Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nimethawabishwa kwa Kufanya Mabadiliko

Nimethawabishwa kwa Kufanya Mabadiliko

Nimethawabishwa kwa Kufanya Mabadiliko

Limesimuliwa na James A. Thompson

Nilipozaliwa kusini mwa Marekani mnamo mwaka wa 1928, kulikuwa na sheria iliyowabagua wazungu na weusi. Kuvunja sheria hiyo kungefanya ufungwe gerezani au upewe adhabu kali zaidi.

KATIKA sehemu fulani za Marekani wakati huo, Mashahidi wa Yehova walilazimika kuwa na makutaniko, mizunguko, na wilaya za wazungu na za weusi. Mnamo mwaka wa 1937, baba yangu akawa mtumishi wa kampuni (sasa anaitwa mratibu wa baraza la wazee) wa kutaniko la watu weusi huko Chattanooga, Tennessee. Henry Nichols alikuwa mtumishi wa kampuni wa kutaniko la watu weupe.

Ninakumbuka mambo mazuri yaliyotukia nilipokuwa kijana. Wakati huo nilizoea kukaa nyuma ya nyumba yetu usiku nikimsikiliza Baba na Ndugu Nichols wakizungumza. Ingawa nilikuwa sielewi kila jambo walilokuwa wakizungumzia, nilifurahia kukaa karibu na Baba alipokuwa akizungumza na Ndugu Nichols kuhusu jinsi ambavyo wangeweza kutimiza vizuri kazi ya kuhubiri chini ya hali hizo.

Mwanzoni mwa mwaka wa 1930, familia yetu ilipatwa na msiba. Mama yangu ambaye alikuwa na umri wa miaka 20 tu, alikufa. Akiwa peke yake, Baba alilazimika kunitunza mimi nikiwa na umri wa miaka miwili tu, na dada yangu, Doris, aliyekuwa na umri wa miaka minne. Ingawa muda mrefu haukuwa umepita tangu Baba abatizwe, alifanya maendeleo mazuri ya kiroho.

Watu Walioniwekea Mfano Mzuri

Mnamo mwaka wa 1933, Baba alikutana na dada mzuri wa kiroho aitwaye Lillie Mae Gwendolyn Thomas, na punde si punde wakafunga ndoa. Wote wawili, Baba na Mama, waliniwekea mimi na Doris mfano mzuri wa kumtumikia Yehova kwa ushikamanifu.

Mwaka wa 1938, makutaniko ya Mashahidi wa Yehova yaliombwa yaunge mkono azimio la kwamba wazee wa kutaniko wawekwe rasmi na makao makuu huko Brooklyn, New York, badala ya kuchaguliwa makutanikoni. Wakati baadhi ya akina ndugu huko Chattanooga waliposita kukubali badiliko hilo, Baba aliunga mkono badiliko hilo la kitengenezo bila kusita. Mfano wake wa ushikamanifu pamoja na mfano ambao Mama aliweka katika kumuunga mkono Baba kwa moyo wote umenisaidia hadi leo.

Ubatizo na Huduma ya Wakati Wote

Mnamo mwaka wa 1940 ndugu na dada kadhaa katika kutaniko letu walikodi basi na kusafiri hadi kwenye kusanyiko lililofanywa huko Detroit, Michigan. Watu wachache tuliosafiri pamoja nao walibatizwa. Wengine walishangaa kwa nini mimi sikubatizwa, kwa kuwa nilikuwa nikihubiri kwa bidii sana tangu nilipokuwa na umri wa miaka mitano.

Waliponiuliza kuhusu jambo hilo, niliwajibu hivi: “Sielewi ubatizo unamaanisha nini.” Baba alisikia yale niliyosema na akashangaa. Kuanzia wakati huo na kuendelea alifanya jitihada kubwa ya kunisaidia nielewe maana ya ubatizo na umuhimu wake. Miezi minne baadaye katika siku yenye baridi kali, Oktoba 1, 1940, nilibatizwa katika kidimbwi nje ya mji wa Chattanooga.

Nilianza kupainia nilipokuwa na umri wa miaka 14 wakati wa likizo za shule. Nilihubiri katika miji midogo huko Tennessee na jimbo jirani la Georgia. Nilikuwa nikiamka mapema, na kuweka chakula cha mchana ndani ya mfuko, na kisha kupanda gari-moshi au basi saa 12 kamili asubuhi ili kwenda kwenye eneo. Nilirudi karibu saa 12 jioni. Mara nyingi chakula nilichobeba kiliisha mapema kabla ya saa ya chakula cha mchana. Ingawa nilikuwa na pesa, singeweza kununua chakula zaidi katika duka lolote kwenye eneo hilo kwa kuwa nilikuwa mweusi. Siku moja, niliingia katika duka fulani ili ninunue aiskrimu na nikafukuzwa. Kwa fadhili, mwanamke mmoja mweupe akaniletea aiskrimu nje.

