Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wazoeze Wengine ili Wajitahidi Kufikia Mapendeleo

Wazoeze Wengine ili Wajitahidi Kufikia Mapendeleo

Wazoeze Wengine ili Wajitahidi Kufikia Mapendeleo

“Kila mtu aliyefundishwa kikamili atakuwa kama mwalimu wake.”—LUKA 6:40.

1. Wakati wa huduma yake duniani, Yesu aliwekaje msingi wa kutaniko la pekee?

AKIMALIZIA simulizi lake la Injili, mtume Yohana aliandika hivi: “Kwa kweli, kuna mambo mengine mengi pia aliyofanya Yesu, ambayo, kama yangeandikwa kirefu, nadhani ulimwengu wenyewe haungeweza kuwa na nafasi ya kuviweka vitabu vya kukunjwa ambavyo vingeandikwa.” (Yoh. 21:25) Kati ya mambo yote ambayo Yesu alitimiza wakati wa huduma yake ya muda mfupi lakini yenye matokeo mazuri sana ni kuwatafuta, kuwazoeza, na kuwapanga wanaume ambao wangeongoza kazi baada ya yeye kurudi mbinguni. Aliporudi mbinguni mwaka wa 33 W.K., Yesu aliacha msingi wa kutaniko la pekee ambalo lingeongezeka haraka na kuwa na maelfu ya watu.—Mdo. 2:41, 42; 4:4; 6:7.

2, 3. (a) Kwa nini kuna uhitaji mkubwa sana wa wanaume waliobatizwa kujitahidi kufikia mapendeleo? (b) Ni nini kitakachozungumziwa katika makala hii?

2 Kukiwa na wahubiri wa Ufalme wenye bidii zaidi ya milioni saba katika makutaniko zaidi ya 100,000 ulimwenguni pote leo, bado kuna uhitaji wa wanaume wa kuongoza katika mambo ya kiroho. Kwa mfano, kuna uhitaji mkubwa sana wa wazee Wakristo. Wale ambao wanajitahidi kufikia pendeleo hilo la utumishi wanastahili kupongezwa, kwa kuwa ‘wanatamani kazi njema.’—1 Tim. 3:1.

3 Hata hivyo, ni lazima wanaume watimize matakwa fulani ili wastahili kupata mapendeleo katika kutaniko. Kuwa tu na elimu ya ulimwengu au uzoefu maishani hakumtayarishi mwanamume kwa ajili ya kazi hiyo. Ili atumikie ifaavyo katika pendeleo hilo, ni lazima mwanamume astahili kiroho. Zaidi ya kuwa na uwezo au kutimiza mambo mbalimbali, ni lazima awe na sifa za kiroho. Wanaume katika kutaniko wanaweza kusaidiwa jinsi gani ili wastahili? Yesu alisema hivi: “Kila mtu aliyefundishwa kikamili atakuwa kama mwalimu wake.” (Luka 6:40) Katika makala hii, tutazungumzia baadhi ya njia ambazo yule Mwalimu Mkuu, Yesu Kristo, alitumia kuwasaidia wanafunzi wake wastahili kupata mapendeleo makubwa zaidi, na tutaona mambo tunayoweza kujifunza kutokana na yale aliyofanya.

“Nimewaita Ninyi Rafiki”

4. Yesu alionyeshaje kwamba alikuwa rafiki wa kweli kwa wanafunzi wake?

4 Yesu aliwatendea wanafunzi wake kama marafiki, wala si kama watu wa hali ya chini. Alitumia wakati pamoja nao, aliwaamini, na ‘kuwajulisha mambo yote ambayo alikuwa amesikia kutoka kwa Baba yake.’ (Soma Yohana 15:15.) Wazia jinsi walivyosisimka Yesu alipojibu swali lao: “Ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” (Mt. 24:3, 4) Pia, aliwaambia wafuasi wake mawazo na hisia zake. Kwa mfano, usiku ambao alisalitiwa, Yesu alimchukua Petro, Yakobo, na Yohana pamoja naye katika bustani ya Gethsemane, ambako alisali kwa bidii akiwa na mahangaiko mengi moyoni. Huenda mitume hao watatu hawakusikia maneno ambayo Yesu alikuwa akisema katika sala, lakini bila shaka waliona jinsi alivyokuwa akiteseka sana. (Marko 14:33-38) Fikiria pia jinsi mitume hao watatu walivyotiwa nguvu awali walipomwona Yesu akigeuka sura. (Marko 9:2-8; 2 Pet. 1:16-18) Urafiki wa karibu ambao Yesu alisitawisha pamoja na wanafunzi wake uliwatia nguvu ili kutimiza migawo mizito baadaye.

