Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Tuongozwe na Roho ya Mungu?

Kwa Nini Tuongozwe na Roho ya Mungu?

Kwa Nini Tuongozwe na Roho ya Mungu?

“Wewe ni Mungu wangu. Roho yako ni nzuri; na iniongoze.”—ZAB. 143:10.

1. Toa mfano wa jinsi nguvu isiyoonekana inavyoweza kumwongoza mtu.

JE, UMEWAHI kutumia dira ili kujua mahali unapoelekea? Dira ni kifaa rahisi kilicho tu na sehemu moja inayozunguka-zunguka, yaani, mshale wenye sumaku unaoelekeza upande wa kaskazini. Nguvu isiyoonekana inayoitwa nguvu ya sumaku ndiyo inayouwezesha mshale huo wa dira kuzunguka. Kwa karne nyingi, wagunduzi na wasafiri wametumia dira ili iwaongoze katika safari zao za nchi kavu na za baharini.

2, 3. (a) Yehova alitumia nguvu gani nyingi miaka mingi iliyopita? (b) Kwa nini tunapaswa kutarajia nguvu ya utendaji ya Mungu isiyoonekana iongoze maisha yetu leo?

2 Kuna nguvu nyingine isiyoonekana ambayo ni muhimu hata zaidi ili kutuongoza. Ni nguvu gani hiyo? Ni ile inayozungumziwa katika mistari ya kwanza ya Biblia. Kitabu cha Mwanzo kinasema hivi kuhusu yale ambayo Yehova alitimiza miaka mingi iliyopita: “Hapo mwanzo Mungu aliumba mbingu na dunia.” Tunajua kwamba Mungu alitumia nguvu nyingi ili kuumba vitu kwa sababu simulizi la uumbaji linaongeza hivi: “Nguvu za utendaji za Mungu zilikuwa zikienda huku na huku.” (Mwa. 1:1, 2) Mungu alitumia nguvu gani? Roho takatifu, nguvu yake yenye msukumo aliyotumia katika uumbaji. Tunashukuru kwamba Yehova alitumia roho hiyo ili kutupatia uhai na kuumba vitu vingine vyote.—Ayu. 33:4; Zab. 104:30.

3 Tukiwa wanadamu hai wanaopumua, je, hatungetarajia nguvu ya utendaji ya Mungu iwe na uvutano zaidi katika maisha yetu? Mwana wa Mungu alijua kwamba tungepaswa kutarajia hilo, kwa kuwa Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Roho . . . atawaongoza ninyi ndani ya kweli yote.” (Yoh. 16:13) Roho hiyo ni nini, na kwa nini tutake ituongoze?

Roho Takatifu Ni Nini?

4, 5. (a) Wale wanaoamini fundisho la Utatu wana maoni gani yenye makosa kuhusu roho takatifu? (b) Eleza roho takatifu ni nini hasa.

4 Inaelekea, baadhi ya watu unaokutana nao katika huduma wanaamini kile ambacho tafsiri ya King James Version na tafsiri nyingine za Biblia zinaita Roho Mtakatifu (Holy Ghost). Wale wanaoamini fundisho la Utatu wanafikiri kimakosa kwamba roho hiyo ni mtu aliye sawa na Mungu Baba. (1 Kor. 8:6) Hata hivyo, inapendeza kujua kwamba mtungaji wa kamusi Mmarekani Noah Webster, katika tafsiri yote ya The Webster Bible, ambayo ilitegemea tafsiri iliyorekebishwa ya King James Version, ambayo ilichapishwa kwanza mwaka wa 1833, alitumia maneno “Roho Takatifu” badala ya “Roho Mtakatifu.” Webster alifanya hivyo kwa sababu alijua kwamba katika Maandiko maneno hayo hayakumaanisha “mzuka,” (apparition, ghost). *

