Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Mimi Ni Mlemavu Sasa, Lakini Sitakuwa Mlemavu Milele!”

“Mimi Ni Mlemavu Sasa, Lakini Sitakuwa Mlemavu Milele!”

“Mimi Ni Mlemavu Sasa, Lakini Sitakuwa Mlemavu Milele!”

Limesimuliwa na Sara van der Monde

Mara nyingi watu wananiambia, “Sara, una tabasamu nzuri sana. Kwa nini sikuzote una furaha?” Ninawaambia kwamba nina tumaini la pekee. Kwa ufupi hili ndilo tumaini langu, “Mimi ni mlemavu sasa, lakini sitakuwa mlemavu milele!”

NILIZALIWA mwaka wa 1974 huko Paris, Ufaransa. Nilizaliwa kwa shida, na baadaye iligunduliwa kwamba nina ugonjwa wa kupooza ubongo. Singeweza kufanya mengi kwa kutumia mikono na miguu yangu, na niliongea kwa njia isiyoeleweka kwa urahisi. Pia, nilipata ugonjwa wa kifafa na niliambukizwa kwa urahisi magonjwa mengi.

Nilipokuwa na umri wa miaka miwili, familia yangu ilihamia Melbourne, Australia. Miaka miwili baadaye, Baba aliniacha mimi na Mama yangu. Ninakumbuka huo ndio wakati ambapo kwa mara ya kwanza nilijihisi nikiwa karibu na Mungu. Mama, ambaye ni Shahidi wa Yehova, aliambatana na mimi kwa kawaida katika mikutano ya Kikristo, ambako nilijifunza kwamba Mungu ananipenda na ananijali. Ujuzi huo, pamoja na upendo na uhakikisho wa mama yangu, ulinisaidia kuhisi nikiwa salama hata ingawa hali zetu zilikuwa zimebadilika.

Pia, Mama alinifundisha jinsi ya kusali kwa Yehova. Kwa kweli, imekuwa rahisi zaidi kwangu kusali kuliko kuongea. Ninaposali, sihitaji kujikakamua ili kusema maneno waziwazi, lakini ni kana kwamba “ninayasikia” waziwazi yakiwa katika akili yangu. Na kwa sababu siongei kwa njia inayoeleweka kwa urahisi, ninatiwa moyo kujua kwamba Yehova anaelewa kila jambo, hata nikilisema kimya-kimya katika akili yangu au nikilisema kwa njia isiyoeleweka.—Zab. 65:2.

Kuvumilia Matatizo

Nilipofikia umri wa miaka mitano, ugonjwa wangu wa kupooza ubongo ulizidi kuwa mbaya hivi kwamba nilihitaji vifaa maalumu vya kunisaidia kutembea. Niliyumbayumba sana nilipotembea kwa vifaa hivyo. Nilipofikia umri wa miaka 11, nilishindwa kabisa kutembea. Baadaye, singeweza kupanda au kushuka kutoka kwenye kitanda bila msaada wa mashini ya umeme ya kuniinua na kunishusha ndani ya kiti cha magurudumu chenye injini. Ninatumia mikono yangu kuendesha kiti hicho kwa kutumia kifaa maalumu.

Ninakiri kwamba nyakati nyingine ulemavu wangu unanifanya nishuke moyo. Lakini ninakumbuka azimio la familia yetu: “Usihangaikie mambo ambayo huwezi kufanya. Fanya tu mambo unayoweza kufanya.” Azimio hilo limenisaidia kufanya mambo kama vile kuendesha farasi, kuendesha mashua yenye tanga, kuendesha mtumbwi, kupiga kambi, na hata kuendesha gari katika barabara ambayo haina magari mengine! Ninapenda sana sanaa, hivyo ninachora picha, ninashona nguo, ninashona matandiko ya kufunika vitanda, ninatia mapambo kwenye vitambaa, na kufinyanga vyombo vya udongo.

Kwa sababu nimelemaa sana, watu fulani wamefikiri kwamba siwezi kufanya uamuzi wa akili wa kumtumikia Mungu. Nilipokuwa na umri wa miaka 18, mwalimu fulani shuleni alinihimiza nitoke nyumbani ili niachane na dini ya mama yangu. Hata alijitolea kunisaidia kupata mahali pa kuishi. Hata hivyo, nilimwambia kwamba siwezi kamwe kuacha imani yangu na nitaondoka nyumbani nikiwa tu tayari kujitegemea zaidi.

Muda mfupi baada ya kishawishi hicho, nilibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova. Miaka miwili baadaye, nilihamia katika chumba kidogo cha kupanga. Ninafurahia kuishi hapa kwa sababu wengine wanaweza kunisaidia na vilevile nina uhuru niliotamani kuwa nao.

Ombi Ambalo Sikutazamia

Kadiri miaka ilivyopita, nilikabili majaribu mengine ya imani. Siku moja nilishtuka sana wakati mwanafunzi mwenzangu, ambaye pia ni mlemavu, aliponiomba nifunge ndoa naye. Mwanzoni, nilifurahi sana. Kama wanawake wengi vijana, mimi pia ninatamani kuwa na mwenzi maishani. Hata hivyo, kuolewa na mlemavu kama mimi hakumaanishi kwamba ni lazima tutakuwa na ndoa yenye furaha. Zaidi ya hayo, mwanamume huyo kijana hakuwa na imani kama yangu. Imani yetu, shughuli zetu, na miradi yetu ilikuwa tofauti kabisa. Basi tungewezaje kuishi pamoja? Niliazimia pia kutii mwongozo wa Mungu ulio wazi kuhusu kuolewa na mwamini mwenzangu tu. (1 Kor. 7:39) Kwa hiyo, kwa fadhili nilimwambia mwanamume huyo kwamba singeweza kukubali ombi lake.

Hata leo, ninajua kwamba nilifanya uamuzi unaofaa. Na hakuna shaka katika akili yangu kwamba nitakuwa na furaha katika ulimwengu mpya ambao Mungu ameahidi. (Zab. 145:16; 2 Pet. 3:13) Kwa sasa, nimeazimia kubaki mshikamanifu kwa Yehova na kuridhika na hali zangu za sasa.

Ninatamani sana siku ambayo nitaweza kuruka kutoka katika kiti changu cha magurudumu na kukimbia kama swala. Wakati huo nitapaaza sauti hivi: “Nilikuwa mlemavu, lakini sasa nina afya nzuri—na nitakuwa nayo milele!”