Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tembea Kupatana na Roho ili Upate Uzima na Amani

Tembea Kupatana na Roho ili Upate Uzima na Amani

Tembea Kupatana na Roho ili Upate Uzima na Amani

‘Tembea, si kupatana na mwili, bali kupatana na roho.’—ROM. 8:4.

1, 2. (a) Ni hali gani mbaya inayoweza kutokea mtu anapokengeushwa wakati anapoendesha gari? (b) Ni hatari gani inayoweza kutokea mtu akikengeushwa kiroho?

WAZIRI wa uchukuzi katika serikali ya Marekani alisema kwamba “inaonekana tatizo la watu kukengeushwa wakati wanapoendesha magari linazidi kuwa baya kila mwaka.” Kwa mfano, madereva wanaweza kukengeushwa ikiwa wanatumia simu ya mkononi wakati wanapoendesha magari. Wengi wameripoti kwamba gari lao limegongwa, au karibu ligongwe na gari lingine linaloendeshwa na dereva anayetumia simu ya mkononi. Huenda watu wakafikiri kwamba wanaokoa wakati wanapotumia simu zao za mkononi wanapoendesha magari, lakini kufanya hivyo kunaweza kusababisha msiba.

2 Inaweza pia kuwa hivyo kuhusu hali yetu ya kiroho. Kama vile tu ambavyo dereva anayekengeushwa anavyokosa mara nyingi kutambua ishara za hatari barabarani, ndivyo mtu anayekengeushwa kiroho anavyoweza kutumbukia kwa urahisi katika hatari. Ikiwa tunajiruhusu wenyewe tupeperushwe na hivyo kuacha maisha yetu ya Kikristo na utendaji wa kiroho, matokeo yake ni kwamba imani yetu inaweza kuvunjika. (1 Tim. 1:18, 19) Mtume Paulo alitoa onyo kuhusu hatari hiyo alipowatahadharisha hivi Wakristo wenzake huko Roma: “Kukaza akili juu ya mwili humaanisha kifo, bali kukaza akili juu ya roho humaanisha uzima na amani.” (Rom. 8:6) Paulo alimaanisha nini aliposema hivyo? Tunawezaje kuepuka “kukaza akili juu ya mwili” na hivyo kuendelea “kukaza akili juu ya roho”?

“Hawana Hukumu ya Hatia”

3, 4. (a) Paulo aliandika kuhusu pambano gani katika mwili wake? (b) Kwa nini tunapaswa kutilia maanani hali ya Paulo?

3 Katika barua yake kwa Waroma, Paulo aliandika kuhusu pambano alilokuwa nalo katika maisha yake, yaani, pambano kati ya mwili wake na akili yake. (Soma Waroma 7:21-23.) Paulo hakuwa akijitetea au kujihurumia kana kwamba alikuwa amelemewa na dhambi na hangeweza kujisaidia. Kwa kweli, alikuwa mtu mkomavu, Mkristo aliyetiwa mafuta kwa roho, aliyechaguliwa kuwa “mtume kwa mataifa.” (Rom. 1:1; 11:13) Kwa nini basi Paulo aliandika kuhusu pambano alilokuwa nalo katika mwili wake?

4 Paulo alikuwa akikiri kwa unyoofu kwamba hangeweza kufanya mapenzi ya Mungu kwa nguvu zake mwenyewe na kwa kiwango ambacho yeye mwenyewe alitamani. Kwa nini? Alisema hivi: “Wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Rom. 3:23) Akiwa mzao wa Adamu, Paulo alipatwa na madhara ya dhambi juu ya mwili usio mkamilifu. Tunaweza kuelewa kwa nini alihisi hivyo kwa sababu sisi sote si wakamilifu na ni lazima tupambane na madhara hayo kila siku. Zaidi ya hayo, kuna mambo mengi yanayoweza kutukengeusha fikira na kutuondoa kwenye ‘barabara inayoongoza kwenye uzima ambayo ina nafasi ndogo.’ (Mt. 7:14) Hata hivyo, Paulo alikuwa na tumaini licha ya hali yake, na ndivyo ilivyo kwetu.

