Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Wakaaji wa Muda” Katika Ulimwengu Mwovu

“Wakaaji wa Muda” Katika Ulimwengu Mwovu

“Wakaaji wa Muda” Katika Ulimwengu Mwovu

‘Katika imani hawa wote walitangaza hadharani kwamba wao ni wageni na wakaaji wa muda katika nchi.’—EBR. 11:13.

1. Yesu alisema wafuasi wake wangekuwa na msimamo gani katika ulimwengu?

“WAO wamo ulimwenguni,” akasema Yesu kuhusu wanafunzi wake. Lakini akaeleza hivi: “Wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile ambavyo mimi si sehemu ya ulimwengu.” (Yoh. 17:11, 14) Hivyo, Yesu alionyesha waziwazi msimamo wa wafuasi wake wa kweli kuhusu “mfumo huu wa mambo,” ambao mungu wake ni Shetani. (2 Kor. 4:4) Ingawa wanaishi katika ulimwengu huu mwovu, wao si sehemu ya ulimwengu. Hali yao katika mfumo huu ingekuwa kama ile ya “wageni na wakaaji wa muda.”—1 Pet. 2:11.

Waliishi Kama “Wakaaji wa Muda”

2, 3. Kwa nini tunaweza kusema kwamba Enoko, Noa, Abrahamu, na Sara waliishi kama “wageni na wakaaji wa muda”?

2 Tangu nyakati za kale, watumishi waaminifu wa Yehova wamekuwa tofauti sana na watu wengine katika ulimwengu usiomwogopa Mungu ambamo wanaishi. Kabla ya Gharika, Enoko na Noa ‘walitembea pamoja na Mungu wa kweli.’ (Mwa. 5:22-24; 6:9) Wote wawili walikuwa wahubiri jasiri wa hukumu za Yehova juu ya ulimwengu mwovu wa Shetani. (Soma 2 Petro 2:5; Yuda 14, 15.) Kwa sababu walitembea pamoja na Mungu katika ulimwengu usiomwogopa Mungu, Enoko alikuwa “amempendeza Mungu vema” na Noa “alionekana kuwa mtu asiye na kosa kati ya watu wa siku zake.”—Ebr. 11:5; Mwa. 6:9.

3 Abrahamu na Sara walimtii Mungu na kuacha maisha yenye starehe ya jiji katika Uru la Wakaldayo na kukubali maisha magumu ya kuhama-hama katika nchi ya kigeni. (Mwa. 11:27, 28; 12:1) Mtume Paulo aliandika hivi: “Kwa imani Abrahamu, alipoitwa, alitii kwa kutoka akaenda na kuingia mahali alipokusudiwa kupokea kuwa urithi; naye akatoka, ijapokuwa hakujua mahali alipokuwa akienda. Kwa imani alikaa kama mgeni katika nchi ya ahadi kama katika nchi ya ugenini, akakaa katika mahema pamoja na Isaka na Yakobo, warithi pamoja naye wa ahadi ileile.” (Ebr. 11:8, 9) Kuhusu watumishi kama hao waaminifu wa Yehova, Paulo alisema hivi: “Katika imani hawa wote walikufa, ijapokuwa hawakupata utimizo wa zile ahadi, bali waliziona kwa mbali na kuzikaribisha na kutangaza hadharani kwamba wao ni wageni na wakaaji wa muda katika nchi.”—Ebr. 11:13.

