Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuongozwa na Roho ya Mungu Katika Karne ya Kwanza na Leo

Kuongozwa na Roho ya Mungu Katika Karne ya Kwanza na Leo

Kuongozwa na Roho ya Mungu Katika Karne ya Kwanza na Leo

‘Roho ileile moja inafanya utendaji huu wote.’—1 KOR. 12:11.

1. Tutazungumzia mambo gani katika funzo hili?

PENTEKOSTE. Neno hilo moja linatukumbusha matukio yenye kusisimua sana! (Mdo. 2:1-4) Kumiminwa kwa roho takatifu wakati huo katika karne ya kwanza kulibadili kabisa jinsi Mungu alivyoshughulika na watumishi wake. Katika makala iliyotangulia, tulichunguza baadhi ya njia ambazo roho ya Mungu iliwawezesha watu waaminifu walioishi zamani kutimiza migawo migumu na yenye maagizo mengi. Lakini kuna tofauti gani kati ya jinsi roho ya Mungu ilivyotenda kazi kabla ya nyakati za Ukristo na jinsi ilivyotenda kazi katika karne ya kwanza? Na Wakristo watafaidikaje kutokana na utendaji wa roho takatifu ya Mungu leo? Acheni tuone.

“Tazama! Kijakazi wa Yehova!”

2. Maria aliona utendaji wa roho takatifu jinsi gani?

2 Maria alikuwa katika chumba kikubwa cha juu huko Yerusalemu wakati roho takatifu iliyoahidiwa ilipomiminwa. (Mdo. 1:13, 14) Hata hivyo, kwa zaidi ya miongo mitatu kabla ya tukio hilo, Maria alikuwa ameona utendaji wa roho ya Yehova kwa njia za ajabu. Yehova alikuwa amehamisha uhai wa Mwana wake kutoka mbinguni hadi duniani, na kutunga mimba katika tumbo la uzazi la Maria alipokuwa angali bikira. Mimba aliyokuwa nayo ‘ilitokana na roho takatifu.’—Mt. 1:20.

3, 4. Maria alionyesha mtazamo gani, na tunaweza kumwiga jinsi gani?

3 Kwa nini Maria alipewa pendeleo hilo lisilo na kifani? Baada ya malaika kumweleza mapenzi ya Yehova kumhusu, Maria alisema hivi: “Tazama! Kijakazi wa Yehova! Na itendeke kwangu kulingana na tangazo lako.” (Luka 1:38) Maria aliposema hivyo, alionyesha mtazamo wa moyo ambao Mungu alikuwa tayari ameona. Jinsi alivyoitikia haraka habari hizo ilionyesha kwamba alikuwa tayari kukubali mapenzi ya Mungu katika jambo hilo. Hakuuliza swali lolote kuhusu jinsi ambavyo watu katika jamii wangeona ujauzito wake au ingekuwaje kwa uhusiano wake na mchumba wake. Kwa kusema kwamba yeye ni mtumishi wa hali ya chini kabisa, Maria alionyesha kwamba alimtegemea kikamili Yehova akiwa Bwana wake.

4 Je, nyakati fulani umehisi kwamba umelemewa na mambo fulani magumu au majukumu katika utumishi wa Mungu? Ni vizuri kila mmoja wetu ajiulize hivi: ‘Je, ninamtegemea Yehova kikamili ili aongoze mambo kupatana na mapenzi yake? Je, kweli ninaonyesha kwamba nina roho ya kujitoa kwa hiari?’ Uwe na hakika kwamba Mungu anawapa roho yake watu ambao wanamtegemea kwa moyo wao wote na kutambua mapenzi yake akiwa mwenye enzi kuu.—Mdo. 5:32.

Petro Alisaidiwa na Roho Takatifu

5. Petro aliona roho takatifu ikitenda kazi kwa njia zipi kabla ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K.?

5 Kama Maria, mtume Petro alijionea utendaji wenye nguvu wa roho takatifu ya Mungu kabla ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. Yesu alikuwa amempa yeye na mitume wengine mamlaka ya kuwafukuza roho waovu. (Marko 3:14-16) Na ingawa Maandiko hayasemi mambo mengi, inaelekea kwamba Petro alitumia mamlaka hayo. Nguvu za Mungu zilionekana pia wakati Yesu alipomruhusu Petro atembee juu ya Bahari ya Galilaya kumwelekea, na Petro akafanya hivyo. (Soma Mathayo 14:25-29.) Ni wazi kwamba Petro aliitegemea roho takatifu ili imsaidie kufanya matendo yenye nguvu. Punde si punde, roho hiyo ingetenda kazi juu ya Petro na wanafunzi wenzake kwa njia mpya.