5. Wazee Wakristo wanaweza kusitawisha urafiki na wengine katika njia zipi?

5 Kama Yesu, wazee Wakristo leo wanasitawisha urafiki na wengine na kuwasaidia. Wanasitawisha urafiki mchangamfu na wa karibu pamoja na waamini wenzao kwa kutumia wakati kuwaonyesha upendezi wa kibinafsi. Ingawa wazee wanatambua umuhimu wa kutunza siri, kuna mambo fulani wanayoweza kuzungumza na wengine. Wazee wanawaamini ndugu zao na wanazungumza nao kuhusu kweli za Kimaandiko ambazo wao wenyewe wamejifunza. Wazee hawamdharau kamwe mtumishi wa huduma mwenye umri mdogo. Badala yake, wanamwona kuwa mwanamume wa kiroho mwenye uwezo ambaye anatimiza utumishi wenye thamani kwa faida ya kutaniko.

“Niliweka Kielelezo kwa Ajili Yenu”

6, 7. Yesu aliwawekea wanafunzi wake kielelezo gani na kilikuwa na uvutano gani juu yao?

6 Ingawa wanafunzi wa Yesu walithamini mambo ya kiroho, nyakati nyingine fikira zao ziliongozwa na malezi na utamaduni wao. (Mt. 19:9, 10; Luka 9:46-48; Yoh. 4:27) Hata hivyo, Yesu hakuwafokea au kuwatisha wanafunzi wake. Wala hakuwalemea kwa kuwaambia wafanye mambo ambayo hawangeweza kufanya au kuwashauri wafanye jambo fulani huku yeye mwenyewe akifanya jambo tofauti. Badala yake, Yesu aliwafundisha kupitia mfano wake.—Soma Yohana 13:15.

7 Yesu aliwaachia wanafunzi wake kielelezo gani? (1 Pet. 2:21) Aliishi maisha rahisi ili aweze kuwahudumia wengine kwa uhuru. (Luka 9:58) Yesu alikuwa mwenye kiasi na sikuzote mafundisho yake yalitegemea Maandiko. (Yoh. 5:19; 17:14, 17) Alikuwa mwenye urafiki na mwenye fadhili. Alichochewa na upendo katika mambo yote aliyofanya. (Mt. 19:13-15; Yoh. 15:12) Mfano wa Yesu ulikuwa na uvutano mzuri juu ya mitume wake. Kwa mfano, Yakobo hakuogopa alipokabili kifo, badala yake aliendelea kumtumikia Mungu kwa ushikamanifu mpaka alipouawa. (Mdo. 12:1, 2) Yohana alifuata kwa uaminifu hatua za Yesu kwa miaka zaidi ya 60.—Ufu. 1:1, 2, 9.

8. Wazee wanawawekea wanaume vijana na wengine mfano gani?

8 Wazee ambao wanajidhabihu, ni wanyenyekevu, na wenye upendo, wanaweka mfano ambao wanaume vijana wanahitaji. (1 Pet. 5:2, 3) Isitoshe, wazee ambao ni mfano mzuri katika imani, kufundisha, maisha ya Kikristo, na katika huduma, wanaridhika wanapojua kwamba wengine wanaweza kuiga imani yao.—Ebr. 13:7.

