Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehu Atetea Ibada Safi

Yehu Atetea Ibada Safi

Yehu Atetea Ibada Safi

YEHU alitetea ibada safi. Alitimiza daraka lake kwa nguvu, bila kuchelewa, kwa uharaka, kwa bidii, na kwa ujasiri. Yehu alionyesha sifa ambazo tunapaswa kuiga.

Yehu alipewa mgawo wakati taifa la Israeli lilipokuwa katika hali mbaya. Nchi hiyo ilikuwa chini ya uvutano mwovu wa Yezebeli, mjane wa Ahabu na mama ya Mfalme Yehoramu, aliyekuwa akitawala. Aliendeleza madhehebu ya Baali badala ya ibada ya Yehova, aliwaua manabii wa Mungu, na kuwachafua watu kwa “uasherati” na “ulozi wake mwingi.” (2 Fal. 9:22; 1 Fal. 18:4, 13) Yehova aliamuru nyumba yote ya Ahabu iangamizwe, kutia ndani Yehoramu na Yezebeli. Yehu alipaswa kuwa mstari wa mbele katika kuchukua hatua hiyo.

Yehu anatajwa kwa mara ya kwanza katika Maandiko akiwa ameketi pamoja na wakuu wa jeshi wakati Waisraeli walipokuwa wakipigana na Wasiria huko Ramothi-gileadi. Yehu alikuwa ofisa mwenye cheo cha juu, au labda kamanda wa jeshi la Israeli. Nabii Elisha alimtuma mmoja wa wana wa manabii ili amtie Yehu mafuta kuwa mfalme na ampe amri ya kumuua kila mwanamume wa nyumba ya Ahabu yenye kuasi imani.—2 Fal. 8:28; 9:1-10.

Maofisa wenzake walipomuuliza Yehu kuhusu kusudi la ziara hiyo, Yehu alisita kuwaambia. Lakini aliposukumwa, aliwaambia ukweli, na yeye pamoja na wenzake wakaanza kupanga njama ya kumwangamiza Yehoramu. (2 Fal. 9:11-14) Inaelekea kwamba wanajeshi fulani walichukia na kupinga sheria zilizowekwa na nyumba ya Ahabu iliyotawala na pia walichukia uvutano mbaya wa Yezebeli. Kwa vyovyote vile, Yehu alifikiria kwa makini sana kutafuta njia bora ya kutimiza mgawo wake.

Mfalme Yehoramu alikuwa ameumizwa vitani na alienda katika mji wa Yezreeli ili apone. Yehu alijua kwamba ili mpango wake ufanikiwe, habari hiyo haikupaswa kamwe kufika Yezreeli. Yehu alisema hivi: “Msiache yeyote akimbie kutoka jijini na kupeleka habari Yezreeli.” (2 Fal. 9:14, 15) Labda alitazamia kupata upinzani fulani kutoka kwa wanajeshi ambao walikuwa washikamanifu kwa Yehoramu. Yehu alitaka kuzuia upinzani wowote kama huo usitokee.

AENDESHA GARI LA VITA KWA KASI SANA!

Ili ashambulie kwa ghafula, Yehu aliendesha gari lake la vita kutoka Ramothi-gileadi hadi Yezreeli, umbali wa kilomita 72. Alipokuwa akikaribia kwa kasi Yezreeli, mlinzi aliyekuwa juu ya mnara aliona “umati unaosukasuka wa watu wa Yehu.” (2 Fal. 9:17) Inaelekea sana kwamba Yehu alienda na jeshi kubwa ili awe na uhakika wa kutimiza kusudi lake.

Akitambua kwamba Yehu mwenye ujasiri alikuwa katika moja ya magari hayo ya vita, huyo mlinzi alisema hivi: “Yeye huendesha kiwazimu.” (2 Fal. 9:20) Ikiwa Yehu alizoea kuendesha gari lake kwa njia hiyo, basi bila shaka wakati huu aliendesha kwa kasi hata zaidi ili atimize kusudi lake.

Baada ya kukataa kuwaambia jambo lolote wale wajumbe wawili ambao walitumwa kwake, Yehu alikutana na Mfalme Yehoramu na rafiki yake Ahazia, mfalme wa Yuda, kila mmoja wao akiwa katika gari lake mwenyewe la vita. Yehoramu alipouliza, “Je, kuna amani, Yehu?”alijibiwa hivi kwa hasira: “Kunaweza kuwa na amani gani wakati kungali na uasherati wa Yezebeli mama yako na ulozi wake mwingi?” Yehoramu alishtuka aliposikia maneno hayo akageuka ili akimbie. Lakini Yehu aliendesha gari lake kwa kasi hata zaidi! Akachukua upinde na kupiga mshale ambao ulipenya ndani ya moyo wa Yehoramu, na mfalme huyo akaanguka na kufa ndani ya gari lake la vita. Ingawa Ahazia alifanikiwa kukimbia, baadaye Yehu alimpata na kuamuru auawe pia.—2 Fal. 9:22-24, 27.

