Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wasaidie Wanaume Wafanye Maendeleo ya Kiroho

Wasaidie Wanaume Wafanye Maendeleo ya Kiroho

Wasaidie Wanaume Wafanye Maendeleo ya Kiroho

“Tangu sasa na kuendelea utakuwa ukiwavua watu wakiwa hai.”—LUKA 5:10.

1, 2. (a) Wanaume waliitikiaje mahubiri ya Yesu? (b) Tutachunguza nini katika makala hii?

YESU na wanafunzi wake walipokuwa wakihubiri kotekote Galilaya, walipanda mashua na kwenda mahali pasipo na watu. Lakini umati uliwafuata kwa miguu. Watu ambao walikuja siku hiyo walikuwa “wanaume karibu elfu tano, bila kuhesabu wanawake na watoto wachanga.” (Mt. 14:21) Pindi nyingine, umati wa watu ulimjia Yesu ili uponywe na kumsikiliza. Umati huo ulitia ndani “wanaume elfu nne, bila kuhesabu wanawake na watoto wachanga.” (Mt. 15:38) Ni wazi kwamba wanaume wengi walikuwa miongoni mwa watu waliomjia Yesu na kupendezwa na mafundisho yake. Kwa kweli, alitazamia wengine wengi wakubali kweli, kwa kuwa baada ya kuwasaidia wanafunzi wake kuvua samaki kimuujiza, Yesu alimwambia Simoni hivi: ‘Tangu sasa na kuendelea mtakuwa mkiwavua watu wakiwa hai.’ (Luka 5:10) Wanafunzi wake walipaswa kushusha nyavu zao ndani ya bahari ya wanadamu na kutazamia kwamba ‘wangevua’ watu kutia ndani wanaume wengi.

2 Leo, wanaume pia wanapendezwa na ujumbe unaotegemea Maandiko ambao tunahubiri na wanaukubali. (Mt. 5:3) Hata hivyo, wanaume wengi wanasitasita na hawafanyi maendeleo ya kiroho. Tunaweza kuwasaidiaje? Ingawa Yesu hakuanzisha huduma ya pekee ya kuwatafuta wanaume, bila shaka alizungumzia mambo ambayo yaliwahusu wanaume katika siku zake. Tukitumia mfano wake, acheni tuchunguze jinsi tunavyoweza kuwasaidia wanaume kushughulikia mambo matatu ya kawaida yanayowahangaisha leo: (1) kutafuta riziki, (2) kuogopa maoni ya watu wengine, na (3) kuhisi kwamba hawastahili.

Kutafuta Riziki

3, 4. (a) Wanaume wengi wanahangaikia nini hasa? (b) Kwa nini wanaume fulani wanatanguliza utafutaji wa riziki badala ya mambo ya kiroho?

3 Mwandishi mmoja alimwambia Yesu hivi: “Mwalimu, mimi nitakufuata mahali popote unapoenda.” Lakini Yesu alipomwambia kwamba “Mwana wa binadamu hana mahali popote pa kulaza kichwa chake,” mwandishi huyo alibadili nia. Inaonekana kwamba mwandishi huyo alikuwa na mahangaiko kuhusu chakula na mahali ambapo angeishi kwa kuwa Biblia haisemi kwamba alikuja kuwa mfuasi wa Kristo.—Mt. 8:19, 20.

4 Kwa kawaida, wanaume wanatanguliza vitu vya kimwili badala ya mambo ya kiroho. Jambo muhimu kwa wengi wao ni kupata elimu ya juu zaidi na kazi yenye mshahara mnono. Wanafikiri kwamba ni muhimu zaidi kutafuta pesa kwa sababu zitawasaidia kupata riziki kuliko kujifunza Biblia na kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu. Huenda wakavutiwa na mambo ambayo Biblia inafundisha, lakini “mahangaiko ya mfumo huu wa mambo na nguvu za udanganyifu za utajiri” zinasonga upendezi wowote kuelekea Biblia ambao wanaweza kuwa nao. (Marko 4:18, 19) Fikiria jinsi Yesu alivyowasaidia wanafunzi wake kurekebisha maoni yao kuhusu mambo waliyohitaji kutanguliza.