Onyo kwa Waisraeli

4. Ni onyo gani ambalo Waisraeli walipewa kabla ya kuingia na kukaa katika nchi yao?

4 Wazao wa Abrahamu, yaani, Waisraeli, wakawa wengi na hatimaye wakapangwa kuwa taifa lililokuwa na nchi yao wenyewe na sheria zilizoandikwa. (Mwa. 48:4; Kum. 6:1) Watu wa Israeli hawakupaswa kusahau kamwe kwamba Mmiliki halisi wa nchi yao alikuwa Yehova. (Law. 25:23) Walikuwa kama wapangaji wanaopaswa kuheshimu maagizo ya Mwenye nyumba. Zaidi ya hayo, walipaswa kukumbuka kwamba “mwanadamu haishi kwa mkate tu”; hawakupaswa kuruhusu utajiri wa kimwili uwafanye wamsahau Yehova. (Kum. 8:1-3) Kabla ya kukaa katika nchi yao, Waisraeli walipewa onyo hili: “Itatukia kwamba Yehova Mungu wako atakapokuleta katika nchi ambayo aliwaapia mababu zako Abrahamu, Isaka na Yakobo, kwamba atakupa, majiji makubwa na yenye kupendeza ambayo wewe hukuyajenga, na nyumba zilizojaa vitu vyote vizuri na ambazo hukuzijaza, na mashimo ya maji yaliyochimbwa ambayo hukuyachimba, mashamba ya mizabibu na mizeituni ambayo hukuipanda, nawe utakapokuwa umekula na kushiba, jiangalie usije ukamsahau Yehova.”—Kum. 6:10-12.

5. Kwa nini Yehova alilikataa taifa la Israeli, na alichagua taifa gani jipya?

5 Hilo halikuwa onyo ambalo halina msingi. Katika siku za Nehemia, kikundi cha Walawi kilikumbuka kwa aibu yale yaliyotokea baada ya Waisraeli kuanza kuimiliki Nchi ya Ahadi. Baada ya watu wa Israeli kukaa katika nyumba zenye starehe na kuwa na divai na chakula kingi, “wakaanza kula na kushiba na kunenepa.” Wakamwasi Mungu, na hata kuwaua manabii ambao aliwatuma wawaonye. Hivyo, Yehova akawaacha mikononi mwa maadui wao. (Soma Nehemia 9:25-27; Hos. 13:6-9) Baadaye, chini ya utawala wa Waroma, Wayahudi hao wasio na imani hata walifikia hatua ya kumuua Masihi aliyeahidiwa! Yehova aliwakataa na kuchagua taifa jipya, taifa la Israeli la kiroho.—Mt. 21:43; Mdo. 7:51, 52; Gal. 6:16.

“Si Sehemu ya Ulimwengu”

6, 7. (a) Unaweza kuelezaje maneno ambayo Yesu alisema kuhusu msimamo wa wafuasi wake kuelekea ulimwengu? (b) Kwa nini Wakristo wa kweli hawakupaswa kuwa sehemu ya mfumo wa Shetani?

6 Kama ilivyoonyeshwa mwanzoni mwa makala hii, Kichwa cha kutaniko la Kikristo, Yesu Kristo, alionyesha wazi kwamba wafuasi wake wangejitenga na ulimwengu, yaani, mfumo mwovu wa Shetani. Muda mfupi kabla ya kifo chake, Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Kama mngekuwa sehemu ya ulimwengu, ulimwengu ungependa kilicho chake. Sasa kwa sababu ninyi si sehemu ya ulimwengu, bali nimewachagua ninyi kutoka ulimwenguni, kwa sababu hiyo ulimwengu unawachukia ninyi.”—Yoh. 15:19.

7 Kadiri Ukristo ulivyoenea, je, Wakristo walipaswa kuwa sehemu ya ulimwengu, na kuiga mazoea yake? Hapana. Mahali popote walipoishi, walipaswa kuwa tofauti kabisa na mfumo wa Shetani. Miaka 30 hivi baada ya kifo cha Kristo, mtume Petro aliwaandikia hivi Wakristo waliokuwa wakiishi sehemu mbalimbali zilizokuwa chini ya utawala wa Waroma: “Wapendwa, nawahimiza ninyi kama wageni na wakaaji wa muda kwamba mwendelee kujiepusha na tamaa za kimwili, ambazo ndizo huendelea kupambana na nafsi. Dumisheni mwenendo wenu ukiwa mzuri katikati ya mataifa.”—1 Pet. 1:1; 2:11, 12.

