Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unakumbuka?

Je, Unakumbuka?

Je, Unakumbuka?

Je, umesoma kwa makini matoleo ya hivi karibuni ya Mnara wa Mlinzi? Ona kama unaweza kujibu maswali yafuatayo:

• Olivétan alikuwa nani, na kwa nini tunapaswa kupendezwa na kazi yake?

Mfaransa Pierre Robert alijulikana kwa jina hilo. Wakati wa Marekebisho ya karne ya 16, alitafsiri Biblia katika lugha ya Kifaransa. Alipendelea neno “mwangalizi” badala ya “askofu,” na “kutaniko” badala ya “kanisa.” Katika sehemu nyingine, alitumia jina la Mungu “Yehova.”—9/1, ukurasa wa 18-20.

• Mungu alimaanisha nini alipowaambia Walawi: “Mimi ni fungu lako”?

Kila kabila la Israeli lilipata urithi wa nchi, lakini Yehova alikuwa “fungu” la Walawi. (Hes. 18:20) Walawi hawangerithi ardhi, lakini walipewa pendeleo la pekee la utumishi. Hata hivyo, Yehova alitosheleza mahitaji yao ya msingi. Leo, watu ambao wana pendeleo la kuendeleza kazi ya Ufalme wanaweza kuwa na hakika kwamba Mungu atawaandalia mahitaji yao ya lazima ya maisha.—9/15, ukurasa wa 7-8, 13.

• Tunajuaje mwaka ambao jiji la kale la Yerusalemu lilishindwa na Wababiloni?

Wanahistoria wa kale wanatoa sababu tofauti-tofauti zinazopingana kuhusu wafalme wa Babiloni na utawala wao. Hata hivyo, wasomi wanakubali kwamba Koreshi wa Pili alilishinda jiji la Babiloni mwaka wa 539 K.W.K., ambao ni mwaka muhimu. Wayahudi waliwekwa huru, na wakafika katika nchi yao mwaka wa 537 K.W.K. Biblia inasema kwamba walikaa uhamishoni kwa miaka 70. Basi ni wazi kwamba Yerusalemu lilishindwa mwaka wa 607 K.W.K. (2 Nya. 36:21, 22; Yer. 29:10; Dan. 9:1, 2)—10/1, ukurasa wa 26-31.

• Ni nini kinachoweza kumsaidia Mkristo kuamua ikiwa tafrija ya aina fulani ni yenye kujenga au haijengi?

Ili kuamua ikiwa tafrija ya aina fulani ni yenye kujenga na yenye kupendeza machoni pa Mungu, ni vizuri kujiuliza hivi: Ni tafrija gani? Nitashiriki wakati gani? Nitashiriki pamoja na nani?10/15, ukurasa wa 9-12.

• Kwa nini ni kosa kutoa mimba?

Mungu anaona uhai kuwa mtakatifu na anaona kiini-tete kuwa kiumbe kilicho hai na cha pekee. (Zab. 139:16) Kumuua mtoto ambaye hajazaliwa ni uuaji, kama inavyoonyeshwa na uhakika wa kwamba chini ya Sheria mtu ambaye alimuumiza mtoto ambaye hajazaliwa alionwa kuwa na hatia. (Kut. 21:22, 23)—11/1, ukurasa wa 6.

• Simulizi la Methali 7:6-23 linaweza kutusaidiaje kuepuka kutazama ponografia?

Andiko hilo linatuambia kuhusu kijana fulani mwanamume ambaye alitembea katika eneo ambalo lilijulikana kuwa na mwanamke mwenye maadili mapotovu. Mwanamke huyo akamtongoza. Leo, tunapaswa kuepuka vituo vya Intaneti ambavyo vina picha chafu za ngono, na ni muhimu kutafuta msaada wa Mungu kupitia sala hata kabla ya kuona picha hizo katika Intaneti.—11/15, ukurasa wa 9-10.

• Tunajuaje ikiwa dunia haitaisha mwaka wa 2012?

Kwa sababu ya mizunguko katika kalenda ya kale ya Wamaya, watu fulani wanafikiri kwamba dunia itaisha mwaka wa 2012. Lakini hilo haliwezekani, kwa kuwa Yehova aliiumba dunia ili ikaliwe. Biblia inasema kwamba dunia itadumu milele. (Mhu. 1:4; Isa. 45:18)—12/1, ukurasa wa 10.

• Ni waandikaji gani wa Biblia waliokuwapo siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K.?

Inaonekana kwamba waandikaji sita wa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo walikuwapo. Mitume watatu walikuwapo, Mathayo, Yohana, na Petro. Ndugu wawili wa kambo wa Yesu walikuwapo pia, Yakobo na Yuda. Na inaelekea kwamba kijana Marko alikuwapo.—12/1, ukurasa wa 22.