‘Yesu Aliwapa Maagizo, Akawatuma’

9. Tunajuaje kwamba Yesu aliwazoeza wanafunzi wake kufanya kazi ya kueneza injili?

9 Baada ya kuhubiri kwa bidii kwa miaka miwili hivi, Yesu alipanua kazi ya kuhubiri kwa kuwatuma mitume wake 12 ili wahubiri. Hata hivyo, aliwapa maagizo kwanza. (Mt. 10:5-14) Kabla ya kuulisha umati wa maelfu ya watu kimuujiza, Yesu aliwaambia wanafunzi wake jinsi alivyotaka wawapange watu na kugawa chakula. (Luka 9:12-17) Basi, ni wazi kwamba Yesu aliwazoeza wanafunzi wake kwa kuwapa mwongozo hususa na ulio wazi. Kielelezo chake katika kuwazoeza wengine, pamoja na uvutano wenye nguvu wa roho takatifu, uliwawezesha baadaye mitume kupanga kazi kubwa sana ya kuhubiri ambayo ilifanywa mwaka wa 33 W.K. na kuendelea.

10, 11. Wapya wanaweza kuzoezwa jinsi gani hatua kwa hatua?

10 Leo, mwanamume anaanza kupokea maagizo ya kiroho anapokubali funzo la Biblia. Huenda tukahitaji kumsaidia kujua kusoma vizuri. Tunaendelea kumsaidia tunapojifunza Biblia pamoja naye. Anapoanza kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida, mazoezi yake ya kiroho yataendelea anaposhiriki katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, anapokuwa mhubiri ambaye hajabatizwa, na kadhalika. Baada ya kubatizwa, anaweza kuzoezwa pia katika mambo kama vile kushiriki katika kutunza Jumba la Ufalme. Baada ya muda, ndugu anaweza kusaidiwa kuona mambo anayohitaji kufanya ili astahili kuwa mtumishi wa huduma.

11 Mzee anapompa ndugu aliyebatizwa mgawo, anahitaji kumweleza vizuri utaratibu unaofaa wa kitengenezo na kumpa maagizo anayohitaji. Ni muhimu ndugu anayezoezwa aelewe jambo analotazamiwa kufanya. Ikiwa kazi aliyopewa ni ngumu kwake, mzee mwenye upendo haamui haraka-haraka kwamba ndugu huyo hastahili. Badala yake, mzee huyo anamweleza tena kwa fadhili mambo hususa anayohitaji kufanya na utaratibu wa kufuata. Wazee wanafurahi wanapoona wanaume wakiitikia vizuri jitihada kama hizo na kupata shangwe ya kuwatumikia wengine.—Mdo. 20:35.

“Anayesikiliza Shauri Ni Mwenye Hekima”

12. Ni nini kilichofanya mashauri ya Yesu yawe yenye matokeo mazuri?

12 Yesu aliwazoeza wanafunzi wake kwa kumpa kila mmoja mashauri kulingana na uhitaji wake. Kwa mfano, aliwakemea Yakobo na Yohana kwa kutaka kuomba moto ushuke kutoka mbinguni na kuwaangamiza Wasamaria fulani ambao hawakumpokea. (Luka 9:52-55) Mama ya Yakobo na Yohana alipomfikia Yesu kwa niaba yao na kuomba kwamba wapewe vyeo vikubwa katika Ufalme, Yesu aliwaambia hivi ndugu hao moja kwa moja: “Kuketi upande wangu wa kuume na upande wangu wa kushoto sina haki ya kutoa, bali wataketi wale ambao Baba yangu amewatayarishia.” (Mt. 20:20-23) Nyakati zote, Yesu alitoa mashauri yaliyo wazi, yanayofaa, na yanayotegemea kabisa kanuni za Mungu. Aliwafundisha wanafunzi wake kufikiria na kutenda kupatana na kanuni hizo. (Mt. 17:24-27) Yesu alitambua pia udhaifu wa wafuasi wake na hakutazamia watende kwa njia kamilifu. Mashauri yake yalichochewa na upendo wa kweli.—Yoh. 13:1.

13, 14. (a) Ni nani anayehitaji shauri? (b) Toa mifano inayoonyesha shauri ambalo mzee anaweza kumpa mtu ambaye hafanyi maendeleo ya kiroho.