8. Mwanahistoria mmoja alisema nini kuhusu uhusiano wa Wakristo wa karne ya kwanza na ulimwengu?

8 Akithibitisha kwamba Wakristo wa karne ya kwanza walijiendesha kama “wageni na wakaaji wa muda” katika maeneo mbalimbali yaliyokuwa chini ya utawala wa Waroma, mwanahistoria Kenneth Scott Latourette aliandika hivi: “Ni jambo linalojulikana vizuri katika historia kwamba katika karne tatu za kwanza za Ukristo, Wakristo waliteswa daima na mara nyingi mateso hayo yalikuwa makali . . . Kulikuwa na mashtaka mbalimbali. Kwa sababu walikataa kushiriki katika sherehe za kipagani, Wakristo waliitwa watu wasioamini kwamba kuna Mungu. Kwa kuwa hawakujihusisha na mambo mengi yaliyokuwa yakifanywa katika jamii—kama vile sherehe za kipagani, vitumbuizo vya umma ambavyo Wakristo waliviona kuwa vimejaa imani, upotovu wa maadili, na mazoea ya kipagani—Wakristo walidhihakiwa kuwa wanachukia jamii ya wanadamu.”

Kutoutumia Ulimwengu kwa Ukamili

9. Tukiwa Wakristo wa kweli, tunathibitisha jinsi gani kwamba sisi ‘hatuchukii jamii ya wanadamu’?

9 Hali ikoje leo? Kuhusiana na “mfumo mwovu wa mambo wa sasa,” msimamo wetu ni kama ule wa Wakristo wa karne ya kwanza. (Gal. 1:4) Kwa sababu hiyo, wengi wanatuelewa vibaya na hata baadhi yao wanatuchukia. Hata hivyo, bila shaka kwa kweli sisi ‘hatuchukii jamii ya wanadamu.’ Kwa sababu tunawapenda wanadamu wenzetu, tunahubiri nyumba kwa nyumba, tunajitahidi kabisa kumhubiria kila mtu “habari njema ya ufalme” wa Mungu. (Mt. 22:39; 24:14) Tunafanya hivyo kwa sababu tunasadiki kwamba hivi karibuni serikali ya Ufalme wa Yehova chini ya Kristo itakomesha utawala wa wanadamu ambao si mkamilifu, na badala yake kuleta mfumo mpya wa mambo wenye uadilifu.—Dan. 2:44; 2 Pet. 3:13.

10, 11. (a) Tunautumiaje ulimwengu kwa kadiri? (b) Taja baadhi ya njia ambazo Wakristo walio macho wanaepuka kuutumia ulimwengu kwa ukamili.

10 Kwa sababu mwisho wa mfumo huu wa mambo unakaribia sana, tukiwa watumishi wa Yehova tunatambua kwamba huu si wakati wa kutafuta maisha ya starehe katika ulimwengu huu unaoangamia. Tunatii maneno ya mtume Paulo: “Nasema hili, akina ndugu, wakati uliobaki umepungua. Tangu sasa . . . wale wanaonunua wawe kama wale wasio na kitu, na wale wanaoutumia ulimwengu wawe kama wale wasioutumia kwa ukamili; kwa maana tamasha ya ulimwengu huu inabadilika.” (1 Kor. 7:29-31) Lakini Wakristo wanautumiaje ulimwengu leo? Wanafanya hivyo kwa kutumia tekinolojia na njia za kisasa za mawasiliano ili kueneza ujuzi wa Biblia ulimwenguni pote katika lugha nyingi. Wanautumia ulimwengu kwa kadiri fulani ili kupata riziki. Wananunua bidhaa na kulipia huduma muhimu ulimwenguni. Hata hivyo, wanajitahidi kutoutumia ulimwengu kwa ukamili katika maana ya kwamba wanaweka mali na kazi za ulimwengu mahali panapofaa.Soma  1 Timotheo 6:9, 10.