6. Petro alifanya nini kupitia roho ya Mungu wakati na baada ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K.?

6 Kwenye Sherehe ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K., Petro na wengine walipewa uwezo wa kimuujiza wa kuzungumza lugha zilizotumiwa na wakaaji wa muda waliotembelea Yerusalemu. Baadaye, Petro aliongoza katika kuhutubia kusanyiko hilo. (Mdo. 2:14-36) Ndiyo, mwanamume huyo ambaye pindi fulani aliogopa au kutenda bila kufikiri alipewa ujasiri wa kutoa ushahidi ingawa alikabili vitisho na mateso. (Mdo. 4:18-20, 31) Mungu alimpa ujuzi kupitia ufunuo. (Mdo. 5:8, 9) Na hata alipewa nguvu za kufufua.—Mdo. 9:40.

7. Ni mafundisho gani ya Yesu ambayo Petro alielewa baada tu ya kutiwa mafuta?

7 Hata kabla ya Pentekoste, Petro alielewa kweli nyingi ambazo Yesu alifundisha. (Mt. 16:16, 17; Yoh. 6:68) Lakini kulikuwa na mambo fulani aliyofundisha Yesu ambayo Petro hakuelewa vizuri kabla ya Pentekoste. Kwa mfano, Petro hakuwa ametambua kwamba siku ya tatu Kristo angefufuliwa akiwa kiumbe wa roho na pia hakuelewa kwamba Ufalme ungekuwa mbinguni. (Yoh. 20:6-10; Mdo. 1:6) Wazo la kwamba wanadamu wangekuwa viumbe wa roho na kutawala katika Ufalme wa mbinguni lilikuwa jipya kwa Petro. Mara tu baada ya yeye mwenyewe kubatizwa kwa roho takatifu na kupewa tumaini la kimbingu, ndipo angeweza kuelewa mafundisho ya Yesu kuhusu mambo hayo.

8. Wakristo watiwa-mafuta na “kondoo wengine” wanapata ujuzi gani?

8 Mambo ambayo wanafunzi wa Yesu hawakuelewa mwanzoni walianza kuyaelewa baada ya roho takatifu kumiminwa. Kwa mwongozo wa roho takatifu, waandikaji wa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo waliandika kwa faida yetu mambo mbalimbali ya kustaajabisha yanayohusiana na kusudi la Yehova. (Efe. 3:8-11, 18) Leo, Wakristo watiwa-mafuta na “kondoo wengine” wanakula chakula kilekile cha kiroho na kuelewa kweli zilezile. (Yoh. 10:16) Je, unathamini ujuzi na uelewaji wa Neno la Mungu ambao roho takatifu inakuwezesha kupata?

Paulo ‘Alijaa Roho Takatifu’

9. Paulo aliweza kutimiza nini kwa uwezo wa roho takatifu?

9 Mwaka mmoja hivi baada ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K., mtu mwingine alipewa na Mungu zawadi ya roho takatifu. Mtu huyo ni Sauli, ambaye baadaye aliitwa Paulo. Roho ilitenda kazi juu yake kwa njia ambazo zinatunufaisha leo. Mtume Paulo aliongozwa na roho kuandika vitabu 14 vya Biblia. Na kama ilivyokuwa kuhusiana na Petro, roho ya Mungu ilimwezesha Paulo kuelewa na kuandika kwa njia ya wazi kuhusu tumaini la kupata uhai wa mbinguni usioweza kufa na usioharibika. Roho takatifu ilimwezesha Paulo kuponya, kufukuza roho waovu, na hata kuwafufua wafu! Hata hivyo, nguvu alizopokea kupitia roho takatifu zilitimiza kusudi muhimu zaidi, kusudi ambalo watumishi wote wa Mungu leo wanapata, hata ingawa si kwa njia ya kimuujiza.

10. Roho takatifu iliboreshaje uwezo wa Paulo wa kusema?

10 Paulo, ambaye alikuwa “amejaa roho takatifu,” alimshutumu kwa ujasiri mlozi fulani. Jambo hilo lilikuwa na matokeo makubwa sana juu ya ofisa mkuu wa Saiprasi, ambaye alikuwa akisikiliza mazungumzo hayo yote! Liwali huyo alikubali kweli, ‘alipostaajabishwa na fundisho la Yehova.’ (Mdo. 13:8-12) Ni wazi kwamba Paulo alijua vizuri umuhimu wa roho takatifu ya Mungu inapohusu kusema kweli. (Mt. 10:20) Baadaye alilisihi kutaniko la Efeso litoe dua kwa ajili yake ili apewe “uwezo wa kusema.”—Efe. 6:18-20.