Mshiriki mwingine aliyeuawa katika nyumba ya Ahabu alikuwa Malkia Yezebeli aliyekuwa mwovu. Kwa kufaa, Yehu alimwita Yezebeli ‘mtu aliyelaaniwa.’ Yehu alipofika Yezreeli, alimwona Yezebeli akitazama chini kupitia dirishani katika jumba la mfalme. Bila kupoteza wakati, Yehu aliwaamuru maofisa wa makao ya mfalme wamwangushe chini Yezebeli kutoka dirishani. Kisha Yehu akamkanyaga-kanyaga kwa farasi malkia huyo aliyechafua taifa lote la Israeli. Baada ya hapo, Yehu aliwaangamiza washiriki wengine wengi wa nyumba ya Ahabu aliyekuwa mwovu.—2 Fal. 9:30-34; 10:1-14.

Ingawa jeuri haipendezi, tunapaswa kutambua kwamba katika siku hizo, Yehova aliwatumia watumishi wake kutekeleza hukumu zake. Maandiko yanasema hivi: “Kuanguka kwa Ahazia kulitokana na Mungu, alipomjia Yehoramu; naye alipokuja, alienda pamoja na Yehoramu kwa Yehu mjukuu wa Nimshi, ambaye Yehova alikuwa amemtia mafuta ili aikatilie mbali nyumba ya Ahabu.” (2 Nya. 22:7) Alipoutupa mwili wa Yehoramu kutoka katika gari lake la vita, Yehu alitambua kwamba tendo hilo lilitimiza ahadi ya Yehova ya kumwadhibu Ahabu kwa sababu ya kumuua Nabothi. Zaidi ya hayo, Yehu alikuwa ameamriwa ‘alipize kisasi damu ya watumishi wa Mungu’ iliyomwagwa na Yezebeli.—2 Fal. 9:7, 25, 26; 1 Fal. 21:17-19.

Leo, hakuna mtumishi yeyote wa Yehova anayetumia nguvu za kimwili kupigana na wapinzani wa ibada safi. Mungu anasema: “Kisasi ni changu.” (Ebr. 10:30) Lakini ili kuondoa watu wanaoweza kuchafua kutaniko, huenda wazee Wakristo wakalazimika kutenda kwa ujasiri kama Yehu. (1 Kor. 5:9-13) Na washiriki wote wa kutaniko wanahitaji kuazimia kuepuka kushirikiana na watu waliotengwa na ushirika.—2 Yoh. 9-11.

YEHU HAKUVUMILIA USHINDANI WOWOTE KUMWELEKEA YEHOVA

Kusudi la Yehu la kutimiza mgawo wake linaonyeshwa na maneno ambayo alimwambia Yehonadabu aliyekuwa mwaminifu: “Enda pamoja nami, utazame jinsi ambavyo sivumilii ushindani wowote kumwelekea Yehova.” Yehonadabu alikubali mwaliko huo, akapanda gari la vita la Yehu, na kwenda pamoja naye Samaria. Wakiwa huko, Yehu “alitenda kwa ujanja, kusudi awaharibu waabudu wa Baali.”—2 Fal. 10:15-17, 19.

Yehu alitangaza kwamba alikusudia kutoa “dhabihu kubwa” kwa ajili ya Baali. (2 Fal. 10:18, 19) Msomi mmoja anasema kwamba “Yehu alitumia maneno ya werevu.” Ingawa neno alilotumia katika andiko hilo “kwa ujumla linamaanisha ‘dhabihu,’ linatumiwa pia kumaanisha ‘kuwachinja’ waasi-imani.” Kwa sababu Yehu hakutaka mwabudu yeyote wa Baali akose tukio hilo, aliwakusanya waabudu wote katika nyumba ya Baali na kuwapa mavazi ya pekee. “Mara tu alipomaliza kutoa lile toleo la kuteketezwa,” Yehu akawaagiza wanaume 80 wenye silaha wawachinje waabudu wa Baali. Kisha akaagiza nyumba ya Baali ibomolewe na kufanya mahali hapo pawe choo, na kupafanya pasifae kwa ajili ya ibada.—2 Fal. 10:20-27.

Ni kweli kwamba Yehu alimwaga damu nyingi. Hata hivyo, Maandiko yanaonyesha kwamba yeye ni mwanamume jasiri ambaye aliwaweka Waisraeli huru kutokana na utawala wenye uonevu wa Yezebeli na familia yake. Ili kiongozi yeyote wa Israeli afanikiwe kufanya hivyo, alihitaji kuwa mwanamume jasiri, mwenye bidii, na mwenye kuazimia. Kamusi moja ya Biblia inasema hivi: “Ilikuwa kazi ngumu na ilitekelezwa kikamili kabisa. Labda kuchukua hatua hafifu hakungekomesha ibada ya Baali katika Israeli.”