Nilipoingia shule ya sekondari, harakati za kutetea haki za raia zilikuwa zikipamba moto katika eneo la Kusini. Mashirika kama NAACP (Chama cha Taifa cha Maendeleo ya Watu Weusi) yaliwahimiza wanafunzi wajiunge na harakati hizo. Tulihimizwa kuwa wanachama. Shule kadhaa za watu weusi kutia ndani ile niliyosomea, ziliweka mradi wa kuhakikisha kwamba wanafunzi wote wanajiunga na mashirika hayo. Nilichochewa “kuunga mkono jamii yetu,” kama walivyosema. Lakini nilikataa, nikawaeleza kwamba Mungu hana ubaguzi na hapendelei jamii moja. Hivyo, ninatazamia wakati ambapo Mungu ataondoa ukosefu wowote wa haki kama huo.—Yoh. 17:14; Mdo. 10:34, 35.

Muda mfupi baada ya kumaliza masomo ya sekondari, niliamua kuhamia New York City. Hata hivyo, nikiwa njiani kuelekea huko niliingia katika jiji la Philadelphia, Pennsylvania, ili niwatembelee marafiki wangu ambao nilikutana nao mapema kwenye kusanyiko. Kutaniko lao lilikuwa ndilo kutaniko la kwanza nililohudhuria ambalo watu weupe na weusi walichangamana. Wakati wa ziara, mwangalizi anayesafiri aliniita kando na kuniambia kwamba nitapewa mgawo kwenye mkutano unaofuata. Hilo lilifanya iwe rahisi zaidi kwangu kuamua kukaa katika kutaniko hilo.

Miongoni mwa marafiki niliowapata huko Philadelphia ni dada mmoja kijana aitwaye Geraldine White au Gerri, kama nilivyomwita. Aliijua Biblia vizuri na alijua kuzungumza vizuri na wenye nyumba katika mahubiri ya nyumba kwa nyumba. Jambo la muhimu hata zaidi kwangu ni kwamba alikuwa na mradi kama wangu wa kuwa painia. Tulifunga ndoa Aprili 23, 1949.

Tunaalikwa Gileadi

Tangu mwanzoni tulikuwa na mradi wa kuhudhuria Shule ya Gileadi na kutumika tukiwa wamishonari katika nchi ya kigeni. Tulifurahia kurahisisha maisha yetu ili tuweze kustahili kuhudhuria Gileadi. Baada ya muda mfupi tuliombwa twende huko Lawnside, New Jersey; kisha Chester, Pennsylvania; na hatimaye Atlantic City, New Jersey. Tukiwa huko Atlantic City, tulitimiza matakwa ya kuhudhuria Gileadi kwa kuwa tulikuwa tumefunga ndoa kwa miaka miwili. Lakini tuliambiwa tungoje. Kwa nini?

Mwanzoni mwa miaka ya 1950, vijana wengi walikuwa wanaandikishwa jeshini ili wapigane katika vita vilivyokuwa vikiendelea huko Korea. Ilionekana kwamba baraza la kuwaandikisha watu katika jeshi huko Philadelphia liliwachukia Mashahidi wa Yehova kwa sababu ya msimamo wetu wa kutokuwamo. Hatimaye, hakimu alinijulisha kwamba uchunguzi uliofanywa kwa siri na Shirika la Upelelezi la Marekani (FBI) ulithibitisha msimamo wangu wa kutokuwamo. Kwa hiyo, Januari 11, 1952, Baraza la Kushughulikia Rufani Lililoundwa na Rais likanipa hati iliyoonyesha kwamba mimi ni mhudumu wa dini.

Mwezi wa Agosti mwaka huo, mimi na Gerri tulipokea mwaliko wa kuhudhuria darasa la 20 la Gileadi, ambalo lilianza Septemba. Tukiwa katika shule hiyo, tulitarajia kupokea mgawo wa kwenda katika nchi ya kigeni. Dada yangu Doris alikuwa amehitimu katika darasa la 13 la Gileadi na alikuwa akitumikia nchini Brazili. Mimi na Gerri tulishangaa sana tulipopokea mgawo wa kazi ya mzunguko ili kutembelea makutaniko ya watu weusi katika jimbo la kusini la Alabama! Kwa kadiri fulani jambo hilo lilituvunja moyo, kwa kuwa tulikuwa tukitazamia sana kutumikia katika nchi ya kigeni.