13 Kila mwanamume anayejitahidi kufikia mapendeleo katika kutaniko la Kikristo anahitaji mashauri ya Kimaandiko mara kwa mara. Andiko la Methali 12:15 linasema hivi: “Anayesikiliza shauri ni mwenye hekima.” Ndugu mmoja kijana anasema hivi: “Niligundua kwamba tatizo langu kubwa zaidi lilikuwa kupambana na udhaifu wangu. Mzee mmoja alinishauri na kunisaidia kuelewa kwamba sikuhitaji kuwa mkamilifu ili kutumika.”

14 Wazee wakiona kwamba mwenendo fulani usiofaa unamzuia mwanamume kufanya maendeleo ya kiroho, wanachukua hatua ya kumrekebisha upya katika roho ya upole. (Gal. 6:1) Nyakati nyingine, wazee wanahitaji kumshauri mtu ili arekebishe tabia fulani isiyofaa. Kwa mfano, ikiwa ndugu fulani anaonekana hapendi kujitoa sana, huenda ikafaa kwa mzee kumwonyesha kwamba Yesu alikuwa mhubiri wa Ufalme mwenye bidii na aliwapa wafuasi wake kazi ya kufanya wanafunzi. (Mt. 28:19, 20; Luka 8:1) Ikiwa ndugu anaonekana kuwa na kimbelembele, mzee anaweza kumwonyesha jinsi Yesu alivyowasaidia wanafunzi Wake kuona hatari za kutafuta umashuhuri. (Luka 22:24-27) Namna gani ikiwa ndugu ana mwelekeo wa kutosamehe? Mfano wa yule mtumwa ambaye alikataa kusamehe deni dogo hata ingawa yeye mwenyewe alikuwa amesamehewa deni kubwa zaidi unaweza kumsaidia sana. (Mt. 18:21-35) Shauri linapohitajiwa, ni vizuri wazee walitoe haraka iwezekanavyo.—Soma Methali 27:9.

“Uwe Ukijizoeza”

15. Familia ya mwanamume inaweza kumsaidiaje ili awatumikie wengine?

15 Wazee wanaongoza katika kuwazoeza wanaume wajitahidi kufikia mapendeleo, lakini wengine wanaweza kuwasaidia wazee katika jitihada hizo. Kwa mfano, familia ya mwanamume inaweza na inapaswa kumsaidia ajitahidi kufikia mapendeleo. Na ikiwa yeye tayari ni mzee, atafaidika akiungwa mkono na mke mwenye upendo na watoto wasio na ubinafsi. Utayari wao wa kumruhusu alitumikie pia kutaniko ni muhimu ili afanikiwe kutimiza madaraka yake. Roho yao ya kujidhabihu inamletea shangwe na inathaminiwa sana na wengine.—Met. 15:20; 31:10, 23.

16. (a) Ni nani aliye na daraka la msingi la kujitahidi kufikia mapendeleo? (b) Mwanamume anaweza kujitahidi jinsi gani kufikia mapendeleo katika kutaniko?

16 Ingawa wengine wanaweza kumsaidia na kumuunga mkono, mwanamume mwenyewe ndiye aliye na daraka la msingi la kujitahidi kufikia mapendeleo. (Soma Wagalatia 6:5.) Bila shaka, si lazima ndugu awe mtumishi wa huduma au mzee ili awasaidie wengine na kushiriki kikamili katika huduma. Hata hivyo, kujitahidi kufikia mapendeleo katika kutaniko kunamaanisha kujitahidi kutimiza matakwa ya kustahili ambayo yameonyeshwa katika Maandiko. (1 Tim. 3:1-13; Tito 1:5-9; 1 Pet. 5:1-3) Kwa hiyo, ikiwa mwanamume anatamani kutumika akiwa mtumishi wa huduma au mzee lakini bado hajawekwa rasmi, anapaswa kukazia fikira mambo anayohitaji kurekebisha ili afanye maendeleo ya kiroho. Hilo linamaanisha kusoma Biblia kwa ukawaida, kujifunza kibinafsi kwa bidii, kutafakari kwa uzito, kusali kutoka moyoni, na kushiriki kwa bidii katika huduma ya Kikristo. Kwa kufanya mambo hayo, anaweza kutumia kibinafsi shauri hili ambalo Paulo alimpa Timotheo: “Uwe ukijizoeza ujitoaji-kimungu ukiwa ni shabaha yako.”—1 Tim. 4:7.