5, 6. Ni nini kilichowasaidia Andrea, Petro, Yakobo, na Yohana kurekebisha maoni yao kuhusu kutanguliza kazi ya kuhubiri badala ya kutanguliza utafutaji wa riziki?

5 Andrea na ndugu yake Simoni Petro walikuwa wakifanya pamoja biashara ya uvuvi. Yohana, na ndugu yake Yakobo, walikuwa pia wakifanya biashara hiyo na baba yao, Zebedayo. Biashara yao ilikuwa imesitawi sana hivi kwamba waliwaajiri wafanyakazi. (Marko 1:16-20) Andrea na Yohana waliposikia kwa mara ya kwanza habari za Yesu kutoka kwa Yohana Mbatizaji, walisadiki kwamba walikuwa wamempata Masihi. Andrea akamwambia ndugu yake Simoni Petro habari hizo, na labda Yohana alimwambia Yakobo, ndugu yake. (Yoh. 1:29, 35-41) Katika miezi iliyofuata, wote wanne walikuwa pamoja na Yesu alipokuwa akihubiri katika Galilaya, Yudea, na Samaria. Kisha hao wanafunzi wanne wakarudia biashara yao ya kuvua samaki. Walipendezwa na mambo ya kiroho, lakini kazi ya kuhubiri haikuwa muhimu sana kwao.

6 Baadaye, Yesu aliwaalika Petro na Andrea wamfuate na kuwa “wavuvi wa watu.” Wanafunzi hao wawili waliitikiaje? “Mara moja wakaziacha nyavu, wakamfuata.” Yakobo na Yohana walifanya vivyo hivyo. “Mara moja wakaacha ile mashua na baba yao, wakamfuata.” (Mt. 4:18-22) Ni nini kilichowasaidia wanaume hao kuanza huduma ya wakati wote? Je, ulikuwa uamuzi wa ghafula uliotegemea hisia? Hapana! Katika miezi iliyotangulia, wanaume hao walimsikiliza Yesu, wakaona akifanya miujiza, wakaona bidii yake kwa ajili ya uadilifu, na kushuhudia watu wengi sana wakikubali ujumbe ambao alihubiri. Mambo hayo yaliwasaidia kuwa na imani yenye nguvu zaidi katika Yehova na kumtegemea zaidi!

7. Tunaweza kuwasaidiaje wanafunzi wa Biblia wajifunze kutegemea uwezo wa Yehova wa kuwatunza watu wake?

7 Tunaweza kumwiga Yesu jinsi gani katika kuwasaidia wanafunzi wa Biblia wajifunze kumtegemea Yehova? (Met. 3:5, 6) Jambo hilo linategemea sana njia yetu ya kufundisha. Tunapofundisha, tunaweza kukazia kwamba Mungu anaahidi kuwa atatubariki sana ikiwa tutatanguliza mambo ya Ufalme. (Soma Malaki 3:10; Mathayo 6:33.) Ingawa tunaweza kutumia maandiko mbalimbali kukazia jinsi Yehova anavyowatunza watu wake, hatupaswi kusahau kwamba mfano wetu wenyewe unaweza kuwachochea. Kuwasimulia mambo ambayo tumejionea maishani mwetu kunaweza kuwasaidia sana wanafunzi wa Biblia wajifunze kumtegemea Yehova. Tunaweza pia kuwasimulia mambo yanayotia moyo tunayosoma katika machapisho yetu. *

8. (a) Kwa nini ni muhimu kwa mwanafunzi wa Biblia ‘kuonja na kuona kwamba Yehova ni mwema’? (b) Tunaweza kumsaidiaje mwanafunzi wetu ajionee mwenyewe kwamba Yehova ni mwema?