11. Paulo aliongozwaje na roho ya Mungu?

11 Roho takatifu haikumwezesha tu Paulo kusema bali pia, nyakati nyingine, ilimkataza kusema katika maeneo fulani. Alipoanza safari zake za umishonari, Paulo aliongozwa na roho ya Mungu. (Mdo. 13:2; soma Matendo 16:6-10.) Bado Yehova anaongoza kazi ya kuhubiri kupitia roho yake. Kama Paulo, watumishi wote watiifu wa Yehova wanajitahidi kutangaza kweli kwa ujasiri na bidii. Hata ingawa mwongozo wa Mungu hauonekani moja kwa moja leo kama ilivyokuwa katika siku za Paulo, tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova anatumia roho yake takatifu kuhakikisha kwamba watu wanaostahili wanasikia kweli.—Yoh. 6:44.

“Utendaji wa Namna Mbalimbali”

12-14. Je, roho ya Mungu inatenda juu ya watumishi wake wote kwa njia ileile? Eleza.

12 Je, masimulizi yanayoonyesha jinsi Yehova alivyolibariki kutaniko la karne ya kwanza la watiwa-mafuta, yanawatia moyo sana watumishi waliojiweka wakfu kwa Mungu leo? Bila shaka! Kumbuka maneno ya Paulo yaliyoongozwa na roho ambayo aliandikia kutaniko la Korintho kuhusu zawadi za kimuujiza za roho katika siku zake: “Basi kuna zawadi za namna mbalimbali, lakini kuna roho ileile; na kuna huduma za namna mbalimbali, na bado kuna Bwana yuleyule; na kuna utendaji wa namna mbalimbali, na bado ni Mungu yuleyule anayefanya utendaji wote katika watu wote.” (1 Kor. 12:4-6, 11) Ndiyo, roho takatifu inaweza kutenda kazi kwa njia tofauti-tofauti juu ya watumishi mbalimbali wa Mungu kwa kusudi fulani. Kwa kweli, roho takatifu inaweza kutenda juu ya “kundi dogo” na “kondoo wengine” wa Kristo. (Luka 12:32; Yoh. 10:16) Hata hivyo, sikuzote haitendi kwa njia ileile juu ya kila mshiriki wa kutaniko.

13 Kwa mfano, wazee wanawekwa rasmi na roho takatifu. (Mdo. 20:28) Lakini si watiwa-mafuta wote wanaotumikia wakiwa waangalizi katika kutaniko. Tunapaswa kukata kauli gani kuhusu jambo hilo? Kwa ufupi ni kwamba roho ya Mungu inatenda kazi kwa njia mbalimbali juu ya washiriki wa kutaniko.

14 Roho ambayo inatia ndani ya watiwa-mafuta “roho ya kufanywa kuwa wana,” au hisia ya kuwa wana, ndiyo roho ileile ambayo Yehova alitumia kumfufua kutoka kwa wafu Mwana wake mzaliwa-pekee na kumpa uhai usioweza kufa mbinguni. (Soma Waroma 8:11, 15.) Ni roho hiyohiyo ambayo Yehova alitumia kuumba ulimwengu wote. (Mwa. 1:1-3) Kwa roho hiyohiyo takatifu, Yehova alimwezesha Bezaleli astahili kufanya kazi ya pekee katika maskani, alimtia nguvu Samsoni afanye matendo yaliyohitaji nguvu nyingi sana, na kumwezesha Petro kutembea juu ya maji. Kwa hiyo, acheni tusifikiri kwamba kuwa na roho ya Mungu ni sawa na kutiwa mafuta na roho ya Mungu, kwa kuwa kutiwa mafuta ni utendaji mmoja tu wa pekee wa roho. Kutiwa mafuta kwa roho kunategemea uamuzi wa Mungu.

15. Je, watu wataendelea kubatizwa kwa roho takatifu milele? Eleza.

15 Nguvu takatifu ya utendaji ya Mungu imekuwa ikitenda kazi kwa njia mbalimbali juu ya watumishi wake waaminifu muda wote, ndiyo, kwa maelfu ya miaka kabla watu hawajaanza kutiwa mafuta kwa roho. Katika Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K., utendaji huo mpya ulianza, lakini hautaendelea milele. Kubatizwa kwa roho kutakoma, lakini roho takatifu itaendelea kutenda kazi juu ya watu wa Mungu ili wafanye mapenzi yake kwa umilele wote.

