Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Usiruhusu Ugonjwa Ukufanye Upoteze Shangwe Yako

Usiruhusu Ugonjwa Ukufanye Upoteze Shangwe Yako

Usiruhusu Ugonjwa Ukufanye Upoteze Shangwe Yako

HEBU wazia ukiamka asubuhi na kutamani siku hiyo iishe kabla hata haijaanza. Ni siku nyingine unayopaswa kuvumilia maumivu ya kimwili au ya kihisia. Huenda ukahisi kama Ayubu, ambaye alisema hivi: “Naona heri kufa kuliko kupata mateso haya.” (Ayu. 7:15, Biblia Habari Njema) Vipi ikiwa hali hiyo inaendelea kwa miaka mingi?

Hivyo ndivyo ilivyokuwa kwa Mefiboshethi, mwana wa Yonathani, rafiki ya Mfalme Daudi. Mefiboshethi alipokuwa na umri wa miaka mitano, ‘alianguka na kulemaa.’ (2 Sam. 4:4) Ni lazima mateso ya kihisia yawe yaliongeza maumivu ya ulemavu wake aliposhtakiwa baadaye kwa uwongo kwamba alimsaliti mfalme na kisha kupoteza mali yake. Hata hivyo, aliendelea kuthibitika kuwa mfano mzuri sana katika kukabiliana na ugonjwa, uchongezi, na hali ya kuvunjwa moyo, na hakuruhusu mambo hayo yamfanye apoteze shangwe yake.—2 Sam. 9:6-10; 16:1-4; 19:24-30.

Mfano mwingine ni ule wa Mtume Paulo. Wakati fulani aliandika kuhusu “mwiba katika mwili” ambao alihitaji kukabiliana nao. (2 Kor. 12:7) Huenda mwiba alioutaja ulikuwa ulemavu wa muda mrefu, au watu waliopinga utume wake. Kwa vyovyote vile, tatizo hilo liliendelea, na alihitaji kukabiliana na maumivu ya kimwili au ya kihisia yaliyosababishwa na tatizo hilo.—2 Kor. 12:9, 10.

Baadhi ya watumishi wa Mungu leo wanakumbwa na magonjwa ya kudumu yenye kudhoofisha au mikazo ya kihisia. Akiwa na umri wa miaka 18, Magdalena, aligunduliwa kuwa ana ugonjwa wa mfumo wa kinga ya mwili (systemic lupus erythematosus). Inaonekana kwamba katika ugonjwa huo, kinga ya mwili hushambulia viungo vya mwili. Magdalena anasema hivi: “Niliogopa sana, kadiri wakati ulivyopita ndivyo hali yangu ilivyozidi kudhoofika na hali ikawa mbaya zaidi kwa sababu ya matatizo ya kutomeng’enya chakula vizuri, vidonda vya mdomoni, na matatizo ya koo.” Kwa upande mwingine, Izabela, analazimika kukabiliana na hali ambazo hazionekani wazi. Anaeleza hivi: “Tangu utotoni nimekuwa nikikabiliana na hali ya kushuka moyo. Hilo limesababisha nishikwe na hofu za ghafla, matatizo ya kupumua, na maumivu ya tumbo. Matokeo yake ni kwamba kwa kawaida ninahisi nikiwa mchovu.”

Kukabiliana na Hali

Magonjwa na udhaifu mbalimbali unaweza kubadili kabisa maisha yako. Hilo linapotokea, ni vizuri kutulia na kuichanganua hali yako kwa unyoofu. Huenda isiwe rahisi kukubali udhaifu ulionao. Magdalena anasema hivi: “Ugonjwa nilionao unazidi kuwa mbaya. Mara kwa mara ninajihisi nimechoka sana nisiweze kutoka kitandani. Kwa sababu ya hali isiyotabirika ya ugonjwa wangu, ni vigumu sana kupanga mambo ya baadaye. Jambo linalonivunja moyo sana ni kwamba siwezi tena kufanya mengi katika utumishi wa Yehova kama nilivyokuwa nikifanya zamani.”

Zbigniew anaeleza hivi: “Kadiri miaka inavyozidi kupita, ndivyo ugonjwa wa yabisi-kavu unavyofanya niishiwe na nguvu hata zaidi, ukiharibu kiungo kimoja baada ya kingine. Nyakati nyingine, maumivu yanapokuwa makali sana, siwezi kufanya hata kazi ndogo tu. Hilo hunivunja moyo sana.”

Miaka kadhaa iliyopita, Barbara aligunduliwa kuwa ana uvimbe uliozidi kukua kwenye ubongo. Anaeleza hivi: “Mwili mwangu umebadilika ghafula. Ninahisi nimelegea, kichwa kinaniuma mara kwa mara, na ninashindwa kukaza uangalifu. Kwa sababu ya hali hiyo mpya, nililazimika kupanga upya kila jambo.”