5 Hivyo basi, roho takatifu ni nini hasa? Biblia ya Marejeo (New World Translation of the Holy Scriptures—With References) inasema hivi katika maelezo ya chini ya andiko la Mwanzo 1:2: “Zaidi ya kutafsiri neno ruʹach [Kiebrania] kuwa ‘roho,’ neno hilo linatafsiriwa pia kuwa ‘upepo’ na linatafsiriwa kwa maneno mengine ambayo yanamaanisha nguvu ya utendaji isiyoonekana.” (Linganisha na maelezo ya chini ya Mwanzo 3:8; 8:1.) Hata ingawa hatuwezi kuona upepo, tunaweza kuona yale unayofanya. Vivyo hivyo, roho takatifu haionekani wala si mtu, lakini tunaweza kuona matokeo ya kazi inayofanya. Roho hiyo ni nishati kutoka kwa Mungu inayotumiwa kutenda juu ya watu au vitu ili kutimiza mapenzi yake. Je, ni vigumu kuamini kwamba nguvu hizo za ajabu zinatoka kwa Chanzo kitakatifu, yaani, Mungu Mweza-Yote? Hapana!—Soma Isaya 40:12, 13.

6. Ni jambo gani muhimu sana ambalo Daudi alimsihi Yehova?

6 Je, Yehova anaweza kuendelea kutumia roho yake kutuongoza katika maisha yetu yote? Alimwahidi mtunga-zaburi Daudi hivi: “Nitakufanya uwe na ufahamu na kukufundisha katika njia unayopaswa kuiendea.” (Zab. 32:8) Je, Daudi alitaka kuongozwa na Mungu? Naam, kwa sababu alimsihi Yehova hivi: “Unifundishe kufanya mapenzi yako, kwa maana wewe ni Mungu wangu. Roho yako ni nzuri; na iniongoze.” (Zab. 143:10) Sisi pia tunapaswa kuwa na tamaa kama hiyo na kuwa tayari kuongozwa na roho ya Mungu. Kwa nini? Chunguza sababu nne.

Hatuna Uwezo wa Kujiongoza Wenyewe

7, 8. (a) Kwa nini hatuwezi kujiongoza wenyewe bila kumtegemea Mungu? (b) Ni mfano gani unaotusaidia kuelewa kwa nini hatupaswi kujaribu kujiongoza wenyewe katika mfumo huu mwovu?

7 Kwanza, tunapaswa kuwa na tamaa ya kutaka kuongozwa na roho ya Mungu kwa sababu hatuna uwezo wa kujiongoza wenyewe. Kumwongoza mtu kunamaanisha kumwonyesha njia inayofaa kufuata. Hata hivyo, Yehova hakutuumba tukiwa na uwezo wa kujiongoza sisi wenyewe, hasa tukiwa katika hali yetu ya kutokamilika. Nabii wake Yeremia aliandika hivi: “Ee Bwana, najua kwamba njia ya mwanadamu haimo ndani yake mwenyewe: mwanadamu hana uwezo wa kuongoza hatua zake.” (Yer. 10:23, The Bible in Basic English) Kwa nini? Mungu alituambia kupitia Yeremia kwa nini hatuwezi kujiongoza wenyewe. Yehova alisema hivi kuhusu mtu tuliye kwa ndani: “Moyo ni wenye hila kuliko kitu kingine chochote nao ni hatari. Ni nani anayeweza kuujua?”—Yer. 17:9; Mt. 15:19.

8 Je, halingekuwa jambo la upumbavu kwa mtu asiye na uzoefu kutembea peke yake kupitia eneo fulani hatari kama vile msituni au nyikani bila dira au ramani? Ikiwa mtu huyo hajui jinsi ya kuishi katika eneo kama hilo na hajui jinsi ya kupata njia iliyo salama, angekuwa akihatarisha maisha yake. Vivyo hivyo, mtu anayefikiri kwamba anaweza kujiongoza mwenyewe katika ulimwengu huu mwovu bila kukubali Mungu amwonyeshe njia inayofaa, anahatarisha maisha yake. Uwezekano pekee tulionao wa kupita kwa mafanikio katika mfumo huu wa mambo ni kumwomba Yehova hivi kama alivyofanya Daudi: “Hatua zangu na zishike njia zako, ambamo hatua za miguu yangu hakika hazitatikiswa.” (Zab. 17:5; 23:3) Tunawezaje kupata mwongozo huo?