Kutaniko la kwanza tulilotembelea ni kutaniko lililokuwa huko Huntsville. Tulipofika, tulipelekwa nyumbani kwa dada Mkristo ambaye tungekaa naye. Tulipokuwa tukishusha mizigo yetu tulimsikia akisema kwenye simu, “Watoto wamefika.” Tulikuwa na miaka 24 tu na tulionekana kuwa wenye umri mdogo hata zaidi. Tuliitwa “Watoto” muda wote tulipotumikia katika mzunguko huo.

Mara nyingi eneo la Kusini liliitwa Eneo la Biblia kwa sababu watu wengi katika eneo hilo waliithamini sana Biblia. Hivyo kwa kawaida tulianzisha mazungumzo kwa kutumia mambo haya matatu:

(1) Maelezo mafupi kuhusu hali ya dunia.

(2) Suluhisho ambalo Biblia inatoa.

(3) Mambo ambayo Biblia inasema tunapaswa kufanya.

Kisha tulitoa kitabu kinachofaa cha kujifunzia Biblia. Kwa sababu tulipata matokeo mazuri kwa kutumia njia hiyo, nilipewa mgawo katika kusanyiko la New World Society mwaka 1953 huko New York. Katika kusanyiko hilo nilionyesha jinsi ya kutumia mambo hayo matatu katika mahubiri.

Muda si muda, katika kiangazi cha mwaka wa 1953, nilipewa mgawo wa kutumikia katika mzunguko wa watu weusi upande wa Kusini nikiwa mwangalizi wa wilaya. Eneo letu lilianzia Virginia hadi Florida na kuelekea upande wa magharibi kuanzia Alabama hadi Tennessee. Ndiyo, waangalizi wanaosafiri walihitaji kubadilika kulingana na hali. Kwa mfano, mara nyingi tuliishi katika nyumba ambazo hazikuwa na maji ya bomba na tulioga kwa kutumia karai nyuma ya jiko. Hiyo ndiyo sehemu iliyokuwa na joto zaidi katika nyumba hiyo!

Tatizo la Ubaguzi wa Rangi

Ili kutumikia katika eneo la Kusini mtu alihitaji kupanga mambo vizuri na kwa ustadi ili aweze kutimiza shughuli mbalimbali. Watu weusi hawakuruhusiwa kutumia mashine za umma za kufua nguo. Hivyo, Gerri angeenda katika sehemu hizo na kueleza kwamba nguo alizonazo ni za “Bi. Thompson.” Wengi walidhani yeye ni mtumishi na “Bi. Thompson” ndiye mama mwenye nyumba. Waangalizi wa wilaya walipokuwa wakionyesha sinema The New World Society in Action, ningepigia simu watu wa duka la vifaa vya sinema na kuwaambia kwamba wamwekee “Bw. Thompson” kitambaa kikubwa cha kuonyeshea sinema. Baadaye, nilienda kwenye duka hilo na kuchukua kitambaa hicho. Sikuzote tulijiendesha kwa adabu na kwa ujumla tulitimiza huduma yetu bila tatizo.

Kulikuwa pia na ubaguzi mwingine, ubaguzi wa majimbo, watu waliotoka upande wa Kaskazini walibaguliwa. Wakati fulani gazeti moja la eneo hilo liliripoti kuwa James A. Thompson, Jr., wa Watchtower Bible and Tract Society of New York atatoa hotuba kwenye kusanyiko. Wengine waliposoma gazeti hilo walifikiri kwamba ninatoka New York, na hivyo kibali tulichopewa cha kutumia ukumbi wa shule kikafutwa. Hivyo, nikaenda kwenye kamati ya shule na kuwaeleza kwamba nilisomea huko Chattanooga. Hatimaye tukapewa ruhusa ya kufanya kusanyiko letu la mzunguko.

Chuki kuelekea jamii fulani iliongezeka hata zaidi katikati ya miaka ya 1950, na nyakati nyingine kulikuwa na jeuri. Katika mwaka wa 1954, baadhi ya Mashahidi walikasirika walipoona kwamba hakuna msemaji mweusi kwenye programu za makusanyiko kadhaa ya wilaya. Tuliwatia moyo ndugu zetu weusi wawe na subira. Kusanyiko lililofuata nikapewa mgawo wa kuwa msemaji. Baada ya hapo, ndugu zaidi weusi kutoka eneo la Kusini wakapewa migawo katika makusanyiko.