Watu hao wote ni watumishi waliojiweka wakfu wa Yehova. Kufanya mapenzi ya Yehova ndilo jambo kuu katika maisha yao. Wanamtegemea Mungu kabisa na wananufaika kutokana na utegemezo wake.—Met. 3:5, 6.

Jinsi Ambavyo Yehova Husaidia

Hatupaswi kufikiri kwamba mateso tunayokabili yanaonyesha kwamba Mungu hapendezwi nasi. (Omb. 3:33) Fikiria mambo ambayo Ayubu alikabili licha ya kuwa mtu “asiye na lawama na mnyoofu.” (Ayu. 1:8) Mungu hamjaribu yeyote kwa mambo maovu. (Yak. 1:13) Magonjwa yote kutia ndani yale ya kudumu na ya kihisia, ni matokeo yenye kusikitisha ya dhambi tuliyorithi kutoka kwa wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa.—Rom. 5:12.

Hata hivyo, Yehova na Yesu, hawatawaacha waadilifu bila msaada. (Zab. 34:15) Wakati wa taabu maishani, ndipo hasa tunapothamini kuwa Mungu ni ‘kimbilio letu na ngome yetu.’ (Zab. 91:2) Basi, unapokabili hali ambazo haziwezi kusuluhishwa kwa urahisi, ni nini kinachoweza kukusaidia udumishe shangwe?

Sala: Kwa kufuata kielelezo cha watumishi wa kale wa Mungu waliokuwa waaminifu, unaweza kumtupia Baba yako wa mbinguni mzigo wako kupitia sala. (Zab. 55:22) Ukifanya hivyo, utaweza kupata “amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote.” Amani hiyo ya akili ‘itaulinda moyo wako na nguvu zako za akili.’ (Flp. 4:6, 7) Kwa kumtegemea Mungu kupitia sala, Magdalena anaendelea kukabiliana na ugonjwa wake wenye kudhoofisha. Anasema hivi: “Kumweleza Yehova yaliyo moyoni mwangu hunituliza na kunirudishia shangwe yangu. Kwa kweli, sasa ninaelewa kumtegemea Mungu siku kwa siku kunamaanisha nini.”—2 Kor. 1:3, 4.

Yehova anaweza kujibu sala zako kwa kukupa nguvu kupitia roho yake takatifu, Neno lake, na ndugu zetu Wakristo. Hutatarajia Mungu aondoe ugonjwa wako kimuujiza. Hata hivyo, unaweza kumtegemea akupe hekima na nguvu unazohitaji ili kukabiliana na kila tatizo. (Met. 2:7) Anaweza kukuimarisha na kukupa “nguvu zinazopita zile za kawaida.”—2 Kor. 4:7.

Familia: Familia yenye huruma na upendo inaweza kukusaidia kuvumilia ugonjwa. Hata hivyo, kumbuka kwamba wapendwa wako pia wanaumia. Huenda wakajihisi hoi kama wewe unavyohisi. Hata hivyo, wako tayari kukusaidia hata wakati wa shida. Kusali pamoja kunaweza kukusaidia kuwa na moyo mtulivu.—Met. 14:30.

Barbara anasema hivi kuhusu binti yake na dada wengine vijana katika kutaniko: “Wananisaidia ili nishiriki katika huduma. Bidii yao inanichangamsha.” Zbigniew huona utegemezo anaopata kutoka kwa mke wake kuwa wenye thamani kubwa. “Yeye hushughulikia karibu kazi zote za nyumbani. Pia, yeye hunisaidia kuvaa nguo na mara nyingi ananibebea mkoba wangu tunapoenda katika mikutano ya Kikristo na katika huduma.”

Waamini wenzetu: Tunaposhirikiana na waamini wenzetu, tunatiwa moyo na kufarijiwa. Lakini vipi ikiwa huwezi kuhudhuria mikutano kwa sababu ya ugonjwa wako? Magdalena anaeleza hivi: “Kutaniko limehakikisha kwamba ninafaidika na mikutano kwa kunirekodia mikutano. Mara kwa mara waamini wenzangu hunipigia simu ili kujua jinsi wanavyoweza kunisaidia. Pia, wao hunitumia kadi zinazotia moyo. Kujua kwamba ndugu na dada wananikumbuka na kujali hali yangu hunisaidia kuendelea kuvumilia.”

Izabela, ambaye ana ugonjwa wa kushuka moyo, anaeleza hivi: “Nina ‘baba’ na ‘mama’ wengi katika kutaniko, wale wanaonisikiliza na kujitahidi kunielewa. Kutaniko ni familia yangu—hapa ndipo ninapopata amani na shangwe.”