5. Paulo alipata wapi msaada na kitulizo?

5 Paulo aliandika hivi: “Ni nani atakayeniokoa . . . ? Shukrani kwa Mungu kupitia Yesu Kristo Bwana wetu!” (Rom. 7:24, 25) Kisha, alizungumza na wale walio “katika muungano na Kristo Yesu,” yaani, Wakristo watiwa-mafuta. (Soma Waroma 8:1, 2.) Kupitia roho yake takatifu, Yehova anawafanya kuwa wana, na kuwaita kuwa “warithi pamoja na Kristo.” (Rom. 8:14-17) Roho ya Mungu, pamoja na imani yao katika fidia au dhabihu ya ukombozi ya Kristo, inawawezesha kuwa washindi katika pambano ambalo Paulo alieleza na hivyo “hawana hukumu ya hatia.” Wanawekwa huru kutokana na “sheria ya dhambi na kifo.”

6. Kwa nini watumishi wote wa Mungu wanapaswa kuelewa maneno ya Paulo?

6 Ingawa Paulo alikuwa anazungumza na Wakristo watiwa-mafuta, yale aliyosema kuhusu roho ya Mungu na dhabihu ya ukombozi ya Kristo yanaweza kuwanufaisha watumishi wote wa Yehova iwe wanatumaini kuishi mbinguni au duniani. Licha ya kwamba Paulo aliongozwa na roho ya Mungu kutoa shauri hilo kwa Wakristo watiwa-mafuta, ni jambo muhimu sana kwamba watumishi wote wa Mungu waelewe yale aliyoandika na wajitahidi kufaidika kutokana nayo.

Jinsi Mungu ‘Alivyoihukumu Dhambi Katika Mwili’

7, 8. (a) Ni katika maana gani Sheria ilikuwa “dhaifu kupitia mwili”? (b) Mungu ametimiza nini kupitia roho yake na kupitia dhabihu ya ukombozi?

7 Katika sura ya 7 ya kitabu cha Waroma, Paulo alikiri kwamba dhambi ina nguvu juu ya mwili usio mkamilifu. Katika sura ya 8, alieleza juu ya nguvu za roho takatifu. Mtume huyo alieleza jinsi roho ya Mungu inavyoweza kuwasaidia Wakristo katika pambano lao dhidi ya nguvu ya dhambi ili waweze kuishi kupatana na mapenzi ya Yehova na kupata kibali chake. Paulo alionyesha kwamba kupitia roho ya Mungu na dhabihu ya ukombozi ya Mwana wake, Mungu ametimiza jambo fulani ambalo Sheria ya Musa haingeweza kutimiza.

8 Sheria, pamoja na amri zake nyingi, ziliwahukumu watenda-dhambi. Zaidi ya hayo, makuhani wakuu wa Israeli waliotumika chini ya Sheria hawakuwa wakamilifu na hawangeweza kutoa dhabihu ya kufunika dhambi kikamili. Hivyo, Sheria ilikuwa “dhaifu kupitia mwili.” Lakini “kwa kumtuma Mwana wake mwenyewe akiwa katika mfano wa mwili wenye dhambi” na kwa kumtoa kuwa dhabihu ya ukombozi, Mungu “aliihukumu dhambi katika mwili,” na hivyo kushinda tatizo la ‘Sheria kutokuwa na uwezo.’ Kwa sababu hiyo, Wakristo watiwa-mafuta wanahesabiwa kuwa waadilifu kwa msingi wa imani yao katika dhabihu ya ukombozi ya Yesu. Wanahimizwa ‘watembee, si kupatana na mwili, bali kupatana na roho.’ (Soma Waroma 8:3, 4.) Kwa kweli, ni lazima waendelee kufanya hivyo kwa uaminifu mpaka mwisho wa maisha yao duniani ili wapewe “taji la uzima.”—Ufu. 2:10.

9. Neno “sheria” linalotumiwa katika Waroma 8:2 linamaanisha nini?

9 Zaidi ya “Sheria,” Paulo alitaja “sheria ya ile roho” na “sheria ya dhambi na kifo.” (Rom. 8:2) Hizo ni sheria gani? Neno “sheria” hapa halimaanishi amri fulani, kama zile zilizo katika Sheria ya Musa. Kitabu kimoja cha marejeo kinadokeza hivi: “Neno la Kigiriki linalotafsiriwa sheria katika mstari huo linamaanisha mambo mema au maovu ambayo watu wanafanya na ambayo yanawaongoza kama sheria. Neno hilo linaweza pia kumaanisha viwango ambavyo mtu anafuata maishani.”