8 Mwanafunzi wa Biblia hawezi kusitawisha imani yenye nguvu kwa kusoma tu na kusikiliza jinsi ambavyo wengine wamebarikiwa na Yehova. Mwanafunzi wa Biblia anahitaji pia kujionea wema wa Yehova katika maisha yake binafsi. Mtunga-zaburi aliimba hivi: “Onjeni mwone ya kuwa Yehova ni mwema; mwenye furaha ni mwanamume ambaye humkimbilia.” (Zab. 34:8) Tunaweza kumsaidiaje mwanafunzi aone kwamba Yehova ni mwema? Tuseme kwamba mwanafunzi ambaye ana mahangaiko ya kifedha anajaribu pia kuacha zoea fulani baya, kama vile kuvuta sigara, kucheza kamari, au kunywa kupita kiasi. (Met. 23:20, 21; 2 Kor. 7:1; 1 Tim. 6:10) Kumfundisha mwanafunzi huyo kusali na kuomba msaada wa Mungu ili kushinda zoea baya, je, hakutamsaidia kuona kwamba Yehova ni mwema? Fikiria pia jambo linaloweza kutokea ikiwa tutamtia moyo mwanafunzi atangulize mambo ya kiroho kwa kutenga wakati wa kujifunza Biblia kila juma, kutayarisha na kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Bila shaka, imani yake itakuwa na nguvu zaidi anapojionea mwenyewe Yehova akibariki jitihada zake!

Kuogopa Maoni ya Wengine

9, 10. (a) Kwa nini Nikodemo na Yosefu, mwenyeji wa Arimathea, walikuwa wanafunzi wa Yesu kwa siri? (b) Kwa nini wanaume fulani leo wanasitasita kumfuata Kristo?

9 Huenda wanaume fulani wakasitasita kumfuata Kristo kikamili kwa sababu ya kusongwa na wengine. Nikodemo na Yosefu, mwenyeji wa Arimathea, walikuwa wanafunzi wa Yesu kwa siri kwa sababu waliogopa mambo ambayo Wayahudi wengine wangesema au kufanya ikiwa wangejua. (Yoh. 3:1, 2; 19:38) Walikuwa na sababu ya kuogopa. Viongozi wa kidini walimchukia sana Yesu hivi kwamba mtu yeyote aliyemwamini alifukuzwa kutoka katika sinagogi.—Yoh. 9:22.

10 Katika sehemu fulani leo, mwanamume akipendezwa sana na mambo ya Mungu, Biblia, au dini, anaweza kusumbuliwa na wafanyakazi wenzake, marafiki, au watu wa ukoo. Katika sehemu nyingine, huenda hata ikawa hatari kusema kwamba unabadili dini yako. Mwanamume anaweza kushutumiwa vikali zaidi hasa ikiwa anatumika katika jeshi, anajihusisha sana na siasa, au ana cheo kikubwa katika jamii. Kwa mfano, mwanamume fulani huko Ujerumani alikiri hivi: “Mambo ambayo ninyi Mashahidi mnahubiri kuhusu Biblia ni ya kweli. Lakini nikiamua kuwa Shahidi leo, kesho kila mtu atakuwa amejua jambo hilo. Wengine watanionaje kazini, katika ujirani, na katika klabu ambacho mimi na familia yangu tunashiriki? Siwezi kuvumilia hali hiyo.”

11. Yesu aliwasaidiaje wanafunzi wake kutowaogopa wanadamu?

11 Ingawa mitume wote wa Yesu walikuwa jasiri, nyakati nyingine waliwaogopa wanadamu. (Marko 14:50, 66-72) Yesu aliwasaidiaje kufanya maendeleo hata ingawa walisongwa sana na watu wengine? Yesu alichukua hatua ili kuwatayarisha wanafunzi wake kukabiliana na upinzani ambao wangepata baadaye. Alisema hivi: “Wenye furaha ni ninyi wakati wowote ule watu wanapowachukia ninyi, na wakati wowote ule watu wanapowatenga ninyi na kuwashutumu na kulitupa nje jina lenu kuwa ovu kwa ajili ya Mwana wa binadamu.” (Luka 6:22) Yesu aliwaonya wafuasi wake kwamba wanapaswa kutazamia kushutumiwa. Shutuma yoyote ambayo wangepata ingekuwa ni “kwa ajili ya Mwana wa binadamu.” Yesu aliwahakikishia pia kwamba Mungu angewatunza ikiwa tu wangemtegemea Yeye ili awasaidie na kuwapa nguvu. (Luka 12:4-12) Zaidi ya hayo, Yesu aliwaalika wapya ili washirikiane kwa uhuru na wanafunzi wake na kuanzisha urafiki nao.—Marko 10:29, 30.