9. Kama inavyoonyeshwa kwenye ukurasa wa 17, roho ya Mungu inaweza kutuongoza kwa uhakika jinsi gani?

9 Ikiwa sisi ni wanyenyekevu na tuko tayari kumtegemea Yehova, atatupatia roho yake takatifu ili iongoze hatua zetu kwa uhakika. Nguvu hiyo ya utendaji itatusaidia jinsi gani? Yesu aliwaeleza hivi wanafunzi wake: “Msaidizi, roho takatifu, ambayo Baba atatuma katika jina langu, hiyo itawafundisha ninyi mambo yote na kuwakumbusha mambo yote niliyowaambia.” (Yoh. 14:26) Tukisali na kujifunza kwa ukawaida Neno la Mungu, kutia ndani maneno yote ya Kristo, roho takatifu itatusaidia kuelewa zaidi hekima yenye kina ya Yehova ili tuweze kumtii. (1 Kor. 2:10) Isitoshe, mambo fulani yasiyotarajiwa yanapotokea katika maisha yetu, roho ya Mungu itatuonyesha njia ya kufuata. Itatukumbusha kanuni za Biblia ambazo tayari tumejifunza na itatusaidia kuelewa jinsi tunavyoweza kufanya maamuzi mazuri.

Yesu Aliongozwa na Roho ya Mungu

10, 11. Ni matarajio gani ambayo Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu alikuwa nayo kuhusiana na roho takatifu, na roho takatifu ilimsaidiaje?

10 Sababu ya pili ya kutaka tuongozwe na roho takatifu ni kwamba Mungu alimwongoza Mwanawe kupitia roho hiyo. Kabla ya kuja duniani, Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu alijua unabii huu: “Roho ya Yehova itatua juu yake, roho ya hekima na ya uelewaji, roho ya shauri na ya nguvu, roho ya ujuzi na ya kumwogopa Yehova.” (Isa. 11:2) Hebu fikiria jinsi Yesu alivyokuwa na hamu kubwa ya kupokea msaada wa roho ya Mungu ili kukabiliana na matatizo hapa duniani.

11 Maneno ya Yehova yalitimia. Simulizi la Injili linasema mambo yaliyotukia mara tu baada ya ubatizo wa Yesu: “Basi Yesu, akiwa amejaa roho takatifu, akarudi kutoka Yordani, naye akaongozwa na roho huku na huku nyikani.” (Luka 4:1) Huko nyikani, Yesu alipokuwa akifunga, kusali, na kutafakari, inaelekea Yehova alimpa maagizo na kumtayarisha Mwanawe kwa ajili ya mambo ambayo yangempata baadaye. Nguvu ya utendaji ya Mungu ilikuwa na uvutano juu ya akili na moyo wa Yesu, ikiongoza fikira na maamuzi yake. Kwa sababu hiyo, Yesu alijua jambo la kufanya katika kila hali, na alifanya sawasawa na yale ambayo Baba yake alitaka afanye.

12. Kwa nini ni muhimu kuomba roho ya Mungu ituongoze?

12 Akijua thamani ya uvutano mzuri wa roho ya Mungu katika maisha yake, Yesu alikazia umuhimu wa wanafunzi wake kuomba wapewe roho takatifu na pia umuhimu wa kuongozwa na roho hiyo. (Soma Luka 11:9-13.) Kwa nini hilo ni jambo muhimu sana kwetu? Kwa sababu roho ya Mungu inaweza kubadili kufikiri kwetu na kutusaidia kuwa na akili ya Kristo. (Rom. 12:2; 1 Kor. 2:16) Kwa kuiruhusu roho ya Mungu iongoze maisha yetu, tunaweza kufikiri kama Kristo na kuiga mfano wake.—1 Pet. 2:21.