11 Wakristo walio macho wanaepuka kuutumia ulimwengu kwa ukamili inapohusu elimu ya juu. Watu wengi katika ulimwengu huu wanaona kwamba elimu ya juu ni njia muhimu ya kupata maisha ya kifahari na ya utajiri. Lakini sisi Wakristo tunaishi kama wakaaji wa muda na tunafuatia miradi tofauti. Tunaepuka ‘kukaza akili juu ya mambo makuu.’ (Rom. 12:16; Yer. 45:5) Kwa kuwa sisi ni wafuasi wa Yesu, tunatii onyo lake: “Endeleeni kufungua macho yenu na mjilinde na kila namna ya tamaa, kwa sababu hata wakati mtu ana vitu vingi uzima wake hautokani na vitu alivyo navyo.” (Luka 12:15) Kwa hiyo, vijana Wakristo wanatiwa moyo kufuatia miradi ya kiroho, wakijitahidi kupata tu elimu itakayowasaidia kutimiza mahitaji yao ya msingi huku wakijitayarisha kumtumikia Yehova ‘kwa moyo, nafsi, nguvu, na akili yao yote.’ (Luka 10:27) Kwa kufanya hivyo, wanaweza kuwa ‘matajiri kwa Mungu.’—Luka 12:21; soma Mathayo 6:19-21.

Epuka Kulemewa na Mahangaiko ya Maisha

12, 13. Tunapotii maneno ya Yesu katika Mathayo 6:31-33 tunakuwa tofauti jinsi gani na watu wa ulimwengu?

12 Watumishi wa Yehova wanatofautiana na watu wa ulimwengu katika mtazamo wao kuelekea vitu vya kimwili. Kuhusu jambo hilo, Yesu aliwaambia wafuasi wake hivi: “Msihangaike kamwe na kusema, ‘Tutakula nini?’ au, ‘Tutakunywa nini?’ au, ‘Tutavaa nini?’ Kwa maana vyote hivi ndivyo vitu ambavyo mataifa yanafuatilia kwa tamaa. Kwa maana Baba yenu wa mbinguni anajua mnahitaji vitu hivi vyote. Basi, endeleeni kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake, nanyi mtaongezewa hivi vitu vingine vyote.” (Mt. 6:31-33) Kutokana na mambo waliyojionea wenyewe, waamini wenzetu wengi wamegundua kwamba Baba yetu wa mbinguni huwaandalia vitu wanavyohitaji.

13 “Kumcha Mungu na kuridhika ni faida kubwa.” (1 Tim. 6:6, Neno Agano Jipya) Hilo ni kinyume kabisa na maoni ya watu katika ulimwengu wa leo. Kwa mfano, vijana wanapofunga ndoa, wengi wao wanatazamia kupata ‘vitu vyote’ mara moja—nyumba yenye vitu vyote, gari zuri, na vitu vya kisasa zaidi vya elektroniki. Hata hivyo, Wakristo wanaoishi kama wakaaji wa muda hawaruhusu tamaa zao ziwaongoze kutafuta vitu vinavyopita kiasi na ambavyo hawana uwezo wa kuvipata. Kwa kweli, wengi wanastahili kupongezwa kwa sababu wameacha vitu fulani vya kimwili vya starehe ili kutumia wakati na nguvu zaidi katika utumishi wa Yehova wakiwa wahubiri wenye bidii wa Ufalme. Wengine wanatumikia wakiwa mapainia, Wanabetheli, waangalizi wanaosafiri, au wamishonari. Sisi sote tunathamini kama nini utumishi wa moyo wote wa waabudu wenzetu wa Yehova!

14. Ni jambo gani tunalojifunza kutokana na mfano ambao Yesu aliutoa kuhusu mpandaji?

14 Katika mfano wake wa mpandaji, Yesu alisema kwamba “mahangaiko ya mfumo huu wa mambo na nguvu za udanganyifu wa utajiri” zinaweza kulisonga neno la Mungu mioyoni mwetu na kutufanya tusizae matunda. (Mt. 13:22) Kuishi na kuridhika kama wakaaji wa muda katika mfumo huu wa mambo kunatusaidia tusianguke katika mtego huo. Badala yake, kunatusaidia kuwa na jicho “rahisi,” au jicho lisilokengeushwa, linalokazia jambo moja, yaani, Ufalme wa Mungu na kutanguliza masilahi yake katika maisha yetu.—Mt. 6:22.