10. Tunaongozwa jinsi gani na sheria ya dhambi na kifo?

10 Mtume Paulo aliandika hivi: “Kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.” (Rom. 5:12) Tukiwa wazao wa Adamu, sisi sote tunaongozwa na sheria ya dhambi na kifo. Mwili wetu wenye dhambi unatuchochea sikuzote kufanya mambo yasiyompendeza Mungu, lakini mambo hayo yanaongoza tu kwenye kifo. Katika barua yake kwa Wagalatia, Paulo aliyaita matendo na tabia kama hizo kuwa “matendo ya mwili.” Kisha akaongeza hivi: “Wale walio na mazoea ya kufanya mambo ya namna hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu.” (Gal. 5:19-21) Watu wa aina hiyo ni sawa na wale wanaotembea kupatana na mwili. (Rom. 8:4) ‘Mambo yanayowaongoza’ na ‘viwango wanavyofuata maishani’ ni vya kimwili kabisa. Je, ni wale tu ambao wanafanya uasherati, kuabudu sanamu, kuwasiliana na pepo, au kutenda dhambi nyingine nzito ndio wanaotembea kupatana na mwili? Hapana, kwa kuwa matendo ya mwili yanatia ndani pia mambo ambayo huenda wengine wakayaona kuwa tu kasoro za utu, kama vile wivu, milipuko ya hasira, ugomvi, na kuwaonea wengine kijicho. Ni nani anayeweza kusema kwamba yeye ameacha kabisa kutembea kupatana na mwili?

11, 12. Ni uandalizi gani ambao Yehova amefanya ili kutusaidia kushinda sheria ya dhambi na kifo, na ni lazima tufanye nini ili tupate kibali cha Mungu?

11 Tunafurahi kama nini kwamba Yehova amefanya iwezekane kwetu kuishinda sheria hiyo ya dhambi na kifo! Yesu alisema hivi: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” Kwa kukubali upendo wa Mungu na kuwa na imani katika dhabihu ya ukombozi ya Yesu Kristo, tunaweza kuwekwa huru kutokana na hukumu ya dhambi tuliyorithi. (Yoh. 3:16-18) Kwa hiyo, huenda tukachochewa kusema hivi kama Paulo: “Shukrani kwa Mungu kupitia Yesu Kristo Bwana wetu!”

12 Hali yetu ni kama ya mtu anayetibiwa ugonjwa mbaya. Ikiwa tunataka kupona kabisa ni lazima tufuate maagizo ya daktari. Ingawa kuwa na imani katika dhabihu ya ukombozi kunaweza kutuweka huru kutokana na sheria ya dhambi na kifo, bado sisi si wakamilifu na tuna dhambi. Mengi zaidi yanahusika ili kuwa na afya nzuri ya kiroho na kupata kibali na baraka za Mungu. Kuhusu kutimiza lile “takwa la uadilifu la Sheria,” Paulo anatuambia pia kwamba ni lazima tutembee kupatana na roho.

Unaweza Kutembeaje Kupatana na Roho?

13. Inamaanisha nini kutembea kupatana na roho?

13 Tunapotembea, tunasonga hatua kwa hatua kuelekea mahali fulani ambapo tunakusudia kufika. Hivyo, ili kutembea kupatana na roho tunahitaji kuendelea kufanya maendeleo ya kiroho, lakini hilo halimaanishi tunafikia ukamilifu wa kiroho. (1 Tim. 4:15) Ni lazima tujitahidi kwa kadiri ya uwezo wetu kutembea, au kuishi, kupatana na mwongozo wa roho. “Kutembea kwa roho” kunatuongoza kupata kibali cha Mungu.—Gal. 5:16.

14. Wale wanaoishi ‘kupatana na mwili’ wana mwelekeo gani?

14 Katika barua hiyohiyo kwa Waroma, Paulo alizungumza kuhusu aina mbili za watu ambao wanakaza akili juu ya mambo mawili yanayotofautiana kabisa. (Soma Waroma 8:5.) Hapa neno “mwili” halimaanishi tu mwili halisi. Katika Biblia, neno “mwili” nyakati nyingine linatumiwa kumaanisha hali ya dhambi na kutokamilika kwa mwili wetu. Hali hiyo ndiyo inayosababisha pambano kati ya mwili na akili, pambano ambalo Paulo alitaja awali. Hata hivyo, tofauti na Paulo, wale wanaoishi ‘kupatana na mwili’ hawajaribu hata kidogo kupambana na tamaa zao mbaya. Badala ya kuchunguza yale ambayo Mungu anataka wafanye na kukubali msaada ambao ameandaa, watu hao wana mwelekeo wa ‘kukaza akili zao juu ya mambo ya mwili.’ Mara nyingi wanakaza akili zao juu ya kutosheleza tamaa zao za mwili na kuponda raha. Kinyume na hilo, wale wanaoishi ‘kupatana na roho’ wana mwelekeo wa kukaza akili zao juu ya “mambo ya roho,” yaani, maandalizi na utendaji wa kiroho.