12. Ni katika njia gani tunaweza kuwasaidia wapya ili wasiwaogope wanadamu?

12 Sisi pia tunahitaji kuwasaidia wanafunzi wa Biblia kutowaogopa wanadamu. Mara nyingi ni rahisi zaidi kushinda tatizo tunapojua mapema jinsi ya kukabiliana nalo. (Yoh. 15:19) Kwa mfano, kwa nini usimsaidie mwanafunzi kutayarisha majibu rahisi yenye kusadikisha yanayotegemea Biblia kwa maswali na vipingamizi ambavyo huenda wafanyakazi wenzake na wengine wakatokeza? Zaidi ya kuwa rafiki yake wa karibu, tunaweza kumtambulisha kwa washiriki wengine wa kutaniko, hasa wale ambao huenda wana mapendezi kama yake. Zaidi ya yote, tunapaswa kumfundisha kusali kwa ukawaida na kutoka moyoni. Jambo hilo linaweza kumsaidia amkaribie Mungu na kumfanya Yehova kuwa Kimbilio na Mwamba wake.—Soma Zaburi 94:21-23; Yakobo 4:8.

Kujihisi Kwamba Hawastahili

13. Hisia za kutostahili zinaweza jinsi gani kuwafanya wengine wakatae mambo ya kiroho?

13 Wanaume fulani wanakataa mambo ya kiroho kwa sababu hawasomi vizuri au hawawezi kujieleza vizuri au kwa sababu tu wanaona haya. Wanaume wengine wanaogopa kutoa maoni yao au kueleza hisia zao hadharani. Huenda wakaona kwamba ni vigumu kujifunza, kutoa maelezo katika mikutano ya Kikristo, au kuwaeleza wengine kuhusu imani yao. Ndugu mmoja Mkristo anakiri hivi: “Nilipokuwa na umri mdogo, nilikuwa nikienda haraka mlangoni, nilijifanya kuwa ninapiga kengele, halafu nilitoka polepole na kwenda nikitumaini kwamba hakuna mtu ambaye angenisikia au kuniona. . . . Wazo la kuhubiri nyumba kwa nyumba lilinifanya niwe mgonjwa kihalisi.”

14. Kwa nini wanafunzi wa Yesu walishindwa kumponya mvulana fulani aliyekuwa na roho waovu?

14 Fikiria jinsi ambavyo wanafunzi wa Yesu walivyokosa uhakika waliposhindwa kumponya mvulana fulani aliyekuwa na roho waovu. Baba ya mwana huyo alimjia Yesu na kusema: ‘Mwanangu, ana kifafa na ni mgonjwa, kwa maana yeye huanguka ndani ya moto na ndani ya maji mara nyingi; nami nilimleta kwa wanafunzi wako, lakini hawakuweza kumponya.’ Yesu alimfukuza huyo roho mwovu na kumponya mvulana huyo. Baadaye wanafunzi walimjia Yesu na kumuuliza: “Kwa nini sisi hatukuweza kumfukuza?” Yesu akawajibu hivi: “Ni kwa sababu ya imani yenu kidogo, kwa maana kwa kweli ninawaambia, Mkiwa na imani inayotoshana na mbegu ya haradali, mtauambia mlima huu, ‘Ondoka hapa uende pale,’ nao utaondoka, na hakuna jambo litakalowashinda.” (Mt. 17:14-20) Imani katika Yehova inahitajiwa ili kushinda matatizo ambayo ni kama mlima. Ni nini kinachotokea mtu anapokosa kukazia fikira jambo hilo na badala yake anaanza kukazia fikira uwezo wake mwenyewe? Atakosa kufanikiwa na hilo litafanya akose uhakika.