“Ulimwengu Unapitilia Mbali”

15. Ni maneno gani ya mtume Yohana yanayoongoza mtazamo na mwenendo wa Wakristo wa kweli katika ulimwengu huu?

15 Sababu ya msingi inayotufanya sisi tukiwa Wakristo kujiona kuwa “wageni na wakaaji wa muda” katika ulimwengu huu ni kwamba tunasadiki kuwa siku za ulimwengu huu zimehesabiwa. (1 Pet. 2:11; 2 Pet. 3:7) Mtazamo huo unatuongoza tunapofanya maamuzi maishani, tunapofuatia mapendezi yetu, na miradi yetu. Mtume Yohana aliwashauri waamini wenzake wasiupende ulimwengu au vitu vilivyo katika ulimwengu kwa sababu “ulimwengu unapitilia mbali na pia tamaa yake, lakini yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.”—1 Yoh. 2:15-17.

16. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tumechaguliwa kuwa watu walio tofauti?

16 Waisraeli waliambiwa kwamba ikiwa wangemtii Yehova, wangekuwa ‘mali yake ya pekee kutoka kati ya vikundi vingine vyote vya watu.’ (Kut. 19:5) Walipokuwa waaminifu, Waisraeli walikuwa tofauti na mataifa mengine yote katika ibada na njia yao ya maisha. Vivyo hivyo leo, Yehova amejichagulia watu ambao wako tofauti sana na ulimwengu wa Shetani. Tunaambiwa hivi: ‘Kataa kabisa kutomwogopa Mungu na tamaa za kilimwengu na uishi kwa utimamu wa akili na uadilifu na ujitoaji-kimungu katikati ya mfumo wa mambo wa sasa, huku tukilingojea tumaini la furaha na kufunuliwa kwenye utukufu kwa Mungu mkuu na kwa Mwokozi wetu, Kristo Yesu, aliyejitoa mwenyewe kwa ajili yetu ili atukomboe sisi kutoka katika kila namna ya uasi-sheria na kujisafishia mwenyewe watu walio wake kwa njia ya pekee, walio na bidii kwa ajili ya kazi njema.’ (Tito 2:11-14) “Watu” hao ni Wakristo watiwa-mafuta pamoja na mamilioni ya “kondoo wengine” wa Yesu, ambao wanawasaidia na kuwategemeza watiwa-mafuta.—Yoh. 10:16.

17. Kwa nini watiwa-mafuta na waandamani wao hawatajuta kamwe kwamba waliishi kama wakaaji wa muda katika ulimwengu huu mwovu?

17 Watiwa-mafuta wana “tumaini la furaha” la kutawala pamoja na Kristo huko mbinguni. (Ufu. 5:10) Tumaini la uzima wa milele litakapotimia hapa duniani, kondoo wengine hawatakuwa tena wakaaji wa muda katika ulimwengu mwovu. Watakuwa na nyumba maridadi na vinywaji na vyakula vingi. (Zab. 37:10, 11; Isa. 25:6; 65:21, 22) Tofauti na Waisraeli, kondoo wengine hawatasahau kamwe kwamba mambo yote hayo yanatoka kwa Yehova, “Mungu wa dunia yote.” (Isa. 54:5) Watiwa-mafuta na kondoo wengine hawatajuta kwamba waliishi kama wakaaji wa muda katika ulimwengu huu mwovu.

Ungejibuje?

• Ni katika njia gani wanaume waaminifu wa zamani waliishi kama wakaaji wa muda?

• Wakristo wa karne ya kwanza walijiendesha jinsi gani kuelekea ulimwengu?

• Wakristo wa kweli wanajitahidi jinsi gani kutoutumia ulimwengu kikamili?

• Kwa nini hatutajuta kamwe kwa sababu ya kuishi kama wakaaji wa muda katika ulimwengu huu mwovu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 18]

Wakristo wa karne ya kwanza walijiepusha na vitumbuizo vyenye jeuri na upotovu wa maadili