17, 18. Ndugu aliyebatizwa anaweza kufanya nini ikiwa mahangaiko, hisia za kutostahili, au kukosa tamaa ya kuwatumikia wengine kunamzuia asijitahidi kufikia mapendeleo?

17 Lakini namna gani ikiwa mwanamume hajitahidi kufikia mapendeleo kwa sababu ya mahangaiko au kuhisi kwamba hastahili? Itakuwa vizuri akifikiria mambo mengi sana ambayo Yehova Mungu na Yesu Kristo wanatufanyia. Kwa kweli, Yehova “hutubebea mzigo wetu kila siku.” (Zab. 68:19) Kwa hiyo, Baba yetu wa mbinguni anaweza kumsaidia ndugu akubali madaraka katika kutaniko. Ndugu ambaye hatumikii akiwa mtumishi wa huduma au mzee atafaidika pia akifikiria uhakika wa kwamba kuna uhitaji mkubwa wa wanaume wakomavu ambao wanaweza kukubali mapendeleo ya utumishi katika tengenezo la Mungu. Kutafakari kuhusu mambo hayo kunaweza kumchochea ndugu ajitahidi kushinda hisia zisizofaa. Anaweza kusali ili apate roho takatifu, akikumbuka kwamba tunda la roho linatia ndani sifa ya amani na kujizuia, sifa ambazo zinahitajiwa ili kushinda mahangaiko na hisia za kutostahili. (Luka 11:13; Gal. 5:22, 23) Na anaweza kuwa na hakika kabisa kwamba Yehova anawabariki wote wanaojitahidi kufikia mapendeleo wakiwa na nia nzuri.

18 Je, inawezekana kwamba kukosa tamaa ya kutumika kunamzuia mwanamume aliyebatizwa asijitahidi kufikia mapendeleo? Ni nini kinachoweza kumsaidia ndugu ambaye hana tamaa ya kutumika? Mtume Paulo aliandika hivi: “[Mungu], kwa ajili ya mapenzi yake mema, anatenda ndani yenu ili ninyi muwe na nia na kutenda pia.” (Flp. 2:13) Tamaa ya kuwatumikia wengine inatoka kwa Mungu, na roho ya Yehova inaweza kumwimarisha mtu ili aweze kutoa utumishi mtakatifu. (Flp. 4:13) Zaidi ya hayo, Mkristo anaweza kusali ili Mungu amchochee kufanya jambo linalofaa.—Zab. 25:4, 5.

19. Kusimamishwa kwa “wachungaji saba, ndiyo, watawala wadogo wanane” kunatuhakikishia nini?

19 Yehova anabariki jitihada za wanaume wazee za kuwazoeza wengine. Pia, anawabariki wale ambao wanakubali kuzoezwa na kujitahidi kufikia mapendeleo katika kutaniko. Maandiko yanatuhakikishia kwamba kati ya watu wa Mungu “wachungaji saba, ndiyo, watawala wadogo wanane,” yaani, idadi inayohitajiwa ya wanaume wenye uwezo, watasimamishwa ili waongoze katika tengenezo la Yehova. (Mika 5:5) Ni baraka kama nini kwamba wanaume wengi sana Wakristo wanazoezwa na kwa unyenyekevu wanajitahidi kufikia mapendeleo ya utumishi ili kumletea Yehova sifa!

Ungejibuje?

• Yesu aliwasaidia namna gani wanafunzi wake wastahili kupata mapendeleo makubwa zaidi?

• Wazee wanaweza kumwiga Yesu jinsi gani wanapowasaidia wanaume katika kutaniko ili waongoze?

• Familia ya mwanamume inatimiza sehemu gani katika kumsaidia ajitahidi kufikia mapendeleo?

• Mwanamume mwenyewe anaweza kufanya nini ili ajitahidi kufikia mapendeleo?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 31]

Unaweza kumzoeza mwanafunzi wako wa Biblia katika njia gani anapojitahidi kufanya maendeleo?

[Picha katika ukurasa wa 32]

Wanaume wanaweza kuonyesha jinsi gani kwamba wanajitahidi kufikia mapendeleo?