Roho ya Ulimwengu Itatuongoza Vibaya

13. Roho ya ulimwengu ni nini, na inatokeza nini?

13 Sababu ya tatu ya kutaka tuongozwe na roho ya Mungu ni kwamba bila roho hiyo tungeongozwa vibaya na roho ya ulimwengu isiyo takatifu ambayo inaongoza maisha ya watu wengi leo. Hiyo ni roho yenye nguvu ambayo inawachochea watu kutenda tofauti kabisa na yale ambayo roho takatifu inatuongoza kutenda. Badala ya kuwasaidia watu kuwa na akili ya Kristo, roho hiyo ya ulimwengu inawachochea watu kufikiri na kutenda kama mtawala wa ulimwengu, Shetani. (Soma Waefeso 2:1-3; Tito 3:3.) Mtu anaporuhusu roho ya ulimwengu imwongoze na kuanza kutenda matendo ya mwili, kunakuwa na matokeo mabaya, ambayo yatamzuia kurithi Ufalme wa Mungu.—Gal. 5:19-21.

14, 15. Tunaweza kufaulu jinsi gani kuipinga roho ya ulimwengu?

14 Yehova ametupatia kila kitu tunachohitaji ili kuipinga roho ya ulimwengu. Mtume Paulo alisema kwamba ‘uendelee kujipatia nguvu katika Bwana na katika uwezo wa nguvu zake ili uweze kupinga katika ile siku ya uovu.’ (Efe. 6:10, 13) Kupitia roho yake, Yehova anatuimarisha ili tupinge jitihada za Shetani za kutupotosha. (Ufu. 12:9) Roho ya ulimwengu ni yenye nguvu, na hatuwezi kuiepuka kabisa. Hata hivyo, tunaweza kuipinga. Roho takatifu ni yenye nguvu hata zaidi, na itatusaidia!

15 Mtume Petro alisema hivi kuhusu wale walioacha Ukristo katika karne ya kwanza: “Wameiacha njia iliyo nyoofu, wamepotoshwa.” (2 Pet. 2:15) Tunaweza kuwa wenye shukrani kama nini kwamba tumepokea “si roho ya ulimwengu, bali roho inayotoka kwa Mungu”! (1 Kor. 2:12) Kwa kuiruhusu roho takatifu ituongoze na kwa kutumia maandalizi yote ambayo Yehova anatupatia ili kuendelea kuimarisha uhusiano wetu pamoja naye, tunaweza kufaulu kuipinga roho ya kishetani ya ulimwengu huu mwovu.—Gal. 5:16.

Roho Takatifu Inatokeza Tunda Zuri

16. Roho takatifu inaweza kutokeza ndani yetu tunda gani?

16 Sababu ya nne ya kutaka kuongozwa na roho ya Mungu ni kwamba inatokeza tunda zuri katika maisha ya wale ambao wanaongozwa nayo. (Soma Wagalatia 5:22, 23.) Ni nani miongoni mwetu ambaye hangetaka kuwa mwenye upendo, shangwe, na amani zaidi? Ni nani miongoni mwetu ambaye hangetaka kuwa na ustahimilivu, fadhili, na wema zaidi? Ni nani miongoni mwetu ambaye hangefaidika kwa kusitawisha zaidi sifa ya imani, upole, na kujizuia? Roho ya Mungu inatokeza ndani yetu sifa nzuri ambazo zinatunufaisha na kuwanufaisha wale tunaoishi nao na kutumika nao. Kwa kuwa hakuna mwisho wa kusitawisha tunda la roho kwa kadiri ambayo tunahitaji na kwa kadiri ambayo tunaruhusiwa kusitawisha, tunapaswa kujitahidi sana kuendelea kusitawisha tunda hilo.