15, 16. Tunaweza kumsaidiaje mwanafunzi wa Biblia ashinde hisia ya kwamba hastahili?

15 Njia nzuri ya kumsaidia mtu anayepambana na hisia za kutostahili ni kumtia moyo amfikirie Yehova badala ya kujifikiria mwenyewe. Petro aliandika hivi: “Jinyenyekezeni chini ya mkono wenye nguvu wa Mungu, ili awainue ninyi katika wakati unaofaa; huku mkitupa mahangaiko yenu yote juu yake.” (1 Pet. 5:6, 7) Hilo linamaanisha kwamba tunapaswa kumsaidia mwanafunzi wetu wa Biblia asitawishe hali ya kiroho. Mtu anayependa mambo ya kiroho anathamini sana mambo ya kiroho. Anapenda Neno la Mungu na kuonyesha ‘tunda la roho’ katika maisha yake. (Gal. 5:22, 23) Ni mwanamume anayedumu katika sala. (Flp. 4:6, 7) Zaidi ya hayo, anamwomba Mungu ampe ujasiri na nguvu anazohitaji ili kupambana na hali yoyote au kutimiza mgawo wowote kwa mafanikio.—Soma 2 Timotheo 1:7, 8.

16 Huenda wanafunzi fulani pia wakahitaji kusaidiwa inavyofaa kuboresha uwezo wao wa kusoma na kuzungumza. Huenda wengine wakahisi kwamba hawastahili kumtumikia Mungu kwa sababu ya mambo mabaya ambayo walitenda kabla ya kumjua Yehova. Katika hali yoyote ile, huenda wanahitaji tu tuwasaidie kwa upendo na kwa subira. Yesu alisema hivi: “Watu wenye afya hawahitaji tabibu, bali wenye kuugua ndio wanaomhitaji.”—Mt. 9:12.

‘Wavue’ Wanaume Wengi Zaidi

17, 18. (a) Tunaweza kuwasaidia jinsi gani wanaume wengi zaidi katika huduma yetu? (b) Tutajifunza nini katika makala inayofuata?

17 Tunatumaini kwamba wanaume wengi zaidi watakubali ujumbe wenye kuridhisha sana ambao unapatikana tu katika Biblia. (2 Tim. 3:16, 17) Basi tunaweza kuwasaidia jinsi gani wanaume wengi zaidi katika huduma yetu? Kwa kutumia wakati mwingi zaidi kuhubiri jioni, Jumamosi na Jumapili alasiri, au siku za sikukuu wakati ambapo wanaume wengi wako nyumbani. Inapowezekana, tunaweza kuomba kuzungumza na mwanamume mwenye-nyumba. Acheni tuwahubirie isivyo rasmi wafanyakazi wenzetu wanaume inapofaa na kuwasaidia waume ambao si waamini katika kutaniko.

18 Tunapomhubiria kila mtu tunayekutana naye, tunaweza kuwa na hakika kwamba watu wenye mioyo minyoofu watakubali kweli. Acheni tuwasaidie kwa subira wote ambao wanapendezwa na kweli kwa unyoofu. Hata hivyo, tunaweza kuwasaidia jinsi gani wanaume waliobatizwa kutanikoni wajitahidi kustahili kupata mapendeleo katika tengenezo la Mungu? Makala inayofuata itajibu swali hilo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Ona Vitabu vya Mwaka vya Mashahidi wa Yehova na pia masimulizi ya maisha yanayochapishwa katika Mnara wa Mlinzi na Amkeni!

Ungejibuje?

• Wanaume wanaweza kusaidiwa jinsi gani ili watangulize mambo ya kiroho?

• Tunaweza kuwasaidiaje wapya washinde msongo kutoka kwa wengine?

• Ni nini kinachoweza kuwasaidia wengine washinde hisia ya kwamba hawastahili?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 25]

Je, unatafuta nafasi za kuwahubiria wanaume habari njema?

[Picha katika ukurasa wa 26]

Unaweza kumtayarishaje mwanafunzi wa Biblia ili aweze kukabiliana na majaribu?