Wale wanaokabiliana na majaribu mbalimbali wanapaswa kuepuka ‘kujitenga na wengine.’ Badala yake, wanapaswa kuthamini kushirikiana na kutaniko. (Met. 18:1) Hivyo, wanakuwa chanzo kikubwa cha kitia-moyo kwa wengine. Huenda mwanzoni ukasita kuwaeleza akina ndugu na dada mahitaji yako. Hata hivyo, waamini wenzako watathamini sana ikiwa utawaeleza waziwazi. Unapofanya hivyo utawapa nafasi ya kuonyesha “upendo wa kindugu usio na unafiki.” (1 Pet. 1:22) Mbona usiwaeleze kwamba unahitaji msaada wa kufika mikutanoni, kwamba ungependa kuhubiri nao, au ungependa kuzungumza nao mambo yaliyo moyoni mwako? Bila shaka, hatupaswi kudai mengi mno badala yake tunapaswa kuthamini msaada wao.

Uwe na mtazamo unaofaa: Kwa ujumla, wewe ndiye uliye na uwezo wa kukabiliana na ugonjwa wa kudumu bila kupoteza shangwe yako. Mtazamo wa kuwa na huzuni unaweza kufanya uwe na maoni yasiyofaa. Biblia inasema hivi: “Roho ya mwanadamu inaweza kuvumilia ugonjwa wake; lakini ni nani anayeweza kuvumilia roho iliyopondeka?”—Met. 18:14.

Magdalena anasema hivi: “Ninajitahidi sana ili nisiyakazie fikira matatizo yangu. Mimi hujitahidi kufurahia siku ambazo ninajihisi vizuri. Ninatiwa moyo sana ninaposoma masimulizi ya maisha ya watu ambao wamebaki wakiwa waaminifu licha ya magonjwa yao ya kudumu.” Izabela anaimarishwa kwa kujua kwamba Yehova anampenda na kumthamini sana. Anasema hivi: “Ninahisi kwamba ninahitajika, na kwamba nina mtu ambaye ninaweza kutumia maisha yangu kwa ajili yake. Pia, nina tumaini zuri ajabu la wakati ujao.”

Zbigniew anasema hivi: “Ugonjwa wangu unanifundisha kuwa mnyenyekevu na mtiifu. Unanifundisha kuonyesha ufahamu na hivyo kufanya maamuzi ya busara na pia kusamehe kutoka moyoni. Nimejifunza kufurahia kumtumikia Yehova bila kujisikitikia. Kwa kweli, nimechochewa kuendelea kufanya maendeleo ya kiroho.”

Kumbuka kwamba Yehova huangalia kwa makini uvumilivu wako. Anajua jinsi unavyoteseka na anakujali. ‘Hatasahau kazi yako na upendo ulioonyesha kwa ajili ya jina lake.’ (Ebr. 6:10) Kumbuka ahadi hii anayowapa wale wote wanaomwogopa: “Sitakuacha wala kukutupa hata kidogo.”—Ebr. 13:5.

Ikiwa nyakati fulani unahisi umevunjika moyo, kazia fikira tumaini zuri ajabu la kuishi katika ulimwengu mpya. Hivi karibuni utajionea mwenyewe baraka za Ufalme wa Mungu hapa duniani!

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 28, 29]

Wanaendelea Kuhubiri Licha ya Kuwa na Ugonjwa wa Kudumu

“Siwezi tena kutembea bila kusaidiwa, hivyo, mke wangu au ndugu na dada wengine huambatana nami katika huduma. Mimi hukariri utangulizi nitakaotumia na maandiko ya Biblia.”—Jerzy, mwenye tatizo la macho.

“Zaidi ya kutoa ushahidi kwa simu, mimi pia huandika barua na kwa kawaida ninawasiliana na watu wachache wanaopendezwa. Nyakati zote ninapokuwa hospitalini mimi huweka Biblia na machapisho kando ya kitanda changu. Hilo limenisaidia kuanzisha mazungumzo mengi mazuri.”—Magdalena, ambaye amegunduliwa kuwa ana ugonjwa wa mfumo wa kinga ya mwili.

“Ninapenda sana kuhubiri nyumba kwa nyumba, lakini ninapohisi siwezi, ninahubiri kwa kutumia simu.”—Izabela, ambaye ana ugonjwa wa kushuka moyo.

“Ninafurahia kufanya ziara za kurudia na kusaidia katika mafunzo ya Biblia. Ninapohisi nafuu, mimi hupenda kuhubiri nyumba kwa nyumba.”—Barbara, ambaye ana uvimbe kwenye ubongo.

“Mimi hubeba magazeti machache sana. Ninashiriki katika utumishi kadiri maumivu ya viungo vyangu yanavyoniruhusu.”—Zbigniew, aliye na ugonjwa wa yabisikavu.

[Picha katika ukurasa wa 30]

Wakubwa kwa wadogo wanaweza kuwa chanzo cha kitia-moyo