Bila shaka, Wakristo wanahitaji kuonyesha sifa fulani nzuri ambazo Yehu alikuwa nazo kwa sababu ya hali ambazo wanakabili leo. Kwa mfano, tunapaswa kutendaje tunaposhawishiwa kushiriki katika utendaji fulani ambao Yehova anashutumu? Tunapaswa kukataa katakata, kwa ujasiri, na kwa bidii. Inapohusu ujitoaji wetu kwa Mungu, hatupaswi kamwe kuvumilia ushindani wowote kumwelekea Yehova.

UWE MWANGALIFU ILI UTEMBEE KATIKA SHERIA YA YEHOVA

Tunapata onyo katika sehemu ya mwisho ya simulizi hilo. Yehu ‘hakugeuka asifuate wale ndama wa dhahabu ambao walikuwa Betheli na Dani.’ (2 Fal. 10:29) Mtu ambaye alionekana kuwa mwenye bidii sana kwa ajili ya ibada safi angewezaje kuvumilia ibada ya sanamu?

Huenda Yehu aliamini kwamba kujitenga kwa ufalme wa Israeli kutoka kwa ufalme wa Yuda kulimaanisha kwamba falme hizo mbili zilipaswa kutengana kidini. Hivyo, kama wafalme wa kale wa Israeli walivyofanya, alijaribu kutenganisha falme hizo kwa kuendeleza ibada ya ndama. Lakini hilo lingeonyesha kwamba hakuwa na imani katika Yehova, ambaye alimfanya kuwa mfalme.

Yehova alimpongeza Yehu kwa sababu ‘alitenda vema kwa kufanya yaliyo sawa machoni pa Mungu.’ Hata hivyo, Yehu “hakuwa mwangalifu ili atembee katika sheria ya Yehova, Mungu wa Israeli, kwa moyo wake wote.” (2 Fal. 10:30, 31) Ukifikiria mambo mengine yote ambayo Yehu alikuwa amefanya, huenda ukashangazwa na kuhuzunishwa na jambo hilo. Hata hivyo, ni somo kwetu. Hatupaswi kamwe kupuuza uhusiano wetu pamoja na Yehova. Kila siku, tunahitaji kusitawisha ushikamanifu kwa Mungu kwa kujifunza Neno lake, kutafakari, na kusali kutoka moyoni kwa Baba yetu wa mbinguni. Hivyo basi, acheni tuwe waangalifu kabisa ili tuendelee kutembea katika sheria ya Yehova kwa moyo wetu wote.—1 Kor. 10:12.

[Sanduku katika ukurasa wa 4]

Yehu Katika Historia ya Ulimwengu

Mara nyingi wachambuzi wametilia shaka ikiwa watu wanaotajwa katika Maandiko waliwahi kuishi. Hivyo, je, kuna ushahidi wowote usiotegemea Biblia kumhusu Yehu?

Kuna angalau hati tatu kutoka katika nchi ya kale ya Ashuru zinazotaja mfalme huyo wa Israeli kwa jina. Inadaiwa kwamba moja ya hati hizo inaonyesha Yehu, au labda mmoja wa wajumbe wake, akimwinamia Mfalme Shalmanesa wa 3 wa Ashuru na kulipa ushuru. Maandishi yanayoambatana na picha hiyo yanasema hivi: “Ushuru wa Yehu (Ia-ú-a), mwana wa Omri (Hu-um-ri); Alinipa fedha, dhahabu, bakuli la saplu la dhahabu, chombo cha dhahabu cha kuwekea maua chenye kitako kilichochongoka, bilauri za dhahabu, ndoo za dhahabu, bati, fimbo ya mfalme, (na) kifaa cha mbao cha puruhtu [maana ya neno hilo haijulikani].” Yehu hakuwa “mwana wa Omri” moja kwa moja, lakini jina hilo lilitumiwa kuwahusu wafalme waliofuatana wa Israeli, inaelekea kwamba aliitwa hivyo kwa sababu ya umaarufu wa Omri na jinsi alivyojenga mji mkuu wa Israeli, Samaria.

Dai la mfalme wa Ashuru kuhusu ushuru uliolipwa na Yehu haliwezi kuthibitishwa. Hata hivyo, anamtaja Yehu mara tatu, yaani, katika hati fulani, kwenye sanamu ya Shalmanesa, na katika kumbukumbu za kihistoria za wafalme wa Ashuru. Habari hizo zote zinaonyesha wazi kabisa kwamba Yehu anayetajwa katika Biblia kwa kweli aliwahi kuishi.