16. Watumishi wa Mungu wanafanya nini sasa kwa msaada wa roho yake?

16 Ni nini hasa kinachotukia duniani sasa kwa uwezo wa roho takatifu ya Yehova? Andiko la Ufunuo 22:17 linajibu hivi: “Na roho na bibi-arusi huendelea kusema: ‘Njoo!’ Na yeyote anayesikia na aseme: ‘Njoo!’ Na yeyote anayeona kiu aje; yeyote anayetaka achukue maji ya uzima bure.” Wakichochewa na roho ya Mungu, leo Wakristo wanampa mwaliko wa Yehova unaookoa uhai, mtu “yeyote anayetaka” kukubali maji ya uzima. Wakristo watiwa-mafuta wanaongoza katika kufanya hivyo. Hata hivyo, washiriki wa kondoo wengine wanajiunga nao katika kutoa mwaliko huo. Jamii zote mbili zinashirikiana na roho ileile takatifu kutimiza kazi hiyo. Washiriki wa jamii zote mbili wameonyesha wakfu wao kwa Yehova kwa kubatizwa “katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu.” (Mt. 28:19) Na wote wanatii mwongozo wa roho ya Mungu katika maisha yao, na kuiruhusu itokeze ndani yao tunda lake. (Gal. 5:22, 23) Kama watiwa-mafuta, kondoo wengine wanaruhusu roho ya Mungu iwasaidie. Kwa msaada wa roho hiyo, wanafanya yote wanayoweza kutimiza matakwa ya Yehova ya utakatifu.—2 Kor. 7:1; Ufu. 7:9, 14.

Endelea Kuomba ili Upewe Roho Takatifu

17. Tunaweza kuthibitishaje kwamba tuna roho ya Mungu?

17 Kwa hiyo, hata kama una tumaini kutoka kwa Mungu la kuishi milele mbinguni au duniani, Yehova anaweza kukupa “nguvu zinazopita zile za kawaida” ili uweze kudumisha utimilifu wako na kupokea thawabu yako. (2 Kor. 4:7) Huenda ukadhihakiwa kwa sababu ya kuendelea kuhubiri habari njema ya Ufalme. Lakini kumbuka kwamba ‘ikiwa unashutumiwa kwa ajili ya jina la Kristo, wewe ni mwenye furaha, kwa sababu ile roho ya utukufu, yaani roho ya Mungu, inatulia juu yako.’—1 Pet. 4:14.

18, 19. Yehova atakusaidiaje kupitia roho yake takatifu, na umeazimia kufanya nini kuhusiana na hilo?

18 Roho takatifu ni zawadi ya bure ambayo Mungu anawapa wale ambao wanaitafuta kwa unyoofu. Inaweza kuzidisha si uwezo wako tu bali pia tamaa yako ya kufanya yote unayoweza katika utumishi wake. “Mungu ndiye ambaye, kwa ajili ya mapenzi yake mema, anatenda ndani yenu ili ninyi muwe na nia na kutenda pia.” Zawadi hiyo ya roho takatifu ambayo ni yenye thamani, pamoja na jitihada zetu nyingi za kuendelea “kulishika sana neno la uzima,” zitatuwezesha ‘kuendelea kuufanyia kazi wokovu wetu wenyewe kwa kuogopa na kutetemeka.’—Flp. 2:12, 13, 16.

19 Basi, ukiwa na uhakika kamili katika roho ya Mungu, timiza kila mgawo kwa moyo wako wote, uwe stadi katika mgawo unaopewa, na umtegemee Yehova ili akusaidie. (Yak. 1:5) Atakupa msaada unaohitaji ili uelewe Neno lake, ukabiliane na matatizo ya maisha, na kuhubiri habari njema. ‘Endelea kuomba, nawe utapewa; endelea kutafuta, nawe utapata; endelea kupiga hodi, nawe utafunguliwa,’ na hilo linatia ndani kupokea roho takatifu. (Luka 11:9, 13) Kwa kweli, endelea kutoa dua kwa Yehova ili uwe kama watumishi waaminifu wa leo na wa kale ambao waliongozwa na roho takatifu ya Mungu.

Je, Unaweza Kueleza?

• Kama Maria, tunaweza kuonyesha mtazamo gani na hivyo kupata baraka?

• Paulo aliongozwa na roho ya Mungu katika maana gani?

• Watumishi wa Mungu wanaongozwa na roho ya Mungu leo jinsi gani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 24]

Roho ya Mungu ilimwezesha Paulo kushinda nguvu za roho waovu

[Picha katika ukurasa wa 26]

Leo, roho takatifu inaweza kuwasaidia Wakristo bila kuzingatia tumaini lao