Baada ya muda, jeuri dhidi ya jamii fulani katika eneo la Kusini ilipungua, na hatua kwa hatua makutaniko yakaanza kuungana. Hivyo wahubiri walihitaji kupangwa upya katika makutaniko mbalimbali kutia ndani kurekebisha maeneo ya makutaniko na kugawa upya majukumu ya akina ndugu waliokuwa wakisimamia. Baadhi ya ndugu fulani weupe na weusi hawakupendezwa na mpango huo mpya. Hata hivyo, ndugu na dada wengi walikuwa kama Baba yetu wa mbinguni ambaye hana ubaguzi. Kwa kweli, wengi walikuwa marafiki wakubwa licha ya rangi zao. Familia yetu ilishuhudia jambo hilo katika miaka ya 1930 na 1940 nilipokuwa nikikua.

Mgawo Mpya

Katika Januari 1969, mimi na Gerri tulipata mwaliko wa kwenda Guyana, Amerika ya Kusini, na tulikubali mgawo huo kwa furaha. Kwanza tulienda Brooklyn, New York, ambako nilizoezwa kusimamia kazi ya kuhubiri huko Guyana. Tulifika Guyana Julai 1969. Lilikuwa badiliko kubwa kufanya kazi ofisini baada ya kufanya kazi ya kusafiri kwa miaka 16. Gerri alishiriki kwa siku nyingi katika utumishi wa shambani akiwa mmishonari, nami nilifanya kazi katika ofisi ya tawi.

Nilifanya kazi za kila aina, kuanzia kufyeka nyasi, kushughulikia maagizo ya vitabu ya makutaniko 28, hadi kuwasiliana na makao makuu huko Brooklyn. Nilikuwa nikifanya kazi kwa saa 14 hadi 15 kila siku. Ilikuwa kazi ngumu kwetu sote, hata hivyo, tulifurahia mgawo wetu. Tulipofika, kulikuwa na wahubiri 950 nchini Guyana; leo kuna wahubiri zaidi ya 2,500.

Ingawa tulifurahia hali nzuri ya hewa, matunda na mboga za majani, shangwe yetu kubwa ilikuwa kwamba watu wanyenyekevu ambao walikuwa na hamu ya kupata kweli ya Biblia walikuwa wakijifunza kuhusu Ufalme wa Mungu. Mara nyingi Gerri aliongoza mafunzo 20 ya Biblia kila juma, na wengi kati ya wale tuliojifunza nao walifanya maendeleo kufikia ubatizo. Baada ya muda, wengine wao wakawa mapainia, wazee wa makutaniko, na hata wakaenda Gileadi na kuwa wamishonari.

Matatizo, Hasa ya Kiafya

Mnamo mwaka wa 1983 wazazi wangu huko Marekani walihitaji kutunzwa. Mimi, Gerri na Doris, tukawa na mkutano wa kifamilia. Doris, ambaye alikuwa amefanya utumishi wa umishonari kwa miaka 35 huko Brazili, alichagua kurudi nyumbani ili kuwatunza. Doris alisema hivi: “Kwa nini tuwaondoe wamishonari wawili kutoka shambani wakati mmishonari mmoja anaweza kufanya kazi hiyo ya kuwatunza wazazi?” Tangu wazazi wetu wafe, Doris amebaki huko Chattanooga na anatumikia akiwa painia wa pekee.

Mwaka wa 1995 niligunduliwa kuwa na ugonjwa wa kansa ya kibofu na hivyo tukalazimika kurudi Marekani. Tuliamua kuishi huko Goldsboro, North Carolina, kwa sababu ni katikati ya mahali ambapo familia yangu inaishi na ile ya Gerri huko Pennsylvania. Ugonjwa wangu wa kansa umepungua kwa kiasi fulani, na tunatumikia katika kutaniko la Goldsboro tukiwa mapainia wa pekee wagonjwa.

Ninapofikiria miaka zaidi ya 65 ambayo nimeshiriki katika utumishi wa wakati wote, kwa kweli ninathamini sana kwamba Yehova amenibariki mimi na Gerri kwa kutusaidia kufanya mabadiliko ili tuweze kumtumikia. Jinsi maneno ya Daudi yalivyo ya kweli: ‘Kwa mtu mshikamanifu [Yehova] atatenda kwa ushikamanifu’!—2 Sam. 22:26.

[Picha katika ukurasa wa 3]

Baba yangu na Ndugu Nichols waliniwekea mfano mzuri

[Picha katika ukurasa wa 4]

Nikiwa na Gerri, tukiwa tayari kwenda Gileadi, mwaka wa 1952

[Picha katika ukurasa wa 5]

Baada ya kuhudhuria Gileadi, tulipewa mgawo wa kusafiri katika eneo la Kusini

[Picha katika ukurasa wa 6]

Waangalizi wanaosafiri na wake zao wakijitayarisha kwa ajili ya kusanyiko la wilaya la mchanganyiko wa watu weupe na weusi, mwaka wa 1966

[Picha katika ukurasa wa 7]

Utumishi wa umishonari huko Guyana ulikuwa wenye shangwe