maana kuhusu wakati wa kutundikwa kwa Yesu juu ya mti ni hili: Kumpiga mtu mijeledi kulionwa kuwa sehemu ya adhabu ya kumtundika mtu mtini. Nyakati nyingine, kupigwa mijeledi kuliumiza sana hivi kwamba mtu alikufa papo hapo alipokuwa akipigwa. Katika kisa cha Yesu, huenda alipigwa sana hivi kwamba ilihitaji mtu mwingine aubebe mti wa mateso baada ya Yesu kuanza kuubeba peke yake. (Luka 23:26; Yoh. 19:17) Ikiwa kupigwa mijeledi kulionwa kuwa mwanzo wa adhabu ya kumtundika mtu mtini, muda fulani ungepita kabla ya Yesu kupigiliwa misumari kwenye mti wa mateso. Kwa hiyo, watu mbalimbali wanaweza kutaja saa zinazotofautiana za kutundikwa kwa Yesu juu ya mti wa mateso, ikitegemea hatua ambayo mtu binafsi aliona katika tukio lote kwa ujumla.

Mtume Yohana aliandika simulizi lake makumi ya miaka baada ya waandikaji wengine wa Injili. Kwa hiyo, angeweza kupata masimulizi ya waandikaji hao wengine. Ni kweli kwamba Yohana alitaja wakati ambao unaonekana kuwa tofauti na ule ambao Marko anataja. Hata hivyo, hilo linatoa uthibitisho ulio wazi wa kwamba Yohana hakunakili tu simulizi la Marko. Wote wawili, Yohana na Marko, waliongozwa na roho ya Mungu. Ingawa hakuna habari za kutosha za Kimaandiko zinazoeleza tofauti hiyo, tunaweza kuyaamini masimulizi hayo ya Injili.