15, 16. (a) Kukaza akili juu ya jambo fulani kunawezaje kuathiri mtazamo wa akili wa mtu? (b) Tunaweza kusema nini kuhusu mambo ambayo watu wengi leo wanakazia akili?

15 Soma Waroma 8:6. Ili kufanya jambo lolote, jema au baya, ni lazima mtu akaze akili juu ya jambo hilo. Watu wanaokaza sikuzote akili zao juu ya mambo ya mwili wanasitawisha haraka mtazamo wa akili au mwelekeo ambao unakazia kabisa mambo ya mwili. Kwa kawaida, hisia zao, mapendezi, na mawazo yao yako juu ya mambo hayo tu.

16 Watu wengi leo wanajishughulisha na nini? Mtume Yohana aliandika hivi: “Kila kitu kilicho katika ulimwengu—tamaa ya mwili na tamaa ya macho na mtu kujionyesha mali yake maishani—hakitokani na Baba, bali hutokana na ulimwengu.” (1 Yoh. 2:16) Tamaa hizo zinatia ndani mambo kama vile upotovu wa kingono, umashuhuri, na mali. Vitabu, majarida, magazeti, sinema, vipindi vya televisheni, na Intaneti vimejaa mambo hayo, hasa kwa sababu hayo ndiyo mambo ambayo watu wengi wanayataka kabisa na wanayakazia akili. Hata hivyo, “kukaza akili juu ya mwili humaanisha kifo,” yaani, kifo cha kiroho sasa na kifo cha kimwili hivi karibuni. Kwa nini? “Kwa sababu kukaza akili juu ya mwili humaanisha uadui na Mungu, kwa maana mwili haujitiishi chini ya sheria ya Mungu, nao kwa kweli hauwezi kujitiisha. Kwa hiyo wale wanaopatana na mwili hawawezi kumpendeza Mungu.”—Rom. 8:7, 8.

17, 18. Tunaweza jinsi gani kuendelea kukaza akili juu ya roho, na matokeo yatakuwa nini tukifanya hivyo?

17 Kwa upande mwingine, “kukaza akili juu ya roho humaanisha uzima na amani,” yaani, uzima wa milele wakati ujao na pia kuwa na amani ya moyoni na amani pamoja na Mungu sasa. Tunaweza jinsi gani kuendelea “kukaza akili juu ya roho”? Ni kwa kukaza akili zetu kwa ukawaida juu ya mambo ya roho na kuruhusu mwelekeo na mtazamo wa kiroho usitawi ndani yetu. Tunapofanya hivyo, tunaonyesha kwamba akili yetu ‘inajitiisha chini ya sheria ya Mungu’ na ‘inapatana na’ mawazo yake. Tunapopatwa na kishawishi, tutakuwa na hakika kuhusu jambo tunalopaswa kufanya. Tutachochewa kufanya uamuzi unaofaa, uamuzi ambao unapatana na roho.

18 Kwa hiyo, ni muhimu kukaza akili zetu juu ya mambo ya roho. Tunafanya hivyo kwa ‘kukaza akili zetu kwa ajili ya utendaji,’ kwa kujenga maisha yetu juu ya mambo ya kiroho ambayo yanatia ndani kusali kwa ukawaida, kusoma na kujifunza Biblia, kuhudhuria mikutano, na kushiriki katika huduma ya Kikristo. (1 Pet. 1:13) Badala ya kuruhusu mambo ya mwili yatukengeushe, acheni tukaze akili zetu juu ya mambo ya roho. Hivyo, tutaendelea kutembea kupatana na roho. Tukifanya hivyo tutapata baraka, kwa kuwa kukaza akili juu ya roho humaanisha uzima na amani.—Gal. 6:7, 8.

Je, Unaweza Kueleza?

• ‘Sheria ilikuwa haina uwezo’ gani, na Mungu alifanya nini ili kushinda tatizo hilo?

• “Sheria ya dhambi na kifo” ni nini, na tunaweza kuwekwa huru kutokana nayo jinsi gani?

• Ni lazima tufanye nini ili tusitawishe mtazamo wa “kukaza akili juu ya roho”?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 12, 13]

Je, unatembea kupatana na mwili au kupatana na roho?