17. Tunaweza kusitawishaje sifa fulani ya tunda la roho kwa kadiri kubwa zaidi?

17 Ni jambo la hekima tuhakikishe kwamba maneno na matendo yetu yanathibitisha kuwa tunaongozwa na roho takatifu na tunazaa tunda lake. (2 Kor. 13:5a; Gal. 5:25) Ikiwa tunaona kwamba tunahitaji kusitawisha sifa fulani za tunda la roho, tunaweza kushirikiana na roho takatifu kwa kadiri kubwa ili tusitawishe sifa hizo. Tunafanya hivyo kwa kujifunza kila sifa kama inavyofunuliwa katika Biblia na kuzungumziwa katika machapisho yetu ya Kikristo. Hivyo tunaweza kutambua jinsi tunavyopaswa kuonyesha tunda la roho katika maisha yetu ya kila siku na kisha kulisitawisha kwa kadiri kubwa zaidi. * Tunapoona matokeo ya utendaji wa roho ya Mungu katika maisha yetu wenyewe na pia katika maisha ya Wakristo wenzetu, tunaona waziwazi kwa nini ni lazima tuongozwe na roho hiyo.

Je, Unairuhusu Roho ya Mungu Ikuongoze?

18. Yesu alituwekeaje kielelezo kwa kukubali roho ya Mungu imwongoze?

18 Akiwa “stadi wa kazi” wa Mungu katika uumbaji wa ulimwengu, Yesu alijua kila kitu kuhusu nguvu za sumaku za dunia ambazo wanadamu wanatumia ili kusafiri duniani. (Met. 8:30; Yoh. 1:3) Hata hivyo, hakuna uthibitisho katika Biblia unaoonyesha kwamba Yesu aliwahi kutumia nguvu hizo ili kuongoza hatua zake alipokuwa duniani. Biblia inasema kwamba akiwa mwanadamu, Yesu alijionea jinsi roho takatifu ya Mungu ilivyotenda kwa nguvu sana katika maisha yake. Alikubali uvutano wa roho hiyo, na ilipomchochea, aliiruhusu imwongoze naye akatenda kulingana nayo. (Marko 1:12, 13; Luka 4:14) Je, wewe unairuhusu roho ya Mungu ikuongoze kama alivyofanya Yesu?

19. Ni lazima tufanye nini ili roho takatifu iwe nguvu yenye kutuongoza maishani?

19 Bado nguvu ya utendaji ya Mungu inatenda kazi juu ya akili na mioyo ili kuwachochea na kuwaongoza wale wanaoikubali. Unawezaje kuiruhusu roho ya Mungu itende kazi juu yako na kukuongoza upande unaofaa? Sali daima kwa Yehova ili akupe roho yake na kukusaidia kukubali mwongozo wake. (Soma Waefeso 3:14-16.) Tenda kulingana na sala zako kwa kutafuta mashauri katika Neno la Mungu lililoandikwa, Biblia, ambalo liliandikwa chini ya mwongozo wa roho takatifu. (2 Tim. 3:16, 17) Tii maagizo yenye hekima yanayotolewa na Biblia na kisha uwe tayari kukubali mwongozo wa roho takatifu. Onyesha una imani kwamba Yehova ana uwezo wa kukuongoza ifaavyo maishani katika ulimwengu huu mwovu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Katika utangulizi wa Biblia yake, Webster aliandika hivi: “Wakati wowote maneno yanapoeleweka kwa njia tofauti na jinsi yalivyoeleweka mwanzoni, na kwa maana tofauti na ile ya lugha za awali, hayamsaidii msomaji kuelewa Neno la Mungu kwa usahihi.”

^ fu. 17 Kwa maelezo zaidi kuhusu kila sifa ya tunda la roho, ona kichwa ‘Tunda la Roho ya Mungu’ na orodha ya kila sifa ya tunda hilo katika Fahirisi.

Je, Ulielewa Mambo Makuu?

• Roho takatifu inaweza jinsi gani kuwa na uvutano juu ya maisha yetu?

• Taja sababu nne za kutaka kuongozwa na roho ya Mungu.

• Tunaweza kutimiza jinsi gani sehemu yetu ili tufaidike kikamili na mwongozo wa roho takatifu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 15]

Roho ya Mungu ilikuwa nguvu iliyomchochea Yesu maishani

[Picha katika ukurasa wa 17]

Roho ya Mungu inatenda kazi juu ya akili na mioyo ili kuwachochea na kuwaongoza